“Maji ya Uhai” Yabubujika Katika KEPI VERDE
“KUWAKO na kuzoea kwa ibada ya Mashahidi wa Yehova katika Kepi Verde tangu mwaka 1958 ni jambo linalostahili kuangaliwa,” akaeleza waziri wa haki wa Jamhuri ya Kepi Verde. Alikuwa akisema na Mashahidi wawili waliokuwa wameitwa ofisini kwake. “Tunasikitika kwamba ilichukuwa muda mrefu sana ili Mashahidi wa Yehova waweze kutambuliwa kisheria,” akaongeza.
Mkutano huo uliofanywa Novemba 30, 1990, utakumbukwa kwa muda mrefu na Mashahidi wa Yehova katika Kepi Verde. Uliashiria kutambuliwa kwao rasmi kisheria wakiwa shirika halali la kidini katika nchi hiyo. Hata hivyo, kwa wale Mashahidi wawili waliokuwako, jambo hilo lilikuwa lenye kuwasisimua kibinafsi, kwani ilikuwa katika 1958 kwamba mmoja wao—Luis Andrade—alikuwa amepata baadhi ya vichapo vya Biblia vilivyochapishwa na Watch Tower Society. Baada ya kusoma vichapo hivyo kutoka jalada hadi jalada, alijua kwamba alikuwa ameipata kweli. Kwa bidii, alishiriki yale aliyokuwa amejifunza pamoja na Fransico Tavares, rafiki yake kwa muda mrefu. Katika miaka michache iliyofuata, wote wawili waliendelea kutwaa ndani maji ya kweli kwa kusoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, yaliyopokewa kwa uandikishaji. Miaka kumi baadaye, katika 1968, walibatizwa katika ziara ya kwanza ya mwangalizi msafiri kwenda Kepi Verde.
Ndugu Andrade na Tavares alitambua daraka lao la kuwa na sehemu katika kutangaza ule mwaliko: ‘Njoni! mkayatwae maji ya uhai bure.’ (Ufunuo 22:17, NW) Walikuwa na nia ya kukubali yale majaribu ya eneo lao lenye kutapakaa na lililo gumu. Kepi Verde ni yenye visiwa kumi vikuu kutia na vijisiwa kadhaa katika Bahari ya Atlantiki, karibu na kilometa 560 magharibi mwa Dakar, Senegal. Jina Kepi Verde, linalomaanisha “Rasi ya Kijani Kibichi,” ilitumiwa awali kwa ile peninsula kwenye pwani ya Afrika. Hata hivyo, visiwa hivyo si vibichi hata kidogo, kwa kuwa mvua huwa kidogo sana, na ni lazima wale wakaaji 350,000 wajitahidi kupata riziki kutoka kwa bara kavu.
Katika miaka 30 iliyopita, wamishonari na mapainia wa pekee wamefanya kazi kwa bidii wakiwa watumishi wa wakati wote wanaoleta maji ya uhai kwa wakaa-visiwani. Matokeo ya jitihada hiyo yamekuwa nini? Hivi karibuni, mwangalizi msafiri kutoka Ureno alifanya ziara kwenye makundi katika Kepi Verde. Tutamwacha atuambie yale aliyopata.
Sāo Vicente Chasikia “Lugha Iliyo Safi”
Kituo chetu cha kwanza katika Kepi Verde kilikuwa ni jiji la Porto Grande kwenye Kisiwa cha Sāo Vicente. Tulipokuwa tukiendesha gari kutoka uwanja wa ndege kuingia mjini, tuliona vilima vyenye miamba vilivyofunikwa mchanga uliopeperushwa na upepo. Hali ya Afrika Kaskazini kugeuka kuwa jangwa tayari imefika kwenye visiwa vya Kepi Verde! Kutoka Desemba hadi Februari, harmattani—ule upepo mkavu, wenye joto utokao Sahara—hupita juu ya bahari na kuvifunika visiwa hivyo mchanga na vumbi. Nyakati nyingine mawingu ya vumbi huwa mazito sana hivi kwamba eropleni haziwezi kuruka. Mimea michache inayobaki hunyaushwa wakati harmattani unapowasili.
