Jina la Mungu
“Isipokuwa Yehova aijenga nyumba, wajenzi wafanya kazi bure.” Ndivyo usomavyo mchoro huu wa Kilatini. Maneno hayo yategemea Zaburi 127:1 katika Biblia, nayo yana kweli yenye kina: Juhudi yoyote ambayo haina baraka ya Yehova itakuwa ya bure hatimaye.
Mchoro huu, wenye tarehe ya 1780, unapatikana kwenye jengo katika Kolombo, Sri Lanka, na unatokeza kwa sababu una jina la Mungu, Yehova. (Ona picha.) Katika karne za mapema jina hilo lilitumiwa sana. Mara nyingi lilichorwa kwenye majengo ya kilimwengu, makanisa, hata kwenye sarafu. Wamishonari walilitumia jina la Mungu walipoipeleka Biblia hadi mabara ya mbali, jambo ambalo bila shaka hueleza sababu ya mchoro huu katika Sri Lanka.
Jinsi mambo yalivyo tofauti leo! Wachache wanaodai kuwa Wakristo hujali juu ya jina la Mungu. Wasomi fulani hata huwachambua Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya kulikazia. Kwa nini? Kulingana na wengine, ni kwa sababu matamshi yalo ya Kiebrania hayajulikani kwa usahihi. Lakini ni wangapi wajuao matamshi ya awali ya Kiebrania ya jina la Yesu? Lakini, jina lake hutumiwa na kustahiwa ulimwenguni pote.
Kwa Yesu, jina la Mungu lilikuwa muhimu sana. Alitufundisha tusali: “Jina lako litukuzwe.” (Mathayo 6:9) Na kabla tu ya kifo chake, alimwambia Mungu hivi: “Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu.” (Yohana 17:6) Wakristo wa kweli ni wafuasi wa nyayo za Yesu. Je! ‘wasidhihirishe jina la Mungu’ pia? Mashahidi wa Yehova hufanya hivyo, na Yehova hubariki sana “nyumba” yao. Zaburi hii ni kweli kuhusu wao: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—Zaburi 144:15, NW.