Je! Wakumbuka?
Je! umeyaona matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi kuwa yenye mafaa kwako? Kwa hiyo kwa nini usitahini kumbukumbu lako kwa maswali yafuatayo:
▫ Wazo lolote lisilo la kiadili linapoingia akili yetu bila kutazamiwa, tunapaswa kufanya nini?
Tunapaswa kubadili habari hiyo kiakili, kufanya matembezi, kusoma kitu fulani, au kufanya kazi fulani ya nyumbani. Sala pia ni msaada wenye nguvu katika hali ya jinsi hiyo. (Zaburi 62:8)—4/15, ukurasa 17.
▫ Kwa nini vijana wawe waangalifu kuhusu aina ya muziki wanaosikiliza?
Muziki una nguvu ya kuchochea hisia za moyoni, ya kusisimua, na ya kuvuta. Kwa kuwa nyimbo nyingi zinazopendwa sana zina idadi yenye kushangaza ya vidokezo vya ngono na marejezo yaliyofichwa ya ukosefu wa adili, ni rahisi kuona kwamba ni lazima mtu awe mwangalifu sana katika kuchagua rekodi, kanda, na diski.—4/15, kurasa 20-1.
▫ Ni nini kinachomaanishwa na “kuja [kuwapo, NW] kwake Bwana wetu Yesu Kristo”? (1 Wathesalonike 5:23)
Hilo larejezea kuwapo kwa kifalme kusikoonekana kwa Bwana Yesu Kristo akiwa Mfalme, tangu 1914, na baada ya kutawazwa kwake mbinguni. (Zaburi 110:1, 2)—5/1, ukurasa 11.
▫ Ni kusudi jipi lililotimizwa kwa Yehova kusafisha hekalu lake la kiroho? (Malaki 3:1-4)
Yehova alitaka hekalu lake liwe katika hali safi ili waabudu wengi wenye matumaini ya kidunia walipoletwa huko, wangepata mahali ambapo enzi yake kuu ya ulimwengu wote mzima inastahiwa, mahali ambapo jina lake la kimungu linatakaswa, na mahali ambapo sheria zake zenye uadilifu zinatiiwa.—5/1, ukurasa 16.
▫ Ni nini vile “vitu” ambavyo Kristo Yesu ampa mtumwa wake aliyewekwa? (Mathayo 24:45-47)
Hivyo “vitu” vinarejezea faida zote za kiroho ambazo zimekuwa mali ya Kristo duniani kuhusiana na mamlaka yake akiwa Mfalme wa kimbingu. Hiyo ingetia ndani ule utume wa kufanya wanafunzi wa Kristo kutoka watu wa mataifa yote. (Mathayo 28:19, 20)—5/1, ukurasa 17.
▫ Wazee Wakristo wa kutaniko huonyeshaje “hiari” katika uchungaji, kulingana na himizo la Petro kwenye 1 Petro 5:2? Mzee Mkristo wa kutaniko anayewajali kondoo atafanya uchungaji wake kwa hiari, kwa kujichagulia mwenyewe, chini ya mwelekezo wa yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo. Kutumikia kwa hiari humaanisha pia kwamba mchungaji Mkristo hujitiisha kwa mamlaka ya Yehova na kudhihirisha staha kwa mpango wa kitheokrasi.—5/15, ukurasa 20.
▫ Yesu alimaanisha nini aliposema kwamba yeyote aliyemfuata alihitaji ‘kujikana mwenyewe’? (Mathayo 16:24)
‘Kujikana mwenyewe’ kunamaanisha kwamba unajitoa kwa Yehova kuwa mali yake. (1 Wakorintho 6:19, 20) Kunamaanisha kwamba unaishi ili kumpendeza Mungu, wala si kujipendeza mwenyewe. (Warumi 14:8)—6/1, ukurasa 9.
▫ Ni nini kinachohitajiwa kumfurahisha mtu?
Kufurahia uhusiano mzuri na Yehova na kuwa na shughuli nyingi katika utumishi wake huleta furaha ya kweli katika maisha ya mtu.—6/1, ukurasa 22.
▫ Kwa nini Yehova alimruhusu Abrahamu aseme naye kwa uhuru hivyo kuhusu kusudi Lake la kuangamiza Sodoma? (Mwanzo 18:22-32)
Sababu moja ilikuwa kwamba Abrahamu alikuwa rafiki ya Mungu. (Yakobo 2:23) Zaidi ya hayo, Yehova alitambua hisia za Abrahamu zenye kusononeka (maumivu ya moyoni). Mungu alijua kwamba mpwa wa Abrahamu Loti, aliishi Sodoma na kwamba Abrahamu alihangaikia sana usalama wa Loti. Kwa sababu hizo Yehova alikuwa na nia ya kujibu maswali ya Abrahamu kuhusu kusudi Lake la kuangamiza Sodoma.—6/15, ukurasa 16.
▫ Je! yale Mapinduzi Makubwa ya Kidini ya Kiprotestanti ya karne ya 16 yalitia alama kurudi kwa Ukristo wa kweli?
La, hayakufanya hivyo! Badala ya kurudisha Ukristo wa kweli, Mapinduzi hayo Makubwa ya Kidini yalitokeza makanisa mengi ya kitaifa au ya kieneo ambayo yamejipendekeza kwa serikali za kisiasa na kuziunga mkono kwa bidii katika vita vyazo.—7/1, kurasa 10-11.
▫ Ni nini zile “hazina mbinguni” ambazo Yesu alisema juu yazo kwenye Mathayo 6:20?
Hizo ni hazina ambazo hazififii kamwe, kutia ndani kuwa na jina zuri na Yehova na rekodi ya utumishi mwaminifu wa Kikristo. Hizo ni miongoni mwa mambo ambayo Yehova hasahau kamwe. (Waebrania 6:10)—7/1, ukurasa 32.
▫ Petro anataja sifa zipi ambazo ni sehemu muhimu ya imani yetu? (2 Petro 1:5-7)
Petro alisema kwamba wema-adili, ujuzi, kujidhibiti, uvumilivu, ujitoaji kimungu, shauku ya kidugu, na upendo zinapaswa kutiwa katika imani yetu.—7/15, ukurasa 13.
▫ Watumishi wa Mungu wanapata onyo gani katika lile simulizi la dhambi ya Daudi pamoja na Bath-sheba? (2 Samweli 11:2-4) Ingawa alikuwa huru kufurahia raha ndani ya ndoa yake mwenyewe, Daudi aliruhusu tamaa ya ngono haramu ikue. Akiona jinsi mke wa Uria alivyokuwa mwenye kuvutia, hakudhibiti mawazo—na matendo yake—ya kupata raha haramu naye. Jambo lilo hilo laweza kumpata mtumishi yeyote wa Mungu ikiwa haepuki aina hiyo ya pupa. (Yakobo 1:14, 15)—8/1, ukurasa 14.