Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 11/1 kur. 3-5
  • Kufumbua Fumbo la Lile Jina Lililo Kuu Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kufumbua Fumbo la Lile Jina Lililo Kuu Zaidi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutafuta Lile Jina Lililo Kuu Zaidi
  • Jina Hilo Lilikujaje Kuwa Fumbo?
  • Lile Jina Lililo Kuu Zaidi na Wakati Wetu Ujao
  • Kwa Nini Ni Lazima Tujue Jina la Mungu
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Jinsi ya Kujua Jina la Mungu
    Amkeni!—2004
  • Jina la Mungu
    Amkeni!—2017
  • Liheshimu Jina Kuu La Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 11/1 kur. 3-5

Kufumbua Fumbo la Lile Jina Lililo Kuu Zaidi

Ni jambo la kupendeza kwamba Kurani ya Kiislamu na Biblia ya Kikristo pia hurejezea lile jina lililo kuu zaidi. Mazungumzo haya yaeleza maana na umuhimu wa lile jina lililo kuu zaidi. Yaonyesha pia jinsi jina hilo liathirivyo ainabinadamu yote na wakati wetu ujao hapa duniani.

MAMILIONI ya wanaume na wanawake wameishi na kufa kwenye dunia hii. Katika visa vilivyo vingi majina yao yamekufa pamoja nao, na kumbukumbu lao limesahauliwa. Lakini majina mengine makuu—kama vile Avicenna, Edison, Pasteur, Beethoven, Gandhi, na Newton—yaendelea kukumbukwa. Majina hayo yanahusiana na mafanikio, magunduzi, na mavumbuzi ya wale waliokuwa nayo.

Hata hivyo, kuna jina lililo kuu zaidi ya mengine yote. Maajabu yote ya wakati uliopita na ya sasa katika ulimwengu wote mzima yanahusiana nalo. Kwani, tumaini la ainabinadamu la maisha marefu na yenye furaha linahusiana na jina hilo!

Wengi wametaka kupata kulijua jina hilo. Wamelitafuta na kuuliza juu yalo, lakini hawajalipata. Limeendelea kuwa fumbo kwao. Kwa kweli, hakuna mtu awezaye kuligundua jina hilo isipokuwa likifunuliwa kwake na Mwenyeji walo. Kwa furaha, fumbo la jina hilo lisilo na kifani limefumbuliwa. Mungu mwenyewe amefanya hivyo ili wale wenye imani katika yeye wajue juu yake. Alifunua jina lake kwa Adamu, kisha kwa Abrahamu, kwa Musa, na kwa watumishi Wake wengine waaminifu wa kale.

Kutafuta Lile Jina Lililo Kuu Zaidi

Kurani chasimulia juu ya mtu fulani “[aliyefahamu sana] Kitabu (cha Mwenyezi Mungu).” (27:40) Katika kueleza mstari huo, kitabu kimoja cha ufafanuzi kiitwacho Tafsīr Jalālayn chasema: “Asaf bin Barkhiyā alikuwa mtu mwadilifu. Alilijua jina la Mungu lililo kuu zaidi, na wakati wowote alipoliitia, alijibiwa.” Hilo latukumbusha juu ya mwandishi wa Biblia Asafu, aliyesema hivi kwenye Zaburi 83:18: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.”

Kwenye Kurani 17:2, twasoma hivi: “Tulimpa Musa Kitabu [Maandiko], na tukakifanya uongofu kwa Bani Israili (Mayahudi).” Katika Maandiko hayo, Musa aongea na Mungu, akisema hivi: “Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia, Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n’nani? niwaambie nini?” Mungu alimjibu Musa kwa kusema: “Waambie wana wa Israeli maneno haya, BWANA [Yehova, New World Translation], Mungu wa baba zenu, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu; hili ndilo jina langu hata milele.”—Kutoka 3:13, 15.

Katika nyakati za kale, Waisraeli walijua jina kuu hilo la Mungu. Hata lilitumiwa likiwa sehemu ya majina yao wenyewe. Kama vile mtu apatavyo sasa jina Abdullah, linalomaanisha “Mtumishi wa Mungu,” watu wa Israeli wa kale walikuwa na jina Obadia, linalomaanisha “Mtumishi wa Yehova.” Mama ya nabii Musa aliitwa Yokebedi, ambalo labda humaanisha “Yehova Ni Utukufu.” Jina Yohana lamaanisha “Yehova Amekuwa Mwenye Neema.” Na jina la nabii Eliya lamaanisha “Mungu Wangu Ni Yehova.”

Manabii walijua jina kuu hilo nao walilitumia kwa staha nyingi. Linapatikana zaidi ya mara 7,000 katika Maandiko Matakatifu. Yesu Kristo, mwana wa Mariamu, alilikazia aliposema hivi katika sala yake kwa Mungu: “Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa . . . Naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo; ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao.” (Yohana 17:6, 26) Katika kitabu chake cha ufafanuzi kilicho mashuhuri juu ya Kurani, Bayḍāwī aeleza juu ya Kurani 2:87, akisema kwamba Yesu alikuwa “akihuisha wafu kwa jina la Mungu lililo kuu zaidi.”

Kwa hiyo, ni nini kilichotukia kikafanya jina hilo liwe fumbo? Jina hilo linahusianaje na wakati ujao wa kila mmoja wetu?

Jina Hilo Lilikujaje Kuwa Fumbo?

Wengine hufikiri kwamba “Yehova” katika Kiebrania humaanisha “Allah” (Mungu). Lakini “Allah” hulingana na neno la Kiebrania ʼElo·himʹ, wingi wa fahari wa neno ʼelohʹah (mungu). Ushirikina fulani ulitokea miongoni mwa Wayahudi uliowazuia wasitamke lile jina la kimungu, Yehova. Kwa hiyo, walipokuwa wakiyasoma Maandiko Matakatifu na kuona lile jina Yehova, ikawa desturi yao kusema ʼAdho·naiʹ, ambalo humaanisha “Bwana.” Katika sehemu nyingine, hata walibadili maandishi-awali ya Kiebrania kutoka “Yehova” kuwa ʼAdho·naiʹ.

Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo walifuata mwendo uo huo. Mahali pa jina Yehova waliweka “Mungu” (“Allah” katika Kiarabu) na “Bwana.” Hilo lilichangia ukuzi wa lile fundisho bandia la Utatu, ambalo halina msingi katika Maandiko Matakatifu. Kwa sababu hiyo, mamilioni huabudu Yesu na roho takatifu kimakosa na kuwaona kuwa sawa na Mungu.a

Kwa hiyo, viongozi wa Dini ya Kiyahudi na wa Jumuiya ya Wakristo wanashiriki lawama la kule kuenea sana kwa ukosefu wa ujuzi kuhusu lile jina lililo kuu zaidi. Lakini Mungu alitoa unabii hivi: “Nami nitalitakasa jina langu kuu, . . . nao mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA [Yehova, NW].” Naam, Yehova atalijulisha jina lake miongoni mwa mataifa yote. Kwa nini? Kwa sababu yeye si Mungu wa Wayahudi tu wala wa taifa lolote au kikundi kingine chochote kimoja. Yehova ndiye Mungu wa ainabinadamu yote.—Ezekieli 36:23; Mwanzo 22:18; Zaburi 145:21; Malaki 1:11.

Lile Jina Lililo Kuu Zaidi na Wakati Wetu Ujao

Maandiko Matakatifu husema hivi: “Kila atakayeliitia Jina la Bwana [Yehova, NW] ataokoka.” (Warumi 10:13) Wokovu wetu wakati wa siku ya hukumu utahusiana na kujua kwetu jina la Mungu. Kulijua jina lake kwatia ndani kujua sifa zake, kazi zake, na makusudi yake na kuishi kulingana na kanuni zake za juu. Kwa kielelezo, Abrahamu alijua jina la Mungu na aliitia jina hilo. Likiwa tokeo, alifurahia uhusiano mwema na Mungu, akaonyesha imani katika yeye, akamtegemea, na kumtii. Hivyo Abrahamu akawa rafiki ya Mungu. Vilevile, kulijua jina la Mungu hutuvuta karibu naye na hutusaidia tukuze uhusiano wa kibinafsi naye, tukishika sana upendo wake.—Mwanzo 12:8; Zaburi 9:10; Mithali 18:10; Yakobo 2:23.

Twasoma hivi katika Biblia: “BWANA [Yehova, NW] akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha BWANA [Yehova, NW], na kulitafakari jina lake.” (Malaki 3:16) Kwa nini twalazimika “kulitafakari” lile jina lililo kuu zaidi? Jina Yehova humaanisha kihalisi “Yeye Husababisha Iwe.” Hilo humfunua Yehova kuwa Yule ajisababishaye kuwa Mtimizaji wa ahadi. Yeye hutimiza makusudi yake sikuzote. Yeye ndiye Mungu mweza yote, yule Muumba pekee, aliye na kila sifa njema. Hakuna neno moja liwezalo kusimulia kikamili uungu wa Mungu. Lakini Mungu alijichagulia mwenyewe lile jina lililo kuu zaidi—Yehova—nalo hukumbusha juu ya sifa, sifa za kustahilisha, na makusudi yake yote.

Katika Maandiko Matakatifu, Mungu hutuambia juu ya makusudi yake kuelekea ainakibinadamu. Yehova Mungu alimuumba mwanadamu kufurahia maisha ya milele, yenye furaha katika Paradiso. Mapenzi yake kwa ajili ya ainabinadamu ni kwamba watu wote wafanyize familia moja, iliyoungana katika upendo na amani. Mungu wa upendo atatimiza kusudi hilo katika wakati ujao ulio karibu.—Mathayo 24:3-14, 32-42; 1 Yohana 4:14-21.

Mungu hueleza sababu za kuteseka kwa ainabinadamu na huonyesha kwamba wokovu unawezekana. (Ufunuo 21:4) Kwenye Zaburi 37:10, 11, twasoma hivi: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Ona pia Kurani 21:105.

Naam, Mungu atajulikana kwa jina lake kuu. Mataifa yatalazimika kujua kwamba yeye ndiye Yehova. Ni pendeleo la ajabu kama nini kujua lile jina lililo kuu zaidi, kulishuhudia, na kushikamana nalo! Kwa njia hiyo, kusudi la Mungu lenye shangwe litatimizwa ndani ya kila mmoja wetu: “Kwa kuwa amekaza kunipenda nitamwokoa; na kumweka palipo juu, kwa kuwa amenijua Jina langu. Ataniita nami nitamwitikia. . . . Kwa siku nyingi nitamshibisha, nami nitamwonyesha wokovu wangu.”—Zaburi 91:14-16.

[Maelezo ya Chini]

a Ili kupata uthibitisho kwamba Utatu si fundisho la Biblia, ona broshua Je! Uamini Utatu? iliyotangazwa katika 1989 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kwenye kichaka chenye kuwaka moto, Mungu alijitambulisha mwenyewe kwa Musa kuwa ‘Yehova, Mungu wa Ibrahimu’

[Hisani]

Musa na Kichaka Chenye Kuwaka Moto, ya W. Thomas, Sr.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki