Kweli Yaenea Katika Kijiji Chenye Maji Mengi
NI AJABU kama nini! Nchi inayojulikana kwa ajili ya maji yayo mengi yapatikana kuwa yenye kiu! Eneo lenye maji mengi lapatikana kuwa kavu na lenye ukame! Ni kiu kiwezacho tu kuzimwa na maji ya kweli kutoka Neno la Mungu, Biblia. Ni hadithi ya Rahbeh, kijiji kidogo chenye wakazi 2,200, kilichomo kati ya milima kaskazini mwa Lebanoni, karibu kilometa 130 kutoka Beirut.
Jina Rahbeh humaanisha katika Kiarabu “mahali penye nafasi kubwa,” nalo latokana na shina la lugha ya Kisemiti linalomaanisha “pana, -enye kuenea.” Kwa kufaa, kijiji hicho kimeenea juu ya vilima vikubwa viwili karibu meta 600 juu ya usawa wa bahari. Wakati wa kipupwe na masika, theluji yaweza kuonekana juu ya milima iliyoko mashariki, ikiongeza fahari kidogo. Lakini, zaidi ya hayo yote, Rahbeh ni kijiji chenye maji mengi. Katika eneo hilo, kuna chemchemi kubwa na ndogo 360, zikiandaa maji yenye thamani kubwa kwa mashamba yenye rutuba ya ngano, aprikoti, pea, mafyulisi, na zabibu katika mabonde ya karibu.
Ya Zamani na Ya Kisasa Yakutana Katika Rahbeh
Katika njia nyingi mambo katika Rahbeh yamebaki vilevile tangu nyakati za Biblia. Nyumba katika kijiji hicho ziko karibu-karibu. Barabara ni nyembamba, zenye kupindapinda, na zenye—punda na ng’ombe wengi. Ingawa kuna motokaa, wanyama ndio walio na haki ya kupita barabara huku. Mara nyingi wenyeji wao huwawekea mizigo kutoka mashambani na kuwatuma nyumbani wakiwa peke yao. Wao hufuata barabara hizo nyembamba, wakikabiliana na hali ngumu, na kurudi nyumbani mwao. Je! hilo lafanana na lile ambalo Isaya alikuwa akifikiria aliposema: “Ng’ombe amjua bwana wake, na punda ajua kibanda cha bwana wake”?—Isaya 1:3.
Rahbeh pia ni mahali penye hali tofauti-tofauti. Huku utapata wahitimu wa chuo kikuu pamoja na wakulima wa kawaida ambao hawajapata kwenda kwenye jiji kubwa. Kuna nyumba kubwa zenye bustani, na kuna vibanda vidogo vyenye mifugo ikikimbia huku na huku. Vifaa vya umeme hupatikana katika karibu kila nyumba, lakini umeme haupatikani sikuzote. Kwa sababu hiyo, nyumba nyingi zina jenereta (mitambo ya umeme). Barabara kuu za kijiji hicho ni za lami, ingawa vijia vingi vinavyoongoza kwenye mashamba si vya lami na ni vya mawe-mawe. Hivyo, njia ya pekee ya kusafirisha mazao ya mashamba ni kwa kutumia wanyama wa kufugwa. Huenda hata ukaona punda akibeba jenereta ya umeme kuelekea shamba ili itumiwe kuendesha mashine za kulimia, zinazotumiwa pamoja na wanyama wenye kuburuta mizigo shambani.
Vivyo hivyo, maisha katika kijiji hicho hayajabadilika sana. Ukikaa katika kijiji hicho usiku mmoja, huenda ukaamshwa na jogoo wenye kuwika saa nane au saa tisa za usiku. Utaratibu wa kila siku huanza mapema, kwa hiyo usishangae ikiwa unasikia kelele ya watu wakipaziana sauti gizani wanapowatayarisha wanyama. Wakati wa mapambazuko, waweza kuona wana-kijiji, wanyama wao wakibeba mizigo, wakielekea mashambani au sokoni kuuza bidhaa zao.
Siku inapoendelea, wavulana na wasichana wadogo hutoka ili kucheza barabarani na mahali pa umma. Vilio na vicheko vyao huenea kotekote, sawa kabisa na ilivyokuwa katika Yerusalemu ya kale kama ilivyoelezwa na nabii Zekaria: “Hizo njia za mji zitajaa wavulana, na wasichana, wakicheza katika njia zake.” (Zekaria 8:5) Pia utawaona wana-kijiji kuwa wenye urafiki mwingi na wadadisi. Unatazamiwa kuamkua kila mwana-kijiji unayekutana naye, kwani wanataka kujua wewe ni nani, mahali utokapo, kwa nini uko huko, na mahali unapokwenda. Watu hupata kujuana vizuri sana.
Maji ya Kweli Yafika Rahbeh
Katika jumuiya hiyo yenye ukaribu sana, habari huenea upesi. Hilo ndilo lililotukia wakati Asaad Younis aliporudi Rahbeh kutoka United States katika 1923. Akitaka kujua ikiwa Asaad alikuwa amekuwa tajiri katika Amerika, rafiki yake Abdallah Blal alienda kumwona. Badala ya kuongea juu ya pesa, Asaad walimpa nakala ya kitabu The Harp of God akamwambia hivi: “Huu ndio utajiri wa kweli.” Abdallah, aliyekuwa Mprotestanti zamani, alisoma kichapo hicho chenye msingi wa Biblia akavutiwa sana. Ingawa Asaad hakufanya mengi kuhusu habari hiyo, Abdallah alisisimuka sana juu ya lile alilokuwa amejifunza akaungama waziwazi kwamba alikuwa amepata kweli.
Wakati fulani baadaye, Abdallah alihamia Tripoli, jiji kubwa kaskazini mwa Lebanoni. Huko, aliweza kuwasiliana na Wanafunzi wa Biblia kadhaa, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo, na yeye akafanya maendeleo zaidi katika mafunzo yake ya Biblia. Baadaye alihamia Rahbeh tena ili kueneza habari njema alizokuwa amejifunza. Alikuwa akiwaingiza wana-kijiji wenzake katika mazungumzo juu ya kichwa kama vile Utatu, kama mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa, moto wa helo, upadri, Misa, na utumizi wa sanamu, akishiriki nao lile ambalo Biblia hufundisha hasa.
Baadhi ya wana-kijiji walionyesha kupendezwa. Watatu au wanne kati yao walijiunga na Abdallah katika kazi ya kuhubiri. Kisha walianza kufanya mikutano ya Jumapili. Hiyo ilitia ndani kusikiliza mahubiri yaliyorekodiwa kutoka kwa rekodiplea au usomaji wa Biblia, uliofuatwa na mazungumzo ya yale waliyotoka kusikia. Baadaye, misaada fulani ya funzo la Biblia ilitumiwa, kutia na vitabu The Harp of God, Riches, na “Let God Be True.” Hudhurio halikuzidi watu kumi, wengi wao wakiwa ni wadadisi zaidi ya kuwa wenye kupendezwa. Wengine walionekana kuwa walikuja hasa ili kupata kile chakula kilichotolewa mwishoni mwa kila mkutano.
Katika miaka ya 1940, Abdallah Blal alipewa daraka la kukitunza kile kikundi katika Rahbeh. Alithibitika kuwa mtumishi wa Yehova mwenye bidii na mwaminifu-mshikamanifu, akiwawekea wengine mfano mwema. Mmoja wao, Ndugu Mattar, akumbuka jinsi walivyofanya kazi yao ya kuhubiri: “Kwa kuwa magari hayakupatikana katika siku hizo, Ndugu Blal na mimi tulikwenda kwa miguu kutoa ushahidi katika vijiji vya karibu. Nilibeba rekodiplea, huku Ndugu Blal akiongoza katika mazungumzo. Kwa kawaida tulikwenda kwa muda wa siku mbili au tatu kabla ya kurudi nyumbani.” Ndugu Blal alimtumikia Yehova kwa uaminifu hadi kifo chake katika 1979 akiwa na umri wa miaka 98.
Maendeleo Yaleta Upinzani
Kazi ilipofanya maendeleo, ndugu walianza kupatwa na upinzani. Katika 1950, kwa uchochezi wa padri wa kijiji hicho, kampeni ya mnyanyaso ilianzishwa dhidi ya ndugu katika Rahbeh. Padri aliwashtaki ndugu juu ya kulichafua kanisa na uhalifu wa vitu vya kidini. Wana-kijiji walighadhabika sana hivi kwamba waliwapiga ndugu kwa mawe, na baadhi ya ndugu wakakamatwa na kufungwa gerezani. Ingawaje, uchunguzi uliofuata ulithibitisha mashtaka hayo kuwa bandia. Hata hivyo, ndugu waliwekwa gerezani kwa siku kadhaa.
Mpinzani mwingine alijaribu kuwafanya wana-kijiji, ambao baadhi yao huenda ikawa hawakuweza kusoma vizuri, watie sahihi karatasi iliyowashtaki ndugu juu ya mambo mengi, yakiwa ni pamoja na kuwasumbua watu kwa kuwatembelea nyumbani mwao kila wakati. Ili apate watu wengi zai-di kutia sahihi karatasi hiyo, aliwaambia kwamba lilikuwa ombi la kwamba mfanya kazi fulani aweze kuhamishwa arudi kijijini. Watu walipopata kujua kwamba kwa kweli lilikuwa shtaka dhidi ya Mashahidi, walifuta sahihi zao. Matukio kama hayo yalisaidia kuwatolea maofisa wengi wa eneo hilo ushahidi mzuri.
Licha ya kushughulikia upinzani huo wa moja kwa moja, ndugu walikabili kizuizi kingine. Katika kijiji kidogo ambako kila mtu amjua kila mtu mwingine, “kuwaogopa wanadamu huleta mtego,” kama vile Biblia huonyesha kwenye Mithali 29:25. Moyo mkuu wahitajiwa ili ndugu wawahubiri majirani, marafiki, na watu wa ukoo, ambao huwachambua na kuwadhihaki daima. Hivyo maneno ya Yesu kwenye Mathayo 10:36 huwa na maana ya kweli: “Adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake.” Hata hivyo, kama vile mithali hiyo inavyoendelea kusema, “amtumainiye BWANA [Yehova, NW] atakuwa salama.” Imani na uvumilivu wa ndugu umekuwa na matokeo ya ajabu.
Kweli Yaenea Katika Rahbeh
Muda wa miaka iliyopita wana-kijiji wamekuja kuuthamini mwenendo mwema wa Mashahidi wa Yehova, na wengi wameikubali kweli. Ndugu walishangilia sana katika 1969 wakati kundi la pili lilipofanyizwa katika Rahbeh. Waliendelea kujitahidi sana. Wengi walianza huduma ya wakati wote, wengine hata walihama wakatumikie katika maeneo mengine, kutia na jiji la Beirut. Yehova alibariki jitihada zao, na kundi la tatu likaanzishwa Rahbeh katika 1983. Wakati uo huo, ndugu wengi zaidi walihamia ugenini au walihama ili wakaishi katika majiji. Bado, ongezeko liliendelea, na kundi la nne likafanyizwa katika Rahbeh katika 1989, kufuatwa na la tano katika 1990.
Kufikia wakati huo karibu kila familia katika kijiji hicho ilikuwa na mtu wa ukoo au rafiki aliyekuwa Shahidi. Uadui uliokuwako wakati mmoja ulikuwa umefifia. Watu walipata kufahamiana zaidi na Mashahidi. Kwa kweli, maneno “mzee,” “painia,” “mwangalizi wa mzunguko,” “kusanyiko,” na “Har–Magedoni” yakawa sehemu ya msamiati wa wana-kijiji. Kwenye pindi za pekee, kama vile ziara ya mwangalizi wa mzunguko au Ukumbusho, barabara zingekuwa tupu na Majumba ya Ufalme kujaa watu pomoni. Makundi mengine hata yaliweka vikuza sauti kwenye roshani ili majirani waweze kusikia kwa urahisi.
Sasa kuna wahubiri wa Ufalme 250 katika Rahbeh. Hiyo inamaanisha kwamba kuna Shahidi 1 kwa karibu watu 8 katika kijiji hicho! Kundi moja la wahubiri 51 lina eneo lenye nyumba 76, na wao hulimaliza kila juma. Ebu wazia lile lililotukia wakati wa miezi ya Machi na Aprili mwaka jana wakati 98 kati ya wale wahubiri 250 walipofanya kazi ya painia msaidizi, pamoja na wale mapainia wa kawaida 13 katika Rahbeh. Eneo hilo lilimalizwa mara nyingi kila juma. Lilikuwa jambo la kawaida kwa nyumba moja kutembelewa na vikundi viwili au vitatu vya wahubiri wawili-wawili kwenye siku iyo hiyo au hata wakati huohuo. Wana-kijiji wengi wamezoea ziara hizo. Lakini mwanamume mmoja alipolalamika, mhubiri mmoja alijibu hivi: “Unapokubali toleo letu la kuwa na funzo la Biblia, ndipo utakapotembelewa mara moja tu kwa juma.” Wao pia huongea na mtu yeyote wanayekutana naye mashambani—watu wanaolima, wanaopanda, wanaotia maji, au ambao wamepanda punda.
Kwa hakika, kweli ya Biblia imeenea katika Rahbeh, kijiji chenye maji mengi. Si hayo tu. Kama vile kijiji cha Rahbeh kimekuwa chanzo cha maji safi kwa vijiji vingi vya karibu, kimeviandalia pia maji ya kweli ya Biblia yenye kutoa uhai. Wahubiri kutoka Rahbeh huwazuru watu katika vijiji vya karibu kwa miguu na kwa vikundi vya magari vilivyopangwa na hufunga safari za kuchukua mchana kutwa kuhubiri katika vijiji vya mbali zaidi. Wahubiri wengine huhama ili kutumikia katika majiji mengine. Kwa baraka ya Yehova, kutakuwako ongezeko zaidi litakaloleta sifa nyingine bado kwa Baba wa kimbingu, Yehova Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Mandhari ya barabara katika Rahbeh