Ona Lile Ambalo Yehova Ametufanyia!
“TULIKUWA tukisali ili kuwa na pindi kama hii,” akasema mwanamume mmoja. Mwingine aliamka kila usiku saa kumi ili asali. Kwa kusudi gani? “Ili kusali kwamba siku moja tuwe na uhuru wa kumwabudu Yehova waziwazi,” akasema. Katika Januari 1992, Mashahidi wa Yehova katika Ethiopia walipokutana pamoja katika Addis Ababa kwa ajili ya “Wapendao Uhuru” Mkusanyiko wa Wilaya wao, ilikuwa wazi kwamba sala hizo za unyenyekevu na weupe wa moyo zilikuwa zimejibiwa.
Mkusanyiko huo wa Ethiopia ulikuwa wonyesho wa jinsi mambo yanavyobadilika katika Afrika. Katika miaka ya hivi karibuni watu wa Yehova katika mabara 13 huko wameshangilia kupokea uhuru wa kisheria ambako walikuwa wamepigwa marufuku au kuzuiwa zamani. Katika Ethiopia, miaka 34 ya kupigwa marufuku rasmi iliisha Novemba 11, 1991, wakati maofisa wa serikali walipotoa utambuzi na kusajiliwa tena kukatukia. Mara hiyo, Mashahidi walifanya mipango ya kufanya mkusanyiko wa kimataifa. Hata hivyo, kuona umati wa 7,573 wakiwa wamekusanyika katika Stediamu ya Jiji la Addis Ababa kulikuwa jambo lililopita mawazio mazuri zaidi ya kila mtu. Tena na tena walikuwa wakiambiana: “Ndugu, ona lile ambalo Yehova Mungu wetu ametufanyia!”—Linganisha Zaburi 66:1-5; 126:1.
Kuwa kwao chini ya marufuku kwa miaka 34 kulitokeza matatizo yasiyotazamiwa. Wengi wao hawakuzifahamu zile nyimbo nzuri za Ufalme. Wangejifunzaje kuziimba kabla ya mkusanyiko? Nyimbo 40, kutia na 17 zilizotumiwa katika programu ya mkusanyiko, zilitafsiriwa katika lugha ya Kiamhariki. Kisha, kikundi cha pekee cha waimbaji kilipangwa ili kurekodi nyimbo hizo katika kaseti. Kila kundi katika jiji kuu lilipokea nakala ya tepu hiyo, na kundi zima lilikuwa linachukua dakika 30 kabla na baada ya mikutano ili kujizoeza nyimbo hizo. Tokeo lilikuwa nini? Stediamu ilijawa na uimbaji wa moyo wote na wenye shangwe wakati wa mkusanyiko.
Kwa sababu ya msukosuko katika sehemu ya mashariki ya nchi hiyo, barabara kuelekea jiji kuu kutoka Diredawa na Harar ilikuwa imefungwa. Njia peke yake ya kusafiri kutoka huko ilikuwa kwa ndege. Wakiwa hawawezi kulipia nauli ya ndege, lakini wakiwa wameazimia kuwako kwenye mkusanyiko, ndugu nane katika Harar walienda kwenye kituo cha kijeshi wakaomba kusafiri katika ndege ya kijeshi. Kwa mshangao wao ombi lao lilikubaliwa. Walisafirishwa bila malipo kwenye mkusanyiko!
Kuona sala zao zikiwa zimejibiwa kulitokeza machozi ya shangwe kwa ndugu hao Waethiopia, ambao kwa miongo mitatu iliyopita walikuwa wamevumilia magumu na minyanyaso na hata walikuwa wamewaona marafiki wao wakiuawa kwa ajili ya imani yao. Mjumbe mmoja alisema hivi: “Nimelia machozi tangu mwanzo wa mkusanyiko.” Mwingine: “Ikiwa mngekuwa na uwezo wa kusoma mioyo, mngeona jinsi nilivyo na furaha.” Naam, Yehova aliwafanyia Mashahidi hao waaminifu jambo zuri ajabu kama nini!—Zaburi 66:16, 19.
Uhuru Mkubwa Zaidi Katika Afrika Magharibi na Kati
Benin ni nchi nyingine ambako kazi ya watu wa Yehova imeandikishwa kisheria hivi karibuni. Mashahidi wahisije juu ya jambo hilo? Msemaji mmoja kwenye kikusanyiko cha Wakristo huko alikiri hivi: “Uhuru wa ibada katika nchi hii kwa kweli ni zawadi kutoka kwa Yehova.” Naam, watumishi wa Yehova huko wanashukuru sana kwamba sasa wanaweza kuonea shangwe uhuru usio na kizuizi wa kukutana pamoja katika ibada na kusema na majirani wao juu ya Ufalme wa Yehova—uhuru mbalimbali ambao wengi wetu huchukua vivi hivi.
Wataonyeshaje shangwe yao? Msemaji aliyenukuliwa juu alionyesha njia moja aliposema hivi: “Kushiriki kwetu katika kazi ya kuhubiri—hasa kwenda kwetu nyumba kwa nyumba tukiwa na habari njema—huonyesha uthamini wetu wa uhuru huo.” Katika Benin imekuwa hivyo kwa hakika. Ukiwa uthibitisho, ebu ona takwimu za mapainia. Katika Januari 1990, mwezi ambao marufuku ya miaka 14 iliondolewa, wahubiri 77 walishiriki katika utumishi wa wakati wote wa kawaida. Miaka miwili baadaye nambari hiyo ilikuwa imeongezeka zaidi ya mara tatu, hadi 244!
Hiyo si kusema kwamba Mashahidi katika Benin hawakuwa wenye kutenda kabla ya marufuku kuondolewa. Kwa kweli, uvumilivu wao ulivuta sana ofisa mmoja wa jeshi aliyekuwa amepewa mgawo kwenye kambi ambako Mashahidi waliletwa walipokamatwa. Kwa kuwa kuazimia kwao kumtumikia Yehova kuliongoza kwenye kukamatwa mara nyingi, karibu daima alijikuta mwenyewe akikutana nao. Lakini hilo lilimkumbusha tu juu ya mazungumzo ya Biblia yenye kufurahisha ambayo alikuwa amekuwa nayo pamoja nao katika siku za mapema zaidi walipokuwa wamefurahia uhuru wa kisheria.
Hatimaye, imani yao yenye nguvu iliamsha hisia ya njaa ya kiroho ndani ya ofisa huyo. Alizuru makanisa na mafarakano tofauti-tofauti lakini hakuweza kamwe kutosheleza njaa hiyo. Ilikuwa tu baada ya marufuku kuondolewa katika Januari 1990 kwamba aliweza kuzungumza juu ya Biblia kwa uhuru pamoja na Mashahidi na kupata jibu la uhitaji wake wa kiroho. Sasa amebatizwa na anatumikia akiwa painia. Katika maana fulani, badiliko lake lakumbusha ndugu katika Benin juu ya lile lililompata Sauli wa Tarso: “Huyo aliyetuudhi hapo kwanza, sasa anaihubiri imani ile aliyoiharibu zamani.”—Wagalatia 1:23.
Katika Desemba 1991, Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingine ya Afrika Magharibi, Naija, walisajiliwa kuwa shirika la kisheria, na vizuizi kwa kazi yao vilikoma. Kulikuwako itikio lenye shangwe huku pia. Tawi la Naijeria, linalotunza Naija, laripoti itikio kwenye mkusanyiko mmoja: “Baada ya hotuba ya msingi kwenye mkusanyiko wa Maradi siku ya Ijumaa, ilitangaziwa ndugu kwamba sasa tunatambuliwa kisheria katika Naija. Walisisimuka sana na kupiga makofi kwa dakika kadhaa. Katika umalizio wa kipindi hicho, ndugu walikuwa wachangamfu sana, wakikumbatiana na kushangilia juu ya habari hiyo njema.” Twaweza kuwazia mandhari hiyo, na twashangilia pamoja nao.
Ndugu wa huko watatumiaje uhuru wao mpya? Dada mmoja painia katika Naija hana shaka juu ya jibu la swali hiyo. Yeye aandika hivi: “Mambo ya hakika yaonyesha kwamba katika eneo letu la Naija, wale watakaotoka katika Babuloni Mkubwa kabla ya mwisho ni wengi sana. Ukiwa uthibitisho wa hilo, nimeweza kuripoti ziara za kurudia 80 hadi 85 kila mwezi na kuongoza mafunzo ya Biblia 13 au 14, ijapokuwa jambo la kwamba nimekabidhi marudio yangu mengi kwa wahubiri wengine.” Dada huyo mwaminifu aongeza hivi: “Kwa sababu ya matatizo yangu ya afya, siwezi nikafanya mengi kadiri nipendavyo katika utumishi wa shambani, lakini kila mtu hufanya kadiri awezavyo.”
Katika Rwanda iliyo katika Afrika ya Kati, hali ya Mashahidi wa Yehova imebadilika kwa kutazamisha pia. Katika Aprili 1992 hati ilitolewa kuonyesha kwamba hatimaye walikuwa tengenezo la kisheria. Hati hiyo ilipokewa juma lile lile la Ukumbusho, na wale wahubiri 1,526 katika Rwanda walisisimuka kuona 6,228 wakihudhuria tukio hilo. Je! ndugu hao wapendwa wataonyesha shangwe na uthamini wao kwa utendaji mwingi zaidi katika kujulisha habari njema? Bila shaka! Katika mwezi uo huo wa Aprili, wahubiri wa kundi walikuwa na wastani wa saa 27.7 katika kazi ya kuhubiri na ziara za kurudia 17, wakiongoza wastani wa mafunzo ya Biblia 2.4. Na karibu asilimia 40 yao walikuwa katika namna fulani ya utumishi wa wakati wote.
Kuandikishwa Kisheria Katika Kusini Mwa Afrika
Chini katika kusini mwa Afrika, pepo mpya za uhuru zilivuma katika nchi mbili zenye uzuri, Msumbiji na Angola. Katika Msumbiji kuandikishwa kisheria kulitolewa katika Februari 1991. Hali ilipokuwa rahisi zaidi huko, Watch Tower Bible and Tract Society ilituma wamishonari katika nchi hiyo, iliyokuwa imeharibiwa sana na vita ya wenyewe kwa wenyewe. Wamishonari walipata udongo wenye rutuba. Fasihi za Biblia—hasa kitabu Maswali Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi—zinatakwa na wengi sana. Mishonari mmoja aripoti aliangusha vitabu 50 kwa wakati usiozidi muda wa saa mbili na nusu.
Watu wenye kupendezwa huitikia upesi. Mishonari mmoja alitembelea anwani moja ambayo Sosaiti ilikuwa imepewa, na kumbe ilikuwa ya mwanamume aliyekuwa jeshini. Mazungumzo mazuri yalifanywa pamoja na mwanamume huyo mwenyewe na watu wawili wa jamaa yake. Kwenye ziara ya kurudia, mazungumzo mengine yenye matokeo yalifanywa pamoja na mwanamume huyo na watu wengine watano. Kisha wakakubali mwaliko kuhudhuria hotuba ya watu wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi—yote hayo katika muda wa siku nne.
Katika Angola Mashahidi wamefurahia uhuru wenye kuongezeka uliokuwa na upeo wao katika kuandikishwa kisheria kwa kazi yao katika Aprili 1992. Wanatumiaje uhuru wao mkubwa zaidi? Wanashiriki katika utumishi wa shambani! Kuna wahubiri karibu 17,000 katika Angola, na wahubiri hao wanaongoza mafunzo ya Biblia karibu 60,000. Hilo ni taraja zuri kama nini la ongezeko la wakati ujao!
Wachanga Washiriki Katika Kutoa Ushahidi
Katika nchi hizo ambako kazi ya kuhubiri imeandikishwa kisheria hivi karibuni, hata wachanga na wale ambao hawajabatizwa bado wanaonyesha uthamini wao kwa utendaji katika huduma. Katika Jamhuri ya Cape Verde, ambako Mashahidi wa Yehova waliandikishwa kisheria katika Novemba 1990, kwenye mkusanyiko mmoja msichana wa miaka 17 alisimama kutoa wonyesho wa peupe wa imani yake. Baada ya ubatizo mgeni mmoja aliona umati ukiwa umemzunguka msichana huyo. Alienda kumpongeza na kuuliza umati huo ulikuwa wa akina nani. “Oh,” akajibu, “hawa ni wanafunzi wangu wa Biblia.” Alikuwa akiongoza mafunzo saba, nao walikuwa hapo wakimpongeza kwa ajili ya ubatizo wake. Alikuwa tayari amepeleka ombi lake la kutumikia akiwa painia msaidizi na alitazamia kustahili hatimaye kuwa painia wa kawaida.
Msichana wa miaka kumi katika Angola aliulizwa ikiwa alikuwa mhubiri. Alijibu: “Ndiyo.” Je! aliongoza mafunzo ya Biblia yoyote? “Bila shaka.” Mangapi? “Saba,” akajibu msichana huyo wa miaka kumi.
Twasoma katika kitabu cha Matendo kwamba wakati mmoja katika karne ya kwanza, “kanisa [kundi, NW] lilipata raha katika Uyahudi wote na Galilaya na Samaria, likajengwa, likiendelea na kuongezeka katika kicho cha Bwana [Yehova, NW], na faraja ya Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].” (Matendo 9:31) Twasali kwamba kwa ndugu zetu katika Afrika, hiki pia kitageuka kuwa kipindi chenye amani. Twashangilia pamoja nao wanapojengwa na twasali kwamba roho ya Yehova iweze kuwa juu yao wanapotumia kwa faida uhuru wao ili kueneza habari njema na kuendelea kuongezeka.
[Ramani katika ukurasa wa 24]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Mabara Ambako Mashahidi wa Yehova Waliandikishwa Kisheria au Vizuizi Juu Yao Vikaondolewa
1. Gambia, Desemba 1989
2. Benin, Januari 1990
3. Jamhuri ya Cape Verde, Novemba 1990
4. Msumbiji, Februari 1991
5. Ghana, Novemba 1991
6. Ethiopia, Novemba 1991
7. Kongo, Novemba 1991
8. Togo, Desemba 1991
9. Naija, Desemba 1991
10. Kenya, Machi 1992
11. Chad, Januari 1992
12. Angola, Aprili 1992
13. Rwanda, Aprili 1992
[Picha katika ukurasa wa 23]
Katika Benin mhubiri wa Ufalme apiga maneno ya Mathaya 24:14 kwenye ngoma yake yenye kuongea
[Picha katika ukurasa wa 25]
Katika mabara mengi ya Afrika, Wakristo wa kweli wanatumia vema uhuru wao mpya
[Picha katika ukurasa wa 26]
Mashahidi wapya wafananisha wakfu wao kwa Yehova kwa ubatizo wa maji