Mpaji wa “Kila Zawadi Njema”
“Pindi moja niliitwa na kasisi mmoja wa kanisa la Reformed. Alitaka kujua jinsi nilivyosimamia kanisa langu. Nilimwambia hivi: . . . ‘Sisi hatulipi mishahara; hakuna jambo lolote la kuwafanya watu wagombane. Sisi hatuombi michango kamwe.’ ‘Mnapokeaje fedha?’ yeye akauliza. Nilijibu, ‘Sasa, Dakt.——, nikikuambia jinsi ilivyo kwelikweli wewe hutaweza kuamini hata kidogo. Watu wanapopendezwa na njia hii, hawaoni kikapu [cha michango] kikizungushwa. Lakini wao huona kwamba kuna gharama. Wanajiambia hivi, “Jumba hili lahitaji kulipiwa. . . . Naweza kuchangaje fedha kidogo kwa kusudi hilo?”’ Alinitazama kana kwamba alikuwa akifikiri, ‘Waniona kuwa mjinga—au nini?’ Nikasema, ‘Sasa, Dakt.——, ninakuambia kweli kabisa . . . Mtu apatapo baraka na akiwa na mali yoyote, yeye hutaka kuitumia kwa ajili ya Bwana. Ikiwa hana mali, kwa nini tumsukume aitoe?’”
—Charles T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society, “Mnara wa Mlinzi,” (Kiingereza) Julai 15, 1915.
SISI hutoa kwa sababu Yehova Mungu alikuwa wa kwanza kutoa. Kutoa kwake kulianza na uumbaji miaka mingi sana iliyopita—kiumbe chake cha kwanza kabisa, “Mwanawe pekee.” (Yohana 3:16) Kwa sababu ya upendo, aliwapa wengine zawadi ya uhai.
Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, ni zawadi iliyo kuu zaidi tuliyopewa na Yehova. Lakini Mwana wa Mungu, mwenyewe, si kikomo cha kutoa kwa Mungu. “Fadhili ya Mungu isiyostahiliwa yenye kupita zaidi” ndivyo mtume Paulo aita ile “zawadi ya bure [itokayo kwa Yehova] isiyoelezeka.” (2 Wakorintho 9:14, 15, NW) Kwa wazi zawadi hiyo hutia ndani jumla yote ya wema na fadhili-upendo zote ambazo Mungu huwatolea watu wake kupitia Yesu. Fadhili hiyo isiyostahiliwa ni ya ajabu sana hivi kwamba hupita zaidi uwezo wa kibinadamu wa kueleza au kufafanua. Lakini, kuna sehemu nyinginezo za kutoa kwa Mungu.
Zamani za kale, mfalme mmoja alikiri kwa hekima na kwa unyenyekevu kwamba kwa kweli vitu vyovyote vizuri alivyotoa vikiwa zawadi vilikuwa mali ya Yehova. Alisema hivi: “Vitu vyote vilivyo mbinguni na duniani ni vyako; ufalme ni wako, Ee BWANA [Yehova, NW], nawe umetukuzwa, u mkuu juu ya vitu vyote. . . . Lakini mimi ni nani, na watu wangu ni nani, hata tuweze kutoa kwa hiari hivi? kwani vitu vyote vyatoka kwako, na katika vitu vyako mwenyewe tumekutolea.”—1 Mambo ya Nyakati 29:11-14.
Kielelezo cha Mungu
Yakobo, mwanafunzi wa Yesu Kristo, alijua kwamba Yehova Mungu ndiye chanzo cha chochote ambacho ni kizuri kwa kila njia. Ni zawadi kamilifu tu ambazo hutoka kwake. Yakobo aliandika hivi: “Kila kipaji chema [zawadi njema, NW] na kila zawadi kamilifu hutoka mbinguni; hutoka kwa Baba, Mwumba wa mianga, ambaye habadiliki wala hana alama yoyote ya ugeugeu.”—Yakobo 1:17, Habari Njema kwa Watu Wote.
Hata kwa habari ya kutoa zawadi, Yakobo aliona jinsi Mungu alivyo tofauti na wanadamu. Wanadamu waweza kutoa zawadi njema lakini hawafanyi hivyo sikuzote. Zawadi hizo zaweza kutokana na kusudi lenye ubinafsi, au zaweza kutumiwa kumshawishi mtu kufanya jambo baya. Yehova hana ugeugeu; yeye habadiliki. Kwa hiyo, kusudi la zawadi zake halibadiliki. Ni safi sikuzote. Sikuzote hizo huendeleza hali njema na furaha ya ainakibinadamu. Ni zenye fadhili na zenye kutoa msaada sikuzote, hazileti uharibifu kamwe.
Makusudi ya Kutoa Zawadi
Katika siku za Yakobo, viongozi mashuhuri wa kidini walizoea kutoa zawadi ili tu kuonwa na watu. Walitoa kwa kusudi baya. Wakiwa na hamu ya kushangiliwa na watu, waliridhiana viwango vyao vyenye uadilifu. Hata hivyo, Wakristo walipaswa kuwa tofauti. Yesu aliwashauri hivi: “Basi wewe utoapo sadaka, usipige panda mbele yako, kama wanafiki wafanyavyo katika masinagogi na njiani, ili watukuzwe na watu. Amin, nawaambieni, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe kwa siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.”—Mathayo 6:2-4.
Kusudi la Mkristo la kutoa zawadi ni ili kusaidia wengine walio na uhitaji fulani au kuwafurahisha au kuendeleza ibada ya kweli. Si kujitukuza mwenyewe. Hata hivyo, macho ya Yehova yaweza kupenya ndani kabisa moyoni mwetu. Yeye aweza kuona kusudi lililo ndani kabisa la kutoa kwetu zawadi za rehema.
Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufuata kielelezo cha Yehova na Mwanawe katika kutoa zawadi. Wao hutoa kutoka katika vile walivyo navyo. Wao wana habari njema za Ufalme, na hutoa habari hizo kwa baraka ya wengine. Wao wajua kwamba Mithali 3:9 husema hivi: “Mheshimu BWANA [Yehova, NW] kwa mali yako, na kwa malimbuko ya mazao yako yote.” Kwa sababu kila ofisi ya tawi, kutaniko, na mtu mmoja-mmoja hujaribu sana kuchangia hali njema ya wote, udugu wote wafanywa imara na wenye ufanisi kiroho. Ufanisi wa kimwili hauongozi kwenye ufanisi wa kiroho, lakini ufanisi wa kiroho huleta ufanisi wa kimwili wa kutosha kwa ajili ya mahitaji ya kazi ya Yehova.
Njia za Kushiriki
Kuna njia nyingi ambazo katika hizo kila mtu aweza kuchangia binafsi kutegemeza habari njema. Njia moja ni kwa habari ya Majumba ya Ufalme. Washiriki wote wa kutaniko hutumia Jumba la Ufalme. Mtu fulani ameandaa fedha kwa ajili ya ujenzi walo au malipo ya kodi, umeme, visawazisha-halijoto, na matumizi yalo. Kwa kuwa ni lazima kila mtu ashiriki katika utegemezo wa kutaniko, masanduku ya michango yanawekwa katika Jumba la Ufalme, na upaji wa kujitolea unaopokewa unatumiwa kulipia gharama za kutaniko. Kutokana na fedha za ziada, michango yaweza kutolewa kwa tawi la Watch Tower la mahali hapo, kulingana na uamuzi wa kutaniko.
Michango yaweza kutolewa kwa tawi la Sosaiti lenyewe kwa ajili ya mazoezi na utegemezo wa wamishonari na mapainia wa pekee katika sehemu za ulimwengu ambamo habari njema hazijawafikia watu kwa ujumla. Gharama nyinginezo katika kuenezwa kwa habari njema zinahusiana na kazi ya waangalizi wasafirio. Mtume Paulo, aliyeweka kielelezo katika kazi ya kusafiri katika karne ya kwanza, alipongeza kutaniko katika Filipi hivi: “Mliniletea msaada kwa mahitaji yangu, wala si mara moja.” (Wafilipi 4:14-16) Zaidi ya gharama za sehemu hizo za utumishi wa wakati wote, ambazo ofisi zote za tawi huwa nazo, kuna kudumishwa kwa kila kao la Betheli na wale waishio humo. Kuandika na kuchapa fasihi yenye ujumbe mzuri wa habari njema ni mapendeleo kwelikweli yanayotolewa na Mungu, lakini kugawanywa kwa fasihi ni jambo la lazima pia, na hilo huleta gharama. Kisha kuna gharama za makusanyiko na mikusanyiko, bila kutaja kesi za mahakamani ambazo zimefanywa ili ‘kuitetea injili na kuithibitisha.’—Wafilipi 1:7.
Wakati utumiwao katika kuhubiriwa kwa habari njema na kila mtumishi wa Yehova ni wa kujitolea, na vilevile kutoa kwake fedha. Kuweka kando kwa kawaida fedha za kutumiwa katika utegemezo wa upanuzi wa ibada ya kweli kunashauriwa na mtume Paulo: “Kwa habari ya ile changizo kwa ajili ya watakatifu, . . . siku ya kwanza ya juma kila mtu kwenu na aweke akiba kwake, kwa kadiri ya kufanikiwa kwake.”—1 Wakorintho 16:1, 2.
Mtu afanyapo upaji, yeye hajui barabara jinsi utakavyotumiwa sikuzote, lakini aona matokeo katika upanuzi wa kuhubiriwa kwa Ufalme. Ripoti katika Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1993 (katika Kiingereza) zaonyesha kwamba habari njema ya Ufalme inahubiriwa katika mabara na visiwa vya bahari zaidi ya 200 na wahudumu Wakristo zaidi ya 4,500,000. Ripoti hizo zinachangamsha moyo. Kwa hiyo zawadi yoyote, haidhuru ukubwa wayo ni nini, husaidia katika kuenezwa kwa habari njema ulimwenguni pote.
Kazi hii inagharimiwa na utoaji wa wote kwa ujumla. Baadhi ya watu huweza kutoa zaidi, jambo ambalo husaidia kazi ya kuhubiri kwa kadiri kubwa zaidi. Wengine hutoa kidogo zaidi. Lakini wale watoao upaji wa kiasi hawahitaji kuhisi aibu au kuhisi kwamba sehemu wanayoshiriki ni ndogo mno. Kwa hakika Yehova hahisi hivyo. Yesu alionyesha hilo kwa wazi sana alipoonyesha jinsi Yehova alivyothamini sana vile visarafu vya mjane. “Akamwona mjane mmoja maskini akitia mle senti mbili. Akasema, Hakika nawaambia, huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote; maana, hao wote walitia sadakani katika mali iliyowazidi, bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo.”—Luka 21:2-4.
Haidhuru hali yetu ya kifedha huenda ikawa nini, twaweza kutoa katika njia zinazompendeza Yehova. Mtunga-zaburi ajumlisha vema jinsi tuwezavyo kumpa Mfalme na Hakimu wetu utukufu. Yeye asema hivi: “Mpeni BWANA [Yehova, NW] utukufu wa jina lake, leteni sadaka mkaziingie nyua zake.” (Zaburi 96:8) Kwa hiyo, na tuige kile kielelezo chenye upendo cha Baba yetu wa kimbingu kwa kutoa kwetu zawadi kwa uchangamfu kwa sababu yeye alikuwa wa kwanza kutupa sisi.
[Sanduku katika ukurasa wa 30]
JINSI AMBAVYO WENGINE HUTOA UPAJI KWA AJILI YA KAZI YA KUHUBIRI-UFALME
◻ MICHANGO KWA KAZI YA ULIMWENGUNI POTE: Wengi huweka kando au hupangia kiasi cha fedha ambazo wao hutia katika masanduku ya michango yaliyo na kibandiko hiki: “Michango kwa Kazi ya Sosaiti ya Ulimwenguni Pote—Mathayo 24:14.” Kila mwezi, makutaniko hupeleka kiasi hicho ama kwenye makao makuu ya ulimwengu katika Brooklyn, New York, ama kwenye ofisi ya tawi iliyo karibu zaidi.
◻ ZAWADI: Upaji wa hiari wa fedha waweza kupelekwa moja kwa moja kwenye Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201, au kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti ya mahali hapo. Vito au mali nyingine zenye thamani zaweza kutolewa pia. Barua fupi yenye kutaarifu kwamba hiyo ni zawadi ya moja kwa moja yapasa iambatane na michango hiyo.
◻ MPANGO WA UPAJI WENYE MASHARTI: Fedha zaweza kupewa kwa Watch Tower Society ili kushikiliwa zikiwa amana hadi kifo cha mpaji, kukiwa na uandalizi wa kwamba kukitokea kisa cha uhitaji wa kibinafsi, zitarudishwa kwa mpaji.
◻ BIMA: Watch Tower Society yaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mpango wa bima ya maisha au katika mpango wa kustaafu kazi/malipo ya uzeeni. Sosaiti yapasa kujulishwa juu ya mipango yoyote kama hiyo.
◻ AKIBA ZA BENKI: Akiba za benki, hati za amana, au akiba za fedha za kustaafu za mtu mmoja-mmoja zaweza kuwekwa zikiwa amana kwa ajili ya au kuweza kulipwa wakati wa kifo kwa Watch Tower Society, kulingana na matakwa ya benki ya hapo. Sosaiti yapasa kujulishwa juu ya mipango yoyote kama hiyo.
◻ HISA NA DHAMANA: Hisa na dhamana zaweza kupewa kwa Watch Tower Society ama zikiwa zawadi ya moja kwa moja ama zikiwa chini ya mpango ambao kwa huo mapato yaendelea kulipwa kwa mpaji.
◻ MASHAMBA NA NYUMBA: Mashamba na nyumba ziwezazo kuuzwa zaweza kupewa kwa Watch Tower Society ama kwa kutoa zawadi ya moja kwa moja ama kwa kuweka shamba au nyumba ya maisha kwa ajili ya mpaji, ambaye aweza kuendelea kuishi humo muda wa maisha yake. Mtu apaswa kuarifu Sosaiti kabla ya kuipa Sosaiti hati yoyote ya mashamba na nyumba.
◻ WASIA NA AMANA: Mali au fedha zaweza kupangiwa kuwa urithi wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania kwa njia ya wasia wenye kutekelezwa kisheria, au Sosaiti yaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mkataba wa amana. Amana inayofaidi tengenezo la kidini yaweza kuandaa faida fulani za kodi. Nakala ya wasia au mkataba wa amana yapasa kupelekwa kwa Sosaiti.
Kwa habari zaidi kuhusu mambo ya jinsi hiyo, andikia International Bible Students Association, P. O. Box 47788, Nairobi, Kenya, au tumia anwani ifaayo iliyoorodheshwa kwenye ukurasa 2.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Jinsi upaji wako unavyotumiwa:
1. Wajitoleaji wa Betheli
2. Ujenzi wa ofisi ya tawi
3. Msaada wa misiba
4. Majumba ya Ufalme
5. Wamishonari