Ubatizo “Ndani ya Jina la”
UCHUNGUZI wa yale maelfu ya hati za mafunjo za kilimwengu za kale zilizopatikana katika michanga ya Misri mwanzoni mwa karne hii mara nyingi huyaelewesha wazi Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Jinsi gani? Kwa kuchunguza njia ambayo maneno fulani yalitumiwa, tunaongozwa kwenye uelewevu sahihi zaidi wa maneno ayo hayo katika mazingira yayo ya Kimaandiko.
Mfano mmoja ni ule utumizi wa Yesu wa maneno “katika jina la” alipowaamuru wanafunzi wake hivi kabla ya kupaa kwake mbinguni: “Enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa [katika, NW] jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].” Yesu alimaanisha nini?—Mathayo 28:19.
Wanachuo wamegundua kwamba katika maandishi ya kilimwengu maneno “katika jina la,” au “ndani ya jina la” (Kingdom Interlinear), hutumiwa kwa kurejezea malipo “katika hesabu ya akiba ya mtu yeyote.” Profesa wa theolojia Dakt. G. Adolf Diessmann aliamini kwamba kulingana na uthibitisho unaotokana na mafunjo, “wazo la msingi . . . la maneno kubatiza ndani ya jina la Bwana, au kubatiza ndani ya jina la Mwana wa Mungu, ni kwamba ubatizo au imani humaanisha kuwa mali ya Mungu au ya Mwana wa Mungu.”—Italiki za Deissmann.
Jambo la kupendeza ni kwamba, maneno ayo hayo yalitumiwa na Wayahudi wa siku ya Yesu, kama inavyoelezwa katika Theological Dictionary of the New Testament: “Kutahiriwa kwa mwongofu hufanywa . . . ‘katika jina la mwongofu huyo,’ ili kumpokea ndani ya Dini ya Kiyahudi. Kutahiriwa huko hutukia . . . ‘katika jina la agano,’ ili kumpokea ndani ya agano.” Hivyo uhusiano huanzishwa na mtu huyo asiye Myahudi anayekuwa mwongofu chini ya mamlaka ya agano.
Kwa hiyo kwa Mkristo, ubatizo baada ya kujiweka wakfu huanzisha uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova Mungu, Mwana wake Yesu Kristo, na roho takatifu. Mwongofu atambua mamlaka zao mmoja mmoja katika njia yake mpya ya maisha. Fikiria jinsi hilo lilivyo kweli kwa kila mmoja wa wale wanaotajwa.
Kwa kutambua mamlaka ya Mungu, tunamkaribia na kuingia ndani ya uhusiano pamoja na yeye. (Waebrania 12:9; Yakobo 4:7, 8) Tunakuwa mali ya Mungu tukiwa watumwa wake, walionunuliwa kwa bei ya dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (1 Wakorintho 3:23; 6:20) Mtume Paulo pia aliwaambia Wakristo wa karne ya kwanza kwamba walikuwa mali ya Yesu Kristo, si mali ya wanaume wowote ambao huenda ikawa walikuwa wamewaletea kweli. (1 Wakorintho 1:12, 13; 7:23; linganisha Mathayo 16:24.) Ubatizo katika jina la Mwana hudokeza kutambua jambo hilo la hakika, kumkubali Yesu kuwa ndiye “njia, na kweli, na uzima.”—Yohana 14:6.
Roho takatifu ni ya muhimu pia kwa uhusiano wetu ufaao pamoja na Yehova na Yesu Kristo. Kubatizwa katika jina la roho takatifu huonyesha kwamba tunatambua daraka la roho katika shughuli za Mungu pamoja na sisi. Twaelekea kufuata mwongozo wayo, si kuipuuza, au kutenda kinyume chayo, kwa kuzuia kazi yayo kupitia sisi. (Waefeso 4:30; 1 Wathesalonike 5:19) Hali ya roho ya kutokuwa na utu haisababishi ugumu wowote kwa habari ya utumizi au maana, sawa na vile utumizi wa “katika jina la agano” usivyosababisha ugumu katika Dini ya Kiyahudi.
Kwa hiyo, wakati wa kujiweka wakfu na kubatizwa, twahitaji kufikiria kwa njia ya sala lile linalotiwa ndani ya uhusiano wetu mpya. Uhusiano huo kama ulivyoonyeshwa katika kielelezo na uandalizi wa fidia ya Yesu Kristo, wahitaji ujitiisho kwa mapenzi ya Mungu yanayopaswa kutimizwa kupitia roho takatifu inapowaelekeza watumishi wa Mungu wote katika upendo na umoja ulimwenguni pote.