Ugumu wa Kuhubiri Katika Mojawapo Bandari Kubwa Zaidi za Ulimwengu
ROTTERDAM, ikiwa mahali ambapo Rhine, mto wa Ulaya wenye shughuli nyingi zaidi, huingia Bahari ya Kaskazini, hufurahia ile sifa ya kuwa mojawapo Bandari kubwa zaidi za ulimwengu. Kukiwako meli za kampuni zaidi ya 500 zenye kuja hapa, Rotterdam ina ufungamano wa moja kwa moja na vituo zaidi ya 800 ulimwenguni pote. Kweli kweli hiyo ni bandari ya kimataifa.
Hata hivyo, bandari hiyo ya Kiholanzi yenye umri wa miaka 650 ni zaidi ya kuwa njia-panda ya kampuni za meli. Hiyo pia ni mahali ambapo watu hukutana. Mtiririko wa mabaharia huwasili kila siku na kila usiku kutoka pande zote za ulimwengu. Mabaharia hao hawajaponyoka uangalifu wa Mashahidi wa Yehova katika Uholanzi. Sawa na Mashahidi kwingineko, wao hutafuta njia za kuhubiri habari zilizo njema zaidi ulimwenguni—kwamba Ufalme wa Mungu karibuni utageuza dunia kuwa Paradiso—kwa watu wa aina zote, kutia na mabaharia.—Danieli 2:44; Luka 23:43; 1 Timotheo 4:10.
“Mgawo wa Mishonari Ulio Kinyume”
Miaka kadhaa iliyopita, Watch Tower Society katika Uholanzi iliomba wahubiri sita wa wakati wote, au mapainia, wahubiri kutoka meli hadi meli katika bandari yote ya Rotterdam. Mapainia hao walitwaa nafasi hiyo kwa moyo. Walikusanya habari kutoka kwa mamlaka ya bandari, wakachunguza vituo, na kutambua upesi kwamba walikuwa na mgawo mgumu.
“Ni kama mgawo wa mishonari ulio kinyume,” asema Meinard, anayeratibu kazi ya kuhubiri katika bandari hiyo. Yeye amaanisha nini? “Kwa kawaida mishonari husafiri mwendo mrefu ili kuwaendea watu, lakini katika kisa chetu watu ndio husafiri mwendo huo mrefu kutujia sisi. Aongeza, “eneo letu la kuhubiri labda lisingeweza kuwa la kimataifa kupita jinsi lilivyo.” Kitabu-mwaka cha 1985 cha Rotterdam Europoort kilitaarifu kwamba katika 1983, mwaka ambao mapainia hao walianza kazi hiyo ya kipekee, bandari ya Rotterdam ilipokea vyombo vya baharini 30,820 kutoka nchi tofauti 71. Ni kimataifa kweli kweli!
Kwa kufaa, hao “wamishonari wa bandari”—kama vile mabaharia walianza kuwaita upesi mapainia hao—huonyesha pia hali ya kimataifa. Geert, Peter, na mke wake, Karin, ni Waholanzi; Daniël na Meinard hutoka Indonesia; na Solomon ni Mwethiopia. Ukoo wao wa Kiulaya, Kiasia, na Kiafrika huongeza vizuizi vingine vinane vya lugha, lakini ili kufanikiwa katika kazi hiyo, walikuwa na vizuizi vingine vya kushinda.
“Kanisa Lenye Kupanda Baiskeli”
“Huwezi kutembea gatini, kupanda ngazi ya mbao, na kuingia tu melini,” asema Peter mwenye umri wa miaka 32, aliyekuwa baharia zamani. “Unahitaji vyeti vya ruhusa vya eneo.” Hilo lamaanisha vyeti vya kuingia gatini na vyeti vya kuingia melini. “Kulikuwako na shughuli nyingi za kiofisi,” akumbuka Peter, “lakini baada ya kupata vyeti vinane vya ruhusa, vikiwa kamili na picha zetu na mihuri rasmi, tulikuwa tayari kusonga mbele kwa bidii yote.” Waligawanya zile kilometa 37 za magati ya bandari katika sehemu tatu, kila moja ikishughulikiwa na mapainia wawili.
Lakini, unashughulikaje na wingi wa lugha zinazosemwa na mabaharia kutoka nchi nyingi sana? Hata ingawa mapainia waliweka akiba ya vichapo vya Biblia katika lugha 30 na kubeba vingi wawezavyo juu ya baiskeli zao, ilionekana havikutosha kamwe. “Hujui kamwe kwa hakika ni lugha zipi utakazohitaji,” akumbuka Solomon mwenye umri wa miaka 30 kwa tabasamu. “Mara nyingi inatokea kwamba mabaharia wanataka vitabu katika lugha ile ile ambayo haukuleta, na kisha wanakuambia kwamba meli yao inaondoka katika muda wa saa tatu hivi.” Ili wasiwatamaushe mabaharia hao, painia mmoja huondoka upesi, achukua vitabu vinavyofaa, na kurudi kwa haraka, na kuwapa mabaharia hao wenye hamu. “Tatizo hilo hilo lilipotokea wakati tulipokuwa tukihubiri katika sehemu za bandari zilizoko mwendo wa muda wa saa tatu kwa baiskeli,” asema Petro, “ilikuwa wazi kwamba tulihitaji njia nyingine ya kushughulikia tatizo hilo.”
Siku moja baadhi ya Mashahidi wanaoishi katika eneo la bandari waliwashangaza mapainia hao kwa kuwapa magari mawili ya kuburutwa kwa baiskeli, kila moja likiwa na ukubwa wa beseni ya kuogea. Mapainia hao waliyajaza magari hayo kwa vichapo katika lugha zote zilizopatikana, wakayafungisha kwenye baiskeli zao, na kwenda zao hadi bandarini. Upesi magari hayo yakawa kitu chenye kuonekana kwa kawaida. “Yalikuwa ishara ya kutambulisha kuwapo kwetu,” asema mmoja wa mapainia hao. “Mlinzi anapotuona tukija, hufungua lango, na kuashiria tupite akipaaza sauti: ‘Kanisa lenye kupanda baiskeli ndilo hilo lapita!’” Nyakati nyingine, mlinzi anapoona “kanisa lenye kupanda baiskeli” likija, hufungua lango na kupaaza sauti: “Kuna meli mbili za Kipolandi na moja ya Kichina!” Vidokezo hivyo vyenye kusaidia huwezesha mapainia hao waingie melini wakiwa na vichapo katika lugha zinazofaa. Lakini ni lazima pia waingie kwa wakati unaofaa. Kwa nini?
Ziara za Wakati Unaofaa Pamoja na Ujumbe Unaofaa
Mapainia hao waweza kuongea na mabaharia hao wakati tu wa vipindi vyao vifupi vya kupata kiburudisho asubuhi na alasiri au saa yao moja ya chakula cha adhuhuri. Hata hivyo, mpishi, ana saa tofauti za kufanya kazi, na kapteni na maofisa wengine waweza kupatikana wakati wowote katika siku. Isitoshe, mapainia hao walipata kujua kwamba meli za Uingereza zinazotia nanga katika Rotterdam hufuata saa za Uingereza (tofauti ya saa moja na saa za Uholanzi), kwa hiyo mabaharia wao huelekea chumba cha chakula wakati mabaharia wasio Waingereza wanaporudi kufanya kazi. Kwa wazi, kwa painia wa bandari, kuwa na saa inayotegemeka ni kwa lazima.
Lakini, je, mabaharia wana nia ya kutumia vipindi vyao vifupi vya kupumzika ili kuwa na mazungumzo ya Biblia? “Kwa ujumla, nawaona kuwa wenye utayari wa kukubali maoni tofauti kuelekea ujumbe wa Ufalme,” asema Geert mwenye umri wa miaka 31. “Hilo labda ni kwa sababu wanajionea wenyewe kushindwa kwa serikali za kibinadamu.” Kwa mfano, baadhi ya mabaharia walimwambia Geert kwamba yale marundo ya nafaka ambayo walikuwa wamepakua kwa ajili ya Waethiopia wenye kufa njaa yalikuwa yangali gudini miezi kadhaa baadaye waliporudi kwenye bandari hiyo tena, lakini sasa nafaka hiyo ilikuwa imeoza na kujaa panya. “Si ajabu mabaharia wengi wamepoteza tumaini katika siasa,” asema Geert. “Kwa hiyo ahadi ya Biblia ya serikali moja kwa ainabinadamu wote huwavutia.”
Peter akubali hilo. “Kapteni mmoja Mjerumani alisema kwamba miaka kumi iliyopita mabaharia wake wangeniondosha melini, lakini hali za ulimwengu za leo zenye kubadilika zilikuwa zimeamsha kupendezwa kwao katika ujumbe wa Biblia wa wakati unaofaa.” Mpishi mmoja wa meli ya Kikorea alisimulia kwamba wakati wa vita ya Iran na Iraq, ile meli kubwa sana inayochukua shehena ya mafuta alimokuwa akifanyia kazi ilipigwa na roketi na kushika moto katika Ghuba ya Uajemi. Alitoa nadhiri kwamba ikiwa angeendelea kuishi, angemtafuta Mungu. Aliokoka. Mapainia walipokutana naye baadaye katika Rotterdam, alitaka vichapo vyote vya Kikorea ambavyo wangeweza kumletea.
Meli zilizo nyingi hukaa katika bandari kwa siku kadhaa. Hilo huruhusu mapainia warudi mara mbili, tatu, au zaidi ili kuendeleza mazungumzo ya Biblia baada ya saa za kazi. Hata hivyo, meli inapokuwa na tatizo la injini, huenda ikakaa bandarini kwa muda wa majuma matatu. “Hilo halifai kampuni,” asema painia mmoja kwa tabasamu, “lakini linafaa kazi yetu.” Halafu, zaidi ya kuendeleza mazungumzo ya Biblia, mapainia hupanga pia kuonyesha mojawapo ya programu za silaidi za Sosaiti, “Biblia—Kitabu cha Kizazi Hiki,” katika chumba cha chakula. Baadhi ya mabaharia huja pia kwenye mikutano ya vikundi vingi vya lugha ya kigeni vya Mashahidi wa Yehova katika Rotterdam. Mikutano hiyo huendelea mpaka injini inapotengenezwa. Kisha ni lazima Biblia zifungwe. Kamba zafunguliwa meli yaondoka, na meli kutoweka bandarini—lakini si kutoka akili za mapaina hao.
Hadithi za Mabaharia Zenye Kutia Moyo
Kupitia orodha za magazeti ya habari au mfumo wa kompyuta wa umma wa usimamizi wa bandari, mapainia wa bandari waweza kujua habari za mwendo wa meli ambazo wamezuru. Mara tu mojawapo inapokuja tena, mapainia hutamani sana kuwatembelea mabaharia hao ili wapate kujua ni jambo gani limetukia tangu ziara ya mwisho. Mabaharia hao husimulia hadithi zenye kutia moyo kama nini!
Baharia mmoja aliwapa wafanyakazi wenzake watano wa melini nakala za kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani baada ya meli yake kuanza kusafiri baharini, na wote sita wakawa na funzo la Biblia. Alirekodi pia ile sura juu ya maisha ya familia kwenye kaseti ya sauti na kuicheza katika chumba cha chakula ili mabaharia wote wanufaike. Katika meli nyingine, baharia mmoja aliyekuwa amezuru Jumba la Ufalme katika bandari ya karibu ya Antwerp aliweka kwenye ukuta wa jumba la chakula ishara yenye maneno “Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova” katika herufi kubwa. Kisha akaalika mabaharia waje humo wakati alipoongoza mkutano wa Biblia. Kabla ya kuondoa tangazo hilo, aliwaalika mabaharia hao kwenye mkutano mwingine. Juma lililofuata, ishara ile na mabaharia walikuwapo mahali pao tena.
Mapainia hao walipata pia kwamba mabaharia wengine hawakuweka vitabu vyao mbali. “Walipoingia chumba cha Isaac, ofisa wa redio kutoka Afrika Magharibi, ilikuwa vigumu kupata mahali pa kuketi,” asimulia Meinard. “Magazeti, vitabu, na konkodansi za Sosaiti zilikuwa kila mahali—na zikiwa zimefunguliwa.” Isaac alikuwa pia na orodha ya maswali ya Biblia tayari, kwa kuwa alikuwa akingojea ziara ya kurudia ya mapainia hao.
Lakini, mabaharia wengine, hawangojei mapainia wawarudie. Usiku mmoja simu ya Geert ililia baada ya yeye kulala usingizi.
“Huyo kwa kweli aweza kuwa nani?” Geert akanung’unika akipapasa ili ainyanyue.
“Habari, huyu ni rafiki yako!” ikajulisha sauti changamfu.
Geert akajaribu kumkumbuka mtu huyo.
“Ni saa tisa asubuhi!” akasema Geert.
“Ndiyo, lakini uliniambia nikupigie simu mara meli yangu irudipo Rotterdam tena. Basi, niko hapa!” Muda mfupi baadaye, Geert alikuwa njiani kukutana na rafiki huyo aliyependezwa na Neno la Mungu.
“Tupa Chakula Chako”
Uthamini kwa ajili ya vichapo vya Biblia huonyeshwa katika barua kutoka kwa mabaharia kwa mapainia. Zifuatazo ni sehemu-sehemu zazo:
‘Nimeanza kukisoma kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani . . . Sasa ninaelewa mambo mengi ambayo sikuwa ninaelewa mbeleni. Natumaini kwamba meli yetu itarudi Rotterdam.’—Angelo.
‘Nilikisoma kitabu hicho, na ninakupelekea maswali hivi kwamba uweze kuyajibu katika barua zako.’—Alberta.
‘Mimi sasa husoma Biblia kila siku. Ninafurahi kuwa rafiki yako. Kupata marafiki wanaoniongoza kwa Mungu ni jambo bora zaidi lililopata kutukia maishani mwangu.’—Nickey.
Barua za jinsi hiyo zenye kuchangamsha moyo huwakumbusha mapainia hao juu ya lile ambalo Biblia husema kwenye Mhubiri 11:1: “Tupa chakula chako usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi.” Wao hushangilia hasa wakati wanapojua kwamba mabaharia wengine wamechukua msimamo wao kwa ajili ya Yehova.
Kwa mfano, baharia wa Polandi Stanislav, alisisimuliwa na yale ambayo alikuwa amejifunza kutoka kwa vitabu vya Sosaiti. Upesi alijipatia maktaba ndogo ya vichapo vya Biblia na, alipokuwa baharini, alijifunza kila kichapo chayo. “Tulipopokea habari kutoka kwake tena,” asema Meinard, “aliandika kwamba alikuwa amebatizwa.”
Folkert, kapteni wa meli zinazosafiri katika mito ya nchini mwake, alisikia ujumbe wa Ufalme mara ya kwanza katika Rotterdam. Kila miezi miwili alirudi kwenye bandari kwa juma moja na kujifunza Biblia siku saba mfululizo. Kisha, kabla ya yeye kuondoka tena kwa safari nyingine ya miezi miwili, mapainia walimpa orodha ya anwani za Majumba ya Ufalme yaliyokuwa kwenye njia ya safari yake. Folkert alizuru majumba hayo naye akasukumwa na ule ukaribishaji mchangamfu aliopokea. Kabla ya muda mrefu, kapteni huyo akabatizwa na sasa humtumikia Yehova kwa bidii.
Mike, ofisa wa Manowari ya Uingereza, alikuwa amekutana na Mashahidi kabla ya hapo na alikuwa amejifunza Biblia alipokuwa baharini. Wakati mmoja, manowari ya matanga alimokuwa akifanyia kazi ilipotia nanga katika Rotterdam, alitumia baiskeli yake iwezayo kukunjwa kuja kwenye Jumba la Ufalme moja. Alivutiwa na ule upendo na umoja alioona na kuwaambia akina ndugu kwamba alikuwa ameamua kuacha kazi yake. Ingawa alikuwa na miaka minne tu kabla ya kupokea malipo makubwa ya uzeeni, alishikamana na uamuzi wake na kubatizwa baadaye.
Meinard asema hivi: “Ile bidii nyingi ya Mike, Stanislav, Folkert, na wengine ya kumtumikia Yehova yatusukuma tuendelee kutafuta-tafuta katika bandari tupate mabaharia walio kama hao.”
Je! Wewe Waweza Kushiriki?
Kuangalia huko nyuma baada ya karibu mwongo mmoja wa kuhubiri katika mojawapo bandari kubwa zaidi za ulimwengu, wale “wamishonari wa bandarini” sita hukubali kwa moyo wote—mgawo huo umekuwa mgumu lakini wenye kuthawabisha. “Baada ya kila siku ya kuhubiri,” amalizia Meinard, “tunarudi nyumbani kwa baiskeli tukihisi kwamba baadhi ya mabaharia hao walikuwa wakingojea ziara yetu.”
Je! yawezekana kwamba kuna mabaharia wanaongojea ziara katika bandari ya eneo lenu? Labda wazee katika kundi lenu wanaweza kufanya mipango ili uweze kushiriki katika kazi hiyo gumu lakini yenye kuthawabisha.
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
KUFIKIA MAENO YALIYOPIGWA MARUFUKU
Katika mwaka mmoja wa karibuni, meli zaidi ya 2,500 kutoka nchi ambazo utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulikuwa umepigwa marufuku zilitia gudini Rotterdam. Na mapainia wa bandarini waliona hilo kuwa nafasi ya kufikia maeneo hayo kwa ujumbe wa Biblia.
Katika mojawapo zile meli za Asia za kwanza walizozuru, mapainia waliangusha ugavi wao wote wa vitabu 23, wakiwaacha mabaharia wengine wakiwa wameudhika kwa sababu walikosa kupata nakala. Kijana aliyefanya kazi jikoni kwenye meli nyingine ya Asia alikuwa mwangalifu zaidi. Baada ya kukubali kitabu kutoka kwa painia, alikirudisha kikiwa kimefungiliwa karatasi yenye anwani juu yayo. Painia huyo alielewa ni kwa nini alifanya hivyo. Lingekuwa jambo la hatari sana kwa kijana huyo kuchukua kitabu hicho mwenyewe aende nacho. Siku hiyo hiyo kilipelekwa na painia huyo kwa posta kwenda Mashariki ya Mbali.
Katika meli moja kutoka Afrika mlikuwamo baharia mmoja aliyekuwa na orodha ya vitabu ambavyo Mashahidi wa nyumbani walitaka. Tangu wakati huo na kuendelea, kila wakati baharia huyo arudipo nyumbani, sanduku lake huwa limejaa vichapo. Baharia mwingine kutoka nchi nyingine ya Afrika alitamauka sana wakati painia aliyekuwa akijifunza naye angeweza kutoa nakala tatu tu za kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha. “Hivyo si kitu!” baharia huyo akasema kwa mshangao, akiashiria kwa mikono yake kwa kukata tamaa. “Ndugu walio nyumbani wanahitaji 1,000!” Kwa ajili ya usalama wake mwenyewe, mapainia walimsadikisha apeleke nakala 20 tu kwa wakati mmoja.
Labda jambo lenye kugusa moyo zaidi lilikuwa wakati mapainia walipopata kujua kwamba meli ilikuwa imekuja kutoka nchi ambayo Mashahidi walinyanyaswa kwa ajili ya imani zao, na wengi walikuwa wamepoteza kazi na mali zao. Walipopata kujua kwamba ofisa wa utumishi wa abiria melini alikuwa Shahidi, walimtembelea kapteni na kumwomba ruhusa ya kupeleka msaada kwa meli yake. Kapteni alikubali, na siku chache baadaye, mifuko mikubwa mia moja yenye nguo, viatu, na vifaa vingine vilikuwa njiani kwenda kwa Mashahidi katika nchi hiyo.
KUHUBIRI MELI KWA MELI—MAONI YA MWANAMKE
“Mwanzoni nilisita kuandamana na Peter,” akumbuka Karin, mwanamke wa pekee miongoni mwa mapainia hao, “kwa sababu nilikuwa nimesikia hadithi kwamba mara nyingi mabaharia hawana adabu na ni walevi. Hata hivyo, nimepata kwamba wengi wao ni wenye adabu. Mara nyingi, baada ya baharia kupata kujua kwamba sisi ni wenzi wa ndoa, yeye atatoa picha ya mke na watoto wake na kuanza kuongea juu ya familia yake. Kwa njia hiyo, tumeangusha nakala nyingi za kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha.”
Kuzuru meli tukiwa mume na mke hufanya iwe rahisi pia kukutana na wake wa mabaharia na wanawake wengine ambao nyakati nyingine hufanya kazi wakiwa wauguzi. “Kwa kawaida wao huwa wanyamavu kuelekea wageni,” asema Karin, “lakini wanaponiona mimi, wanajihisi huru zaidi kushiriki katika mazungumzo.”
Ni nini lililokuwa jaribu kubwa zaidi katika mgawo wake? “Ngazi za kamba,” ajibu Karin. “Nilivichukia vitu hivyo vyembamba.” Je! aliushinda woga wake? “Ndiyo. Wakati mmoja niliposita kupanda moja, kikundi cha mabaharia kutoka Paraguay walitazama na kupaaza sauti: ‘Utaweza. Mtumaini Mungu tu.’ Pasipo shaka,” asema Karin akicheka, “baada ya maneno hayo, sikuwa na la kufanya ila kupanda.” Asema mume wake anayemsifu: “Baada ya miaka minne ya kupanda ngazi nyingi za kamba, sasa yeye huzipanda kama baharia.”
Karin na mume wake, Peter, walihudhuria darasa la 89 la Watchtower Bible School of Gilead katika United States. Katika Septemba 28, 1990, waliondoka kwenda kwenye mgawo wao mpya, Ekuadori, nchi yenye bandari. Ni lazima iwe wanajihisi wakiwa kwao kabisa.
[Sanduku katika ukurasa wa 21]
KUHUBIRI MELI KWA MELI-MAONI YA MWANAMKE
Je! Wewe Ni Baharia?
Je! unataka kuhudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova wa lugha ya Kiingereza wakati meli yako inapotia nanga katika mojawapo bandari kubwa za ulimwengu? Basi weka karibu orodha hii ya anwani za sasa za Majumba ya Ufalme na nyakati za mikutano:
Hamburg, Schellingstr. 7-9; Jumamosi, 10:00 alasiri; simu: 040-4208413
Hongkong, 26 Leighton Road; Jumapili, 3:00 asubuhi; simu: 5774159
Le Harve, 65 rue de Trouville; Jumapili, 8:30 alasiri; simu: 35 44 54 27
Marseilles, 5 Bis, rue Antoine Maille; Jumapili, 4:00 usiku; simu: 91 79 27 89
Naples, Castel Voltumo (Kilometa 40 kaskazini mwa Naples),
Via Napoli, kona ya Via Salerno, Parco Campania; Jumapili, 8:45 alasiri; simu: 081/5097292
New York, 167 W. 107 Street; Jumapili, 10:00 alasiri; simu: 212-662-8143
Rotterdam, Putsestraat 20; Jumapili, 4:00 asubuhi; simu: 010-41 65 653
Tokyo, 5-5-8 Mita, Minato-ku; Jumapili, 10:00 alasiri; simu: 03-3453-0404
Vancouver, 1526 Robson Street; Jumapili, 4:00 asubuhi; simu: 604-689-9796