Uvumbuzi wa Aina Tofauti Katika Bahamas
KAMA mawe ya kukanyagia kutoka upande mmoja hadi mwingine wa bahari za rangi ya buluu kati ya Florida na Kyuba, visiwa vya Bahamas vilipokea uangalifu usio na kifani kutoka kwa vyombo vya habari katika 1992. Kwa nini? Kwa sababu wenye mamlaka huona visiwa vya Bahamas kuwa ndiyo mabara yaliyoonwa kwanza katika safari ya kihistoria ya Christopher Columbus katika 1492, alipovumbua visiwa vya Amerika. Mwaka wa 500 wa kuwasili kwa Columbus katika Oktoba 12 kulivuta uangalifu wa kimataifa.
Hata hivyo, msisimuko wa mwaka huo wa 500 haukukosa vipingamizi wavyo. Akihutubia Baraza la Kitaifa la Mawakili Weusi la 23, John Carew (profesa wa masomo ya kimataifa) yaripotiwa alisema kwamba Columbus “alisababisha vifo vya wakaaji wengi wa Visiwa vya Karibea.”—The Nassau Guardian.
Leo, hakuna yeyote kati ya wakaaji wenyeji 250,000 wa Bahamas awezaye kufuatia ukoo wake hadi kwa wale wenyeji wenye amani ambao Columbus alikutana nao na aliowasimulia kuwa “watu wenye umbo zuri, wenye miili yenye kupendeza na nyuso nzuri sana.” Ni nini kilichowapata wakaa-visiwani hao? A History of the Bahamas chajibu hivi: “Kati ya 1500 na 1520 wakaaji wote wa Bahamas, labda Walukaya karibu 20,000, walipelekwa kwa lazima” kuwa watumwa ili kufanya kazi katika migodi ya dhahabu katika Hispaniola.
Visiwa vya Bahamas vikiwa vimeondolewa wakaaji hivyo, “vilivumbuliwa upya” kwanza na Uingereza na baadaye na vikundi vikubwa vya “waaminifu-washikamanifu” (kuelekea serikali fulani). Hao wa pili walikuwa hasa wale waliomiliki mashamba yaliyopandwa mimea waliotoka koloni za Amerika ya Kaskazini. Wakiwa waaminifu-washikamanifu kwa Serikali ya Uingereza, walitoroka ile vita ya kupigania uhuru iliyokuwa ikichemka wakati huo katika bara la Amerika ya Kaskazini. Wabahamas wa leo hasa ni wazao wa masetla hao na watumwa wao. Walipowekwa huru, watumwa wengi waliendelea kutumia majina ya wale waliokuwa mabwana wao.
Uvumbuzi wa Aina Nyingine
Hakuna shaka kwamba Columbus alijiona mwenyewe kuwa mishonari wa aina fulani. Yaripotiwa kwamba alisema: “Mungu alinifanya mjumbe wa mbingu mpya na dunia mpya. . . . alinionyesha mahali pa kuipata [dunia hiyo mpya].” Hata hivyo, uharibifu uliotokea ulithibitisha vingine. ‘Mbingu mpya na dunia mpya’ yenye uadilifu iliyoahidiwa na Mungu ilihitaji kungoja uvumbuzi wa aina nyingine.—2 Petro 3:13, Habari Njema kwa Watu Wote.
Katika 1926, Edward Mckenzie na mke wake waliwasili katika Bahamas. Tofauti na wale wavumbuzi kabla yao, wenzi wa ndoa hawa wanyenyekevu waliotoka Jamaika walikuja kutafuta watu wenye mioyo ya kufuatia haki ambao wangeweza kuwapa hazina. Walikuwa wa kwanza kuleta habari njema za Ufalme wa Mungu katika Bahamas. (Mathayo 13:44; 24:14) Baadaye mwaka huo Wajamaika wengine wawili, Clarence Walters na Rachel Gregory walijiunga nao. Kufikia 1928 kulikuwako wahubiri wa Ufalme saba katika Bahamas. Kwa miaka minne walifanya kazi kwa bidii katika kuhubiri habari njema kwa wakaa-visiwani.
Halafu akaja E. P. Roberts, msemaji mwenye nguvu kutoka Trinidad. Hotuba zake za peupe katika majumba ya kukutania yaliyojulikana sana yalichangia sana kuondolea mbali imani bandia na yalichochea mioyo ya wengi kwenye kweli ya Biblia. Donald Oscar Murray, ambaye alijulikana baadaye kwa shauku kuwa D. O., alikuwa akiketi miongoni mwa wasikilizaji akiwa amesisimuka. Hatimaye alikuja kuongoza katika kazi.
Mishonari Nancy Porter akumbuka vema jinsi D. O. Murray alivyosema juu ya sala zake zenye bidii ili kupata msaada katika kazi ya kuhubiri. Katika 1947, Nancy na mume wake, George, pamoja na wengine wawili walikuwa wamishonari wa kwanza waliotumwa Bahamas na Watch Tower Society. Yeye akumbuka hivi: “Mkutano wa kwanza tuliohudhuria ni jambo ambalo sidhani tutapata kusahau wakati wowote. Tulikuwa karibu tisa au kumi. Ndugu Murray alikuwa mwenyekiti na akafungua kwa sala, akimshukuru Yehova kwa ajili ya kuwasili kwa wamishonari. Msaada ulihitajiwa, akasema, na ‘tumeomba msaada kwa muda mrefu sana.’ Sosaiti ilikuwa imeahidi kutuma msaada, na sasa tulikuwa hapo. Sala hiyo ilikuwa yenye kugusa moyo sana hivi kwamba ikatufanya tuhisi kwamba tulitaka kukaa na hatukutaka kuondoka kamwe.” Sasa, miaka 45 hivi baadaye na ijapokuwa kifo cha mume wake, Dada Porter angali akiwapelekea wakaa-visiwani ujumbe wa Ufalme wenye kufariji.
Hasa tangu 1947 kazi ya kuhubiri Ufalme katika Bahamas imefaidika sana kutokana na wahudumu wa wakati wote na wengine ambao wamezuru visiwa hivyo kwa mashua. Mara nyingi walihitaji kuongoza mashua kwa uangalifu kupitia mafungu ya mchanga na maji machache yenye viwimbi na kisha kutembea majini hadi ufukoni ili kupeleka habari njema kwenye makao ya mbali. Jitihada hizo za mapema zinatokeza matunda hata leo.
Jambo la maana lilitukia katika 1950. Katika Desemba wa mwaka huo, Nathan H. Knorr, aliyekuwa wakati huo msimamizi wa Watch Tower Society, pamoja na katibu wake, Milton G. Henschel, walizuru Bahamas kwa mara ya kwanza. Knorr aliwahutubia watu 312 waliosongamana katika jumba liitwalo Mother’s Club Hall, jengo dogo la mbao kwenye barabara ya Jail Alley. Watu kadhaa mashuhuri walikuwapo, kutia na mbunge mmoja na mhariri wa gazeti la habari la kila siku. Usiku huo, Ndugu Knorr alitangaza kufunguliwa kwa ofisi ya tawi ya Sosaiti katika Bahamas.
Itikio la Kirafiki la Wakaa-Visiwani
Kwa ujumla watu wenye urafiki wa Bahamas wameusikiliza ujumbe wa Ufalme. Bado, ni jambo gumu kuwafikia wote. Kwa nini? Ingawa watu wengi huishi katika jiji kuu, Nassau, na kwenye kisiwa cha karibu Grand Bahama, wengine wametawanyika kotekote katika vile visiwa 15 vikubwa zaidi na baadhi ya vile vijisiwa na visiwa vya matumbawe 700 vinavyofanyiza kikundi hiki cha visiwa.
Wakiona uhitaji huo, idadi yenye kuongezeka ya Mashahidi wa mahali hapo na wengi kutoka kwingineko wamehamia vikundi vidogo vya visiwa ili kusaidia na kazi ya kuhubiri. Kwa kustahili pongezi, wamefanya hivyo kwa kujidhabihu na kujigharimu wenyewe sana. Lakini jitihada hizo zimethawabishwa sana.
Wenzi wa wawili wachanga walihamia kile kisiwa kikubwa cha Andros. Walipokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba siku moja, walikutana na mhamiaji mmoja kutoka Haiti. Kuna maelfu ya watu hao katika Bahamas. Mtu huyo alikubali kwa utayari kuwa na funzo la Biblia nyumbani. Funzo lilianzishwa usiku uo huo, kwa kutumia nakala za Kiingereza na za Kifaransa za kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Jioni iliyofuata, alihudhuria mkutano wa Kikristo wake wa kwanza. Upesi, mtu huyo aliacha kuvuta sigareti, akafanya maendeleo ya haraka, na kuanza kushiriki katika kazi ya kuhubiri.
Katika asubuhi ya siku ambayo mtu huyo alikuwa abatizwe, alipokea tepu kutoka familia yake katika Haiti, ingawa hakuwa amepata habari kutoka kwao kwa miaka mitano. Wao walitaka kumwambia nini? Walisimulia jinsi walivyokuja kuwa Mashahidi wa Yehova. Walieleza kwamba dada yake tayari alikuwa painia wa kawaida, au mhubiri wa wakati wote, wakamhimiza awatafute Mashahidi wa Yehova na kujifunza Biblia pamoja nao. Bila shaka, mwanamume huyo alibatizwa siku hiyo akiwa na uhakika kamili kwamba alikuwa akifanya jambo linalofaa.
Maitikio yenye idili kama hayo yamechangamsha mioyo ya Mashahidi wa mahali hapo. Idadi zenye kuongezeka daima za wao zimechukua kazi ya kueneza evanjeli wakati wote, na hilo limechangia ukuzi. Kwa hiyo ikawa kwamba katika 1988 idadi ya wapiga mbiu ya Ufalme katika Bahamas ilifika 1,000. Leo, katika makundi 19, kuna karibu wahubiri wa ufalme 1,300, kwenye karibu visiwa vyote vikuu.
Kuwa Tayari kwa Ajili ya Wakati Ujao
Kwa sababu ya ukuzi wao wa idadi, Mashahidi wamekuwa na ugumu wa kupata vifaa viwezavyo kugharimika ambavyo ni vikubwa vya kutosha kwa ajili ya mikusanyiko yao ya kila mwaka. Mikusanyiko miwili ililazimika kufanywa kwenye visiwa viwili tofauti ili kushughulikia umati. Hivyo, mipango ilifanywa ya kujenga Jumba la Kusanyiko pamoja na ofisi mpya ya tawi. Kazi ilianzishwa katika Desemba 1989. Mamia ya wafanyakazi wa kujitolea wa kimataifa na wa mahali hapo walifanyia kazi mradi huo “kwa moyo, kama kwa Bwana [Yehova, NW].”—Wakolosai 3:23.
Bila shaka, kusanyiko la Mashahidi lililo kubwa zaidi na lenye furaha zaidi katika Bahamas kufikia leo lilitukia kwenye pindi ya kuwekwa wakfu kwa ofisi mpya ya tawi na Jumba la Kusanyiko katika Februari 8 na 9, 1992. Matazamio yenye hamu yaliongezeka wakati ndugu katika sehemu zote za visiwa walipokuwa wakifanya matayarisho kwa ajili ya tukio hilo. Halihewa ilikuwa yenye ubaridi isivyo kawaida, na ilinyesha usiku kabla ya programu ya kuwekwa wakfu. Lakini hakuna lolote ambalo lingeweza kupunguza shangwe ya ule umati wenye furaha wa watu 2,714 wakati John E. Barr, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alipokuwa akitoa hotuba ya kuwekwa wakfu, yenye kichwa “Wimbo wa Ongezeko la Theokrasi.”
Mioyo ilifurika na shukrani kwa Baba wa kimbingu, Yehova Mungu, kwa ajili ya pindi yenye shangwe na msisimuko wa jinsi hiyo. Wale waliokuwapo waliazimia hata zaidi kutumia nishati yao kamili katika kazi ya elimu ya kiroho iliyokuwa imefanya upanuzi halisi uwe wa lazima.
Kama uvumbuzi wa Columbus lilikuwa badiliko kuu la kufanyia maendeleo visiwa hivyo labda ni jambo litakaloendelea kubishaniwa. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova katika Bahamas ni wenye umoja katika shukrani yao kwa Mungu kwa ajili ya kuandaa wapiga mbiu ya Ufalme ambao roho yao ya kujidhabihu iliwasukuma wakabili kwa ushujaa mambo yasiyojulikana ili kuleta habari njema zenye utukufu katika maeneo ya bahari ambayo hayakuwa yamevumbuliwa kiroho. Kazi yao na “uvumbuzi” wao umetokeza utajiri wa kiroho usioweza kulinganishwa kwa watafutaji kweli wote katika Bahamas.
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 24, 25]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Grand Bahama
Abaco
Andros
New Providence
Nassau
Eleuthera
Cat Island
Great Exuma
Rum Cay
San Salvador
Long Island
Crooked Island
Acklins Island
Mayaguana
Little Inagua
Great Inagua
CARIBBEAN SEA
FLORIDA
CUBA
[Picha]
Kuhubiri katika Soko la Nyasi
Kutembea majini hadi ufukoni ili kushiriki habari njema
Ofisi ya tawi iko kwenye kilima ambacho kutoka hapo Jumba la Ufalme laonekana chini