Hata hivyo, kusema kiroho, vyanzo vya maji hupatikana kwa urahisi. Mashahidi wa Yehova wameanzisha makundi mawili katika Porto Grande, na wahubiri wa Ufalme 167 wanashughulika kupeleka maji yenye kutoa uhai ya kweli kwa wale wakaaji 47,000 wa Kisiwa cha Sāo Vicente. Katika miisho-juma, watu 400 hivi huja kwenye mikutano yenye msingi wa Biblia kwenye Jumba la Ufalme.
Katika ziara hizo za muda wa juma moja, matayarisho ya mwisho yalikuwa yakifanywa kwa ajili ya “Lugha Iliyo Safi” Mkusanyiko wa Wilaya ambao ungefanywa kwenye jumba la michezo lililo bora zaidi katika jiji hilo. (Sefania 3:9) Pamoja na watu wa mahali hapo, wahudhuriaji kutoka visiwa vya Santo Antāo na Sāo Nicolau walifanya hudhurio liwe la kilele cha 756. Watu ishirini na wanne walibatizwa. Programu hiyo ilitia ndani drama ya Biblia iliyotolewa na Mashahidi. Mwanamume mmoja aliyekuwa mkurugenzi wa mazoezi ya utoaji wa filamu alihudhuria drama hiyo na kuonelea hivi: “Tulijizoeza kwa muda wa mwaka mmoja na bado tulikuwa na matatizo mengi. Washiriki katika drama yenu walifanya vema zaidi wakiwa na miezi miwili tu ya kuzoezwa.” Mkusanyiko ukiwa umeisha kwa mafanikio, wakati ulikuwa umefika wa sisi kuendelea hadi jiji la Praia, jiji kuu la Jamhuri ya Kepi Verde, kwenye kisiwa cha Sāo Tiago.
Watu Waliosafishwa
Katika miaka ya hivi karibuni wakaaji wengi wa visiwa vingine wamemiminikia jiji kuu wakitafuta kazi. Tokeo ni kwamba, maelfu ya vibanda sahili vimejengwa nje nje ya jiji, hiyo ikipunguza hata zaidi ugavi wa maji na maandalizi ya kuondoa uchafu. Ili kuongezea mapato yao, familia nyingi hufuga mbuzi, nguruwe, na kuku. Ni kawaidi kuona wanyama hao wakitembea-tembea kwa uhuru barabarani. Hilo limechangia mweneo wa magonjwa.
Hata hivyo, ijapokuwa hali hizo ngumu, sasa kuna makundi mawili yenye kusitawi katika Praia, kukiwa na jumla ya karibu wahubiri wa Ufalme 130. Mashahidi hao wenye furaha kwa hakika ‘wamepata faida’ kwa kutumia yale ambayo wamejifunza kutoka kwa Biblia. Wakijitahidi kuwa watu safi na watakatifu, ndugu zetu na watoto wao wameonea shangwe afya bora zaidi, kiroho na kimwili. Ingawa maisha yao ni magumu, wao ni matajiri kiroho.—Isaya 48:17; 1 Petro 1:15, 16.
Tulipowasili, ndugu walikuwa wakishughulika kutayarishia mkusanyiko wao wa wilaya. Mashahidi na watu wenye kupendezwa kutoka Sāo Tiago pamoja na visiwa vya Sal na Fogo walikuja kwenye mkusanyiko, na Yehova aliwabariki na hudhurio la kilele cha 472. Kila mtu alifurahi sana, kutia na wadogo wengi wenye nyuso zenye kung’aa! Tulipoketi miongoni mwa kundi hilo lenye usikivu, ilikuwa wazi kwamba hatupaswi kamwe kudharau “siku ya mambo madogo.” (Zekaria 4:10) Hayo yote yamekua kutoka watu wawili waliojifunza kweli miaka 30 na kitu tu iliyopita!
Kabla ya kuondoka kisiwa hicho, tulienda kuzuru vikundi vidogo viwili, Vila Assomada na Tarrafal, nje ya jiji. Kisiwa hicho kilikuwa chenye vilima, ukiwa, na kikavu. Lakini hapa na hapa, tuliona vipande vyenye mimea na miti mibichi—maekari ya minazi, ndizi, mapapaya, maembe, na kadhalika. Hilo lilitukumbusha unabii wa Isaya kwamba siku moja hata jangwa litachanua maua. (Isaya 35:1) Kama oasisi (mahali penye maji jangwani), hata sasa vikundi vidogo viwili hivyo vya Mashahidi hutoa chakula na kinywaji kingi cha kiroho kwa wale maelfu wanaoishi kana kwamba katika bara kavu la kiroho.
Bidii Yenye Moto Katika Kisiwa cha Fogo
Kisiwa kilichofuata kilikuwa Fogo, linalomaanisha “moto.” Chanzo chayo cha kivolkeno hueleza jina lacho. Kilele Cano kingali volkeno yenye kutenda. Kinainuka kutoka bahari karibu katika namna ya pia kamilifu kufikia kilele cha meta 2,800. Kisiwa hicho kilikuwa kimepata tu kiasi kikubwa cha mvua, cha kwanza chenye nguvu hiyo kwa muda wa miaka mingi. Kulikuwako hali ya msisimuko miongoni mwa watu, nao walikuwa wakishughulikia mimea yao ya maharagwe na mihogo, vyakula kuu katika Kepi Verde.
Hata hivyo, watu hao wenye kuthamini hawakuwa wenye shughuli mno wasiweze kutua na kutwaa ndani maji ya kweli kutoka kwa Biblia. Tuliweza kukutana na vikundi vitatu tofauti, hata ingawa ilikuwa vigumu kuvifikia kwa sababu magari yalikuwa machache na katika hali mbaya. Tulishangilia sana wakati jumla ya watu 162 walipokuja mikutanoni, kwani kulikuwako wahubiri wa Ufalme 42 peke yao kwenye kisiwa hicho. Hilo lilikuwa wonyesho wa bidii ya kikundi hicho kidogo cha ndugu na dada, wanaotu-mia wastani wa saa 15 kila mwezi wakiyapeleka yale maji ya ufananisho ya kweli na uhai kwa wale wakaaji 32,000 wa kisiwa cha Fogo.
Matunda Katika Bara La Kikatoliki
Tulihitaji bado kuzuru ndugu zetu kwenye visiwa vya Santo Antāo na Sāo Nicolau. Kama vile majina hayo huonyesha, Kanisa la Katoliki ya Kiroma limekuwa na uvutano juu ya visiwa hivyo kwa muda wa karne nyingi. Ingawa Ukatoliki hubaki kuwa dini kuu katika Kepi Verde, watu wengi wenye mioyo myeupe wanageukia Biblia ili kupata maji yayo yenye kuburudisha ya kweli.
Wahubiri wa Ufalme 49 katika yale makundi madogo mawili kwenye pande mbalimbali kabisa za Santo Antāo hufanya kazi kwa bidii ili kutosheleza mahitaji ya kiroho ya wakaaji wacho 44,000. Wakati watu 512 walipokuja kwenye hotuba ya Biblia ya watu wote kwenye Kundi la Porto Novo, ilikuwa wazi kwa wale wahubiri wa Ufalme 32 huko kwamba watu wengi wenye mfano wa kondoo katika Santo Antāo wana kiu ya kupata maji ya kweli.
Kazi ilianza kwenye Kisiwa cha Sāo Nicolau miaka fulani iliyopita wakati dada painia katika Ureno alipoongoza funzo la Biblia kwa barua pamoja na familia kwenye kisiwa hicho. Halafu, katika 1978, painia mwingine katika Ureno aliamua kurudi kwenye kisiwa alikozaliwa, Sāo Nicolau, ili kushiriki kweli ya Biblia pamoja na wakaaji wacho 15,000. Alipoongoza mkutano wa Biblia wa kwanza kwenye kisiwa hicho, hudhurio lilikuwa mtu mmoja tu—mwanamume! Lakini Yehova Mungu alijibu sala za bidii alizotoa kwenye mkutano huo. Katika ziara yetu, wale wahubiri 48 katika makundi yale matatu walisisimuka kuona kwamba jumla ya watu 334 walikuwa wamekuja mikutanoni.
Kusanyiko la mzunguko la kwanza kwenye kisiwa hicho lilifanywa wakati wa ziara yetu, na jumba la michezo la mahali hapo lilipatikana kwetu bila malipo. Maofisa wa mji waliandaa vyombo vya sauti na usafirishaji wa bila malipo. Wale wahubiri 19 wa kundi lenye kukaribisha walishughulikia mahali pa kukaa pa wahudhuriaji 100 na kutayarisha vyakula kwa ajili ya wale 208 waliohudhuria. Yajapokuwa magumu yale mengi ambayo ndugu zetu hukabili kila siku, walichangia ile Akiba ya Jumba la Ufalme ya Sosaiti.
Mwenendo mzuri wa Mashahidi wa Yehova hujulikana sana hapa, na waajiri-kazi wengi huwatafuta wakati wafanya kazi huhitajika. Kwa mfano, mwenye stesheni ya petroli mmoja kwenye kisiwa hicho alimwomba Shahidi amfanyie kazi, kwa kuwa alihitaji mtu mwenye kufuatia haki. Ndugu huyo alikuwa na kazi tayari lakini alisema angechunguza kuona ikiwa angeweza kupata mtu mwingine. “Ikiwa tu yeye ni Shahidi aliyebatizwa!” akasisitiza mwenye stesheni huyo. Miezi miwili baadaye alimwambia ndugu yetu: “Mashahidi wa Yehova peke yao ndio wapaswao kushughulikia pesa!”
Kituo cha Mwisho—Kisiwa Sal
Kituo chetu cha mwisho kwenye safari hiyo kilikuwa kisiwa Sal. Jina lacho humaanisha “chumvi,” na hilo laonyesha kwa wazi kiwanda kikuu kwenye kisiwa hiki. Hapa lile kundi dogo lina wahubiri 22, wanaofanya kazi kwa bidii ili kuleta ujumbe wa Ufalme kwa wakaaji 6,500. Kulipendeza kweli kweli kushiriki habari njema pamoja na wakaa-visiwani hao, kwani tulikaribishwa ndani ya karibu kila nyumba na tuliweza kuongea na washiriki wengi wa familia.
Ziara ya Kisiwa cha Sal ilikamilisha safari yetu. Ilikuwa baraka iliyoje kufanya kazi pamoja na watumishi hao waaminfu wa Yehova katika Kepi Verde! Sasa kuna wahubiri wa Ufalme 531 kwenye visiwa hivyo, na idadi hiyo itaongezeka kwa hakika wakati wale 2,567 waliohudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo katika 1991 wanapoendelea kupokea maandalizi ya kiroho. Ingawa walio wengi wa Mashahidi wa Yehova hapa hawana mengi kimwili, wao ni matajiri na wenye kulishwa vizuri kiroho. Na wanashukuru kama nini kwamba Yehova anasababisha maji ya uhai yabubujike kwa wingi kwenye visiwa hivyo kwa utukufu na sifa yake!
[Ramani katika ukurasa wa 24]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa.)
KEPI VERDE
SANTO ANTĀO
SĀO VICENTE
SĀO NICOLAU
SANTA LUZIA
SAL
BOA VISTA
MAIO
SAO TIAGO
FOGO
BRAVA
Praia
Bahari ya Atlantiki