Tengenezo la Kutaniko la Kikristo
INGAWA makutaniko ya Kikristo ya Mungu yalianzishwa katika mahali mbalimbali, hayakutenda kivyayo. Badala yake, yote yalitambua mamlaka ya baraza lenye kuongoza la Kikristo katika Yerusalemu. Washiriki wa baraza hilo lenye kuongoza walikuwa mitume na wanaume wazee wa kutaniko la Yerusalemu, kwa kuwa hakukuwa mabaraza yenye kushindana yaliyotafuta kusimamia kutaniko. Baraza lenye kuongoza la Kikristo jaminifu la karne ya kwanza W.K. ndilo lililopelekewa suala la tohara lilifikirie. Baraza lenye kuongoza lilipofanya uamuzi walo, kama lilivyoelekezwa na roho takatifu, uamuzi huo ulikubaliwa na ukawa wajibu wa makutaniko yote ya Kikristo, hayo yaliutii kwa moyo wa kupenda.—Matendo 15:22-31.
Baraza la Kikristo katika Yerusalemu lilituma nje wawakilishi wasafirio. Hivyo, Paulo na wengine walipeleka uamuzi wa baraza lenye kuongoza uliotajwa sasa hivi, ikitaarifiwa hivi: “Basi walipokuwa wakipita kati ya miji ile, wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike.” Kuhusu matokeo yaliyofanyizwa, inasemwa hivi: “Makanisa yakatiwa nguvu katika ile Imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku.” (Matendo 16:4, 5) Mapema zaidi, wakati mitume katika Yerusalemu “waliposikia ya kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu wakawapelekea Petro na Yohana; ambao waliposhuka, wakawaombea wampokee Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].”—Matendo 8:14, 15.
Yale makutaniko moja moja yalishikamana karibu-karibu na mwelekeo wa baraza lenye kuongoza la Kikristo, ambalo lilisimamia kuwekwa rasmi kwa wanaume wazee. (Tito 1:1, 5) Hivyo ikawa kwamba, kama walivyoelekezwa na baraza lenye kuongoza la Kikristo chini ya uvutano wa roho takatifu, waangalizi pamoja na wasaidizi wao, watumishi wa huduma, waliwekwa katika kila kutaniko. Wanaume waliowekwa katika vyeo hivyo vya uangalizi na daraka walipaswa kutimiza sifa hususa. (1 Timotheo 3:1-13; Tito 1:5-9) Wawakilishi wasafirio wa baraza lenye kuongoza, kama vile Paulo walifuata Kristo na kuweka kielelezo chema cha kuigwa. (1 Wakorintho 11:1; Wafilipi 4:9) Kwa kweli, wote hao waliokuwa katika vyeo vya wachungaji wa kiroho walipaswa kuwa ‘vielelezo kwa kundi’ (1 Petro 5:2, 3), walipaswa kuonyesha hangaiko lenye upendo kwa watu mmoja mmoja katika kutaniko (1 Wathesalonike 2:5-12), na walipaswa kuwa msaada halisi kwa wale wagonjwa kiroho.—Wagalatia 6:1; Yakobo 5:13-16.
Kwa hiyo, kama vile Yehova alivyopanga kitengenezo kutaniko la Israeli chini ya wanaume wazee, vichwa, mahakimu, na maofisa (Yoshua 23:2), Yeye alihakikisha kwamba kuna usimamizi wa kutaniko la Kikristo likiwa na wanaume wazee waliowekwa rasmi kwenye vyeo vya uangalizi humo. (Matendo 14:23) Na, kama vile nyakati nyingine wanaume wazee walitenda wakiwa wawakilishi kwa kutaniko lote la Israeli, kama katika mambo ya kihukumu (Kumbukumbu la Torati 16:18), Mungu alipanga kila kutaniko la Kikristo liwakilishwe jinsi iyo hiyo katika mambo hayo na wanaume waliowekwa kwa roho takatifu wenye kuchukua daraka kwa uzito katika vyeo vya mamlaka. (Matendo 20:28; 1 Wakorintho 5:1-5) Hata hivyo, ikiwa kwamba magumu yatokea miongoni mwa washiriki wa kutaniko la Kikristo la Mungu, maneno ya Yesu Kristo yaliyoandikwa kwenye Mathayo 18:15-17 (yaliyotamkwa kabla ya kutaniko la Kiyahudi la Mungu kukataliwa na Yehova na hivyo yakitumikia hapo kwanza kwalo) yalitumikia kuwa msingi wa kumalizia au kushughulikia matatizo hayo.
Yehova Mungu ameweka washiriki katika “mwili” wa kiroho wa Kristo “kama alivyotaka.” Naye Paulo alitaarifu hivi: “Na Mungu ameweka wengine katika Kanisa, wa kwanza mitume, wa pili manabii, wa tatu waalimu, kisha miujiza, kisha karama za kuponya wagonjwa, na masaidiano, na maongozi, na aina za lugha.” Si wote waliofanya utendaji ule ule, lakini wote walihitajiwa na kutaniko la Kikristo. (1 Wakorintho 12:12-31) Paulo alieleza kwamba kuwekwa kwa mitume, manabii, waeneza evanjeli, wachungaji, na walimu kwa ajili ya kutaniko la Kikristo ulitolewa “kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo.”—Waefeso 4:11-16.
Kutaniko la Israeli liliandaliwa sheria za Mungu nalo lilifanywa lithamini kwamba “mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali kwa kila litokalo katika kinywa cha BWANA [Yehova, NW].” (Kumbukumbu la Torati 8:1-3) Yesu Kristo alitambua pia kwamba mwanadamu hangeweza kuishi kwa mkate pekee “ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” (Mathayo 4:1-4) Kwa hiyo, maandalizi ya kutosha yamefanywa kwa ajili ya kutaniko la Kikristo ili liwe na chakula cha kiroho kinachohitajiwa, Kristo mwenyewe akitaja yule “mtumwa” ambaye kupitia kwake chakula hicho kinatolewa kwa “watu wa nyumbani” (NW) Wakristo. Ikiwa sehemu ya unabii wake kuhusu kuwapo kwake mwenyewe na “umalizio wa mfumo wa mambo,” (NW) Yesu alionyesha kwamba, akiisha kuwasili, “bwana” huyo angemweka huyo “mtumwa mwaminifu mwenye akili” “juu ya vitu vyake vyote.”—Mathayo 24:3, 45-47.
Kukusanyika kwa ajili ya ibada ya Yehova na kuzungumza sheria zake kulikuwa kwa maana kwa kutaniko la Israeli. (Kumbukumbu la Torati 31:12; Nehemia 8:1-8) Hali kadhalika, mikutano kwa ajili ya ibada ya Yehova na funzo la Maandiko ni sehemu ya lazima ya kutaniko la Kikristo la Mungu, mwandikaji kwa Waebrania aliwaonya kwa upole wapokeaji wa barua yake wasiache kukusanyika pamoja. (Waebrania 10:24, 25) Utendaji katika masinagogi ya nyakati za baadaye ya Kiyahudi ulitia ndani kusoma na kufundisha Maandiko, kutoa sala, na kumpa Mungu sifa. Mambo hayo yaliendelezwa na kuingizwa katika mikusanyiko ya Kikristo, ingawa ilifanywa bila nyongeza za sherehe zilizositawi hatimaye katika ibada za sinagogi. Katika sinagogi hakukuwa na jamii ya kikuhani iliyowekwa kando, kila mwanamume Myahudi mwenye ujitoaji akiwa na nafasi ya kushiriki kusoma Maandiko na kuyafafanua. Kwa ulinganisho, hakukuwa na mgawanyiko kati ya jamii ya makasisi na watu wa kawaida au migawanyiko inayofanana na hiyo katika kutaniko la Kikristo la mapema. Bila shaka, wala katika kutaniko wala katika sinagogi wanawake hawakufundisha au kutumia mamlaka juu ya wanaume.—1 Timotheo 2:11, 12.
Kudumishwa kwa utaratibu ufaao katika mikutano ya kutaniko la Kikristo la Mungu kulipatana na uhakika wa kwamba Yehova, ambaye alifanya uandalizi kwa ajili ya mpango wa kutaniko miongoni mwa wafuasi wa Kristo, ni “Mungu, si wa machafuko, bali wa amani.” Hali ya utaratibu huo ilitumikia pia kuleta manufaa kubwa za kiroho kwa wote waliohudhuria.—1 Wakorintho 14:26-35, 40.