Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 11/15 kur. 23-27
  • Kuhubiri Kijiji kwa Kijiji Katika Uhispania

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuhubiri Kijiji kwa Kijiji Katika Uhispania
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Utambuzi wa Kisheria Wachochea Utoaji Ushahidi Mashambani
  • ‘Tafuteni Wale Wanaostahili’
  • Wasomaji Biblia Waitikia kwa Utayari
  • Chuki Zisizo na Sababu Zashindwa
  • Kuitafuta-Tafuta Biblia Ili Kupata Kweli
  • Mavuno Mazuri
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 11/15 kur. 23-27

Kuhubiri Kijiji kwa Kijiji Katika Uhispania

YESU KRISTO alisafiri “jiji kwa jiji na kijiji kwa kijiji, akifundisha na kuendelea na safari yake hadi Yerusalemu.” (Luka 13:22, NW) Ili kuitimiza huduma, Yesu na wanafunzi wake hawakuhubiri “jiji kwa jiji” tu bali pia “kijiji kwa kijiji.” Ingawa ingalikuwa rahisi zaidi kukazia fikira majiji, wao hawakupita kando-kando ya vile vijiji vingi mashambani.a

Mashahidi wa Yehova katika Uhispania walikabiliwa na kazi kama ile iliyomkabili Yesu. Baadaye sana katika 1970, kulikuwa maeneo makubwa mno ya mashambani ambayo hayakupata kutembelewa yaliyokuwa tayari kuvunwa. (Mathayo 9:37, 38) Mamia ya vijiji katika milima yenye mvua ya kaskazini, kwenye nyanda kavu za kati, na karibu na mwambao hayakuwa yamefikiwa kwa ujumbe wa Ufalme.

Mashahidi wa Yehova Wahispania waliazimia kujitahidi sana ili kupeleka habari njema kwenye mikoa hiyo. Lakini kwa nini watu katika maeneo hayo walihitaji kungoja muda mrefu sana ili kusikia ujumbe wa Ufalme? Nao waliitikiaje?

Utambuzi wa Kisheria Wachochea Utoaji Ushahidi Mashambani

Kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Uhispania ilikuwa imekuwa chini ya marufuku tangu mwisho wa vita ya wao kwa wao katika 1939. Katika miaka ya 1950 na 1960, Mashahidi wenye bidii walihubiri kwa hadhari katika majiji, ambako kuwapo kwao hakukuonekana wazi sana. Kazi yao ilipohalalishwa kisheria hatimaye katika 1970, kulikuwa wahubiri wa Ufalme karibu 10,000 katika Uhispania. Karibu wote waliishi katika majiji na miji mikubwa, lakini vijiji vya Uhispania vilihitaji pia kusikia ujumbe wa Ufalme. Ni nani wangetimiza kazi hiyo?

Katika miaka ya 1970 kampeni ilianzwa ya kufika maeneo yote ya peninsula hiyo kwa habari njema. Karibu kila mwezi kutoka 1973 hadi 1979, matangazo ya pekee yaliyoorodhesha uhitaji katika mikoa tofauti ya nchi yalionyeshwa katika Huduma ya Ufalme Yetu, kile kichapo cha utumishi cha kila mwezi kwa ajili ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Familia nyingi zenye nia na zenye kuitikia zilijibu mwito huo zikajitolea kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi.

Kielelezo cha kawaida ni kile cha Rosendo na mke wake, Luci. Walitumwa wakiwa mapainia wa pekee (wahubiri wa Ufalme wa wakati wote) kwenye kijiji cha uvuaji samaki katika Uhispania kaskazini-magharibi wakaamua kubaki katika eneo hilo walipokuwa wazazi. “Ni lazima nikubali kwamba tulipitia nyakati ngumu sana,” akiri Rosendo. “Kazi ya kimwili ilikuwa ngumu kupata, lakini tulitegemea msaada wa Yehova na hatukupata kamwe kuwa na njaa au kukosa makao. Hayo yalistahili kwa hakika.” Kwa muda wa miaka iliyopita, wameweza kusaidia katika kufanyizwa kwa makutaniko manne katika mkoa huo wa Uhispania.

‘Tafuteni Wale Wanaostahili’

Yesu aliwaambia wanafunzi wake ‘watafute’ wale wanaostahili katika kila jiji au kijiji. (Mathayo 10:11, NW) Katika maeneo ya mashambani ya Uhispania, kutafuta huko hutaka bidii-nyendelevu na ujianzishaji, kama vile ilivyogunduliwa na Ángel, ndugu kutoka Alcoy (Alicante). Alikuwa ametoka tu kumaliza kutembelea nyumba kadhaa katika kijiji cha Masías aliposikia sauti ya jogoo akiwika. Alijiambia mwenyewe, “Ikiwa kuna jogoo, ni lazima kuwe kuna nyumba mahali fulani—nyumba ambayo hatujatembelea.” Baada ya kutafuta kotekote, Ángel alipata kijia kilichoongoza kwenye kilele cha kilima na hatimaye kwenye nyumba iliyotengwa.

José na Dolores, ndugu na dada wa kimwili walio katika miaka yao ya 60, waliishi katika nyumba hiyo. Walisikiliza kwa uangalifu na kukubali toleo la funzo la Biblia mara hiyo. Hata hivyo, haikuwa rahisi kujifunza pamoja na watu hao wanyenyekevu, kwa kuwa hawakuweza kusoma wala kuandika, na kila jambo lilipasa litafsiriwe kutoka Uhispania hadi lugha ya Kivalencia, lugha pekee waliyoelewa. Zaidi ya hayo, walikabili upinzani mwingi kutoka kwa majirani wao. Vijapokuwa vizuizi hivyo, José na pia Dolores walifanya maendeleo katika kweli, hata ingawa kuhudhuria mikutano kulimaanisha safari ndefu juu ya milima. Hatimaye, walistahili kubatizwa, na wote wawili waendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu.

Rosendo na Luci, waliotajwa mapema, wakumbuka jinsi mtu mmoja mwenye kupooza aliyekuwa katika nyumba fulani iliyotengwa iliyokuwa karibu na Moaña, Uhispania ya kaskazini-magharibi, alivyokubali kweli. Jina lake lilikuwa María. Aliposema na Mashahidi mara ya kwanza, hakuweza ama kusoma ama kuandika na alikuwa amekuwa kitandani kwa miaka kadhaa kwa sababu ya kuambukizwa ugonjwa wa polio akiwa mtoto. Nyumba yake ilikuwa karibu kilometa mbili kutoka kwenye barabara iliyo karibu zaidi. Hata hivyo, alikuwa na hamu ya kujifunza Biblia, na upesi azimio lake la kumtumikia Yehova likaja kuonekana wazi. María alijifunza kusoma na kuandika akaanza kuhudhuria mikutano, kwa sababu ya jitihada za kutaniko za kujitoa. Akina ndugu walimbeba kwa umbali wa meta 200 kutoka nyumba yake hadi kwenye barabara isiyo ya lami ambako walikuwa wakimshusha ndani ya gari kwa uangalifu. Ujapokuwa upinzani kutoka familia yake mwanzoni, alifanya maendeleo kufikia hatua ya ubatizo. Kwa sababu ya uhakika ambao maendeleo yake ya kiroho yalimpa, sasa amejifunza kuendesha gari ambalo limerekebishwa kipekee na amemaliza mtalaa wa elimu ya msingi. “Kuweza kusaidia watu kama María kwafanya dhabihu yoyote istahili,” aeleza Rosendo.

Wasomaji Biblia Waitikia kwa Utayari

Katika miaka ya 1970 Biblia iliweza kupatikana kwa umma kwa mara ya kwanza katika Uhispania. Wahispania wengi walinunua nakala, na wengine wakaanza kusoma Maandiko. Pilar, kutoka Medina del Campo (Valladolid), alikuwa tayari akisoma Biblia wakati Mashahidi wa Yehova walipokuja kwenye mji wake kwa mara ya kwanza katika 1973. Akiwa Mkatoliki, alikuwa na hadhari juu ya kukubali fasihi kutoka kwa Mashahidi, lakini alitaka kuielewa Biblia. Kwa hiyo, alikubali kuwa na mazungumzo ya kila juma ili kujibu maswali yake ya Biblia.

Akitumia vizuri fasihi iliyotangazwa na Watch Tower Society, yule dada painia aliyemtembelea Pilar aliweza kujibu maswali yake mengi. Akivutiwa na yale aliyokuwa akijifunza, baada ya majuma kadhaa Pilar alikubali funzo la Biblia kwa kutumia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Kabla ya kumaliza funzo lake la kitabu Kweli, alimaliza kusoma Biblia nzima akasadiki kwamba alikuwa ameipata kweli. Akaja kuwa Shahidi wa kwanza katika Medina del Campo, ambayo sasa ina Jumba la Ufalme zuri na kutaniko lenye wahubiri 63.

Mashahidi Wahispania bado hupata watu ‘wanaofahamu uhitaji wao wa kiroho’ na wanaosoma Biblia kwa kawaida wakijitahidi kuelewa mapenzi ya Mungu. (Mathayo 5:3) Pepi, aliyekuwa Mkatoliki ambaye wakati mmoja alifundisha katekisimu katika parishi ya Zumaia (Uhispania ya kaskazini), alikuwa akihubiri katika kijiji cha karibu alipokutana na padri wa parishi hiyo.

“Pepi, wapoteza wakati wako,” padri huyo akamwambia. “Katika kijiji hiki cha Itziar, kuna watu wawili tu—mume na mke—walio na mbetuko wa kiroho. Wengine wote huenda kanisani likiwa zoea tu.”

“Basi,” akajibu Pepi, “ikiwa kuna watu wawili walio na mbetuko wa kiroho, watakuwa Mashahidi wa Yehova.”

Pepi aliendelea na kazi yake ya kuhubiri nyumba kwa nyumba pamoja na wale Mashahidi wengine mpaka kijiji hicho kilipomalizwa. Na kama ilivyotazamiwa, katika nyumba iliyotengwa, ndugu hao walipata mume na mke ambao padri alikuwa amewataja. Walikuwa wakisoma Biblia lakini hawakuielewa. Walikubali funzo la Biblia kwa hamu, wakafanya maendeleo kwa haraka, na kubatizwa katika Aprili 1991.

Watu fulani wenye mioyo yenye kufuatia haki wamejifunza kweli kwa kusoma peke yao tu fasihi yenye msingi wa Biblia iliyotangazwa na Watch Tower Society. Mathalani, Mashahidi kutoka Almadén (Ciudad Real) walikuwa wakihubiri katika mji mdogo wa Ciruelas (Badajoz) walipompata mwanamke mmoja aliyesikiliza ujumbe wao kwa uangalifu. Kwa sababu ya kupendezwa kwake kulikoonekana wazi, walimtolea funzo la Biblia nyumbani. Hata hivyo, alikataa akisema kwamba mwanamume fulani mzee-mzee alikuwa tayari akimpa masomo ya Biblia. Watu wengine kadhaa katika eneo hilo walitaja jambo hilohilo. Udadisi wao ukiwa umechochewa, ndugu hao waliuliza juu ya mwanamume huyo mzee-mzee. Walipata anwani ya mahali anapoishi wakaenda kumtembelea.

Kwa mshangao wao waligundua kwamba mtu huyo, aitwaye Felipe, alikuwa amepata kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani katika Madrid. Baada ya kukisoma chote, alielewa kwamba alikuwa na daraka la kushiriki habari njema pamoja na majirani wake. Kwa hiyo, alikuwa akitumia kitabu hicho kuwapa masomo ya Biblia. Akina ndugu walifanya mipango ya kujifunza naye. Mwanamke mmoja aliyekuwa amejifunza naye Biblia alikubali funzo pia. Ingawa ana umri wa miaka 80 na hana afya njema, Felipe anafanya maendeleo mazuri katika kweli.

Chuki Zisizo na Sababu Zashindwa

Maeneo ya mashambani hutokeza matatizo fulani ya pekee. Kwa kawaida mapokeo ya kidini na ushirikina huwa na mshiko wenye nguvu katika maeneo hayo, na watu wengi wanaoishi mashambani wana shaka lililokwama sana juu ya “dini mpya.” Wanavijiji wengine ni wenye hisia nyepesi sana hasa na jinsi ambavyo majirani na watu wao wa ukoo wangehisi ikiwa wangebadili dini yao. Lakini nguvu za Neno la Mungu zaweza kuyashinda matatizo hayo na kubadili maisha ya mtu. Ndivyo ilivyokuwa katika kijiji cha uvuaji samaki cha Cangas de Morrazo katika Uhispania ya kaskazini-magharibi.

Roberto, mwenyeji mmoja wa kijiji hicho, alikuwa mbaharia akiwa na umri wa miaka 14 kwa sababu alitamani sana kujitegemea. Maisha yake akiwa mbaharia mchumi ulimfanya ashirikiane na mabaharia wengine wachanga waliokunywa kileo kingi na kutumia dawa za kulevya ili kupisha ule muda wa saa nyingi zenye upweke uliotumiwa baharini. Upesi, Roberto akawa pia mwenye kunywa kileo kingi na mzoelevu wa dawa za kulevya.

Baadaye Roberto alirudi nyumbani lakini hakuweza wala hakuwa na nia ya kuyaacha mazoea yake mabaya. Ili kulipia uzoelevu wake wa dawa za kulevya, alikuja kuwa mwizi na alifungwa gerezani kwenye pindi sita tofauti-tofauti. Alipokuwa na miaka 18, alikunywa mchanganyiko wa divai na vitulizaji ambao karibu umuue. Madaktari waliokoa uhai wake, lakini hakuweza kutumia tena mikono na miguu yake. Aliondoka hospitali akiwa mlemavu mikono na miguu. Hata kuwa kwenye kiti cha magurudumu hakukumfanya aache zoea la kutumia dawa za kulevya. Alifadhaishwa na dini, na dawa za kulevya zilionekana kuwa jambo pekee alilokuwa nalo lililofanya maisha yastahili—mpaka miaka mitatu baadaye alipotembelewa na Mashahidi wa Yehova.

Kujifunza juu ya unabii mwingi wa Biblia uliotimizwa kulimsaidia Roberto ashinde kutilia kwake shaka. Ule ukaribishaji mchangamfu aliopokea kwenye Jumba la Ufalme ulimsadikisha kwamba dini ya kweli hufanya maisha za watu ziwe zenye maana zaidi. Katika muda wa miezi tisa, Roberto alikuwa ameshinda uzoelevu wake wa dawa za kulevya akabatizwa. Ujapokuwa ulemavu wake wa kimwili, amekuwa akitumikia akiwa painia kwa miaka minane. Pia amekuwa mzee wa kutaniko kwa muda wa miaka miwili iliyopita. Francisco, mmoja aliyekuwa mshiriki wake, alivutiwa sana na mabadiliko katika maisha ya Roberto hivi kwamba yeye pia alikuja kuwa Shahidi na sasa ni mtumishi wa huduma. Badiliko hilo la kutokeza katika mzoelevu huyo aliyedhaniwa hawezi kuponyeka lilisaidia watu katika eneo hilo kuthamini zaidi asili ya kazi yetu. Mwanamke mmoja hata alimleta mwana wake mchanga aliye mzoelevu wa dawa za kulevya kwenye Jumba la Ufalme kuona ikiwa Mashahidi wangeweza kumponya.

Kuitafuta-Tafuta Biblia Ili Kupata Kweli

Kwa ujumla, watu wa mashambani huithamini sana kweli hivi kwamba mara nyingi hilo huwaaibisha wale wenye hekima ya kilimwengu. (1 Wakorintho 1:26, 27) Adelina, mwanamke wa makamo mwenye haya, ni mmoja wa wale wanaothamini. Alikuwa akichukua imani yake ya Katoliki kwa uzito sana. Kila asubuhi bila kukosa alikuwa akipiga magoti ili kusali, akisema sala kadhaa za Baba Yetu na Salamu Mariamu. Alikuwa akielekeza sala zake kwa “mtakatifu” tofauti kila siku ya juma—ili tu kuhakikisha kwamba angaa sala fulani zilisikiwa.

Adelina alipoanza kujifunza Biblia, alielekeza bidii iyo hiyo ya kidini kwenye imani yake mpya. Hata kuona kwake haya hakukumzuia, ingawa mara ya kwanza yeye na mume wake walipokwenda kwenye Jumba la Ufalme iliwachukua dakika kumi kupata moyo mkuu wa kutosha ili kuingia. Hata hivyo, mara walipoingia, alisikiliza kwa uangalifu. Katika pindi moja, alijifunza juu ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Habari hiyo ilimsisimua, na aliporudi nyumbani, alitaka kusoma zaidi juu yao katika Biblia yake. Lakini wala yeye wala mume wake hawakujua mahali habari hiyo ingeweza kupatikana, ingawa walifikiri ilitajwa mahali fulani katika kitabu cha Ufunuo. Kwa hiyo Adelina alianza kusoma kitabu cha Ufunuo usiku huo akaendelea kukisoma mpaka hatimaye alipofikia sura ya 20 alfajiri.

Kwenye pindi nyingine, Adelina alijifunza kwamba ilifaa kwa mume kumwakilisha mke wake katika sala. Ingawa mume wake alikuwa na nia ya kusali, yeye hakujua la kusema katika sala. Usiku uleule, Adelina aliamua kutafuta maagizo kutoka Biblia. Saa nane za usiku, alimwamsha mume wake ili kumwambia kwamba alikuwa amepata Mathayo sura ya 6, inayozungumzia habari ya sala kwa urefu. Hatimaye baada ya kusoma maagizo ya Yesu, mume wake alitoa sala kwa ajili yao wawili. Sasa Adelina na mume wake pia ni Mashahidi wa Yehova.

Mavuno Mazuri

Baada ya karibu miaka 25 ya utoaji ushahidi mashambani wa watumishi wa Yehova wenye bidii, sehemu zote za Uhispania zimesikia habari njema. Kama ilivyokuwa katika Esia Ndogo katika karne ya kwanza, ‘neno la Yehova laenea katika nchi ile yote.’ (Matendo 13:49) Kwa hiyo, maelfu ya wanavijiji wameitikia kwa upendelevu.

Katika Uhispania na kwingineko, kuhubiri kikamili katika maeneo ya mashambani hutaka subira na kujidhabihu. Lakini kwa kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wote waokolewe,” Mashahidi wa Yehova wanafurahi kuwatafuta wale wanaothamini. (1 Timotheo 2:4) Na kama vile hayo maono yanayotangulia yaonyeshavyo, Yehova amethawabisha sana jitihada za kuhubiri kijiji kwa kijiji katika Uhispania.

[Maelezo ya Chini]

a Yosefo alihesabu kwamba kulikuwa jumla ya “majiji na vijiji” 204 katika Galilaya, na alisimulia mkoa huo kuwa wenye “vijiji vingi sana.”

[Ramani page 23]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

UFARANSA

URENO

UHISPANIA

VISIWA VYA BALEARIC

VISIWA VYA CANARY

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 24]

Vilac, Lérida

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 24]

Puebla de Sanabria, Zamora

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 25]

Casarabonela, Málaga

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 25]

Sinués, Huesca

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]

Lekeitio, Vizcaya

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki