Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 8/15 kur. 21-25
  • Kuhubiri Katika Maputo Jiji Kuu la Msumbiji Lenye Kusisimua!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuhubiri Katika Maputo Jiji Kuu la Msumbiji Lenye Kusisimua!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Maputo, Jiji Kuu
  • “Wavuvi wa Watu”
  • Kupeleka Vichapo Kwenye Bohari
  • Maendeleo ya Kitheokrasi Vijapokuwa Vizuizi
  • “Mavuno ni Mengi”
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 8/15 kur. 21-25

Kuhubiri Katika Maputo Jiji Kuu la Msumbiji Lenye Kusisimua!

Katika 1991, Mashahidi wa Yehova walipewa utambuzi wa kisheria katika Msumbiji. Tangu wakati huo kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu kumefanya maendeleo ya ajabu katika nchi hiyo ya kitropiki kwenye pwani ya kusini-mashariki mwa Afrika. Ufuatao ni usimulizi wa jinsi Mashahidi wa Yehova huendeleza kazi yao ya elimu ya Biblia katika Msumbiji, hasa karibu na Maputo, jiji kuu.

HALI yayo ya anga ikiathiriwa na ile Bahari ya Hindi yenye ujoto, Msumbiji huonea shangwe hali-joto yenye kuburudisha. Fuko bora sana zenye minazi ukingoni na miamba ya matumbawe imejaa kotekote kwenye pwani. Kusini mwa nchi hiyo mna ghuba kubwa yenye maji yaliyozingirwa—mahali pafaapo zaidi kwa jiji layo kuu, Maputo.

Hata hivyo, uzuri na utulivu wa nchi hiyo, hufichwa na ile jeuri ya historia yayo. Kwa karne kadhaa ilipambana chini ya utawala wa kigeni, kwanza Waarabu na kisha Wareno. Hao wa pili walikuja wakiwa na ruhusa kamili ya Kanisa la Katoliki ya kupora nchi hiyo ili kupata hazina zayo—pembe za ndovu, dhahabu, na watumwa. Hatimaye, baada ya karne kadhaa za uonevu wa kikoloni, pambano kali ndani ya nchi hiyo lilitokea lililoongoza kwenye uhuru katika 1975. Kwa kusikitisha, badiliko hilo halikufanya maisha yawe na usalama zaidi, kwani nchi hiyo ikaanza kuhusika katika vita vya wenyewe kwa wenyewe, ikitokeza kuteseka kwingi kwa watu, hasa kwa wakazi wa mashambani wasio na hatia.

Maputo, Jiji Kuu

Katika mwongo uliopita, maelfu ya Wasumbiji wametoroka kwenda kwenye ule usalama wa kadiri wa miji na majiji. Hilo laonekana hasa katika Maputo, ambapo mchanganyiko wa ustadi wa ujenzi wa Kireno wa zamani wenye kupendeza na Afrika yenye rangi-rangi hulipa jiji hilo hali ya msisimuko. Kutembea leo kwenye zile barabara za Maputo zilizo pana, zenye miti kila pande, jambo la kwanza utakaloona ni yale makutano ya watu wakienda huku na huku kutimiza shughuli zao za kila siku. Lakini kuna tofauti moja. “Ujapokuwa msongamano huo na ugumu wa maisha ya kila siku, watu wako tayari sikuzote kufanya urafiki,” aonelea Rodrigo, mishonari katika Maputo. “Ni vigumu kupata watu wasio na adabu!” Naam, Wasumbiji wanajulikana kuwa watu wanaojitolea na wenye urafiki.

Bila shaka, kama ilivyo katika sehemu kubwa ya Afrika, mahali pa kawaida pa kukutana na watu ni kwenye soko la mahali hapo. Ili kufika hapo unaweza kusafiri kwa Chapa 100, jina la huko la (matatu) yale magari ya pikapu yanayotumiwa kwa usafirishaji wa umma. Kama kawaida, watu wengi zaidi huonekana wakining’inia wakiwa nje ya gari hilo kuliko wale walio ndani. Labda ni bora zaidi kutembea.

Wasumbiji ni wafanya biashara wastadi wasioweza kubadilika kwa urahisi. Ni lazima mtu anayetembelea Maputo aone ni wangapi wanaojiajiri wenyewe kazi kwa kujenga vibanda vidogo kando-kando ya barabara na kwenye pembe za barabara. Je! ungependa kununua matunda, mboga, mimea, au viungo vilivyotoka shambani hivi karibuni? Ni vingi vya kutosha wote. Namna gani kuku aliye hai, korosho, au matete ambayo kwayo waweza kujenga nyumba yako? Hakuna jambo lolote linalotatiza sana, na kila jambo linafanywa katika roho yenye urafiki. Utumishi mbalimbali kama vile kung’arishiwa viatu vyako au kuoshewa gari lako unapatikana pia. Kwa kutumia ufito wa chuma ulio moto na shiti ya plastiki, mvulana mchanga ataweza hata kuunganisha hati zako zenye thamani katika tabaka nyembamba.

