Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Wale “wana wa Mungu” waliokuwa baba za Wanefili walikuwa nani?
Wale “wana wa Mungu” waliohusika walikuwa nani? Je! walikuwa watu waliokuwa waabudu wa Yehova (tofauti na ainabinadamu waovu kwa ujumla), kama vile wengine wanavyodai? Bila shaka la. Biblia hudokeza kwamba kufunga kwao ndoa pamoja na binti za wanadamu kulisababisha uchochezi wa uovu duniani. Noa na wana wake watatu, pamoja na wake zao, peke yao ndio waliokuwa na upendeleo wa Mungu na ni wao pekee waliohifadhiwa kupitia Gharika.—Mwanzo 6:9; 8:15, 16; 1 Petro 3:20.
Kwa hiyo, ikiwa “wana [hao] wa Mungu” walikuwa wanadamu tu, swali hili latokea, Kwa nini wazao wao walikuwa “watu wenye sifa” kuliko wana wa watu waovu, au wana wa Noa aliyekuwa mwaminifu? Pia, swali hili laweza kuulizwa, Kwa nini kufunga kwao ndoa pamoja na binti za wanadamu kutajwe kuwa jambo la pekee? Ndoa na kuzaa watoto kulikuwa kumetukia kwa miaka zaidi ya 1,500.
Kwa hiyo, ni lazima iwe kwamba wale wana wa Mungu wanaotajwa kwenye mwanzo 6:2 walikuwa malaika, “wana wa Mungu” wa roho. Usemi huo unatumiwa kuhusu malaika kwenye Ayubu 1:6; 38:7. Maoni hayo yanaungwa mkono na Petro, anayesema juu ya “roho waliokaa kifungoni, . . . wasiotii hapo zamani, uvumilivu wa Mungu ulipokuwa ukingoja, siku za Nuhu.” (1 Petro 3:19, 20) Pia Yuda aandika juu ya “malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu.” (Yuda 6) Malaika walikuwa na uwezo wa kujivika miili ya nyama wawe na umbo la kibinadamu, na malaika wengine walifanya hivyo ili kuleta ujumbe mbalimbali kutoka kwa Mungu. (Mwanzo 18:1, 2, 8, 20-22; 19:1-11; Yoshua 5:13-15) Lakini mbinguni ndiyo makao yawafaao watu wa roho, na malaika walio huko wana vyeo vya utumishi chini ya Yehova. (Danieli 7:9, 10) Kuacha makao hayo na kukaa duniani na kuacha utumishi waliogawiwa ili kuwa na mahusiano ya kimwili kungekuwa uasi dhidi ya sheria za Mungu, na upotevu.
Biblia hutaarifu kwamba wale malaika wasiotii sasa ni “roho waliokaa kifungoni,” wakiwa ‘wametupwa katika tartaro’ na ‘kuwekwa akiba kwa hukumu kwenye mashimo yenye giza zito.’ Hilo laonekana likionyesha kwamba wamezuiwa sana, wasiweze tena kujivika miili ya nyama kama walivyofanya kabla ya Furiko.—1 Petro 3:19; 2 Petro 2:4, NW; Yuda 6.
Wale “waliokuwa watu hodari zamani, watu wenye sifa” waliozaliwa katika ndoa hizo, hawakuwa watu wenye sifa kwa Mungu, kwani hawakuokoka Furiko, kama vile Noa na familia yake. Walikuwa “Wanefili,” wachokozi, wafidhuli, ambao bila shaka walisaidia kufanya hali ziwe mbaya zaidi. Baba zao wa kimalaika, wakijua jinsi mwili wa kibinadamu ulivyofanyizwa na wakiweza kujivika miili hiyo, hawakuwa wakiumba uhai, bali waliishi katika miili hiyo ya kibinadamu na, wakiishi pamoja na wanawake, walikuwa baba za watoto. Kwa hiyo, watoto wao, “watu hodari,” walikuwa mivyauso (wazao wa jamii yenye mchanganyiko) wasiostahili kuzaliwa. Yaonekana hao Wanefili hawakupata watoto baadaye.