Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 11/15 kur. 24-25
  • Kutoa Uelewevu Katika Namibia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoa Uelewevu Katika Namibia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Kufikia Hatua ya Maana
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 11/15 kur. 24-25

Kutoa Uelewevu Katika Namibia

WEWE umesikia maneno “Mimi sijui” katika lugha ngapi? “Hi nokuzuva,” akasema mwanamke mmoja Mherero, mwenye nguo ndefu ya kitamaduni na kifuniko cha kichwani chenye umbo la pembe. “Nghi udite ko,” akaitikia msichana Mkwanyama, akitabasamu. “Kandi uvite ko,” akajibu mwana-kijiji Mndonga, akikunja mabega yake. “Kapi na kuzuvha,” akasema mchunga mbuzi Mkwangali.

Watu hao wote walikuwa wakisema, “Mimi sijui.” Hilo laonyesha vema kama nini kwamba Mashahidi wa Yehova katika Namibia hukabili matatizo makubwa ya lugha wanapojaribu kuwafikia wale wakaazi 1,370,000 katika eneo hilo pana la kilometa mraba 824,000!

Na haishangazi! Kwani si Waherero na Wanama tu walio na lugha zao wenyewe bali pia Waovambo, Wakavango, Watswana, Wakaprivia, Wahimba, Wana-Msituni, na Wadamara wa Namibia. Kinyume na hilo, Mashahidi walikuwa na fasihi ya Biblia katika lugha ya Kiingereza na Kiafrikana tu. Kwa wazi, ili kweli iweze kueleweka kwa watu wengi zaidi, kazi ya kutafsiri ilikuwa ya muhimu. Hiyo ilianza kwa njia ndogo sana miaka mingi iliyopita katika Windhoek, jiji kuu la mahali palipoitwa wakati huo Afrika ya Kusini-Magharibi.

“Katika Windhoek, kulikuwako upinzani mkali dhidi ya kazi yetu ya kutoa ushahidi kutoka kwa kanisa na polisi,” akumbuka Dick Waldron. Akiwa pamoja na mke wake, Koralie, alikuja kwenye nchi hiyo katika 1953 akiwa mhitimu wa Watch Tower Bible School of Gilead. “Hatukuruhusiwa kuingia maeneo ambamo watu weusi waliishi, na nyakati nyingine tulitatanishwa tulipoonwa tukisema na watu weusi. Hatimaye tulipata mahali ambapo tuliachwa bila kusumbuliwa—pito kavu la mto Gammans! Hapo palikuwa nje tu ya mji. Tukiwa tumefichwa chini na vichaka vya msanduku, tuliongoza mafunzo ya Biblia huko.”

Huko ndiko vichapo vya Watch Tower vilikotafsiriwa mara ya kwanza katika lugha za huko. Vilitia ndani baadhi ya trakti katika Kikwanyama na kijitabu “Habari Njema Hizi za Ufalme” katika Kinama. Ndugu Waldron akumbuka ono lenye kuchekesha kuhusiana na kijitabu hicho, ambacho mtu mwenye kupendezwa alikuwa akisaidia kutafsiri. Ulinganifu wa Kinama haukuweza kupatikana kwa ile sentensi, “Adamu alikuwa mwanamume mkamilifu.” Kwa hiyo mwanamume huyo mwenye kupendezwa alisema hivi: “Andika tu kwamba Adamu alikuwa kama fyulisi lililoiva. Wanama wataelewa kwamba alikuwa mkamilifu.” Huo, basi, ndio uliokuwa mwanzo wa kutoa uelewevu wa Maandiko kwa wengi miongoni mwa wenyeji wa Namibia.—Linganisha Danieli 11:33.

Kufikia Hatua ya Maana

Hatua ya maana ilifikiwa katika miaka ya mapema ya 1970 wakati kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele kilipotafsiriwa katika Kindonga na Kikwanyama. Hizo ndizo lugha mbili kuu zinazosemwa na Wanamibia wengi katika Ovamboland, karibu kilometa 700 kaskazini mwa Windhoek. Nyumba ya mapainia ilianzishwa wakati huo katika Ondangwa, kao moja la Ovamboland. Ili kuwasaidia watu wenye kupendezwa katika eneo hilo wanufaike kutokana na mazungumzo ya Biblia ya kila juma yenye msingi wa Mnara wa Mlinzi, mapainia wa pekee waliotumikia katika Ovamboland walipewa mgawo wa kutafsiri muhtasari wa makala ya mafunzo ya Kiingereza katika Kindonga na Kikwanyama.

“Ofisi” ya kutafsiri ilikuwa kona moja iliyotengwa ya nyumba ya kuegeshea gari ambako nakala za habari ya Mnara wa Mlinzi iliyotafsiriwa zilichapishwa kwenye mashine ya zamani ya kunakili. Haikuwa rahisi kukazia fikira kazi hiyo iliyotaka wakati na jitihada nyingi sana, kwa kuwa hali zilikuwa ngumu na halijoto za kiangazi zilikuwa na wastani wa digrii 38 hadi 44 sentigredi. Hata hivyo, huko ndiko broshua mpya na kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani vilitafsiriwa.

Makundi yalipokuwa yakifanyizwa katika Ovamboland na kwingineko katika Namibia, itikio lilikuwa kubwa sana hivi kwamba majengo makubwa na bora zaidi yalihitajiwa. Kwa kuongezea, mahali pa katikati zaidi palitamanika ili mahitaji katika sehemu nyinginezo za nchi yaweze kupewa uangalifu. Wakati uleule, chuki isiyo na sababu dhidi ya kazi ya kuhubiri Ufalme ilikuwa imepungua. Kwa hiyo ruhusa ilipatikana ya kuanza ujenzi kwenye shamba kubwa lililotolewa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika Windhoek. Upesi, wafanyakazi wa hiari 40 walipewa makao kwenye mahali pa ujenzi, na katika Desemba 1990 ofisi za utafsiri zikakamilishwa.

Sasa, katika ofisi na vyumba vyenye kupendeza katika jengo hilo la ki-siku-hizi, kazi ya kuleta uelewevu kwa wengi inaendelea kwa kasi. Fasihi mpya inatafsiriwa daima katika Kiherero na Kikwangali. Kwa habari ya Kindonga na Kikwanyama, chapa ya Mnara wa Mlinzi ya kila mwezi yenye lugha hizo mbili hutokea katika rangi. Chapa hiyo ina makala zote za mafunzo pamoja na habari nyingine. Hilo bila shaka, ni jambo lililo tofauti kabisa na ule mwanzo mdogo katika lile pito kavu la mto miaka mingi sana iliyopita.

“Mimi sijui” husikiwa mara chache sasa. Badala ya hivyo, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 600 katika Namibia wanamshukuru sana Baba yao wa kimbingu, na sasa wanaweza kusema hivi: “Maelezo ya maagizo yako huleta mwanga; huwapa ufahamu [uelewevu, NW] wasiojua kitu.”—Zaburi 119:130, HNWW.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kupiga Mbiu ya habari njema miongoni mwa Waherero

Kutafsiri vichapo vya Kikristo ili kuwanufaisha watu wa Namibia

Ofisi za utafsiri katika Namibia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki