Kung’aa Kama Vimulikaji Katika Ulimwengu
KATIKA ulimwengu uliojaa ukaidi na upotovu wa kiadili, Wakristo wa kweli duniani pote wanapaswa wawe vyanzo vya nuru. Wanapaswa wawe vimulikaji katika ulimwengu wenye giza. (Wafilipi 2:15) Maelfu mengi wana nia ya kufanya hivyo wakiwa mapainia, au wahubiri wa wakati wote. Idadi kubwa yao wametumia miaka mingi katika utumishi huu na wamethawabishwa kwa kuona watu wa aina zote wakifanya mabadiliko maishani mwao kuwa wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo.—Mathayo 28:19.
Ili kuwatia moyo hao mapainia waendelee katika utumishi mtakatifu na kufanya maendeleo katika stadi zao za kufundisha, Mashahidi wa Yehova wamepanga kuwe na Shule ya Utumishi wa Upainia. Hiyo ni mtaala wenye msingi wa Biblia wa muda wa siku kumi unaokusudiwa kuwasaidia mapainia katika mambo matatu: kutembea pamoja na Yehova wakiwa wafuasi wa Yesu Kristo; kuongeza upendo wao kwa ajili ya ushirika mzima wa ndugu; kung’aa wakiwa vimulikaji katika ulimwengu.
Shule ya Upainia Katika Jamhuri ya Afrika ya Kati
Katika Bangui, jiji kuu la Jamhuri ya Afrika ya Kati, wanafunzi 48 na wafunzi 2 walikutana pamoja katika Agosti 1991. Hao wanafunzi wangepokea maagizo na madokezo yenye kutumika kwa ajili ya kazi yao. Ni nini kuhusu darasa hilo la Bangui lililosisimua sana?
Kwanza, 21 kati ya wanafunzi hao walikuwa bado wakihudhuria shule ya kilimwengu. Wakiwa shuleni, waliweza kupanga ratiba zao ili kuonea shangwe utumishi wa upainia wa kawaida. Walitumia miezi yao ya likizo, miisho-juma yao isiyo na shughuli nyingi, na nyakati za alasiri ili kuhubiri na kufundisha.
Vijana hao wameona umaana wa kumtumikia Muumba wao sasa. (Mhubiri 12:1; linganisha 1 Wakorintho 7:29.) Jambo lenye kutokeza lilikuwa kwamba 12 kati yao walikuwa na wazazi wasioamini. Nyumbani ni wao pekee waliokuwa katika kweli. Wavulana wawili wachanga, ambao ni ndugu wa kimnofu, walilazimishwa na baba yao waondoke nyumbani kwa sababu ya imani yao. Wenzi wa ndoa wachanga katika kundi waliwakaribisha wavulana hao waishi pamoja nao.
Hali ilikuwa tofauti kwa Michée na Sulamithe Kaleb. Wote wawili ni mapainia nao huenda shuleni pia, lakini wazazi wao ni Mashahidi wa Yehova. Kwa kweli, baba yao alikuwa mwanafunzi katika darasa ilo hilo la Shule ya Upainia!
Makundi katika Bangui yalishiriki katika shule hiyo pia, lakini katika njia tofauti. Walishughulikia mahitaji ya kimwili, kama vile chakula. Pesa, pamoja na kuku, sukari, mchele, na mihogo ilichangwa ili kulisha darasa hilo.
Vikundi vya wapishi vilipangwa na makundi ya karibu ili kutayarisha milo sahili lakini mitamu. Jamhuri ya Afrika ya Kati hujulikana kwa mlo wayo uitwao ngunza, mlo ambao kila mtu huthamini. Unapikwaje? Majani ya muhogo, mawese, vitunguu, na vitunguu saumu vingi, kiasi kikubwa cha siagi ya njugu, na saburi ili mlo huo uweze kuiva vizuri. Kila kikundi kilikuwa na njia yacho ya pekee ya kuutayarisha. Upishi huo ulifaulu sana. Hakuna mtu ambaye angeweza kukataa kula chakula hicho kitamu.
Nje ya Bangui madarasa mengine mawili yalifanywa, moja katika Bouar na jingine katika Bambari, hesabu ya wanafunzi wote ikijumlika kuwa 68. Katika miaka miwili iliyopita, Jamhuri ya Afrika ya Kati imeona ongezeko katika idadi ya mapainia. Katika Januari 1992 kulikuwako mapainia wa kawaida 149 na mapainia wa pekee 17 pamoja na mapainia wasaidizi 78. Hiyo imetokeza ongezeko la utendaji katika nchi nzima kukiwa na vilele vipya katika wahubiri, saa, ziara za kurudia, na mafunzo ya Biblia. Kunapokuwa wafanya kazi wengi zaidi, mavuno huongezeka.—Isaya 60:21, 22; Mathayo 9:37, 38.
Shukrani zetu zamwendea Yehova Mungu kwa ajili ya maandalizi hayo na kwa tengenezo lake la kidunia kwa ajili ya kupangia madarasa hayo. Yanawasaidia wanafunzi na wafunzi pia wang’ae wakiwa vimulikaji katika ulimwengu huu wenye giza.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Wanafunzi wa shule ya upainia 21 walio katika shule ya upili
[Picha katika ukurasa wa 25]
Wavulana hawa wawili walilazimika kuondoka nyumbani kwa sababu ya kweli