Athawabishwa na “Taji ya Uhai”
MTUME Yohana aliambiwa amwandikie yule malaika wa kundi la Smirna hivi: “Uwe mwaminifu hata kufa, nami nitakupa taji ya uzima [uhai, NW].” (Ufunuo 2:8, 10) Kwa hiyo, ni lenye huzuni na shangwe pia tangazo hili linalotolewa hapa kwamba Frederick William Franz, msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., pamoja na mashirika mengine ya kitheokrasi, alimaliza mwendo wake wa kidunia katika asubuhi ya Desemba 22, 1992.
Ni tangazo lenye huzuni kwa sababu latuambia juu ya mwisho wa utendaji mbalimbali wa kidunia wa mtumishi wa Yehova, mpendwa sana na mwaminifu kwa njia yenye kutokeza. Hata hivyo, ni tangazo lenye shangwe pia kwa sababu maneno haya ya Ufunuo 14:13 yanatumika sasa kumhusu Ndugu Franz mpendwa wetu: “Heri [wenye furaha ni, NW] wafu wafao katika Bwana tangu sasa. Naam, asema Roho, wapate kupumzika baada ya taabu zao; kwa kuwa matendo yao yafuatana nao.” Ndugu Franz alikuwa mwenye kiasi na mnyenyekevu, mhudumu mwenye bidii na mwenye matokeo sana aliyetumiwa sana na Yehova Mungu akiwa mshiriki wa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ili kusaidia katika kuandaa chakula cha kiroho kwa “watu [wa nyumbani, NW]” na waandamani wao.—Mathayo 24:45-47.
Ndugu Franz alizaliwa Septemba 12, 1893, katika Covington Kentucky. Alipata kweli kupitia kaka yake [ndugu yake mkubwa]. Wakati huo alikuwa akihudhuria Chuo Kikuu cha Cincinnati, akijitayarisha kuwa mhudumu Mpresbiteri. Badala yake, alijitenga na Kanisa Presbiteri akaja kushirikiana na Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Alibatizwa Novemba 30, 1913, na mwaka uliofuata aliacha chuo kikuu na kuingia katika kazi ya kolpota (painia). Katika Juni 1, 1920, akawa mshiriki wa familia ya Betheli ya Brooklyn. Punde si punde, alipewa usimamizi wa dawati ya kolpota, na katika 1926 akahamishwa kuletwa kwenye idara ya uhariri, alikotumikia kwa matokeo sana. Katika 1945 akawa makamu wa msimamizi wa Watch Tower Society na mashirika mengineyo yanayohusiana nayo. Katika 1977, baada ya kifo cha aliyekuwa msimamizi wakati huo, Nathan H. Knorr, alikuja kuwa msimamizi wa Watch Tower Society. Alitumikia katika cheo hicho hadi kifo chake. Katika muda wa maisha yake, Ndugu Franz aliona idadi ya Mashahidi wa Yehova ikiongezeka kutoka elfu chache hadi yapata milioni nne u nusu. Alifurahia mapendeleo mengi ya utumishi, kutia ndani kutoa hotuba kwenye mikusanyiko ya kimataifa na kuzuru matawi na makao ya mishonari katika sehemu nyingi za ulimwengu. Masimulizi ya maisha yake yalitokea katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1987.
Katika jioni ya Jumatatu, Desemba 28, 1992, hotuba ya ukumbusho ilitolewa katika Jumba la Ufalme la Betheli ya Brooklyn. Hotuba yenye kuchangamsha sana na yenye kujenga kiroho ilitolewa na Ndugu Albert D. Schroeder wa Baraza Linaloongoza. Familia za Betheli za Watchtower Farms, Patterson, Mountain Farm, na Kingdom Farm, pamoja na familia ya Betheli kwenye Tawi la Kanada, ziliunganishwa kwa simu.
Wote, hasa wale waliofanya kazi kwa ukaribu naye, watamkosa sana Ndugu Franz. Alikuwa mwenye ufahamu, mwenye kutia moyo, na mwenye saburi kuelekea kila mtu aliyetumikia pamoja naye na kusafiri naye. Kwa kweli, waamini wenzake walimwitikia kwa roho ya Waebrania 13:7: “Wakumbukeni wale waliokuwa wakiwaongoza, waliowaambia neno la Mungu; tena, kwa kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, iigeni imani yao.”
Katika Desemba 30, 1992, Ndugu Milton G. Henschel alichaguliwa kuwa msimamizi wa Sosaiti wa tano,kumwandama Ndugu Franz.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Frederick W. Franz katika 1913
Kwenye kiwanda cha Sosaiti cha Myrtle Avenue katika 1920
Akiwa na Nathan H. Knorr katika Yankee Stadium katika 1953