Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Je! Mathayo 28:17 linamaanisha kwamba baadhi ya mitume waliendelea kuona shaka kwa muda mrefu baada ya Yesu aliyefufuliwa kutokea kwao?
La, hatupaswi kufikia mkataa huo kutokana na Mathayo 28:16, 17, linalosema hivi: “Wale wanafunzi kumi na mmoja wakaenda Galilaya mpaka mlima ule aliowaagiza Yesu. Nao walipomwona, walimsujudia; lakini baadhi yao waliona shaka.”
Hapo awali sana Yesu alijaribu kuwasaidia wanafunzi watambue “ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka.” (Mathayo 16:21) Hata hivyo, kukamatwa na kuuawa kwake kuliwaacha wanafunzi wakiwa wamevunjika moyo na kufadhaika. Ufufuo wake ulionekana kuja kama jambo la kushangaza. Na alipojidhihirisha mwenyewe katika namna ya kibinadamu, mwanzoni baadhi yao ‘walikuwa hawajaamini kwa furaha.’ (Luka 24:36-41) Lakini, kutokea-tokea kwake baada ya ufufuo kuliwasaidia wafuasi wake wa karibu wakubali uhakika wa ufufuo wake; hata mtume Tomasi alisadikishwa kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa.—Yohana 20:24-29.
Baadaye wale mitume waaminifu 11 “wa[li]enda Galilaya.” (Mathayo 28:16; Yohana 21:1) Walipokuwa huko, Yesu “aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja.” (1 Wakorintho 15:6) Ni katika mazingira hayo kwamba Mathayo 28:17 linataja kwamba “baadhi yao waliona shaka.” Kwa hiyo wale waliokuwa na shaka bado wangaliweza sana kuwa miongoni mwa wale wafuasi 500.
Ona elezo lenye kupendeza juu ya hilo, lililotolewa na C. T. Russel, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society:
“Hatuwezi kudhani ifaavyo kwamba wale walioona shaka walikuwa mmojawapo wa wale mitume kumi na mmoja, kwani waliridhika kikamili, wakiwa wamesadikishwa kabisa, na walikuwa wamesema hivyo wakati wa nyuma. Tunafikiri, ni lazima wale walioona shaka walikuwa kati ya wale ‘ndugu mia tano’ waliokuwako kwenye mkutano huo uliopangwa, ambao hawakuwa wamekutana naye tangu ufufuo wake, na baadhi yao ambao, inawezekana, walikuwa wadhaifu zaidi katika imani kuliko mitume na wale marafiki wa karibu ambao Yesu alikuwa amesema nao baada ya ufufuo wake. Taarifa ya kwamba ‘baadhi yao waliona shaka’ ni uthibitisho wa unyoofu wa maandishi ya Mwevanjeli huyo. Inatuonyesha pia kwamba wafuasi wa Bwana hawakuwa wepesi sana wa kuamini bila uthibitisho, bali walikuwa na mwelekeo wa kuchunguza na kuhakikisha uthibitisho uliotolewa, na bidii, nishati pamoja na roho ya kujidhabihu ya baadaye ya wale walioamini hutupa sisi uthibitisho mwingi wa weupe wa usadikisho wao kuhusu ufufuo wa Bwana wetu, ambao wao pamoja na sisi hutambua kuwa ndilo jiwe kuu la msingi la imani yetu katika yeye. Ikiwa Kristo hakufufuka imani yetu ni bure na tungali katika dhambi zetu.—1 Kor. 15:17.”—Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence, Mei 1, 1901, ukurasa 152.
Wakati tungali tunazungumzia hili, twaweza kuona kwamba njia ambayo Mathayo anataja jambo hilo inatuandalia uthibitisho wa kutegemeka na unyoofu wa Biblia. Ikiwa mtu alikuwa akitunga hadithi, angeelekea kuandaa mambo madogomadogo ambayo yangeweza kufanya hadithi yake iliyotungwa ionekane yenye kuaminika; yaelekea angehisi kwamba mambo madogomadogo yaliyoachwa au yale yaonekanayo kuwa mapengo yangetilia shaka utungaji wake. Namna gani Mathayo?
Yeye hakuhisi ni lazima aandae maelezo mengi juu ya maneno yake kwamba “baadhi yao waliona shaka.” Masimulizi ya Marko, Luka, Yohana hayasemi lolote juu ya hilo, kwa hiyo maneno ya Mathayo yakichukuliwa peke yayo yaweza kuonekana kuwa yanawashtaki wale mitume 11, ambao alikuwa mmoja wao. Hata hivyo, Mathayo alitoa elezo hilo fupi bila habari ya kuelewesha wazi. Miaka 14 baadaye, mtume Paulo aliandika kitabu cha Wakorintho wa Kwanza. Kulingana na habari aliyoandaa kwenye 1 Wakorintho 15:6, tunaweza kufikia ule unaoelekea kuwa mkataa kwamba wale walioona shaka hawakuwa mitume bali wanafunzi katika Galilaya ambao Yesu hakuwa ametokea kwao bado. Hivyo elezo la Mathayo kwamba “baadhi yao waliona shaka” yasikika kuwa kweli; linasikika ifaavyo kuwa la mwandishi mwenye moyo mweupe anayesimulia jambo la kweli bila kujaribu kueleza ki-ila jambo dogo-dogo.