Kwa kweli, si biashara zote za barabarani ni halali kikamili. Hata hivyo zinafanywa. Wachuuzi haramu huitwa dumba nenge, linalomaanisha “tegemea miguu yako.” Hilo bila shaka ni kwa sababu wenye mamlaka wanapokuja kufanya uchunguzi, uwezo wa kupiga mbio kwa kasi ni wa muhimu kwa ajili ya wokovu wa biashara yao isiyo yenye usalama.

Kupitia harufu, ni lazima tunakaribia soko la samaki! Katika saa za baadaye za alasiri, kotekote ufukoni mwa Costa Do Sol, utendaji mwingi huzunguka mashua ya kuvulia samaki zinapoleta mivuo yao ya siku. Pamoja na samaki wa namna na ukubwa wote kuna kaa, kamba wa bahari, na, bila shaka, maduvi wa Msumbiji wanaojulikana sana. Hata hivyo, huenda ukapendezwa na aina nyingine ya kuvua samaki inayofanywa katika na karibu na Maputo.

“Wavuvi wa Watu”

Tangu walipopata utambuzi wa kisheria katika Msumbiji, Mashahidi wa Yehova wamepokea itikio mzuri kutoka kwa watu. Mtu mmoja alionyesha uthamini wake kwa kusema hivi: “Katika London mimi nimeona wengi wenu barabarani. Kwa kweli, mahali popote ambapo nimetembelea, nimewaona Mashahidi wa Yehova. Sasa kunanifanya nihisi vizuri kuwaona huku pia.”

Ikiwa kukubali kwao Biblia na vichapo vyenye msingi wa Biblia ni ishara ya jambo lolote, basi kwa kweli watu hawa wana mwelekeo wa kiroho. Paula, mishonari mwingine, huripoti kwamba katika asubuhi ya Jumamosi ya wastani, yawezekana sana kuangusha magazeti zaidi ya 50 kwenye soko kuu. Kile kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi kinathibitika kuwa chenye kupendwa sana. Vijana wengi wamepoteza makao yao au kufiwa na wazazi wao wakati wa vita, na yaonekana wanathamini zile kanuni na mwelekezo ambao kitabu hicho huandaa.

Katika njia ya kawaida ya Kiafrika isiyozuilika, vikundi vikubwa vya watu wenye kupendezwa watamzunguka mishonari ili kusikia lile linalosemwa. Vikusanyiko hivyo vya kando-kando ya barabara mara nyingi husitawika kuwa mazungumzo machangamfu ya Kimaandiko. Dada mmoja hukumbuka ono lenye kusisimua.

“Nilipokuwa nikitoa ushahidi wa barabarani pindi moja, nilishtuka kwa hofu wakati gari moja la jeshi aina ya jipu lilipopiga breki kwa mkwaruzo kutua karibu na mimi. Askari-jeshi mchanga alipaaza sauti kuelekea watu fulani waliokuwa karibu na hapo: ‘Aisee, nyinyi, mwambieni mwanamke huyo aje hapa.’ Nilipomkaribia, askari-jeshi huyo alitoa tabasamu pana aliposema hivi: ‘Ninyi ni watu wazuri. Tunafurahi kuwaona hapa. Ninadhani unacho kitabu kuhusu vijana. Ningependa kimoja pia.’ Nilijibu kwamba sikuwa na chochote, lakini nilimhakikishia kwamba mara vilipokuwa akibani tena, ningepeleka kimoja nyumbani kwake.”

Kupeleka Vichapo Kwenye Bohari

Ili kutosheleza uhitaji wa vichapo wenye kuongezeka, ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Afrika Kusini hupeleka ugavi wa vichapo kwenye bohari moja katika Maputo kila majuma mawili. Manuel, mishonari mmoja, hushughulikia bohari hilo naye ana daraka la kupanga ugawanyaji wa vichapo.

Asubuhi moja mwanamume mmoja wa makamo aliingia humo polepole na kuuliza mahali hapo palitumiwa kwa kusudi gani. Manuel alijibu kwamba hilo lilikuwa bohari la vichapo vya Biblia. Mwanamume huyo aliondoka, lakini katika dakika moja alirudi.

“Ulisema kwamba hivi ni vitabu vya Biblia, sivyo?” akauliza.

“Naam, ndivyo,” Manuel akajibu.

“Hili ni tengenezo la nini?” mwanamume huyo akauliza.

“Mashahidi wa Yehova,” Manuel akajibu, akiongeza, “Sisi huendelea kupelekea Makundi yetu ya hapa ugavi wa vichapo hivi.”

“Lo, Mashahidi wa Yehova!” Uso wa mwanamume huo ukachangamka. “Kuna mengi sana ninayopenda kuhusu nyinyi watu. Lakini wakati uo huo, kuna jambo fulani nisilopenda kuhusu nyinyi.”

“Basi, ni nini unachopenda kuhusu sisi?” akauliza Manuel kwa busara.

“Ninavipenda vile vitabu vyenye kupendeza na kuelimisha ambavyo mnatokeza,” mwanamume huyo akaeleza. “Lile ambalo sipendi ni kwamba siwezi kamwe kuvipata vya kutosha. Huwezi kuamini jinsi tulivyo na hamu ya kupata vichapo kama vyenu katika Maputo.” Kisha akatoa orodha iliyoandikwa ya vichapo vya Watch Tower Society, kutia na matoleo mengi ya zamani ya magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, aliyokuwa ameyakosa.

“Mimi hubeba orodha hii popote niendapo,” akamwambia Manuel. “Wakati wowote ninapokutana na Mashahidi wa Yehova, mimi hujaribu kupata vichapo vyovyote walivyo navyo. Ikiwa waweza kunisaidia nipate kilichomo katika orodha yangu, nina nia ya kulipa bei ya juu sana.”

Mazungumzo yakafuata. Manuel akapata kujua kwamba mwanamume huyo alikutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza katika miaka ya 1950 aliposoma kile kitabu Creation. Lakini tangu kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipopigwa marufuku chini ya serikali ya Ureno, alifanya maendeleo madogo sana.

Baadaye alipomtembelea mwanamume huyo ofisini mwake, Manuel aliona kwamba vichapo vyote vya Watch Tower alivyokuwa navyo vilikuwa vimefunikwa na plastiki na kufailiwa kinadhifu. Manuel aliweza kumpa mwanamume huyo vichapo alivyohitaji ili kukamilisha mkusanyo wake, na akapanga kuongoza funzo la Biblia pamoja na mwanamume huyo na familia yake.

Kupanda na kutia maji kwa kiroho huko kote kunaanza kutokeza matunda mengi Mungu anapoendelea “kukuza.” Kuna ishara thabiti kwamba mavuno ya watu mmoja mmoja wenye mioyo ifaayo yatakuwa na matokeo mengi katika Msumbiji!—1 Wakorintho 3:6; Yohana 4:36.

Maendeleo ya Kitheokrasi Vijapokuwa Vizuizi

Leo, kuna makundi zaidi ya 50 katika na karibu na jiji la Maputo. Hata hivyo, hakuna Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova hata moja linalopatikana. Hiyo ni kwa sababu gani? Kwa sababu ya hali za uchumi zenye umaskini, makundi hayajaweza kujenga hata ingawa mengi yamekuwa na shamba kwa miaka kadhaa.a

Hata hivyo, vizuizi hivyo havipingi maendeleo. Kwa sasa kuna mafunzo ya Biblia nyumbani zaidi ya 5,000 yanayoongozwa katika sehemu ya kusini ya Msumbiji. Wanaotaka kujifunza ni wengi sana hivi kwamba ni lazima mambo ya muhimu yatangulizwe. Ikiwa mtu fulani aomba funzo, inadhaniwa kwamba atahudhuria mikutano yote ya kundi.

Kundi moja lililomo katika eneo lenye nyumba za vibanda hivi karibuni lilikuwa na watu 189 kwenye mikutano ya Jumapili hata ingawa kuna wahubiri wa habari njema 71 tu. Kikundi hicho kikubwa hukutana nje katika ua wa nyumba moja. Eneo hilo linafichwa lisionwe na watu wote kwa bati na ua wa matete. Kabla ya kila mkutano, eneo hilo hufagiliwa liwe safi, na sehemu kubwa ya wasikilizaji, kutia na watu wazima wengi, huketi chini kwenye mikeka ya matete. Wao husikiliza programu kwa makini kama nini! Kwa kuwa wapya wengi hawana nakala ya Mnara wa Mlinzi ambayo kwayo wanaweza kufuatana, wanajifunza kusikiliza kwa makini wakati mafungu yanaposomwa, na mikono mingi huinuliwa kwa kuitikia maswali ambayo kiongozi huuliza.

Kundi jingine lenye wahubiri 59 kwa kawaida huwa na wahudhuriaji zaidi ya 140. Wao kwa kawaida hukutana kwenye varanda ya chini iliyo wazi. Lakini wakati wa mvua, kundi hilo husongamana katika vyumba viwili vya nyumba ndogo. Wasikilizaji wa ziada huanza kujaza ukumbi, jiko, na varanda ya juu. Mara nyingine tena, ni lazima mtu aone uthamini na usikivu wakati kila mtu, kutia na vijana, wanapofuata programu kwa makini.

Uwezekano wa ukuzi wa wakati ujao katika Msumbiji hauonekani zaidi mahali popote pengine kuliko kwenye makusanyiko. Hivi karibuni kusanyiko la mzunguko lilifanywa kwenye uwanja wa michezo wa zamani wa kupigana na fahali katikati ya jiji. Waweza kuwazia mshangao kwa upande wa wale wahubiri 3,000 hivi wakati watu zaidi ya 10,000 walipohudhuria vipindi hivyo?

“Mavuno ni Mengi”

Maono hayo huonyesha kwa wazi kwamba bado kuna kazi nyingi ya kufanywa katika Msumbiji. Makundi mengine yamepokea hivi karibuni tu ziara yao ya kwanza ya mwangalizi asafiriye aliyetumwa na ofisi ya tawi. Wanapokea msaada unaohitajiwa sana kuwasaidia wafuate taratibu za kitengenezo zifaazo katika makundi.

Makundi huthamini sana pia wale wamishonari wa Gileadi waliowasili hivi karibuni. Fransisko, mzee katika Maputo, huonelea hivi: “Kwetu hiyo ni hatua kubwa kuelekea mbele. Tulikuwa na bidii. Tulikuwa na upendo. Hata hivyo, hatukuwa na habari ya karibuni kuhusu mambo ya kitengenezo. Tunachohitaji kwa kweli ni mtu mwenye ujuzi ulio bora kabisa atufundishe jinsi mambo yanavyopaswa kufanywa. Sasa, tunafurahi sana kuwa na wamishonari pamoja na sisi.”

Kwa upande wao, wamishonari hufurahi kuwatumikia ndugu zao. Hans, ambaye hivi karibuni alipewa mgawo kwenda Msumbiji baada ya kutumikia miaka 20 katika Brazili, hujumlisha mambo hivi: “Kufanya kazi katika shamba la Msumbiji ni pendeleo kubwa! Twahisi kwamba tunakaribia sana ongezeko kubwa mno huku. Kuna kazi nyingi sana ya kufanya. Tungeweza kufaidika na wamishonari wengine 10 au 20 katika Maputo tu.”

Utendaji wa kitheokrasi unaoongezeka katika Msumbiji humkumbusha mtu juu ya maneno haya ya Yesu ya hima: “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.” (Mathayo 9:37, 38) Kuna kila sababu kuamini kwamba Yehova atajibu sihi hiyo ya hima kwa ajili ya watumishi wake katika Msumbiji.

Maelfu ya Mashahidi wa Yehova walitumia miaka 12 au zaidi katika vituo vya wafungwa katika kaskazini-magharibi mwa Msumbiji. Wakati baadhi yao waliporudi Maputo hivi karibuni, kitu cha kimwili walichokuwa nacho tu kilikuwa kipande cha nguo cha kujifungia kwenye viuno vyao. Walichokuwa nacho kwa wingi ni imani! Michango mingi ya chakula na nguo kutoka kwa Mashahidi wenzao katika nchi za karibu iliwasaidia waanze maisha upya.

[Maelezo ya Chini]

a Mtu akijaliwa vya kutosha kupata kazi huko, mshahara wa wastani ni kutoka dola 20 hadi dola 30 kwa mwezi.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Makundi hufurahia kuona wengi wakitoka Jumamosi asubuhi kwa ajili ya utoaji ushahidi wa Kikristo

[Picha katika ukurasa wa 24]

Huyo ni Jaimito mwenye umri wa miaka 5. Alizaliwa katika kambi ya wafungwa. Leo, wazazi wa Jaimito hufurahi kuwa wamerudi Maputo. Kila juma Fransisko, Baba ya Jaimito, hukusanya familia nzima kwa ajili ya funzo la Biblia. Wazazi wote wawili hutumia wakati mwingi wakifunza watoto wao kuwa walimu wenye matokeo katika utumishi wa shambani. Jaimito hufurahia kuangusha vichapo kwenye soko kuu

[Picha katika ukurasa wa 25]

Jambo la kwamba makundi hayana Majumba ya Ufalme yawezayo kutumia halizuii maendeleo yayo. Katika visa vingi, zaidi ya maradufu ya idadi ya wahubiri huhudhuria mikutano

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki