Kukusanya “Vitu Vinavyotamaniwa” Katika Polandi
POLANDI yasemwa kuwa nchi ya Kikatoliki. Kulingana na takwimu rasmi, asilimia 93 ya wakazi ni wa Kanisa Katoliki. Hata hivyo, mabadiliko ya kisiasa na ya kijamii ya hivi karibuni yanayotukia huko yameathiri sana watu na maisha yao ya kidini. Utafiti mbalimbali unaonyesha kwamba ni karibu asilimia 50 tu ya wale walioulizwa maoni yao waliojiona wenyewe kuwa Wakatoliki wenye kutenda.
Katika Mei 1989, Mashahidi wa Yehova walitambuliwa kisheria kuwa tengenezo la kidini katika Polandi. Tangu wakati huo, watu wapya wapatao 11,000 wamejiunga na idadi zao wakiwa wahubiri wa habari njema za Ufalme. Sasa wahubiri wa Ufalme zaidi ya 106,000 wanashirikiana na makundi zaidi ya 1,300, na watu 200,422 walihudhuria mwadhimisho wa Ukumbusho wa kifo cha Yesu wa 1991. Hivyo, kule kukusanywa kwa “vitu vinavyotamaniwa na mataifa” kunatukia katika Polandi. (Hagai 2:7) Hivi karibuni, mikusanyiko ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova iliyofanyiza habari kuu ya magazeti ya habari ilifanywa katika Polandi. Lakini kutazama baadhi ya miji midogo zaidi katika nchi hiyo kutaonyesha hasa jinsi kazi ya kukusanya inavyoendelea katika bara hilo.
Mapainia Wafungua Njia
Sztum ni mji wenye wakazi wapatao 10,000 ulioko karibu na mahali ambapo Mto Vistula huingia Bahari ya Baltiki. Mji huo umeonwa kwa muda mrefu kuwa eneo lenye miamba kwa habari ya kazi ya kuhubiri. Katika 1987 kulikuwako wahubiri wanane tu katika eneo hilo. Hata hivyo, mambo yalianza kubadilika wakati mapainia, au wapiga mbiu ya Ufalme wa wakati wote, walipowasili. Kwenye mkutano wa tano, uliofanywa katika jumba la sinema, watu 100 wenye kupendezwa walihudhuria! Kundi lilifanyizwa baada ya miaka miwili ya bidii-nyendelevu. Sasa wahubiri 90 wana Jumba la Ufalme lao wenyewe, na watu 150 huhudhuria mikutano yao kwa ukawaida.
Kama ilivyotazamiwa, upinzani ulianza upesi kutoka kwa Kanisa Katoliki. Mtawa wa kike “mwenye ustadi” alitoa hotuba zenye kuwasingizia Mashahidi, akiwashtaki juu ya kufundisha mafundisho bandia. Lakini kama vile inavyotukia mara nyingi, hilo lilikuwa na matokeo yasiyotazamiwa. Hotuba zake ziliwafanya watu watake tu kupata kujua mambo ya hakika. Wengi wao wamejifunza kweli na sasa ni mapainia wa kawaida! Wanasema hivi: ‘Tulipokuwa tukijifunza kweli, tulifikiri kwamba kila mmoja aliyetaka kuwa Shahidi alipaswa kuwa kama mwalimu wake, lililomaanisha kuwa painia.’ Kwa hiyo roho ya upainia imeenea katika kundi zima.
Likiwa tokeo, mafunzo ya Biblia yapatayo 180 yanaongozwa katika eneo hilo. Kupitia kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, wengine hata wamefunzwa kusoma. Wakati huo huo, wamejifunza kweli. Mafunzo ya Biblia ya kawaida ya muda wa dakika kumi yanaongozwa na kikundi cha wafungwa gerezani la huko wanapotoka kusafisha barabara. Mmoja wao alimtetea Shahidi mmoja wakati mwanamke aliyekuwa akipita alipoanza kumtukana. Mfungwa huyo alikimbia hadi kwa dada huyo, akachukua kitabu Kuishi kutoka mikononi mwake, akakiinua juu, na kumwuliza mwanamke huyo mwenye kutukana: “Je! huwezi kusoma? Ni nini kilichoandikwa hapa? Unaweza kuishi milele katika Paradiso duniani! Je! umewahi kusikia jambo kama hilo? Kwa nini basi wamtukana Mungu na waabudu wake?”
Kichwa cha Maongezi Mjini
Kruszwika, uliokuwa wakati mmoja jiji kuu la Polandi la kihekaya, ni ngome ya Ukatoliki. Hata kufikia katikati ya 1990, kulikuwako Mashahidi wachache tu miongoni mwa wakazi wao 9,300. Lakini baraka nyingi za Yehova zilikuwa juu ya jitihada za wapiga mbiu ya Ufalme.
Wakiona unafiki wa viongozi wao wa kiroho, watu zaidi na zaidi—hasa vijana—waliwageukia Mashahidi kupata majibu. Katika muda mfupi sana, mafunzo ya Biblia 20 yalianzishwa. Padri wa parishi alitoa mahubiri makali juu ya Mashahidi wa Yehova, lakini hilo halikuwavunja moyo watu wanyofu wasihudhurie mikutano yao. Mashahidi walikuja kuwa kichwa kikuu cha mazungumzo madukani na bustanini na hata kanisani. Baada ya nusu ya mwaka, vikundi viwili vikubwa vya funzo la kitabu vilifanyizwa. Mji wa Kruszwika sasa una kundi lenye bidii sana la waabudu wa Yehova wapatao 35. Wanaongoza mafunzo ya Biblia 75 na wanaleta kwa bidii nyingi “vitu vinavyotamaniwa” ambavyo wakati mmoja vilikuwa katika utumwa wa dini bandia.
Miongoni mwa hivyo mlikuwa Bogdan mwenye umri wa miaka 23, mshiriki wa familia yenye kufuata sana Ukatoliki. Yeye akumbuka hivi: “Nilikuwa nikinywa vileo, nikivuta sigareti, na kuishi maisha yasiyo ya kiadili. Nilijulikana kuwa mkorofi na mleta ghasia, na hakuna yeyote aliyeonekana kujali. Hata hivyo nilipoanza kujifunza Biblia, mama yangu alitisha kujilisha sumu. Niliposhindwa kuvumilia mbano huo, niliacha kabisa kuwasiliana na Mashahidi. Baadaye, kwa msaada wenye upendo wa mapainia wa pekee, niliweza kujiweka huru na mazoea yote mabaya. Nikiwa nimebatizwa kwenye ‘Wapendao Uhuru’ Mkusanyiko wa Wilaya, nimechagua huduma ya wakati wote iwe mradi wangu maishani na nimekuwa nikifanya upainia msaidizi tangu wakati huo.”
Slawomir mwenye umri wa miaka 21 alikuwa ametatanika katika uwasiliani-roho na Ushetani, alioacha alipoona kwamba Biblia hushutumu mazoea ya jinsi hiyo. “Lakini Shetani alisisitiza,” yeye asema. “Usiku mmoja rekodiplea ilianza kucheza bila kuwashwa, nikasikia muziki wa kishetani, ingawa nilikuwa nimeondoa kutoka nyumbani kila kitu kilichohusiana na ibada ya Ibilisi. Nilisali kwa Yehova, na alinisaidia kupata usawaziko wa kiroho tena. Daktari wa ugonjwa wa akili ambaye nilikuwa nikimwona kwa kusihiwa na wazazi wangu alitambua mabadiliko makubwa katika hali yangu na akakata maneno kwamba nilikuwa na afya njema. Aliandika hivi kwenye chati yake ya kuonyesha maendeleo yangu: ‘Ameponywa na Mashahidi wa Yehova.’”
Kupinga Roho ya Kilimwengu
Kusini-magharibi mwa Kruszwika ni Środa Śląska. “Vitu vinavyotamaniwa” vinatokea pia katika mji huo mdogo wenye watu 9,000. Miaka minne iliyopita, ni mmoja tu wa dada zetu wa kiroho aliyekuwa akiishi huko. Hata hivyo, sasa idadi ya wahubiri wa Ufalme imeongezeka hadi 47. Walio wengi wa Mashahidi walikuwa wamenaswa katika mitego ya uwasiliani-roho, uzoevu wa dawa za kulevya, na ukosefu wa adili. Wanaona kwamba hilo lilikuwa hasa kwa sababu ya hali ya utupu wa kiroho iliyoko kanisani iwezayo tu kushutumu watu kiroho, si kuwasaidia. Mashahidi wanawatolea watu kitulizo cha kweli.
Wachanga kundini wamefanya shule kuwa eneo lao la kibinafsi la kufanyia kazi ya kuhubiri. “Wanashule wenzangu huniambia mara nyingi: ‘Unatumia vibaya ujana wako,’” aripoti Kasia mwenye umri wa miaka 18. “Lakini nimeepuka shida nyingi, na maisha yangu yamekuwa yenye maana. Ninaongoza mafunzo ya Biblia kadhaa shuleni nami sipuuzi wala masomo yangu ya kufanyiwa nyumbani wala funzo langu la kibinafsi. Wasichana wasemao ‘ninatumia vibaya ujana wangu’ ni akina mama tayari, wanaong’ang’ana na matatizo mengi.”
Vichapo vya Watch Tower vimekuja kupendwa sana katika shule za huko. Kwa mfano, mwalimu mmoja wa lugha ya Kipolandi aliwaambia wanafunzi wake watumie lugha dhahiri ya jarida letu Amkeni! kuwa mfano wao katika kuandika insha zao. Painia msaidizi Ewa aona broshua Shule na Mashahidi wa Yehova kuwa yenye kufaidi. “Ninathamini sana kichapo hiki. Walimu wangu wanakifahamu sana. Sijapata kamwe kuwa na tatizo lolote kupata ruhusa ya kuacha masomo ili kuhudhuria mikusanyiko mikubwa.” Mtazamo mzuri wa jinsi hiyo kwa upande wa vijana huufurahisha moyo wa Yehova—Mithali 27:11.
Wahalifu Shupavu Wabadilishwa
Mashariki mwa Środa Śląska ni Strzelke Opolskie, mahali palipo na magereza mawili. Moja ni gereza lenye ulinzi wa juu la wahalifu wasiorudika. Mashahidi huzuru magereza hayo kwa ukawaida kuleta kweli kwa wafungwa gerezani, wengi wao walikuwa pia watumwa wa Babuloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini bandia.—Ufunuo 18:1-5.
Mashahidi hujifunza Biblia na wafungwa gerezani mmoja mmoja na vikundi vidogo vya wafungwa gerezani, wengine kati yao wakiwa wamebatizwa. Ingawa ni lazima wamalize vifungo vyao, wao huhubiri habari njema kwa bidii kwa wafungwa gerezani wengine. Mfungwa gerezani mmoja aliyekuwa akijitayarisha kwa ajili ya kubatizwa alifanya mabadiliko yenye kutokeza sana hivi kwamba wenye mamlaka wa gereza walimruhusu aende nyumbani mara moja kwa juma. Wengine wameandikia familia zao wakionyesha azimio lao la kuondoka gerezani, si wakiwa wahalifu, bali wakiwa Mashahidi wa Yehova.
Ofisa mkuu wa mojawapo ya magereza hayo alilalamika kwamba mapadri Wakatoliki walikuwa wakija lakini hawakutimiza chochote. Aliwauliza Mashahidi hivi: “Ni nini kinachowawezesha mwabadili na kuwarekebisha tabia?” Barua kutoka kwa mfungwa gerezani mmoja kwa familia yake yajibu: “Hapa gerezani, Mashahidi wa Yehova wameniambia juu ya ahadi ya Mungu ya ajabu kuhusu ile serikali mpya, Ufalme wa Yehova, itakayotawala juu ya dunia hivi karibuni. Hapa nimekuwa na wakati wa kuchanganua maisha yangu ya mbeleni kupatana na Biblia. Baada ya kufanya mikataa yenye kutia uchungu, nimepatwa na tamaa ya kuwa mtu huru na kujipata mwenyewe kuwa raia wa Ufalme wa Mungu. Leo mimi ni Shahidi wa Yehova aliyebatizwa.”
Katika gereza jingine, wengi wanatumikia hukumu za muda wa miaka 25 kwa ajili ya uuaji wa kimakusudi. Funzo la Biblia la kawaida linaongozwa na wanaume 12. Mmoja wao aliweka maisha yake wakfu kwa Yehova na akabatizwa, na wengine wanapanga kuchukua hatua hizo. Akiyathamini matokeo mazuri ya njia za kuelimisha zinazotumiwa na Mashahidi wa Yehova, ofisa mkuu wa gereza hilo alisema hivi: “Mimi sina wafungwa gerezani 12. Nina 600. Tafadhali mnisaidie kuwarekebisha tabia. Nitawapa kila kitu mnachohitaji, lakini tafadhali tayarisheni programu hiyo. Washughulikieni!”
Akina ndugu walifanya lilo hilo. Walitoa programu ya Biblia inayoshughulikia kusudi la uhai, tumaini la wakati ujao, na umaana wa kuacha mazoea mabaya. Pia walisimulia maono ya mfungwa gerezani mmoja wa zamani yaliyekuja kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na baadaye akawekwa rasmi kuwa mzee wa kundi. Mashahidi hao walitoa pia mambo makuu kutoka kwa hadithi za maisha za mwizi wa almasi na mzoevu wa dawa za kulevya waliojifunza kweli.a Wafungwa gerezani 20 waliokuwako waliona programu hiyo kuwa yenye kupendeza sana na wakauliza maswali mengi, baadhi yao hata wakiomba mafunzo ya Biblia.
Imani na Uvumilivu Vyatahiniwa
Lubakzów ni mji mdogo wenye wakazi 12,000 ulio karibu na mpaka wa Ukrainia. Kazi ya kueneza evanjeli huko iliongezeka mwendo katika 1988 wakati mapainia walipohamia huko ili kuwasaidia wale wahubiri 12 wa huko. Sasa kuna wahubiri wa Ufalme wenye kutenda 72, na watu 150 walihudhuria mwadhimisho wa Ukumbusho wa 1991 katika Jumba la Ufalme lililojengwa karibuni.
Katika Juni 1991, Papa John Paul wa 2 alizuru Lubakzów. Lakini hilo halikufanya chochote kuimarisha imani ya kweli miongoni mwa watu. Wengi wao wana mashaka na maswali mengi juu ya kusudi la uhai na tumaini la wakati ujao. Wanaposhindwa kupata majibu ya kutosheleza kutoka kwa makasisi, wanawageukia Mashahidi wa Yehova. Ingawa watu hao huenda mwanzoni wakaumizwa sana na dhamiri zao kwa ajili ya kuigeuzia dini yao visogo vyao, kweli ya Biblia wanayojifunza huwasaidia waone kwamba wamefanya uamuzi unaofaa.
Ono la kawaida ni lile la Honorata, ambaye sasa ni painia wa kawaida. Karibu mwaka mmoja uliopita, alimwuliza padri wakati wa ungamo ni nini jina la Mungu. “Mungu ni upendo—hilo ndilo jina lake lenye kupendeza zaidi,” akajibu padri. Baada ya muda fulani, padri aliongeza hivi: “Wewe ni kama ndoo yenye maji safi kama fuwele ambamo mtu ametia wino. Matokeo hayawezi kugeuzwa.” Hivyo akapata jibu lake. “Niliamua wakati huo kwamba ningekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova,” asema Honorata. “Hilo pia haliwezi kugeuzwa.”
Karibu kila mtu aliyejifunza kweli katika Lubakzów alihitaji kuvumilia upinzani wenye nguvu, hata wenye ushupavu. Lakini hilo halikuwazuia wasikubali kweli ya Biblia na kuuchukua msimamo wao kwa ajili ya Yehova.
Elżbieta asimulia hivi: “Mwanzoni walinipiga nyumbani. Halafu familia yangu ikaingia ndani ya Jumba la Ufalme kwa kishi-ndo. . . . Walinipeleka nyumbani na kuanza ‘kutekeleza hukumu’ kwa kutumia kijiti chenye vipingili. Nilipigwa kwa kijiti na kupigwa mateke kuanzia kichwani mpaka kidole cha mguu kwa sababu tu ya kushirikiana na Mashahidi. Nilipigwa vibaya sana hivi kwamba nikahitaji utabibu wa haraka nami nikapelekwa hospitali. Yehova alinisaidia, nakapona. Familia yangu ilinikatalia mbali. Nilipomtajia padri hilo, alinifanya mdogo, akisema: ‘Umekuja kulalamika kwa sababa ya makofi machache tu?’”
Dada mwingine akumbuka hivi: “Kila mwaka nilikuwa nikienda Chestochowa kutembea Njia ya Msalaba, jambo nililoona kuwa wajibu wa kila Mkatoliki mnyofu. Ningali nina makovu magotini pangu.” Akiwa na miaka 18 alijifunza kweli na akamwambia padri na familia yake kwamba asingerudi kanisani. Alipigwa vibaya sana—“vibaya sana hivi kwamba nilikuwa na jeraha la ubongo,” yeye aripoti. “Lakini hospitalini nilipona vya kutosha kuweza kuhudhuria ‘Wapendao Uhuru’ Mkusanyiko wa Wilaya. Nililia machozi kwa shangwe wakati nilipoona umoja na upendo wa kweli miongoni mwa watu bila ushupavu wa dini—mambo ambayo sikuwa nimeona Chestochowa. Ninafurahi kama nini kwamba nimeona wema wa Yehova na nimejifunza kumtumaini yeye.” Yehova huwaimarisha na kuwategemeza wale wanaomtwika mizigo yao.—Zaburi 55:22.
Watumwa wengi wa Babuloni Mkubwa sasa wanatii mwito wa ‘kutoka kwake’ katika nchi hii ya Kikatoliki, sawa na vile wanavyofanya kwingineko. Ikiwa ni mapenzi ya Yehova, watu wake wasio na hofu wataendelea kukusanya vingine zaidi vya vile “vitu vinavyotamaniwa” vilivyotawanyika kotekote Polandi. Kwa hakika, wengi zaidi wataitikia ule mwito: “Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.”—Ufunuo 18:4; 22:17.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Amkeni! la Oktoba 8, 1983, kurasa 16-19, na la Novemba 22, 1987, kurasa 21-3, (Kiingereza).
[Ramani katika ukurasa wa 24]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa.)
POLANDI
Sztum
Poznan
Kruszwika
Warsaw
Środa Śląska
Chestochowa
Strzelke Opolskie
Lubakzów
[Picha katika ukurasa wa 26]
Kuhubiri ujumbe wa Ufalme katika Kruszwika, Polandi