Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 12/15 kur. 24-28
  • Kufikia “Namna Zote za Watu” Katika UBELGIJI

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kufikia “Namna Zote za Watu” Katika UBELGIJI
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Uanzilishi Waleta Matokeo
  • “Tupa Chakula Chako [Mkate Wako, NW]”
  • Ugumu wa Lugha Mbalimbali
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 12/15 kur. 24-28

Kufikia “Namna Zote za Watu” Katika UBELGIJI

MTUME Paulo aliwakumbusha Wakristo wapakwa-mafuta wenzake juu ya kusudi la Mungu kwamba “namna zote za watu waokolewe na kuja kwenye maarifa yaliyo sahihi ya kweli.” Ili hilo liwezekane walihitaji kusali kwamba wapate “maisha ya utulivu na kimya” ili waweze kupiga mbiu ya habari njema za Ufalme kwa wote waliotaka kusikia.—1 Timotheo 2:1-4, NW.

Leo, kufikia “namna zote za watu” na habari njema kuna maana ya pekee kwa Mashahidi wa Yehova katika Ubelgiji. Tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu 2, nchi hiyo ndogo, ambayo ingeweza kwa urahisi kutoshea ndani ya Ziwa Tanganyika au nusu ya Ziwa Michigan, imepatwa na mabadiliko makubwa katika umbo layo la kikabila na kitamaduni. Kwa kuongezea jumuiya zayo tatu za kawaida—Waflemu (Waholanzi), Wafaransa, na Wajerumani—sasa katika Ubelgiji kuna vikundi tofauti-tofauti vya kilugha na kitamaduni. Kuna wakazi Waarabu, Waturuki, Wahindi, Wachina, Wafilipino, Waafrika, na Waamerika, kwa kutaja wachache tu. Imekadiriwa kwamba mmoja katika ya kila watu 10 katika Ubelgiji ametoka ugenini.

Hivyo, Mashahidi katika Ubelgiji, kama vile Wakristo wenzao ulimwenguni pote, wana-kabiliwa na ugumu wa kuwafikia “namna zote za watu” na habari njema. Kukoje kuhubiri miongoni mwa watu wa mataifa tofauti-tofauti? Mtu aweza kuwakaribiaje watu mmoja mmoja walio na malezi ya kitamaduni na ya kidini yaliyo tofauti kabisa? Na ni nini itikio lao kwa ujumbe wa Biblia?

Uanzilishi Waleta Matokeo

Kuongea na “namna zote za watu” juu ya habari njema za Ufalme ni ono la furaha na lenye kusisimua. Kwenye barabara zenye shughuli nyingi, sokoni, katika magari ya umma, kutoka nyumba kwa nyumba, watu kutoka kontinenti zote wanaweza kupatikana. Kwa kuwa mwanzilishi, mhubiri wa Ufalme anaweza kuanzisha mazungumzo kwa urahisi, na mara nyingi hilo huongoza kwenye matokeo yenye kuthawabisha.

Kwenye kituo cha basi, Shahidi mmoja alianzisha mazungumzo pamoja na mwanamke Mwafrika kwa tabasamu tu yenye uchangamfu. Upesi mwanamke huyo akaonyesha shangwe yake ya kusikia kuhusu Ufalme wa Mungu, na akataka kujua zaidi juu ya Biblia. Alikubali magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! akampa Shahidi huyo anwani yake. Shahidi huyo aliposema kwamba angemtembelea karibuni, mwanamke huyo alikataa. “La! La! Acha tufanye mpango mahususi ili niwe nyumbani unapokuja.”

Siku tatu baadaye, Shahidi huyo alipokuwa amtembelee, alipata kwamba alikuwa amepoteza anwani ya mwanamke huyo. Lakini akikumbuka jina la barabara, alienda na kuchunguza katika kila nyumba kuona ikiwa angepata jina la Kiafrika. Alifika mwisho wa barabara hiyo bila kupata alichokuwa akitafuta. Huo ulikuwa utamausho ulioje! Kwa ghafula, alipokuwa akijitayarisha kuondoka, mwanamke yuleyule aliyekuwa akimtafuta alikuwa akisimama mbele yake, kana kwamba alikuwa ametokea kimuujiza, na huo ulikuwa wakati uleule ambao walikuwa wamekubaliana kukutana! Funzo la Biblia nyumbani likaanzishwa.

Namna gani zile tamaduni, imani, na mapokeo tofauti-tofauti? Kwa mfano, namna gani imani za Dini ya Hindu? Painia mmoja alikumbuka yale aliyokuwa amesoma katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko. Kinasema hivi: “Badala ya kushughulika na magumu ya falsafa ya Kihindu, eleza tu kweli zenye kuridhisha zinazopatikana katika Biblia Takatifu. . . . Kweli zilizo wazi katika Neno lake zitaifikia mioyo ya wale wanaoona njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu.”

Painia huyo alifanya hivyo barabara alipokutana na Kashi, mwanamke mmoja kutoka India aliyekubali funzo la Biblia. Ka-shi alifanya maendeleo ya utaratibu, na upesi alikuwa akiongea na marafiki wake juu ya yale aliyokuwa akijifunza. Siku moja painia huyo alikutana na mke wa balozi mmoja, aliyeuliza hivi: “Je! wewe ndiye unayemfundisha Kashi Biblia?” Painia huyo alishangaa kama nini wakati mwanamke huyo aliposema hivi: “Yeye ni mwalimu mzuri kama nini! Ameweza kunisadikisha juu ya mambo mengi. Ebu wazia, yeye, Mhindu, akinifundisha mimi, Mkatoliki, Biblia!”

Unapokutana na Wafilipino, unatambua mara moja kwamba wengi wao huipenda Biblia. Wao ni wachangamfu na wakaribishaji-wageni, na ni rahisi sana kuanzisha mazungumzo nao. Mwanamke mmoja Mfilipino alikubali kwa utayari magazeti mawili, lakini kwa kuwa alikuwa Mkatoliki, aliyatupilia mbali. Majuma kadhaa baadaye alikubali magazeti mawili tena, ambayo aliacha mkobani mwake. Usiku mmoja alikuwa na hamu ya kusoma. Baada ya kutafuta kotekote ili kupata kichapo chenye kupendeza, aliyapata magazeti hayo. Kwa kusitasita, alianza kuyasoma, na kupendezwa kwake kukaongezeka. Muda mfupi baadaye, Shahidi mmoja alimtembelea nyumbani kwake, na mwanamke huyo akauliza maswali mengi. Hiyo ilikuwa mara yake ya kwanza kulinganisha imani zake za Katoliki na yale ambayo Biblia husema. Utoaji wa Kimaandiko wenye usababu ulimsadikisha kwamba alikuwa hatimaye ameipata kweli.

“Tupa Chakula Chako [Mkate Wako, NW]”

Wakaaji wengi wa kigeni wamo Ubelgiji kwa sababu za kibiashara au ili kufanya kazi kwenye mojawapo ya ofisi za ubalozi 150 zilizoaminishwa au kwenye Ofisi ya Ubalozi ya Jumuiya ya Ulaya. Wengi wao hukaa kwa muda wa miaka michache tu. Kuwatolea ushahidi na kujifunza Biblia nao huenda kukaonekana mwanzoni kutokuwa na matokeo. Lakini Biblia hutukumbusha hivi: “Tupa chakula chako [mkate wako, NW] usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi.” (Mhubiri 11:1) Mara nyingi matokeo ni yenye kuthawabisha kwa njia yenye kushangaza.

Ndivyo ilivyokuwa kwa mwanamke mmoja Mwamerika aliyepokea magazeti kwa kawaida kutoka kwa Shahidi mmoja. Baadaye Shahidi huyo alimwonyesha faida ya kujifunza Biblia kwa kawaida, na akajitolea kujifunza naye. Mwanamke alikubali na akafanya maendeleo ya haraka. Upesi akaona tofauti kati ya dini ya kweli na bandia. Kwa hiyo aliondoa sanamu zote za kidini kutoka kwa nyumba yake. Halafu wakati ukafika wa yeye kurudi United States. Je! hilo lilimaanisha mwisho wa maendeleo yake ya kiroho? Ebu wazia shangwe na mshangao wa yule Shahidi alipopokea simu kutoka Shahidi mmoja katika United States akimwambia kwamba mwanamke yule alikuwa ameendelea na funzo lake, alikuwa amejiweka wakfu kwa Yehova Mungu, na alikuwa amebatizwa! Kwa kweli, alikuwa tayari akitumikia akiwa mhudumu painia msaidizi.

Ndivyo ilivyokuwa kwa Kashi, yule mwanamke Mhindi, na kwa yule mwanamke Mfilipino waliotajwa mapema. Kashi aliporudi India, yeye na mume wake walianza tena funzo lao la Biblia. Mwishowe wote wawili walijiweka wakfu kwa Yehova wakashiriki katika kazi ya kuhubiri. Kwa kuwa waliishi katika eneo ambapo hakukuwa Mashahidi wengine, walitoa nyumba yao kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kundi. Kashi alitumikia akiwa painia msaidizi kadiri ambavyo afya yake ilimruhusu, na amekuwa akiongoza mafunzo ya Biblia nyumbani sita, yakihusisha watu wanaojumlika kuwa 31. Vivyo hivyo, baadaye yule mwanamke Mfilipino alihamia United States, akafanya maendeleo hadi wakfu na ubatizo, akawa painia wa kawaida. Matokeo yenye furaha kama hayo ni miongoni mwa mengi ambayo wahubiri wa Ufalme katika Ubelgiji hufurahia wanapoendelea kuwahubiri watu katika eneo lao.

Ugumu wa Lugha Mbalimbali

Ili kutimiza ile kazi ya kuhubiri kwa “namna zote za watu,” ofisi ya tawi inalazimika kuwa na fasihi ya Biblia katika lugha zaidi ya mia moja. Sasa kuna makundi ya Kibelgiji katika lugha kumi. Makundi 61 kati ya yale 341 ni ya lugha za kigeni, na wahubiri wa Ufalme 5,000 kati ya 26,000 ni wa nchi za kigeni. Kundi moja linatia ndani wanaume na wanawake kutoka nchi tofauti-tofauti 25. Ebu wazia zile rangi na tamaduni tofauti-tofauti zenye kupendeza kwenye mikutano yao! Hata hivyo ule upendo na umoja miongoni mwa ndugu ni ushuhuda wenye nguvu wa uanafunzi wa Kikristo wa kweli.—Yohana 13:34, 35.

Kwa kuwa kuna wakaaji wengi sana katika Ubelgiji wanaohitaji kusikia habari njema katika lugha za kigeni, wahubiri wengine wamekubali ugumu wa kujifunza lugha zilizo ngumu, kama vile Kituruki, Kiarabu, na Kichina. Jitihada zao zimethawabishwa sana.

Wale wanaohubiri miongoni mwa wakazi Waarabu huona kwamba mara nyingi wanaweza kuchochea kupendezwa katika Biblia kwa kukazia thamani yayo yenye kutumika. Mhubiri wa Ufalme mmoja alikuwa na mazungumzo yenye kupendeza pamoja na profesa Mwarabu mmoja, kisha kwa muda wa miaka mitatu baadaye hakuweza kumpata profesa huyo tena. Asiweze kuvunjika moyo kwa urahisi, mhubiri huyo aliamua kumwachia profesa huyo barua fupi yenye maswali ya Biblia. Hilo lilimsisimua sana profesa huyo hivi kwamba alikuwa na nia ya kuchunguza Biblia bila upendeleo. Alishangaa sana juu ya yale aliyoona hivi kwamba yeye na mke wake, wote wakiwa Waislamu, waliweka kando jioni fulani ili kuisoma Biblia pamoja.

Wale wanaojaribu kuwasaidia wale wakazi wengi Wachina katika miji mikubwa wana kizuizi kingine cha kushinda kuongezea kile kizuizi cha lugha. Wachina wengi hawaamini katika Mungu kuwa ndiye Muumba au katika Biblia kuwa ndilo Neno la Mungu. Hata hivyo, wao ni wadadisi na wanataka kujua Biblia inahusu nini. Nao ni wasomaji wenye bidii. Ni jambo la kawaida kwao kumaliza kusoma fasihi ya Biblia yoyote wanayoachwa nayo, au hata sehemu kubwa ya Biblia, katika siku chache tu. Moyo wao ukifaa, wanasukumwa na nguvu ya Neno la Mungu.

Mwanamke mmoja Mchina aliliona kuwa jambo gumu kukubali wazo la kuwako kwa Muumba. Lakini katika funzo la pili, machozi yalitoka machoni pake aliposema hivi: “Sasa ninaamini katika Yehova Mungu, kwani ikiwa Biblia iliandikwa kwa kipindi cha miaka 1,600 na watu tofauti-tofauti 40 na bado inapatana kabisa na kichwa kikuu kimoja, basi ni lazima iwe kwamba Yehova Mungu alikuwa akielekeza uandikaji. Habari hiyo yafuatana sana!”

Mwanamke mwingine Mchina alikaribiwa na Shahidi mmoja kwenye gari la reli la barabara. “Je! wewe ni Mkristo?” akamwuliza Shahidi huyo. Kisha akasema kwamba alitamauka sana kuona kupingana kwingi miongoni mwa wale wanaodai kuwa Wakristo. Shahidi huyo alikubaliana na yale aliyosema lakini alieleza kwamba Biblia haijipingi yenyewe. Wakati nao ukafika wa mwanamke huyo kushuka kwenye gari. Alimpa Shahidi huyo anwani yake, na wakati Shahidi huyo alipomtembelea, mwanamke huyo alipaza sauti kwa mshangao: “Laiti tu ningalijua, ningalichukua gari hilo mwaka mmoja mapema zaidi!” Alipoulizwa alilomaanisha, mwanamke huyo alieleza hivi: “Hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kwenda kwenye chuo kikuu kwa gari hilo. Waweza kuwazia? Nimepoteza mwaka mmoja!” Alifurahi sana kuweza kujifunza Biblia hata kwa miezi michache tu kabla ya kurudi Uchina.

Maono ya jinsi hiyo yamewafundisha Mashahidi Wabelgiji somo fulani. “Asubuhi panda mbegu zako, wala jioni usiuzuie mkono wako,” Biblia husema, “kwa maana wewe hujui ni zipi zitakazofanikiwa, kama ni hii au hii, au kama zote zitafaa sawasawa.” (Mhubiri 11:6) Jitihada zinazofanywa za kushinda vizuizi vya lugha, tamaduni, na mapokeo zinastahili sana matokeo. Maitikio yenye kuchangamsha moyo yanathibitisha, zaidi ya yote, kwamba Mungu kwa kweli “hana upendeleo, bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”—Matendo 10:34, 35.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki