Utume wa Kupeleka Msaada Ukrainia
RIPOTI za kutia hofu zajaza vyombo vya habari tena. Mchafuko wa kiuchumi, ukosefu wa chakula, na njaa zainyemelea dunia—wakati huu katika sehemu fulani za mahali palipokuwa Urusi zamani. Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova hivi karibuni liliomba ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Denmark lipange ili msaada wapelekewe Mashahidi wenye uhitaji katika Ukrainia. Ndugu wa Denmark walifanya nini?
Walianza kazi mara moja! Ofisi hiyo ya tawi ilituma akina ndugu mara hiyo ili watafute vyakula vilivyo bora zaidi katika masoko. Habari ilipelekwa kwa makundi yote ya watu wa Yehova katika Denmark, ikiyajulisha juu ya uhitaji huo. Tawi laripoti hivi: “Makundi yote yalikuwa na nia sana ya kutoa michango. Hatimaye, tuliweza kutoa ushuhuda wenye kuonekana wazi wa huruma tuliyokuwa nayo kwa ajili ya wale waliokuwa wakiteseka.” Wakati ule ule, ofisi ya tawi ya Sosaiti katika Ujerumani ilipeleka malori matano Denmark yaliyokuwa yametolewa kuwa upaji. Hayo, pamoja na magari makubwa mawili na madereva wenye kujitolea kwa hiari 14, waliwasili kwenye tawi la Denmark Jumamosi, Desemba 7, 1991. Wafanya kazi wa tawi waliyajaza malori hayo na vyakula walivyokuwa wamenunua.
Jumatatu adhuhuri, Desemba 9, msafara huo ulianza safari yao ndefu kupitia Ulaya hadi Ukrainia. “Ilikuwa mandhari yenye kugusa moyo wakati familia yote ya Betheli ilipokusanyika kuwaaga,” tawi laandika. “Tukijua kwamba utume mwingi mbalimbali wa kupeleka msaada umekuwa ukishambuliwa, tuliwafuata ndugu zetu na sala nyingi njiani kote.”
Desemba 18 hali ya wasiwasi iliisha. Tawi la Denmark lilipokea habari kwamba msafari huo ulikuwa umefika salama katika Lvov, Ukrainia. Akina ndugu katika Ukrainia walikuwa wamepokea ule msaada. Walifarijika kama nini kupokea vifurushi vya kilo 20 vya ukubwa wa familia, 1,100—kila kimoja kikiwa na nyama, unga, mchele, sukari, na vyakula vinginevyo! Kwa ujumla, msafara huo ulipeleka ugavi wa tani 22 hivi. Tawi la Denmark laandika hivi: “Shangwe yetu ni nyingi, tunapomshukuru Yehova kwa ajili ya ulinzi wake na kwa ajili ya kutupa sisi nafasi hii ya kutoa msaada.”
Kuna mpango wa kusafirisha nguo pia. Tawi hilo laripoti kwamba kwa habari hiyo pia, “itikio la makundi yote limekuwa kubwa sana.” Yehova kwa kweli ‘huwatajirisha watu wake kwa ajili ya kila aina ya ukarimu.’ (2 Wakorintho 9:11, NW) Wao, nao, huhisi kwa kina kirefu ile shangwe inayotokana na kutolea ndugu na dada zao kwa wingi. Ule upendo wanaoonyesha hivyo ni alama ya kutambulisha wafuasi wa Yesu. (Yohana 13:35) Upendo wa jinsi hiyo uko haba sana katika ulimwengu huu wenye uhitaji.