Yehova Abadili Nyakati na Majira Katika Romania
MIELEKEO ya badiliko ilipitia kotekote katika Ulaya Mashariki katika 1989. Katika miezi kadhaa, serikali ambazo wakati mmoja zilikuwa kama ngome zisizoweza kushindwa zilipinduliwa moja baada ya nyingine. Pamoja na badiliko hilo la kisiasa kukaja mabadiliko ya kijamii, kiuchumi, na lenye kupendeza zaidi kwa Mashahidi wa Yehova, badiliko la kidini. Katika nchi moja baada ya nyingine, Mashahidi wa Yehova walipewa utambuzi wa kisheria, na wakarudishiwa uhuru wa kuendeleza utendaji wao wa kidini.
Lakini ilionekana kana kwamba mambo yangekuwa tofauti katika Romania. Serikali ilikuwa na mshiko imara sana juu ya watu hivi kwamba ilionekana kwamba mielekeo ya badiliko isingeiathiri sana. Mashahidi wa Yehova wa huko waliposikia yale yaliyokuwa yakitukia katika nchi nyingine za Ulaya Mashariki, walijiuliza hivi, ‘Je! tutapata kufurahia uhuru wa ibada wakati wowote kabla ya Har–Magedoni?’ Mioyo yao ilitamani wakati wangeweza kukusanyika kwenye mikutano ya Kikristo pamoja na ndugu na dada zao wa kiroho, kuhubiri habari njema hadharani, na kujifunza vichapo vya Biblia waziwazi, bila kuwa na tatizo la kuvificha wakati wote. Hayo yote yalionekana kuwa kama ndoto tu.
Halafu ndoto hiyo ikawa jambo halisi! Hilo lilitukia katika Desemba 1989. Kwa mshangao wa kila mtu, utawala wa Ceauşescu ukapinduliwa kwa ghafula. Kwa ghafula wale Wakristo wakapata kitulizo. Katika Aprili 9, 1990, Mashahidi wa Yehova walitambuliwa kisheria kuwa tengenezo la kidini katika Romania. Yehova alikuwa amebadili nyakati na majira kwa ajili ya wale Mashahidi wa hapo wenye bidii 17,000.—Linganisha Danieli 2:21.
Historia Ndefu
Katika 1911, Carol Szabo na Josif Kiss walirudi Romania kutoka United States, ambako walikuwa wamejifunza kweli ya Biblia na walikuwa wameweka wakfu maisha zao ili kufanya mapenzi ya Yehova. Walitaka kushiriki habari njema pamoja na watu wa nchi yao. Mara walipokuwa Romania, walianza kuhubiri mara moja. Wakati Vita ya Ulimwengu 1 ilipoanza, walikamatwa kwa ajili ya lile walilokuwa wakifanya. Bado, mbegu za Ufalme ambazo walikuwa wamepanda zilianza kuwa na matokeo. Kufikia 1920, wakati kazi hiyo ilipopangwa upya kitengenezo, kulikuwa wahubiri wa Ufalme karibu 1,800 katika Romania.
Kufikia wakati huo roho ya mapinduzi iliyowaka sana katika mabara ya Balka ilikuwa ikizidi kuhisiwa katika Romania, na misukosuko ilikuwa mingi. Zijapokuwa nyakati hizo ngumu, ndugu zetu wa kiroho waliendelea na kazi. Katika 1924 Watch Tower Society ilifungua ofisi kwenye Barabara ya 26 Regina Maria katika Cluj-Napoca ili kutunza kazi katika Romania, Hangari, Bulgaria, Yugoslavia, na Albania.
Lakini, hali ya kisiasa ilizidi kuwa yenye mkazo mwingi sana, na zaidi ya taabu kutoka kwa wenye mamlaka, kulikuwa taabu ndani ya tengenezo. Kitabu 1930 Year Book charipoti hivi: “Kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu wa mmoja aliyekuwa ametumwa na Sosaiti, akina ndugu wametawanywa na uhakika wao umedhoofishwa sana. Sosaiti imekuwa ikitazama ili kupata fursa ya kuanzisha kazi upya tena katika nchi hiyo, lakini wenye mamlaka wa huko wanakataza kila jambo, na ni lazima tungojee mpaka Bwana anapofungua njia ifaayo zaidi.” Halafu, katika 1930, Martin Magyarosi, Shahidi Mromania aliyebatizwa katika 1922, akawekwa akiwa mtumishi mpya wa tawi, na ofisi hiyo ikahamishwa baadaye hadi Barabara ya 33 Crişana, Bucharest. Mwishoni, baada ya shindano refu, Sosaiti ilisajiliwa kuwa shirika la kisheria katika Romania katika 1933.
Hali Ngumu Ziliendelea
Majaribu makali yaliendelea kuwajia Mashahidi katika Romania. Kitabu 1936 Year Book charipoti hivi: “Bila shaka ndugu katika sehemu nyingine za dunia hawafanyi kazi katika hali ngumu sana kuliko akina ndugu katika Rumania.” Ijapokuwa dhiki hiyo yote, ripoti za utumishi za 1937 zilitaja makundi 75 yenye wahubiri 856 katika Romania. Kwenye Ukumbusho, 2,608 walikuwapo.
Vita ya Ulimwengu 2 ilipoanza, Romania ilihusika pia. Katika Septemba 1940, Jemadari Ion Antonescu alitwaa mamlaka katika serikali akaanza utawala uliofanana na ule wa Hitla. Matendo yenye kuhofisha yalikuwa ya kawaida sana. Mamia ya akina ndugu zetu walikamatwa, wakapigwa, na kuteswa. Ndugu Magyarosi alikamatwa katika Septemba 1942, lakini aliweza bado kuratibu kazi kwa ajili ya eneo la Transylvania akiwa gerezani.
Mnyanyaso uliendelea wakati vikosi vya Hitla vilipopitia kotekote nchini katika 1944. Ripoti moja kutoka Bucharest ilisimulia hali chini ya utawala wa Nazi: “Mashahidi wa Yehova katika nchi hii walinyanyaswa vibaya sana. Walifungwa gerezani pamoja na Wakomunisti, walishtakiwa na makasisi waliomwunga mkono Hitla kuwa wabaya kuliko Wakomunisti, wengi wetu tulihukumiwa ama kifungo cha miaka 25, hadi vifungo vya maisha, ama kifo.”
Hatimaye vita iliisha, na katika Juni 1, 1945, ofisi ya Sosaiti katika Bucharest ikaanza utendaji tena. Yajapokuwa magumu ya kupata karatasi, wafanyakazi wenye kujitoa walipiga chapa vijitabu zaidi ya 860,000 na nakala za Mnara wa Mlinzi zaidi ya 85,000 katika Kiromania na Kihangari. Yehova alibariki sana kazi yao yenye bidii. Kufikia 1946 wapya karibu 1,630 walikuwa wamebatizwa. Jambo kuu la mwaka huo lilikuwa ule mkusanyiko wa kitaifa uliofanywa katika Bucharest katika Septemba 28 na 29. Makasisi walijaribu sana kusumbua na kuzuia mkusanyiko huo, lakini hawakufanikiwa, na karibu watu 15,000 walihudhuria hotuba ya watu wote. Ilikuwa mara ya kwanza kwa akina ndugu katika Romania kuweza kuwa na mkusanyiko kama huo.
Sosaiti ilimtuma Ndugu Alfred Rütimann kutoka tawi la Uswisi kwenda Romania. Katika Agosti 1947 aliweza kusema na ndugu zaidi ya 4,500 katika mahali-mahali 16, akiwajenga kwa ajili ya yale yaliyokuwa mbele. Upesi mibano ingewajia Mashahidi tena, wakati huu kutoka kwa utawala wa Kikomunisti. Katika Februari 1948 wenye mamlaka walikataza utendaji wetu wa kuchapisha na kuhubiri. Halafu, katika Agosti 1949, ofisi kwenye Barabara ya 38 Alion ilishambuliwa. Baadaye ndugu wengi, kutia na Ndugu Magyarosi, walikamatwa. Wakati huu, wakishtakiwa kuwa mabeberu, walifungwa gerezani au katika kambi za kazi ngumu. Kwa miaka 40 iliyofuata, kazi ilipigwa marufuku, na Mashahidi wakateseka sana. Taabu zilizochochewa na maadui ndani ya tengenezo ziliongezea msononeko huo. Hatimaye, utawala wa Ceauşescu ukapinduliwa katika 1989, nao wakawa huru! Wangefanya nini sasa na uhuru wao?
Kuhubiri Peupe Tena
Mashahidi hawakupoteza wakati wowote. Walianza mara moja kuhubiri nyumba kwa nyumba. Lakini hilo halikuwa rahisi kwa wale ambao kwa miaka kadhaa walikuwa wameendelea kufanya kazi hiyo kichinichini kwa moyo mkuu kwa kutoa ushahidi wa vivi hivi. Walikuwa na wasiwasi sasa kwa kuwa wangeweza kuhubiri peupe. Wengi wao hawakuwa wamefanya hivyo kabla ya hapo, na mara ya mwisho ambao yeyote wao alikuwa amehubiri nyumba kwa nyumba ilikuwa miaka ya mwisho-mwisho ya 1940. Wanapata matokeo ya aina gani? Acheni tuone.
Mahali pafaapo zaidi pa kuanzia ni katika jiji kuu, Bucharest, ambalo lina wakaaji milioni 2.5. Miaka miwili iliyopita, kulikuwa makundi manne tu katika jiji hilo. Sasa kuna makundi kumi, na watu zaidi ya 2,100 walihudhuria mwadhimisho wa Ukumbusho wa 1992. Mafunzo ya Biblia nyumbani mengi yenye kufanya maendeleo yakiwa yanaongozwa, makundi mengine mapya huenda yakafanyizwa karibuni.
Craiova ni jiji lenye wakaaji karibu 300,000, katika sehemu ya kusini-magharibi mwa nchi. Kufikia 1990, kulikuwa Mashahidi karibu 80 tu katika jiji lote. Halafu roho ya upainia ikaongezeka, na kazi ikasonga mbele. Katika 1992 peke yake, watu 74 walibatizwa, na mafunzo ya Biblia zaidi ya 150 yanaongozwa. Kukiwa na wahubiri zaidi ya 200, wanatafuta kwa hamu mahali pafaapo pa Jumba la Ufalme.
Katika Tirgu-Mures, dada mmoja aliye Shahidi pamoja na ndugu wawili walimwendea padri wa dini ya Orthodoksi ili jina la dada huyo liondolewe kutoka katika vitabu vya kanisa. Alipopata kujua kusudi la ziara yao, padri huyo aliwakaribisha ndani, wakawa na mazungumzo mazuri. Kisha padri huyo akasema hivi: “Ninawaonea wivu lakini si kwa njia mbaya. Tunapaswa kuwa tukifanya kazi mnayofanya. Ni vibaya sana kwamba Kanisa Orthodoksi ni jitu linalolala usingizi!” Alikubali kuchukua broshua Je! Uamini Utatu? na nakala moja ya Mnara wa Mlinzi. Dada huyo anafurahi kwamba yeye si sehemu tena ya hilo “jitu linalolala usingizi.”—Ufunuo 18:4.
Ni jambo la maana kwamba wengi wa wale wanaojifunza kweli leo ni vijana. Kwa nini? Yaonekana walitazamia mengi kutokana na badiliko la serikali, lakini wakafadhaishwa. Wanafurahia kujifunza kwamba ni Ufalme wa Yehova tu unaoweza kuleta suluhisho lenye kudumu kwa matatizo yetu.—Zaburi 146:3-5.
Mambo Makubwa Yanatukia Katika Mahali-Mahali Padogo
Ocoliş ni kijiji kidogo katika kaskazini mwa Romania. Katika 1920 mtu mmoja aitwaye Pintea Moise alirudi kutoka vitani Urusi, ambako alikuwa amekamatwa akiwa mfungwa wa vita. Alikuwa amekuwa Mkatoliki wakati mmoja, lakini kabla ya kurudi kwake alikuwa Mbatisti. Majuma matatu baadaye, Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, walimtembelea. Baada ya ziara hiyo, alijulisha hivi: “Sasa nimeipata kweli kuhusu Mungu!” Kufikia 1924 kulikuwa kikundi cha watu 35 katika Ocoliş.
Leo, miongoni mwa wale wakaaji 473, kuna wahubiri wa Ufalme 170 huko. Kila mhubiri ana karibu nyumba mbili ambazo amegawiwa kuwa eneo lake, na wao pia huhubiri katika vijiji vinavyozunguka hapo. Bado, wana matazamio mazuri. Hivi karibuni walijenga Jumba la Ufalme zuri lenye viti 400. Kazi yote ilifanywa na Mashahidi wa huko.
Valea Largă ni mahali ambapo Ndugu Szabo na Kiss walipokaa katika 1914. Katika 1991, miongoni mwa wakaaji walo 3,700, kulikuwa makundi manane na wahubiri wa Ufalme 582. Kwenye Ukumbusho wa 1992, watu 1,082 walikuwapo—karibu mtu 1 kati ya 3 katika bonde hilo.
Mapainia wa Pekee Waitayarisha Njia
Mapainia wa pekee wana sehemu kubwa katika kupeleka habari njema kwa watu katika maeneo ya mbali zaidi. Mara uhuru wa kuhubiri ulipotolewa, Ionel Alban alianza kuhubiri katika majiji mawili, akitumia siku mbili kila juma katika Orşova na siku tano katika Turnu-Severin.
Hakukuwa Mashahidi katika Orşova wakati ambapo Ionel aliwasili. Juma la kwanza, alianza funzo la Biblia pamoja na mvulana mwenye umri wa miaka 14. Kijana huyo alifanya mabadiliko mengi sana baada ya miezi miwili hivi kwamba rafiki na jirani mmoja pia wakaanza kujifunza. Jirani huyo, Roland, aliyekuwa Mkatoliki alifanya maendeleo ya ajabu. Baada ya mwezi mmoja na nusu tu, aliambatana na Ionel katika kazi ya kuhubiri, na katika miezi mitano akabatizwa. Aliingia utumishi wa wakati wote mara iyo hiyo. Mama yake pia alianza kujifunza akabatizwa kwenye “Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1992. Sasa kuna wahubiri kumi katika Orşova, nao wanaongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 30.
Mtu wa kwanza kukubali kweli katika Turnu-Severin alikuwa mpokezi kwenye hoteli ambako Ionel alikaa. Baada ya miezi miwili mtu huyo alikuwa mhubiri asiyebatizwa, na akabatizwa baada ya miezi mitatu. Sasa yeye ni mmoja wa wale wahubiri 32 wa huko wanaoongoza jumla ya mafunzo ya Biblia nyumbani 84.
Painia mwingine wa pekee, Gabriela Geica, alitumikia akiwa painia wa kawaida hata wakati kazi yetu ilipokuwa chini ya marufuku. Tamaa yake ilikuwa ni kufanya kazi mahali palipokuwa na uhitaji mkubwa zaidi. Alipewa mgawo wa eneo kubwa mno. Nyakati nyingine alisafiri kutoka kilometa 100 hadi kilometa 160 ili kuwatembelea watu waliopendezwa. Jiji moja alikofanyia kazi lilikuwa Motru, ambako kulikuwa Mashahidi wanne tu. “Kwa sababu ya ongezeko la utendaji katika Motru, mapadri na vikundi vingine vya kidini walianza kutupinga,” yeye asimulia. “Walishawishi meya na polisi waweke mbano juu ya familia zilizonipa makao. Ziliniondosha, kwa hiyo karibu kila miezi miwili nililazimika kutafuta mahali pa kukaa.”
Gabriela alianza funzo pamoja na mtu katika Orşova, ambaye hakuamini kuwako kwa Mungu, na aliyesema kwamba hakupendezwa na dini wala Biblia. Lakini baada ya miezi minne tu ya kujifunza, mwanamke huyo alianza kuitetea Biblia. Ingawa mume wake alimfungia nje usiku na akatisha kumtaliki au kumwua, yeye alidumisha uaminifu-maadili wake. Hata kabla ya yeye kubatizwa, aliongoza mafunzo ya Biblia kumi.
Mataraja Mazuri Ajabu Yako Mbele
Katika Agosti 1992, Romania ilifika kilele cha wahubiri 24,752 katika makundi 286. Hudhurio la Ukumbusho lilikuwa zaidi ya 66,000. Kwenye ile ofisi ndogo ya tawi katika Bucharest, wafanyakazi 17 wanajitahidi kadiri wawezavyo ili kutunza mahitaji ya kiroho ya ndugu zao. Wanatazamia hivi karibuni kuanza ujenzi wa tawi lililo kubwa zaidi.
Mashahidi wa Yehova katika Romania hawawezi kuzuia mshangao wao juu ya yale mabadiliko yote ya haraka katika miaka michache ambayo imepita. Wanamshukuru Yehova Mungu kwamba wao ni sehemu ya lile kundi la kimataifa lenye jina lake na linaloongoza watu kwenye ujuzi sahihi juu yake na kusudi lake lisiloweza kubadilika. Baada ya miaka mingi sana ya ugumu na mnyanyaso, wanamshukuru Yehova kama nini kwamba yeye kwa kweli amebadili nyakati na majira katika Romania!
[Ramani katika ukurasa wa 23]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
HANGARI
ROMANIA
Bucharest
Cluj-Napoca
Craiova
Tirgu-Mures
Orşova
Turnu -Severin
Motru
Turda
BULGARIA
[Picha katika ukurasa wa 24,25]
1. Karibu Mashahidi 700 wakiwa wamekusanyika msituni katika 1947
2. Kikaratasi cha mwaliko kwenye hotuba ya watu wote katika 1946
3. Kikusanyiko katika Alba Iulia katika 1992
4. Kutoa ushahidi leo katika Cluj-Napoca
5. Jumba la Ufalme karibu na Turda
6. Familia ya Betheli katika Bucharest