Kupata Utajiri wa Kweli Katika Hong Kong
HONG KONG ni mahali ambapo fedha nyingi zaweza kuchumwa katika wakati mfupi—ikiwa hali zote zakufaa. Katika miaka yapata 40 iliyopita, koloni hiyo ya Uingereza imekua kutoka kuwa bandari isiyo na utendaji mwingi hadi kuwa kani ya kiuchumi yenye umaana sana si katika Esia Kusini-Mashariki tu bali pia kwenye mandhari ya biashara ya ulimwenguni pote.
Kiwango cha chini cha kodi huwavutia wafanya biashara wa kigeni na kuwaandalia kichocheo wale wafanyakazi wenye bidii wanaopatikana miongoni mwa wakaaji milioni sita wa Hong kong. Mahali pia panafaa, pakiwa lango katikati ya kusini mwa China na mkoa wa Esia na Pasifiki na mbali zaidi. Kukiwa na mifumo ya usafiri na mawasiliano na mfumo uliositawishwa vema wa uuzaji wa jumla na wa rejareja, Hong Kong yaweza kuitikia upesi mahitaji ya biashara ya kimataifa.
Mafanikio ya kiuchumi yameipa Hong Kong mojawapo viwango vya juu zaidi vya maisha ulimwenguni. Hata hivyo, je, ufanisi huo wote wa kimwili umewaletea wakaaji wa Hong Kong uradhi na furaha ya kudumu? La, lakini wengine wametafuta na kupata utajiri wa aina bora zaidi.
Walipata Utajiri wa Kiroho
Miongoni mwa wale waliopata utajiri wa kiroho wenye thamani kubwa sana ni Alfred aliyezaliwa Hong Kong. Alikuwa na kazi-maisha yenye mafanikio akiwa mkurugenzi wa biashara ya kimataifa yenye makao makuu katika Uingereza. Kama vile wengine wengi katika Hong Kong, mradi wake maishani ulikuwa kuchuma fedha nyingi, kuwa na nyumba yake mwenyewe, kula vizuri, na kuishi maisha mazuri. Akiwa na cheo na machumo hayo, alionekana kana kwamba alikuwa ametimiza hayo yote. Lakini je, alikuwa na furaha? “Nilipata kujionea mwenyewe kwamba fedha kwa kweli zina mipaka yazo,” Alfred akaomboleza. Alikuwa na wasiwasi daima juu ya ni muda mrefu kadiri gani fedha zake akibani zingeendelea kuwako ikiwa angepoteza kazi yake. Alipotumia wakati zaidi kazini, matatizo ya familia yalianza. Mke wake, Emily, alisononeka wakati mwana wao alipokufa kwa ghafula. “Nilitaka kujua alikokuwa ili niweze kumsaidia kwa njia fulani,” mke wake akasema. Kwa kuwa mke wake hakuweza kufanya lolote, alishuka moyo sana.
Baba ya Justina alikufa alipokuwa mchanga. Lakini kwa kujitahidi alihitimu chuo kikuu kimoja mashuhuri kiitwacho Hong Kong University. Hilo liliongoza kwenye kazi ya serikali. Katika Kikantoni hiyo huitwa gum fan woon, bakuli ya wali ya dhahabu—usalama wa kazi na mshahara mzuri. Hata hivyo, Justina hakuwa na furaha wala uradhi. Mara nyingi alijiuliza ni nini kusudi la uhai na wakati ujao ungeleta nini. Mume wake, Francis, alihisi pia kwamba uhai haukuwa na kusudi. Alijihisi kama kisehemu kidogo katika mashine kubwa mno, mtu asiye na maana, aliyekamatwa ndani ya utaratibu usio na mwisho.
Halafu kuna Ricky, meneja wa biashara fulani. Ingawa alikuwa akichuma fedha nyingi, alianza kuona sehemu nyingine ya maisha—ushindani mkali miongoni mwa wafanyakazi wenzake na matatizo katika ndoa yake. Fedha hazikuweza kumsaidia kusuluhisha matatizo hayo. Kulingana na maoni ya mke wake Wendy, kazi-maisha inayostahiki, fedha nyingi sana, na kuishi katika jamii iliyo thabiti kisiasi kulimaanisha usalama. Lakini maisha yake yaliyoonekana kuwa yenye usalama yangedumu muda mrefu kadiri gani? Hilo lilimsumbua kwa sababu uhalisi wa kifo ulimwacha akihisi kwamba uhai haukuwa na maana wala kusudi.
David pia asimulia hadithi yake. Elimu yake ya chuo kikuu ilimletea kazi nzuri na usalama wa kiuchumi, lakini yeye hakupata uradhi. Kwa nini? Aliamini sana mageuzi na falsafa, na aliamini kwamba uhai haupiti kuwapo kwa sasa. David alihisi kwamba hakuwa na lolote la kutazamia, na utajiri wake wote wa kimwili haukumzuia asijihisi akiwa hoi.
Ingawa kila mmoja wa watu hao alikuwa na malezi tofauti sana, walishiriki jambo moja. Wote walikuwa wametimiza lile walilofikiria lingeleta maisha yenye furaha na uradhi. Hata hivyo, walipofikia hatua ambapo walifikiri ndoto zao zingetimizwa, maisha yao yalikuwa matupu.
Kujitajirisha kwa Mungu
Hali ya Alfred, Justina, na wale wengine waliotajwa sasa hivi ilifanana sana na ile ya yule tajiri katika mfano wa Yesu. ‘Alijiwekea nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.’ (Luka 12:21) Hata hivyo, kwa furaha wao walipata jambo fulani bora zaidi—maisha yaliyojaa utajiri wa kweli. Ni lazima wale wanaotamani furaha na uradhi wa kweli “wasiutumainie utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha.” (1 Timotheo 6:17) Naam, kupata kumjua Mungu wa kweli, Yehova, na kumtumaini kulibadili maisha ya kila mmoja wa watu hao. Acheni tuone jinsi hayo yote yalivyotukia.
Alfred na Emily waliumia sana wakati mwana wao alipokufa kwa ghafula, na vitu vyao vyote vya kimwili havikuweza kutuliza uchungu wao. Walienda kanisani lakini bado walihisi utupu na kutoridhika. Halafu mmoja wa Mashahidi wa Yehova alikuwa mlangoni pao akauliza: “Ni nini tumaini la wanadamu kwa wakati ujao?” Alfred alijibu kulingana na yale aliyokuwa ameambiwa kanisani kuhusu mbingu na helo. Hata hivyo, alionyeshwa kutoka katika Biblia kwamba wafu “hawajui neno lo lote” na kwamba wale waliomo katika kumbukumbu la Mungu wamo katika kaburi la ujumla la ainabinadamu wakingojea ufufuo. (Mhubiri 9:5, 10; Yohana 5:28, 29) Hilo lilisikika kwa Alfred kuwa jambo la akili na kusababu kuzuri. Sasa aling’amua kwamba mwana wake hakuwa akiteseka mahali fulani lakini alikuwa akilala usingizi katika kifo, akiwa na tumaini labda la kuungana tena na familia yake kupitia ufufuo. Hiyo ilikuwa faraja na kitulizo kilichoje! Baadaye Alfred na mke wake walikubali funzo la Biblia nyumbani wakaanza kwenye njia ya kushika kwa uthabiti utajiri wa kweli unaotolewa na Biblia.
Justina alifadhaika aliposhindwa kupata miongoni mwa wafanyakazi wenzake roho ya hiari ya kusaidia kuwatunza watu. Akiwa Mkatoliki mchaji, alikata tamaa alipoona kwamba padri alikuwa akivuta sigareti na kwenda kucheza dansi, kama vile wanaume wengine. Halafu alikutana na Mashahidi wa Yehova akaanza kupata majibu ya Kimaandiko yenye kuridhisha kwa maswali mengi. Padri hakuwa amempa chochote ila maoni yake ya kibinafsi, na Justina hakuwa amefungua Biblia katika miaka 16, hata ingawa alikuwa mhudhuriaji-kanisa wa kawaida na alikuwa amekuwa mfanyakazi wa kidini kwa miaka 10.
Mashahidi walipojifunza Biblia pamoja na Justina na mume wake, Francis, mume huyo alivutiwa sana na umoja wao wa imani na tendo wa ulimwenguni pote. Francis alianza kusadikishwa kwamba Mungu ni halisi. Kwa vyovyote vile, ni Mungu wa kweli pekee aliye hai ambaye angeweza kuwa na uvutano huo juu ya kikundi cha watu cha kimataifa. Wenzi hao wa ndoa ni wenye furaha kama nini hivi kwamba wamepata utajiri wa kweli!
Ricky na Wendy walijua kwamba walihitaji kufanya jambo fulani walipoona kwamba walikuwa wakididimia polepole ndani ya matatizo mazito ya kibinafsi. Kwa kuwa wote wawili walikuwa wamekutana na Mashahidi wa Yehova wakati uliopita, kila mmoja wao alichukua hatua ya kwanza kuwatafuta tena. Kupitia jitihada nyingi, Ricky na Wendy walipata si masuluhisho tu yafaayo kwa matatizo yao bali pia utajiri wa kweli katika uhusiano wa kibinafsi na “Mungu mwenye furaha,” Yehova.—1 Timotheo 1:11, NW.
Maisha ya David yalibadilika pia wakati Mashahidi wa Yehova walipomtembelea. Aliwaruhusu warudi lakini akiwa na kusudi la kufunua makosa yao. Hata hivyo, hatimaye macho yake yalifumbuka, kwani alianza kuona kwamba Biblia ni sahihi kisayansi, kihistoria, na kwa njia nyinginezo. Yote hayo yalimsaidia David aione Biblia kuwa kitabu chenye kweli kilichompa kusudi la kweli maishani. Hilo lilikuwa badiliko lenye furaha na la kutajirisha kama nini kwake!
Kuwasaidia Wengine Wengi Kupata Utajiri wa Kweli
Miongoni mwa wale wakaaji wengi wa Hong Kong, Alfred, Emily, Justina, Francis, na wale wengine waliotajwa hapa ni wachache tu kati ya wale ambao wamepata utajiri wa kweli unaotia ndani kweli ya Biblia na imani katika Yehova Mungu. Katika 1992 Mashahidi wa Yehova 2,600 hivi walitumia jumla ya karibu muda wa saa 900,000 wakiwatembelea watu wa Hong Kong na kuongoza pamoja nao mafunzo ya Biblia nyumbani zaidi ya 3,800. Hata hivyo, mwendo wa maisha katika Hong Kong ni wa haraka, na watu wana shughuli nyingi. Kwa hiyo, kuongezea kule kufanya ziara za nyumba kwa nyumba, wapiga mbiu ya Ufalme wanapata mafanikio mengi katika kutoa ushahidi barabarani. Wao pia hukutana na watu kazini mwao kwa kuwatembelea wafanyakazi wa ofisini, wenye duka, wakulima, na wanaume wanaorudi kutoka safari za uvuvi katika Bahari ya China Kusini.
Yaweza kusemwa kwa kweli kwamba “mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache” katika Hong Kong. (Mathayo 9:37) Kwa sasa, uwiano wa Mashahidi kwa wakaaji ni 1 kwa 2,300. Wakitambua uharaka wa kazi ya mavuno, karibu 600 wa wale wahubiri wa Ufalme 2,600 wa huko ni mapainia, au wahubiri wa habari njema wa wakati wote. Mashahidi wa Yehova katika Hong Kong, kama wale wa kwingineko, hung’amua kwamba ‘baraka ya Yehova humtajirisha mtu.’ (Mithali 10:22) Kwa hiyo, wanajitahidi kuwasaidia watu wengi zaidi katika jumuiya hiyo yenye ufanisi kupata utajiri wa kweli.
[Ramani katika ukurasa wa 23]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
BAHARI YA CHINA KUSINI
CHINA
Hong Kong
Kilometa
Maili
15
15