Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 10/15 kur. 23-26
  • Kuhubiri Katika Bara Lenye Hali Tofauti-Tofauti

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuhubiri Katika Bara Lenye Hali Tofauti-Tofauti
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Njema Zasitawi
  • Majumba ya Kujengwa Upesi Katika Maeneo Yaliyotengwa
  • Kuelekea “Ukingo wa Juu”
  • Hadi Chemchemi za Alice na Kuondoka Sehemu za Ndani Kabisa Barani
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 10/15 kur. 23-26

Kuhubiri Katika Bara Lenye Hali Tofauti-Tofauti

KANGARUU, koala, wombati, na pulatipasi, Mwamba wa Ayers na lile Tuta Tumbawe Kuu—hayo ndiyo majina yanayokumbukwa wakati watu wanapofikiria Australia. Lakini ingawa huenda ikashangaza sana, yaelekea kwamba Waaustralia walio wengi hawajazuru kamwe Mwamba wa Ayers wala lile Tuta Tumbawe Kuu wala hawajaona koala, wombati, wala pulatipasi wakiwa nje ya hifadhi za wanyama. Sababu ni kwamba asilimia 85 ya wakaaji milioni 17.3 wa nchi hiyo ni wakaaji wa majijini, wakiishi katika majiji matano makuu yaliyo karibu na pwani.

Mtu akiondoka ukingo wa bahari na kusafiri umbali wa kilometa 200 hivi kuelekea barani, anafikia mwanzo wa zile sehemu maarufu za ndani kabisa za bara hilo. Sura ya nchi yabadilika kutoka msitu wenye mvua ulio na mimea mingi na bara la ukulima lenye rutuba hadi nchi wazi, yenye joto, iliyo kavu, ambako vichaka na nyasi nzito tu zaweza kukua. Hata hivyo kuna uhai mbalimbali katika sehemu hizo za ndani sana barani. Nyanja kubwa za kufugia kondoo na ng’ombe, au stesheni kama ziitwavyo, zaenea hadi mamia ya maili za mraba. Ndani zaidi barani kuna majangwa yenye joto jingi sana, ambako watu hufa nyakati nyingine wasipochukua hatua zifaazo za kujihadhari.

Habari Njema Zasitawi

Hiyo ndiyo mandhari ambayo katika hiyo habari njema za Ufalme wa Mungu zinahubiriwa katika bara hilo lililo chini kabisa (Australia). Kila mwaka maelfu wanaitikia ahadi ya Yehova ya ulimwengu mpya wenye uadilifu. Mwaka wa utumishi uliopita, idadi ya wahubiri wa Ufalme ilifika kilele cha zaidi ya watu 57,000, karibu maradufu ya kile cha miaka kumi iliyopita. Ingawa wahubiri walio wengi wanaishi katika majiji ya pwani hasa, kama vile sehemu kuu ya wakaaji, habari njema zasitawi barani pia.

Ili kupata ono fupi tu la jinsi ilivyo kuhubiri katika bara hilo kubwa lenye hali tofauti-tofauti, acheni tujiunge na mmoja wa waangalizi wa wilaya wetu watano pamoja na mke wake wanapozuru baadhi ya makutaniko katika maeneo ya mbali ya ndani kabisa barani. Safari zao hutia ndani jimbo la Australia Magharibi, nusu ya jimbo la Queensland, na Eneo la Kaskazini, eneo la zaidi ya kilometa za mraba milioni 4.7. Hilo ni karibu nusu ya ukubwa wa Ulaya, bila kutia ndani sehemu iliyokuwa Muungano wa Sovieti.

Safari yetu yaanza katika Perth, jiji kuu la Australia Magharibi. Sasa kuna makutaniko 49 ya Mashahidi wa Yehova, katika jiji hili la ki-siku-hizi kabisa lenye watu milioni 1.2. Kuongezea makutaniko ya Kiingereza, kuna makutaniko ya Kigiriki, ya Kihispania, ya Kiitalia, na ya Kireno, pamoja na vikundi vidogo zaidi katika lugha nyinginezo. Pia kuna kutaniko lenye ndugu na dada Waaborijini pekee, wanaokazia jitihada zao za kuhubiri miongoni mwa watu hao walio wenyeji wa bara hilo. Sasa wengi kati ya watu hao wanyenyekevu wanaitikia ujumbe wa Ufalme. Lakini hali ikoje nje ya majiji hayo makubwa?

Kutoka Perth twasafiri kilometa 1,800 kuelekea kaskazini hadi Port Hedland, ambako kusanyiko la mzunguko litafanywa. Wengi wa wale watu 289 waliohudhuria wamesafiri kati ya kilometa 200 na 700 ili kuwapo. Wanatoka maeneo yaliyotengwa ambako kutaniko lililo karibu zaidi nao laweza kuwa umbali wa kilometa 250 kupitia barabara zisizo na lami zenye mawe yenye ncha kali ambayo hutoboa tairi za magari mara nyingi. Hivi karibuni makutaniko matatu katika eneo hili yamejenga Majumba ya Ufalme yakitumia njia ya kujenga upesi.

Majumba ya Kujengwa Upesi Katika Maeneo Yaliyotengwa

Kuna tofauti iliyoje kati ya kujenga Jumba la Ufalme katika maeneo haya na kujenga moja katika majiji au miji mikubwa zaidi! Ni lazima vifaa vingi vya ujenzi visafirishwe kwa lori kutoka Perth, umbali wa kilometa 1,600 kuelekea kusini. Mamia ya akina ndugu na dada husafiri umbali huo na wengi zaidi hufanya hivyo kwenye mwisho-juma uliotajwa kimahususi ili kuja na kujenga Jumba la Ufalme katika halijoto ya digrii 40 hadi 45 sentigredi. Mmiminiko wenyewe wa watu wakiingia jumuiya ndogo zilizotengwa, ni ushahidi wenye kutokeza. Jumba la Ufalme lilipojengwa katika Tom Price, mji mdogo ambako timbe za chuma huchimbwa, ukurasa wa mbele wa gazeti la habari la mahali hapo ulipiga mbiu hivi: “Karibisho changamfu kwa mafundi na wasaidizi wenye kujitolea wanaohusika katika kule ‘kujenga upesi’ kwa muda wa siku tatu kwa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova katika Tom Price.”

Ilionekana kana kwamba karibu kila mtu mjini humo alikuwa na hamu ya kushirikiana. Badala ya kuomba bei ya kawaida ya dola 11,000 (za Australia) ili kuleta tani 50 za vifaa vya ujenzi, mwenye lori mmoja mwenye ukarimu aliwaomba akina ndugu wachangie mafuta ya gari tu. Wenye biashara za kuuza rangi wa mahali hapo walifanya utoaji wa lita 100 za rangi. Wenye biashara za kuchimba ardhi kabla ya ujenzi, walitoa mashine, na ile kampuni ya kuchimba timbe za chuma ilitoa krini moja bila malipo. Kuwatafutia wageni 300 makao kulitokeza tatizo, lakini ushirikiano wa watu wa mjini ulikuwa wenye kutokeza. Wengine walipiga simu na kutoa vitanda. Mwanamume mmoja alipiga simu kusema kwamba hangekuwako mwisho-juma huo lakini angeuacha mlango wa nyuma wa nyumba yake bila kuufunga kwa kufuli. Alisema: “Mwaweza kutumia nyumba kwa muda wa mradi huo.”

Tukio lenye kuchekesha lilitukia wakati ndugu fulani walipopewa habari kuhusu mahali walipopaswa kuchukua trela lililokuwa la mzunguko wa mahali hapo. Walitatanika kuona ishara kwenye lango iliyosema, “Wageni wa Kidini Hawakubaliwi.” Lakini trela lilikuwa hapo. Kwa hiyo walimjulisha mama wa nyumba hiyo kwamba walikuwa wakichukua trela hilo, lililojaa takataka. Walipokuwa wakilisafisha, walikuja kung’amua kwa ghafula kwamba halikuwa trela la mzunguko! Mwenye trela hilo alipokuja nyumbani, mke wake alimwambia kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wamelichukua trela lake. Upesi ndugu hao walirudi wakiwa na lile trela lililokuwa tupu sasa, wakieleza kosa. Mazungumzo mazuri yalifuata, na hao waliokuwa wapinzani walikuwa na maswali mengi kuuliza juu yetu na juu ya kazi yetu. Sasa walikuwa na hamu ya kuja na kuona lile Jumba la Ufalme jipya.

Kuhubiri habari njema katika eneo hili kwahitaji uvumilivu. Kwanza, kunahusisha kusafiri mbali sana. Dada mmoja painia pamoja na mume wake huendesha gari kwa kawaida umbali wa ujumla wa kilometa 350 kwenda na kurudi kwenye barabara zisizo na lami, zenye mavumbi, kutoka Port Hedland hadi Marble Bar, ili kufanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia. Marble Bar ni mojawapo sehemu zenye joto jingi zaidi katika Australia, mara nyingi halijoto zikifika zaidi ya digrii 50 sentigredi kutoka Oktoba hadi Machi.

