Habari Njema Zafika Maeneo ya Mashambani ya Afrika Kusini
GHASIA za watu wenye hasira, polisi wa kukomesha ghasia, gesi ya machozi. Katika miaka ya hivi karibuni, miji na majiji ya Afrika Kusini yamepatwa na ugomvi wa jinsi hiyo. Hata maeneo ya mashambani yenye kupendeza—ambapo asilimia zaidi ya 40 ya wakaaji huishi—hayajaepuka madhara ya jeuri ya kisiasa. Hata hivyo, kati ya yote hayo Mashahidi wa Yehova wameendelea kutangaza “Habari Njema ya amani.”—Waefeso 6:15, HNWW.
Kwa miaka mingi Mashahidi wamefanya kampeni ya kuhubiri miezi mitatu kila mwaka yenye kuelekezwa hasa kwa wakaaji wa mashambani. Kwa mfano, katika 1990 wahubiri wa Ufalme zaidi ya 12,000 kutoka makundi 334 walishiriki katika kampeni hiyo. Kwa kawaida, ni lazima vizuizi vingi vishindwe ili kuwafikia wakaaji hao wa mashambani wa kusini mwa Afrika waliotapakaa.
Kati ya mambo mengine, ni lazima Mashahidi washughulike na tamaduni na lugha nyingi mbalimbali. Na huo ni mchanganyiko wa mambo tofauti-tofauti ulioje! Kwa mfano, kuna wakulima wasemao Kiingereza na Kiafrikaani, na pia Wapedi, Wasotho, Watsonga, Watswana, Wavenda, Waxhosa, na Wazulu. Kila kikundi kina utamaduni na lugha yacho chenyewe iliyo tofauti. Pia mifikio ni ya mbali sana na barabara ni zenye mashimo-mashimo. Yote hayo huhitaji roho ya kujidhabihu na utumizi wa wakati na pesa nyingi. Hata hivyo, Yehova amebariki sana jitihada zilizofanywa. Acheni tuwaambie kidogo juu ya magumu na mafanikio ya sehemu hii ya pekee ya kazi ya kuhubiri.—Linganisha Malaki 3:10.
“Shule ya Jumapili” Katika Zululand
Katika kitovu chenyewe cha Zululand ambayo ni nusu-tropiki, kuna bonde lenye kina kirefu la Mto Umvoti. Akiwa kwenye magenge, mtu aweza kuona vikundi vya vijumba vya Kizulu vilivyoezekwa makuti vinavyoenea mbali. Jumapili moja katika 1984, wahubiri wa Ufalme wawili waliingia katika bonde hilo kwenye barabara yenye kujipinda, iliyo ya vumbi. Kuna joto na unyevu mwingi sana huko hivi kwamba eneo hilo laitwa jina la kupanga Kwa-Sathane (Kwa Shetani)—ambalo kwa wazi ni mtajo wa fundisho la uwongo la moto wa helo unaowashwa na Ibilisi!
Wakiwa wamelowa jasho, ndugu hao walimkaribia mwanamke aitwaye Doris, aliyekuwa akiongoza darasa la shule ya Jumapili. Baada ya kusikia ujumbe wa Ufalme, Doris aliwakaribisha Mashahidi hao mara moja wahutubie kikundi chake cha karibu vijana 40. Tokeo likawa nini? Ndugu hao walirudi juma iliyofuata wakiwa na nakala 70 za kichapo Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia wazitumie katika shule ya huko. Katika majuma machache, hali katika shule hiyo ya Jumapili iligeuka ikawa ya kikundi cha funzo la Biblia. Badala ya nyimbo za kanisa, nyimbo za Ufalme ziliimbwa kwa njia ya Kiafrika, kukiwa na ulinganifu wa sauti wa kiasili wenye kupendeza. Upesi kikundi hicho kikaongezeka hadi watu zaidi ya 60. Ndugu mmoja alisema kwa mshangao: “Lilikuwa ono lenye kuchangamsha moyo kama nini kushiriki katika kuigeuza hiyo shule ya Jumapili kuwa mahali pa ibada ya kweli!”
Katika Mbuga Yenye Vumbi
Kwa sababu ya kuhusika kwa kanisa katika msukosuko wa kisiasa, wakulima weupe wengi ni waangalifu sana au hata hutilia shaka mtu yeyote anayewajia na ujumbe wa Biblia. Angalia ripoti hii ya kikundi kutoka Johannesburg kilichosafiri kilometa 640 hivi kuhubiri habari njema katika kisehemu fulani cha Transvaal.
“Tumekuwa tukisafiri kaskazini kuvuka mbuga zenye miinuko na miteremko kwa muda wa saa nne sasa. Mazigazi yanaruka-ruka kwenye barabara iliyonyooka yakimetameta chini ya jua la Afrika. Kwa ghafula, barabara ya lami yafika mwisho, kisha yaanza barabara yenye mikwaruzo yenye mashimo-mashimo. Hatimaye, njia yenye mchanga yatuelekeza kwenye shamba moja.
“‘Habari za asubuhi, Meneer [Bwana],’ twamsalimu mkulima mwenye maungo mapana.
“‘Sijambo,’ ajibu vikali. ‘Je! naweza kuwasaidia?’
“Baada ya kujitanguliza wenyewe kwake, tunaeleza sababu ya ziara yetu. Tukiwa bado twazungumza yeye asema kwa nguvu: ‘Dominee [kasisi] wangu alinionya juu ya nyinyi watu! Nyinyi nyote ni Wakomunisti na Wapinga-Kristo. Ondokeni shambani mwangu mara moja kabla sija . . . !’
“Hali ya mkulima huyo inaonyesha kwamba aweza kuwa mwenye jeuri wakati wowote. Tukiwa hatuna budi, tunaamua kuondoka na ‘kukung’uta mavumbi ya miguuni mwetu.’ (Mathayo 10:14) Huko kuna mavumbi ya kutosha kufanya hivyo kihalisi.
“Kwenye shamba linalofuata itikio ni hilo hilo. Kisha tunatambua kwamba simu ya huko imekuwa ikitumiwa sana na kasisi wa Kanisa la Dutch Reformed, ambaye amekuwa akilionya ‘kundi lake’ juu ya ‘hatari’ ya karibu sana iliyopo katika ujirani. Hatimaye twakutana na mkulima ambaye, ingawa hapendezwi mwenyewe, asema: ‘Naam, mwaweza kuongea na wafanya kazi wangu.’
“Tumekuwa tukingojea jambo hilo tu. Karibu na miti ya jamii ya mkayakaya kuna fungu la vibanda vidogo kumi hivi vya hali ya chini vya udongo mwekundu wa kuchomwa. Tunaporundika vichapo katika marundo nadhifu kwenye funiko la mbele la gari tunahisi macho yenye udadisi yakichungulia kutoka kwenye vibanda hivyo. Rundo moja la Biblia, jingine la kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, na rundo la Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, na broshua mbalimbali zinakamilisha onyesho hilo. Mmoja wa vijana wa huko akimbia kuwajulisha wenyeji wa vijiji kuhusu kuwasili kwetu. Upesi umati wa watu karibu 30 wakusanyika kuzunguka gari kuusikia ujumbe.
“Wanawekewa mahubiri yaliyorekodiwa kimbele katika Kitswana. Hawa watu ni wenye kufurahi kama nini kusikia katika lugha yao wenyewe habari njema za Ufalme wa Mungu na tumaini la Paradiso! Kuna maongeo mengi yenye usisimuko wakati vichapo vinapotolewa. Kabla ya muda mrefu, inakuwa vigumu kwetu kuhesabu vichapo ambavyo tumeangusha. Mzee asema atatoa kiasi fulani cha pesa ili tumpe tepu rekoda ile. Twaguswa moyo sana wakati uthamini kwa habari njema unapoangazwa katika njia nyingi ndogo-ndogo—tabasamu yenye haya, mguso, ‘asante’ yenye upole.
“Kwa hiari, watoto wanafanya mstari usio wenye utaratibu na kuimba wimbo wa kitamaduni wa kuaga. Kwa ghafula, barabara yenye vumbi, yenye mashimo na zile nyakati nyingine zenye maitikio yasiyofaa zafifia na kuwa mambo madogo. Ziara yetu imestahili jitihada zetu zote!”
Jumbe (Chifu) Atoa Amri!
Kundi moja kutoka Soweto lilikuwa na mgawo wa kuhubiri katika eneo la kikabila karibu na mji wa mashariki wa Piet Retief. Desturi huko ni kwamba ni lazima mgeni ataarifu shughuli yake kwa induna (jumbe) wa eneo hilo. Ndugu walifuata mpango huo. Ilishangaza kama nini wakati jumbe alipowakaribisha kwa uchangamfu na hata kuwatolea mahali pa kulala katika nyumba yake mwenyewe! Kuongezea hayo, akitumia muhuri yake ya kirasmi, aliandika barua ya kuwajulisha ambayo wahubiri wangeweza kubeba mlango kwa mlango. Ilisema hivi: “Hawa ni wahubiri wa Ufalme wa Mungu. Wakaribishe nyumbani mwako, na kuwasikiliza.”
Wengi sana waliitikia hivi kwamba Mashahidi walipanga kuwa na hotuba ya watu wote katika ua wa nyumba ya jumbe alasiri ya Jumapili hiyo. “Jumba” hilo la nje lilijaa kabisa, na mkutano ulifunguliwa na kufungwa kwa wimbo na sala. Maono kama hayo pamoja na wale walio na mwelekeo unaofaa yamefurahiwa katika maeneo mengine ya mashambani.
Mtu mmoja wa jinsi hiyo alikuwa Nathaniel, katika kijiji kidogo cha Pitsedisulejang katika sehemu ya pembeni ya Bophuthatswana yenye ukame. Yeye alikuwa mwenye kuendeleza hali ya jumuiya aliyeshughulika na programu ya kufundisha watu wa huko kukuza mazao kwa mafanikio. Aliota juu ya kugeuza mahali hapo pakavu pawe paradiso. Lakini alipojifunza kwamba paradiso ya tufe lote ingekuja karibuni, macho yake yalimetameta. Aliandika kwa moyo kila andiko ambalo wahubiri walimwonyesha. Nathaniel aliarifiwa haraka kuhusu kundi lililo karibu zaidi naye, umbali wa karibu kilometa 30.
Kuwasaidia kwa Shangwe Watafutaji Wengi wa Kweli
“Yehova alituonyesha kwamba umaskini hauzuii mtu mwenye njaa ya kiroho asijifunze kweli,” asema Monika, painia, au mpiga mbiu ya Ufalme wa wakati wote. Yeye alikuwa mmoja katika kikundi cha mapainia waliohubiri shamba kwa shamba kuvuka nyanda pana za Orange Free State katika sehemu ya kati ya nchi. Mapainia walihisije juu ya kujitoa wenyewe katika kuchukua habari njema kwa watu hao? “Kuna nani awezaye kuweka bei ya faida zote ambazo tumeona?” wakajibu. Kwa kweli, mapainia hao walithawabishwa sana kiroho kwa jitihada zao.
Hata kutoweza kusoma hakumzuii mtu mwenye njaa ya kiroho asijifunze kweli ya Kimaandiko. Broshua Furahia Milele Maisha Duniani! yenye picha nzuri hupokewa sana na wale wasioweza kusoma au wanaosoma kidogo sana. Vijana kwa wazee husisimuliwa na picha za paradiso za rangi-rangi. Mfanyakazi wa wakati wote anayesaidia katika kuchapa habari ya jinsi hiyo alionelea hivi: “Broshua hii husaidia watu waone Paradiso kuwa kitu cha hakika na huongeza staha na kicho chao asili kwa Biblia.”
Kwa sababu iyo hiyo, kichapo Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kimependwa na watu wengi sana. Katika eneo la kikabila la Lebowa lililo mbali, wawili wa dada zetu wa kiroho walishangaa kupata kwamba mzee mmoja aliye nusu-kipofu pamoja na mke wake walikuwa na nakala ya kitabu hicho katika lugha ya Sepedi. Wenzi hao walikitumia kuwa kitabu cha kuwafundisha watoto wa huko. Kwa kweli, kitabu hicho kilikuwa kimesomwa na kutiwa alama sana hivi kwamba kilikuwa kinararuka. Walifurahi kama nini kupokea nakala mpya!
Kwa hiyo ni kweli kwamba vichapo vya Kikristo vinatosheleza uhitaji mkubwa katika kuwasaidia wale wenye njaa ya kweli. Kwa kupendeza, sehemu kubwa ya vichapo vyote katika lugha za huko kusini mwa Afrika vina-tolewa na Watch Tower Society. Katika 1990 pekee, vitabu, broshua, na magazeti 113,529 vilivyochapwa na Sosaiti viligawanywa katika maeneo ya mashambani ya Afrika Kusini.
Mazao ya Kazi Ngumu
Je! maono mazuri hayo na vichapo vilivyoangushwa vimetokeza mazao ya kudumu katika maeneo ya mashambani ya Afrika Kusini? Kwa hakika yametokeza. Tangu 1989 makundi manne na vikundi tisa vya sehemu za peke yazo vimefanyizwa vikiwa tokeo la moja kwa moja la kupiga mbiu ya habari njema katika maeneo ya mashambani ya Afrika Kusini. Mapainia wa pekee wa muda na mapainia wa kawaida walifanya sehemu kubwa ya kazi hiyo.
Je! wamkumbuka Doris na shule yake ya Jumapili katika lile bonde la mbali sana huko Zululand? Leo, yeye ni Shahidi wa Yehova aliyejiweka wakfu na kubatizwa. Isitoshe, kikundi chenye kusitawi cha wahubiri wa Ufalme tisa kinazidi kufanya maendeleo ya kiroho huko. Watu wapya wengi huhudhuria mikutano inayofanywa katika nyumba ya Doris, na watu saba ambao aliongoza mafunzo ya Biblia pamoja nao walibatizwa kwenye mkusanyiko wa wilaya uliofanywa huko Durban katika Desemba 1990.
Mazao ya jinsi hiyo ni kichocheo chenye kuchangamsha moyo kwa wahubiri wa Ufalme katika Afrika Kusini. Wanazingatia moyoni maneno ya Paulo: “Kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema.” (Wagalatia 6:10) Naam, watumishi wa Yehova wana nia thabiti ya kuwafikia watu wote wenye moyo mweupe, kutia na wale wanaoishi katika maeneo ya mashambani ya “sehemu [hii] ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Matendo 1:8, NW.
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 24]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Lebowa
TRANSVAAL
Soweto
Piet Retief
Bophuthatswana
ORANGE FREE STATE