Askofu Mkuu Hawezi Kukabiliana na Hilo!
MWAKA jana, baraza la kitawa la makardinali lilipangwa ili kuzungumzia mambo fulani yanayohangaisha sana Kanisa la Katoliki. Mojawapo ya hayo, kulingana na gazeti la habari Il Sabato, ni “kule kuongezeka sana kwa mafarakano.” Hata hivyo, gazeti hilo la habari lilisema hivi: “Halipaswi kuwa tatizo kwa makardinali kufikia mapatano katika jambo hilo. Wote huafikiana kwamba kuna uhitaji wa kujifunza kwa kina zaidi juu ya kutokea kwa harakati mpya za kidini na pia uhitaji wa kuzuia, kadiri iwezekanavyo, upanuzi wazo.”
Hata hivyo, ni wazi kwamba “kule kuongezeka sana kwa mafarakano” si tatizo lililoko Italia tu. Il Sabato huripoti hivi: “Alipokuwa akizuru Vatikani hivi karibuni, Askofu Mkuu Kirill wa Smolensk [mojawapo ya miji ya Urusi ya kale zaidi] . . . alimwuliza papa ampe msaada ambao ungeweza kutumiwa ulimwenguni pote ili kukabiliana na ule ukuzi mkubwa sana wa Mashahidi wa Yehova na vikundi kama hivyo katika nchi za Muungano wa Sovieti.”
Katika karne ya kwanza, viongozi wa ile dini madhubuti walikuwa na malalamiko kama hayo wakati Ukristo ulipoenezwa kwa bidii nyingi sana na wafuasi wao. Pindi moja Wayahudi wenye hasira waliwalalamikia watawala wa mji hivi: “Watu hawa walioupindua ulimwengu wamefika huku nako”! (Matendo 17:6) Wakati huo wa nyuma, viongozi wa kidini walijaribu sana kuukomesha mweneo wa Ukristo, lakini walishindwa. Leo pia, jitihada yoyote ya kuukomesha mweneo wa fundisho la Kikristo la kweli itashindwa kabisa. Mungu mwenyewe aahidi hivi: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa BWANA [Yehova, NW], na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema BWANA [Yehova, NW].”—Isaya 54:17.