Kuhubiri kwa Uvumilivu Katika Bara la Barafu na Moto
ICELAND imo katika Atlantiki Kaskazini karibu katikati ya Amerika Kaskazini na Ulaya. Ingawa iko chini tu ya Kizingo cha Aktiki, hali yayo ya hewa ni ya kiasi kuliko vile huenda ikatazamiwa, kwa sababu ya matokeo yenye kutia joto ya Mkondo wa Ghuba. Iceland imeitwa bara la barafu na moto kwa sababu lina barafuto (barafu kama mto) iliyo kubwa zaidi katika Ulaya na ni mojawapo sehemu zenye volkeno amilifu zaidi ulimwenguni. Chemchemi moto na solfatara zalo, sehemu za volkeno zinazotoa mivuke yenye joto na gesi zenye sulfa, zinajulikana sana.
Wale wakaaji 260,000 wa kisiwa hiki cha Ulaya ambacho ni cha pili kwa ukubwa ni wazao wa Maharamia wa zamani kutoka kaskazini mwa Ujerumani, waliofanyiza makao hapa zaidi ya miaka 1,100 iliyopita. Kwa msingi Kiiceland kinafanana na Kijerumani cha Kaskazini cha Zamani, ile lugha ya Skandinavia ya enzi ya wale Maharamia wa zamani kutoka kaskazini mwa Ujerumani. Imeendelea bila kubadilika sana kwa sababu Waiceland walipenda sana kusoma visa vyao vya zamani, vilivyoandikwa hasa katika karne ya 13.
Kufikia karne ya 16, Biblia ilianza kutafsiriwa katika Kiiceland. “Agano Jipya” lilitokea katika 1540 na Biblia nzima ikatokea kufikia 1584. Zaidi ya asilimia 90 ya watu ni wa Evangelical Lutheran Church, ambayo ndiyo dini rasmi ya Serikali. Ingawa Biblia inapatikana katika karibu kila nyumba, watu wachache huamini kwamba hilo ndilo Neno la Mungu. Waiceland wengi wana maoni ya hiari juu ya dini, na, kwa ujumla, ni watu wenye kufikiri wasiotegemea maoni ya wengine.
Habari Njema Zafikia Iceland
Waiceland wa kwanza waliosikia habari njema za Ufalme walikuwa wakiishi Kanada wakati huo. Mmoja wao alikuwa Georg Fjölnir Lindal. Wazazi wake walitoka Iceland, naye alisema Kiiceland. Muda mfupi baada ya kuweka maisha yake wakfu kwa Yehova Mungu, akawa mhubiri wa habari njema wa wakati wote. Katika 1929, alipokuwa na miaka 40, alipeleka habari njema kwa watu katika bara hilo la barafu na moto.
Hiyo ilikuwa kazi kubwa kama nini kwa mtu mmoja! Iceland ni karibu kilometa 320 kutoka kaskazini hadi kusini na kilometa 500 hivi kutoka mashariki hadi magharibi. Pwani, kutia na hori na ghuba, ni karibu kilometa 6,400 kwa upana. Wakati huo, hakukuwa barabara halisi wala magari au njia nyinginezo za kisasa za kusafiri. Lakini, Ndugu Lindal alieneza kisiwa chote katika miaka kumi, akaangusha maelfu ya vitabu. Alisafiri kando ya pwani kwa mashua, na alipozuru mashamba ya barani, alitumia farasi wawili, mmoja wa kumbeba na mwingine wa kubeba fasihi yake na mali zake.
Kwa karibu miaka 18, Ndugu Lindal alikuwa ndiye Shahidi pekee katika Iceland. Ijapokuwa kazi yake ngumu, hakumwona yeyote akichukua msimamo kwa ajili ya Ufalme wakati huo. Kukaa kwake huko kwa muda mrefu, na kwa upweke kuliisha Machi 25, 1947, wakati wamishonari wa kwanza wa Watchtower Bible School of Gilead walipowasili. Waweza kuwazia furaha yake wakati Yehova alipojibu sala zake hatimaye za kupata wafanyakazi zaidi kwa ajili ya mavuno. (Mathayo 9:37, 38) Ndugu Lindal aliendelea na utumishi wake katika Iceland hadi aliporudi Kanada katika 1953.
Wafanyakazi Zaidi kwa Ajili ya Mavuno
Wamishonari waliokuja katika 1947 walikuwa ndugu wawili Wadenmark. Wamishonari zaidi waliwasili miaka miwili baadaye. Walipoendeleza kazi ya kuhubiri pamoja na marafiki wachache waliokuwa wamehamia Iceland, maelfu ya vichapo viligawanywa. Waiceland wengi ni wasomaji wenye bidii, lakini si wengi walioitikia habari njema. Baada ya miaka 27 ya kupanda na kutia maji, hao ndugu wenye subira walianza kuona matunda ya kazi yao ngumu. Katika 1956 wapya saba walichukua msimamo wao kwa ajili ya Ufalme, wakaweka wakfu maisha zao kwa Yehova.
Katika miaka kumi iliyopita, idadi ya wahubiri wa Ufalme imeongezeka zaidi ya mara mbili. Sasa, kuna makutaniko saba na kikundi kimoja cha mbali, jumla ya wapiga mbiu ya habari njema 280. Acheni tusafiri kuzunguka kisiwa hiki ili kutembelea makutaniko hayo.
Kuzunguka Jiji Kuu
Ndugu na dada waliovumilia miaka hiyo yote wamethawabishwa sana. Sasa kuna makutaniko mawili yenye mafanikio katika Reykjavík, jiji kuu. Yanakutana katika Jumba la Ufalme zuri lililo katika jengo moja na ofisi ya tawi, iliyowekwa wakfu katika 1975.
Friðrik na Ada walikuwa miongoni mwa wale saba waliobatizwa huko nyuma katika 1956. “Nakumbuka kwamba tulikuwa tukifanya mikutano katika chumba kidogo cha orofa ya juu kabisa katika nyumba ambamo wamishonari waliishi,” asema Friðrik. “Kulikuwa nafasi ya viti 12, lakini nyakati fulani, wakati wengi zaidi ya kawaida walipohudhuria, tulifungua mlango kuelekea chumba kidogo kilichofuata. Ni tofauti kama nini leo wakati makutaniko mawili yanapolijaza Jumba la Ufalme!”
Friðrik alisimamia Idara ya Utumishi wa Chakula wakati makusanyiko ya kwanza yalipofanywa. “Nilifanya sehemu kubwa ya kazi nikiwa peke yangu, na wakati uo huo, ilikuwa kawaida kwangu kuwa na sehemu tatu au nne kwenye programu kila siku. Nilipokuwa nikifanya kazi jikoni, nilivaa aproni. Wakati ulipofika wa kutoa hotuba, nilivaa koti langu na kuharakisha kwenda kwenye jumba. Nyakati kadhaa akina ndugu walilazimika kunikumbusha niivue aproni. Sasa tuna watu kuanzia 400 hadi 500 wanaohudhuria makusanyiko, kutia na wazee wema wanaoshiriki katika kushughulikia sehemu-sehemu za programu. Pia kuna wengi wenye nia ya kusaidia katika Idara ya Utumishi wa Chakula.”
Kutaniko lililo karibu zaidi ya Reykjavík ni Keflavík, karibu kilometa 50 kuelekea magharibi. Kusafiri kwa gari kunatupitisha katika nyanja zenye lava. Asilimia kumi ya Iceland imefunikwa kwa lava. Mimea ya kwanza kutokea katika nyanja hizo inatia ndani kuvumwamba na mosi, lakini katika nyanja zenye lava za zamani zaidi, utaona beri za kondeni na vichaka vifupi.
Kutaniko katika Keflavík lina wahubiri 19 nalo lilifanyizwa katika 1965. Uwanja wa ndege wa kimataifa, na kituo cha kijeshi cha U.S., viko karibu na hapo. Ingawa Mashahidi hawajapata kamwe kufanya kazi ya nyumba kwa nyumba kwenye kituo hicho chenyewe, mafunzo ya Biblia mengi yameongozwa humo, na watu kadhaa wamejifunza kweli.
Kutaniko jingine liko katika Selfoss, kilometa 55 mashariki mwa Reykjavík. Hapa twaona mashamba ya kijani kibichi yenye ng’ombe na kondoo, kutia na shamba la ng’ombe wa maziwa ambalo ndilo kubwa zaidi katika Iceland. Njiani, twapita Hveragerði, mji mdogo katika bonde lenye kupendeza sana. Kwa mbali twaona safu za mvuke kutoka katika chemchemi moto zilizoko kotekote bondeni. Hii ni mojawapo maeneo makubwa zaidi yenye kutokeza joto ardhini, na majumba mengi ya kioo ya kupandia mimea yamejengwa ili kutumia nyenzo hizo na kuandaa nyanya, matango na maua mbalimbali yenye kupandwa ndani ya majumbo ya kioo yenye joto.
Katika eneo hili kuna kutaniko dogo lakini lenye bidii la wahubiri wa Ufalme 19. Sigurður na Guðrún Svava walihama kutoka Reykjavík ili kuunga mkono kikundi hiki kidogo karibu na wakati kutaniko hilo lilipofanyizwa katika 1988. Sigurður pekee ndiye mzee hapa. Kabla ya yeye kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova karibu miaka kumi iliyopita, alikuwa mwanamuziki mashuhuri, akipiga ngoma katika beni mbalimbali. Leo, anajiruzuku akiwa msafishaji wa madirisha, na pia yeye hufundisha muziki. Mtindo-maisha wake akiwa mtumbuizaji ulimletea matatizo mengi, kama vile matumizi mabaya ya madawa, kunywa kileo sana, na ndoa iliyovunjika. Sasa ameridhika kama nini akiwa na kusudi maishani na kumtumikia Yehova!
Hadi Mwisho wa Sehemu ya Mashariki
Tukiondoka Selfoss, twaanza safari ya gari ya kilometa 680, hasa kwenye barabara nyembamba na zenye changarawe zisizo laini. Tunaelekea kutaniko lifuatalo, katika mji wa Reyðarfjörður, kwenye pwani ya mashariki. Katika muda wa nusu saa, twaona Hekla, volkeno maarufu zaidi ya Iceland. Imelipuka mara nne katika karne hii.
Katika 1973 mlipuko wa volkeno wenye kutazamisha ulitokea kwenye Vestmannaeyjar (Visiwa Westmann). Wakaaji wote waliokuwa 5,300 hivi walihamishwa kwa usalama hadi bara kuu katika muda wa saa chache tu. Baada ya mji huo kurudishwa upya, wengi wa wakaaji walirudi kidogokidogo. Sasa Mashahidi wawili huishi huko na kuhubiri habari njema kwa watu katika jumuiya hiyo ndogo. Tukienda kwa gari kwa muda wa saa mbili nyingine, tunafurahia mandhari yenye kupendeza ya Vatnajökull yenye fahari, ambayo kwa ukubwa hupita kwa mbali barafuto zote za Iceland, ikiwa na eneo la kilometa za mraba 8,300. Njiani, twapita pia maporomoko ya maji na mito mingi yenye kupendeza.
Tukiwa tumetumia muda wa saa kumi barabarani, twafika kule tunakoenda. Katika Reyðarfjörður twakutana na wale wahubiri 12 wa kutaniko lililo changa zaidi katika Iceland. Hakuna Mashahidi waliokuwa wakiishi katika eneo hilo hadi makao ya mishonari yalipofunguliwa katika sehemu ya mwisho ya 1988. Kjell na Iiris, mume wa mke wamishonari Waswede ambao wametumikia katika Iceland tangu 1963, wamepewa mgawo wa kufanya kazi miongoni mwa wale watu 15,000 katika eneo hili la mashambani. Wengi huishi katika vijiji vidogo vya kuvua samaki karibu na pwani, inayonyooka kilometa 500 hivi.
Kjell asimulia hivi: “Hakuna shaka kwamba Yehova amebariki sana kazi ya Ufalme katika sehemu hii ya Iceland. Katika Januari 1, 1993, kutaniko lilifanyizwa, na tunaongoza mafunzo mengi ya Biblia pamoja na watu mmoja-mmoja wanaofanya maendeleo mazuri. Ingawa njia za kusafiri zimebadilika tangu Ndugu Lindal aliposafiri kwa farasi, si rahisi sikuzote kuendesha gari kupitia vipito vya milima kwenye barabara zenye barafu wakati wa miezi yenye giza ya kipupwe, hata ukiwa na gari aina ya Jeep ambayo magurudumu yalo yote manne hudhibitiwa na usukani. Wakati mmoja, gari hilo lilivumishwa kutoka barabarani, likapinduka mara mbili au tatu chini ya mtelemko. Tulifurahi kama nini kunusurika bila majeruhi!”
Baada ya miaka 30 katika Iceland, Iiris asema hivi: “Kwa miaka iliyopita wengi wamekuja kutoka nchi nyinginezo ili kusaidia. Ingawa wengi wao wamelazimika kuondoka kwa sababu mbalimbali, kwa hakika wameshiriki sehemu kubwa katika kazi ya kupanda na kutia maji. Tunafurahi kwamba tunaweza kubaki, kwa kuwa sasa tuna pendeleo la kuona mavuno yakiingia. Yehova anaharakisha kazi yake huku pia.”
Sehemu kubwa ya ongezeko imetokea kwa sababu wapya huwatolea ushahidi wafanyakazi wenzao. Atli alijifunza kweli kutoka kwa wamishonari, akaanza kuongea na wengine katika kampuni ya ujenzi alikokuwa akifanya kazi. Sasa wawili kati ya wafanyakazi wenzake wanashiriki katika kazi ya kuhubiri, mmoja wao alibatizwa pamoja na mke wake katika Novemba 1992. Mfanyakazi wa tatu amekuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi.
Kuchukua Njia ya Kaskazini
Tukiondoka Reyðarfjörður, twaelekea magharibi. Kutaniko lifuatalo liko mwendo wa kilometa 300 kutoka huku, katika mji wa Akureyri. Wahubiri wa pekee wa wakati wote walipewa mgawo wa kufanya kazi huko katika miaka ya mapema ya 1950. Tangu mwanzo kabisa, kazi ilipatwa na upinzani mkali kutoka kwa makasisi fulani. Makala zilichapwa katika magazeti ya habari ya hapo ili kuwaonya watu dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Watu wengi wa mji huo walihusika pia na uwasiliani-roho. Lakini kwa sababu ya uvumilivu na subira ya mapainia na wamishonari mbalimbali, leo kuna kutaniko lenye bidii na upendo la wahubiri wa Ufalme 35.
Friðrik, mmoja wa wazee wa huku, alikuwa mvuvi. Baada ya kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya katika 1982, alisadiki kwamba yale aliyokuwa akijifunza yalikuwa ndiyo kweli. Alirudi Akureyri akiwa ameazimia kutolea ushahidi familia yake, marafiki wake, na wafanyakazi wenzake. Friðrik alifanya mipango ya kuacha kazi yake ya uvuvi ili aweze kuwa na wakati zaidi pamoja na kutaniko. Alimwambia rafiki yake msichana, Helga, kwamba hawangeweza kuendelea kuishi pamoja mpaka walipooana, kwani alikuwa karibu kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Pia Friðrik alitaka Helga ajifunze Biblia kwa sababu hangemwoa ‘asiye mwamini.’ (1 Wakorintho 7:39) Kwa mshangao wake Helga alianza kujifunza. Walioana katika Februari 1983, wakabatizwa muda mfupi baadaye. Hatimaye mama na dada ya Friðrik walikubali kweli pia.
Kituo chetu cha mwisho ni Akranes, kilometa 350 kutoka Akureyri, ng’ambo ya safu tatu za milima na ng’ambo ya mabonde mengi yenye kupendeza. Hapa barabara imefanyizwa kwa mawe laini, ikifanya safari hiyo iwe yenye kupendeza kwa kulinganishwa na zile barabara nyembamba zenye changarawe zisizo laini ambazo tumesafiria kwa sehemu kubwa ya safari. Katika Akranes tuna kutaniko lililo dogo zaidi katika Iceland—wahubiri watano, wawili kati yao wakitumikia wakiwa wazee. Lina familia mbili zilizoitikia mwito wa Makedonia, zikaacha mojawapo ya makutaniko makubwa zaidi katika Reykjavík, na kufanyiza makao katika mji huu mdogo ili kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi. (Matendo 16:9, 10) Kwa zaidi ya miaka miwili sasa, wamehubiri habari njema kwa subira katika eneo hili, wakiwa na hakika kwamba Yehova atakuza mambo.—1 Wakorintho 3:6.
Mataraja Maangavu ya Ongezeko
Wakiwa na majumba ya kioo yanayopashwa moto kwa nishati ya jotoardhi na mwangaza usio wa asili, wakulima Waiceland wameweza kupanda aina nyingi mbalimbali za matunda, mboga, na mimea mingine. Vilevile, Mashahidi, wakiwa na kweli ya kiroho, hali ya uchangamfu ya mvuto mwanana, na baraka ya roho takatifu ya Yehova, wamekuwa wakijionea matokeo mazuri ajabu katika shamba la Iceland.
Mwaka huu watu 542 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo, na sasa mafunzo ya Biblia nyumbani 200 hivi yanaongozwa. Kwa kuongezea, itikio chanya kwa kile kitia-moyo cha kutumikia katika maeneo yasiyogawiwa mtu linatupa sisi uhakika kwamba watu wote wenye mfano wa kondoo katika kisiwa hiki kikubwa watasikia sauti ya yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo. (Yohana 10:14-16) Hilo litakuwa tokeo lenye shangwe kama nini kwa wale wapiga mbiu ya Ufalme waaminifu ambao wameonyesha subira na uvumilivu mwingi katika kuhubiri habari njema katika bara la barafu na moto katika ile miaka 64 ambayo imepita!
[Ramani katika ukurasa wa 24]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Akureyri
Akranes
Keflavík
Selfoss
Vestmannaeyjar
Reyðarfjörður
Hekla
Geysir
VATNAJÖKULL
REYKJAVÍK
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 24]
Yategemea ramani ya Jean-Pierre Biard