Kuelekea “Ukingo wa Juu”

Darwin, umbali wa kilometa 2,500 kuelekea kaskazini zaidi, ni mji unaofuata wa kufanyia kusanyiko la mzunguko. Mwangalizi wa wilaya na mke wake hutumia ule muda wa saa nyingi wa kusafiri kwa gari kudumisha funzo la kibinafsi. Kwanza wanasoma na kuzungumzia andiko la kila siku. Kisha wanasikiliza usomaji wa Biblia kwenye kaseti. Wanapoendesha gari kwa zamu, wanasoma makala kutoka Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa zamu pia.

Ishara ya barabara yawaonya wajihadhari na “magarimoshi ya barabarani.” Hayo ni malori yenye nguvu nyingi sana yanayoburuta matrela matatu au manne na yana urefu wa ujumla wa meta 55. Kwa hiyo nafasi kubwa sana yahitajiwa wakati wa kuyapita. Hayo hutumiwa kubebea ng’ombe na bidhaa nyinginezo hadi miji iliyotengwa.

Hali ya hewa ni yenye joto sikuzote na eneo la mashambani ni kavu daima. Mandhari hiyo kavu ingeweza labda kuonwa kimakosa kuwa mahali papana sana pa makaburi kwa sababu ardhi imejaa vichuguu vyenye umbali sawa kati yavyo. Vichuguu hivyo vina rangi mbalimbali, ikitegemea udongo uliotumiwa na chungu kuvijenga, navyo vyaweza kufikia kimo chochote kutoka meta 1 hadi 2.5. Kisha, wasafiri wetu wanapovuka Mto Viktoria, wanaona ishara nyingi za kuandikwa kwa mikono. “Hatari: Kuogelea Hakuruhusiwi. Mamba Wanaowala Watu Wamo Katika Mito Hii!” yasema moja yazo. Kwa hekima, wanaamua kutafuta njia nyinginezo za kuoga na kupata ubaridi!

Mwishowe, wanafika ukingo wa kaskazini kabisa wa Australia, kunakojulikana kama “Ukingo wa Juu.” Darwin, jiji kuu la Eneo la Kaskazini, lina makutaniko ya Mashahidi wa Yehova mawili makubwa. Hali ya Darwin ya kuwa na tamaduni nyingi yaweza kuonwa kwa urahisi wakati wa kuhudhuria kusanyiko la mzunguko. Kutana na Charles mwenye miaka 30, aliyetoka Tomor Mashariki katika Indonesia, yenye kukumbwa na vita. Wazazi wake Wachina walimlea kuzoea ibada ya wazazi wa kale waliokufa. Alikuwa pia amehusika sana katika mbinu za kupigana na watu. Haikuwa rahisi kuziacha hizo kwa sababu ya uhusiano wazo wenye nguvu na uwasiliani-roho. Hata hivyo, akikumbuka ahadi ya Yesu kwamba “kweli itawaweka huru,” alijiweka huru na njia hiyo ya maisha. (Yohana 8:32) “Leo,” yeye asema, “nina dhamiri safi mbele ya Yehova, na kwa sasa ninatumikia nikiwa mtumishi wa huduma. Mradi wangu ni kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma.”

Halafu, kutana na Beverly kutoka Papua New Guinea. “Mwanzoni sikuwa na ujasiri mwingi wa kutoa ushahidi kwa watu weupe,” akiri Beverly, “kwa sababu Kiingereza kilikuwa lugha yangu ya pili na semi nyingine, pamoja na lafudhi ya Kiaustralia, zilifanya iwe vigumu kwangu kuelewa. Lakini nikikumbuka kwamba Biblia hutuambia tumtumaini Yehova na kuonja na kuona ya kuwa yeye ni mwema, nilianza huduma ya painia ya wakati wote katika Januari 1991. Mwanafunzi wa Biblia wangu wa kwanza ni painia sasa. Wawili wa mabinti zake wamekubali kweli pia, na mmoja wao anapainia pamoja, na mume wake.”

Kabla ya kuondoka Darwin, acheni tusafiri upesi umbali wa kilometa 250 kuelekea mashariki hadi Mbuga ya Kitaifa ya Kakadu, inayojulikana sana kwa ndege wayo wengi sana. Huku twakutana na Debbie, aliye mhubiri pekee wa habari njema katika eneo hilo lote. Twamwuliza jinsi anavyoweza kuendelea imara kiroho akiwa ametengwa hivyo. Yeye ajibu hivi: “Kwanza, kwa kusali. . . . Na ninapata faraja kutoka katika maandiko kama vile Isaya 41:10, linalosema: ‘Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.’”

Katika Jilkmingan, umbali wa kilometa 450 kusini mwa Darwin, twakutana na kikundi kidogo cha Waaborijini. Kwa miaka mingi jumuiya hiyo ya Kiaborijini ilijulikana kuwa jumuiya ya Mashahidi wa Yehova kwa sababu wengi sana walihudhuria mikusanyiko na makusanyiko kwa ukawaida, hata ingawa hakuna yeyote kati yao aliyekuwa amebatizwa. Jumuiya hiyo ilijulikana kwa usafi wayo. Kwa furaha, wengine sasa wamechukua msimamo imara kwa ajili ya kweli na wamebatizwa. Wamo miongoni mwa Waaborijini wa mashambani wa kwanza kufanya hivyo. Ujasiri na kutegemea roho takatifu ya Yehova kwahitajiwa kikweli ili watu hawa wanyenyekevu wajiweke huru kutoka katika mapokeo na mazoea ya uwasiliani-roho ya tangu zamani za kale ya watu wa kabila lao.

Hadi Chemchemi za Alice na Kuondoka Sehemu za Ndani Kabisa Barani

Sasa ndio wakati wa kuondoka “Ukingo wa Juu” na kuelekea kilometa 1,600 kusini hadi Chemchemi za Alice, katika “Kitovu Chekundu” cha bara hilo, karibu na Mwamba wa Ayers ulio maarufu. Humu katika Jumba la Ufalme lenye vifaa vya kurekebisha halijoto, viti vya kustarehesha vinaandaliwa kwa ajili ya kusanyiko, kukiwa na watu 130 au zaidi wakihudhuria kutoka yale makutaniko mawili katika eneo hili. Tena, twaona Wahindi, Wazungu, na Waaborijini wenye furaha wakichangamana pamoja katika ushirika wa Kikristo.

Mwishowe twaondoka Chemchemi za Alice na kuanza mkondo wa mwisho wa safari hiyo pamoja na mwangalizi wetu wa wilaya asafiriye na mke wake. Safari hii yatupeleka umbali wa kilometa 2,000 ng’ambo ile nyingine ya bara, tukielekea kaskazini na mashariki. Tunapofanya hivyo, twaziaga sehemu hizo za ndani kabisa barani, kwani hatimaye twafikia ule msitu wa kitropiki wenye mvua ulio na mimea mingi wa Queensland. Huku, kwenye pwani ya kaskazini mwa Queensland—bara la lile Tuta Tumbawe Kuu—kuna makutaniko mengi yenye uwiano wa juu wa Mashahidi kwa wakaaji.

Hata hivyo, hatujamaliza kusafiri kabla ya sisi kuhudhuria kusanyiko la mzunguko jingine moja. Tukipanda ndege katika Kairns—ule mji wa kitropiki wa Queensland ulio maarufu kwa ajili ya Tuta Tumbawe—twaondoka bara kuu la Australia kwa safari fupi juu ya ukingo wa kaskazini mwa Peninsula ya Cape York, kuvuka Lango-Bahari la Torres, hadi Kisiwa cha Thursday. Huku kuna kutaniko dogo la wahubiri 23 tu. Ni shangwe iliyoje kuona watu 63 wakiwa wamehudhuria kusanyiko letu la mwisho kwenye safari hii!

Twatumaini umefurahia ono hili fupi tu la kazi ya kuhubiri Ufalme inayofanywa katika bara hili lenye hali tofauti-tofauti. Labda siku moja utaweza kututembelea katika bara hili lenye kusisimua lililo chini kabisa na kupata kukutana kibinafsi na akina ndugu na dada wanaofanya huduma yao kwa uaminifu katika mgawo wao wa aina yao.

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 23]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Port Hedland

Canberra

Tom Price

Marble Bar

Newman

Darwin

Katherine

Chemchemi za Alice

Mwamba wa Ayers

Kisiwa cha Thursday

Cairns

Adelaide

Melbourne

Hobart

Sidni

Brisbane

Perth

[Picha katika ukurasa wa 24]

Perth, jiji kuu la Australia Magharibi

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kutoa ushahidi barabarani huleta matokeo mazuri

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki