Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 11/1 kur. 20-23
  • Ubatizo—Takwa la Kikristo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ubatizo—Takwa la Kikristo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAANA YAKE YABADILIKA
  • NI WA MAANA KADIRI GANI?
  • NI MWANZO TU
  • Maana ya Ubatizo Wako
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Ubatizo
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Kwa Nini Ubatizwe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Ubatizo​—Takwa kwa Wakristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 11/1 kur. 20-23

Ubatizo​—⁠Takwa la Kikristo

UBATIZO umekuwa sehemu ya Ukristo tangu ulipoanza. Ubatizo ni wonyesho wa nini? Je! ni jambo la maana namna gani kwamba watu wabatizwe? Ebu na tuchunguze habari fulani ya msingi juu ya ubatizo na unachofananisha kulingana na maoni ya Biblia Takatifu.

Maandiko yanaonyesha kwamba njia ya kubatiza iliyo sahihi ni kuzamishwa kabisa. Neno “kubatiza” linatokana na neno la Kigiriki baptizein, linalomaanisha “kuchovya, kutumbukiza.” Wakati mtu anapozamishwa katika maji, mtu anazikwa kwa muda asionekane kisha anainuliwa kutoka katika maji.

Mtajo wa kwanza wa ubatizo katika Biblia unahusu utendaji wa Yohana Mbatizaji. Katika mwaka 29 W.K., Mungu alimpa Yohana ruhusa ya kubatiza. Maandiko yanataja kwamba Yohana alifika “nchi yote iliyo karibu na Yordani, akihubiri ubatizo wa toba liletalo ondoleo la dhambi.”​​—⁠Luka 3:1-3.

Kuingia ndani ya maji na kutoka kulionyesha kwamba mtu alikuwa ametubu kwa unyofu wa moyo, au alisikitikia kuvunja sheria ya Mungu iliyotolewa kupitia kwa Musa. Ndiyo kusema, mtu alikuwa akifia mwendo huo na kuwa hai katika jitihada mpya za kuitii Sheria hiyo. Kwa kuwa sheria ya Musa ilikuwa na kusudi la kuwa “kiongozi kutuleta kwa Kristo,” ubatizo wa Yohana ulikuwa hatua ya maana katika kuwatayarisha Waisraeli wampokee Masihi aliyeahidiwa.​​—⁠Luka 1:16, 17; 3:4-6; Gal. 3:24.

Yesu mwenyewe alikubali kubatizwa na Yohana. Wakati wa tukio hilo roho takatifu ya Mungu ilishuka juu ya Yesu, ikimtia mafuta kuwa Masihi aliyeahidiwa. (Marko 1:9-11) Ijapokuwa hakuwa mtenda dhambi aliyehitaji kutubu, Yesu alianza mwendo mpya wa maisha wakati huo. (1 Pet. 2:22) Baada ya tukio hilo alipaswa kufanya “mapenzi” ya pekee ya Baba yake ambayo yangetia ndani kutoa uhai wake kama dhabihu ya ukombozi kwa ajili ya dhambi za wanadamu.​​—⁠Zab. 40:6-8; Ebr. 10:5-10.

Yesu hakuukomesha utendaji wa kubatiza watu wa Yohana Mbatizaji. Kwa kweli, twasoma kwamba mwanzoni katika huduma yake, Yesu alikuwa “anafanya wanafunzi wengi kuliko Yohana, na kuwabatiza, (lakini Yesu mwenyewe hakubatiza, bali wanafunzi wake.)” (Yohana 4:1, 2) Ubatizo huu ulioongozwa na Yesu ulikuwa kama wonyesho wa toba kwa namna ile ya ubatizo wa Yohana.

MAANA YAKE YABADILIKA

Baada ya kifo cha Yesu, kufufuliwa na kupaa kwake mbinguni, sheria ya Musa ilifikia mwisho wake. (Rum. 10:4; Efe. 2:15) Je! hiyo iliondoa uhitaji wa ubatizo? Sivyo, walakini sasa, kwa Wayahudi, ulikuwa wonyesho wa kujitoa kwao kwa Yehova Mungu kwa msingi wa dhabihu yenye kufunika dhambi ya Yesu Masihi. Hata hivyo, upesi kabla Yesu hajapaa mbinguni, aliwapa wanafunzi wake amri hii: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu. Kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”​​—⁠Mt. 28:19, 20, NW.

Je! umeona kwamba sasa ubatizo haungepasa Wayahudi peke yao bali hata na “watu wa mataifa yote”? Wakati wa maisha yake ya kidunia Yesu alitabiri kwamba kibali ya pekee ya Mungu kwa Wayahudi ingekoma. (Mt. 8:11, 12; 21:43) Jambo hilo lilitimia katika mwaka 36 W.K. wakati Mungu alipomwongoza mtume Petro aingie katika nyumba ya Kornelio, mtu asiye Myahudi, na kutangaza ujumbe wa Kikristo kwake na kwa watu wa jamaa yake. Baada ya tukio hilo Mataifa walikubali kweli juu ya Yesu Kristo, walipokea karama za kimwujiza za roho takatifu na kubatizwa.​​—⁠Matendo 10:1-48.

Kwa kuwa sasa Mungu hakuwa akishughulika na taifa fulani la watu waliowekwa wakf kipekee tangu kuzaliwa, kuanzia wakati huo na kuendelea ubatizo ukawa wonyesho unaofaa wa kujitoa kwa moyo kwa Mungu. Kuingia chini ya maji kungeonyesha kwamba mtu alikuwa akifia mwendo wake wa maisha wa kujipendeza yeye mwenyewe. Kuinuliwa kutoka katika maji kungeonyesha kuwa hai kwa kutanguliza mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa. (Linganisha Mathayo 6:33; Wafilipi 1:10) Yesu alionyesha hili kuwa takwa aliposema hivi: “Ikiwa ye yote anataka anifuate mimi, mwacheni ajikane mwenyewe na kuchukua mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote.”​​—⁠Mt. 16:24, NW.

Ni nini sababu ya kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu”? (Mt. 28:19, NW) Twaweza kufahamu hili vizuri zaidi kwa kufikiria maneno ya Yesu kama yalivyoandikwa katika Mathayo 10:41: “Yeye ambaye humpokea nabii katika jina la nabii atapata thawabu ya nabii; na yeye ambaye humpokea mtu mwenye haki katika jina la mtu mwenye haki atapokea thawabu ya mtu mwenye haki.” (Authorized Version; Rotherham) Hii ina maana ya kumpokea nabii au mtu mwenye haki kwa kukubali vile alivyo. Wanaotaka ubatizo wa Kikristo lazima wakubali Baba, Mwana kama walivyo na roho takatifu vilevile: Baba kuwa ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote aliye Mkuu kupita wote; Mwana kuwa ndiye mkombozi na mfalme; nayo roho takatifu kuwa nguvu ya utendaji ya Mungu ambayo husaidia watu wafanye mapenzi ya kimungu.​​—⁠Zab. 83:18; Mt. 20:28; Ufu. 19:16; Yohana 14:16, 17.

NI WA MAANA KADIRI GANI?

Ni jambo la maana kadiri gani kwamba watu wakubali ubatizo wa Kikristo? Fikiria shauri la mtume Petro wakati wa Pentekoste ya 33 W.K., alilolitoa kwa Wayahudi walioshiriki daraka la kijamii la kufanya dhambi ya kumtundika Masihi au Kristo katika mti, na ambao walihitaji kusafishwa kutokana na dhambi hiyo: “Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha [roho takatifu].” (Matendo 2:38) Kulingana na Maandiko, watu ambao wanataka msamaha wa dhambi kupitia kwa Yesu Kristo lazima watubu na kubatizwa.

Je! hii inamaanisha kwamba maji ya ubatizo yanasafisha dhambi? Ingekuwa makosa kukata maneno hivyo. Anapotoa maelezo juu ya gharika ya siku za Nuhu, Petro anaonyesha maana kubwa zaidi ya ubatizo, akisema hivi: “Lile linalolingana na hili [kule kupitia ndani ya maji ya Gharika kwa watu wanane wakiwa ndani ya safina] pia linaokoa ninyi sasa, yaani, ubatizo, (si kuondolewa kwa uchafu wa mwili, bali ombi linalofanywa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema,) kupitia kwa ufufuo wa Yesu Kristo.”​​—⁠1 Pet. 3:21, NW.

Kwa hiyo kujiweka kwetu wakf kwa Mungu kupitia kwa Kristo kunafanyiza “ombi linalofanywa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema.” Sisi wenyewe katika hali yetu ya kutokamilika yenye dhambi, hatukubaliki kwa Mungu. Kwa hiyo, kwa sababu tunatubu dhambi na kugeuka na kujiweka wakf, Yehova anatumia damu ya dhabihu yenye kufunika dhambi ya Kristo kwetu, hivyo anatuondolea laana ya dhambi na kutupa dhamiri njema kwake. Kwa hiyo, kuingia katika maji ya ubatizo kwa kutii kunaonyesha kujiweka wakf kwetu kwa Yehova Mungu kupitia kwa Yesu Kristo.

Je! hiyo inamaanisha kwamba baada ya ubatizo mtu hapaswi kujiona tena kuwa mkosaji? Sivyo hata kidogo. Hata Paulo, Mkristo aliyebatizwa na tena aliyekuwa mtume wa Yesu Kristo, alisikitika hivi: “Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi.” (Rum. 7:25) Kwa hiyo, Wakristo hawapaswi kujiona kulemewa na maono ya moyoni yenye hatia kwa sababu ya mwendo wao wa maisha uliopita na hali yenye dhambi iliyorithiwa.

NI MWANZO TU

Je! watu wanapaswa kuuona ubatizo wao kuwa ushuhuda wa kwamba wamekwisha “kufaulu” na wako tayari kupata uzima wa milele? Hilo lisingekuwa jambo la hekima, kwa sababu Biblia inauonyesha ubatizo kuwa mwanzo tu wa utumishi mtakatifu wa mtu wa kujitoa kabisa kwa Mungu. Kumbuka kwamba, ubatizo wa Yesu ulitukia mwanzoni mwa utumishi wake wa Kimasihi. Hata na kwa mitume wake na wanafunzi wengine wa kwanza ulikuwa hatua ya kwanza. Je! uliona usemi wa mtume Petro kwamba ubatizo ‘pia unaokoa ninyi sasa?’ (1 Pet. 3:21, NW) Kitabu cha maelezo ya Biblia cha G. F. C. Fronmüller kinasema hivi: ‘Namna ya kiarifa cha tendo la wakati uliopo cha neno la Kigiriki linalomaanisha “kuokoa” kinatumiwa kwa sababu kuokoa huku kumeanza hivi sasa tu na bado si kamili.’​​—⁠Mt. 10:22; Rum. 13:11; Flp. 2:12; Ufu. 2:10.

Maneno ya mtume Paulo yanayofuata yanaonyesha kwamba mengi yanahitajiwa ili kupata wokovu zaidi ya kubatizwa tu: “Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu.” (Rum. 10:9, 10) Ni wazi kutokana na hili kwamba licha ya imani na ubatizo, ‘kukiri’ kwamba Yesu Kristo ni Bwana na kwamba Mungu alimfufua kutoka kwa wafu ni takwa la wokovu.

Ingawa tangazo hili la hadharani hufanywa wakati wa kubatizwa kwa mtu, hii haimaanishi kwamba baada ya hapo hakuna uhitaji wa kuendelea kutangaza kwa wengine tumaini la mtu. Tofauti na hilo, Biblia inaonyesha kwamba lazima tuendelee kutangaza hivyo kwenye mikutano ya kundi, mbele ya mamlaka ya kiserikali au mamlaka ya mahakmani ambayo huenda wakadai kupata sababu ya tumaini letu la Kikristo, na katika kutangaza mbele ya watu wote “habari njema” za ufalme wa Mungu.​—⁠Ebr. 10:23; 1 Pet. 3:15; Mt. 24:14.

Ni wazi kwamba, kwa wote wanaotaka kupata msimamo wenye kukubaliwa na Mungu, ubatizo wa Kikristo ni takwa la lazima. Kwa sababu ya yale unayofananisha, ubatizo haupaswi kuchukuliwa vivi hivi tu au mtu kubatizwa kabla ya kujitayarisha mapema. Je’ unafikiria kubatizwa karibuni? Ikiwa ndivyo, fikiria kwa uzito maana yake. Uwe na nia ya kuishi milele kulingana na kujiweka kwako wakf kwa Mungu kunakofananishwa na ubatizo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki