Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 12/15 kur. 25-29
  • Kuweka Jicho Letu Likiwa “Sahili” Katika Kazi ya Ufalme

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuweka Jicho Letu Likiwa “Sahili” Katika Kazi ya Ufalme
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Kuweka Jicho Likiwa Limekazwa Ifaavyo
  • Utendaji wa Ufalme Ulioongezeka
  • Uthamini kwa Ajili ya Fasihi Yetu
  • Kujenga kwa Ajili ya Upanuzi
  • Jicho Likiwa Limekaziwa Ufalme wa Mungu
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 12/15 kur. 25-29

Kuweka Jicho Letu Likiwa “Sahili” Katika Kazi ya Ufalme

ILE Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani, au iliyoitwa Ujerumani Mashariki, haikuwa hata imefikia miaka ya makamo. Miaka 41 ya kuwako kwayo ilimalizika mnamo Oktoba 3, 1990, wakati eneo layo, karibu lenye ukubwa wa Liberia au jimbo la Tennessee katika United States, lilipounganishwa na Jamhuri ya Muungano ya Ujerumani, iliyokuwa imeitwa Ujerumani Magharibi.

Kuunganishwa upya kwa nchi hizo mbili za Ujerumani kumemaanisha marekebisho mengi sana. Si mpaka halisi tu uliokuwa umezitenganisha nchi hizo mbili, bali pia mpaka wa itikadi nyingi. Hayo yote yalimaanisha nini kwa watu huko, na maisha yamebadilikaje kwa Mashahidi wa Yehova?

Yale mapinduzi yaliyoitwa Wende, katika Novemba 1989 yaliyowezesha kule kuunganishwa upya, yalifuata upesi ile miongo minne ya ujamaa mgumu. Katika kipindi hicho, utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulikuwa umepigwa marufuku, na nyakati nyingine kunyanyaswa kwao kulikuwa kwingi sana.a Uhuru ulipokuja kwa Ujerumani Mashariki, msisimuko ulienea kotekote miongoni mwa wakazi. Lakini furaha ilipofifia, wengi walifadhaika, wakakata tamaa, hata kutamauka. Kazi ngumu ya kuunganisha nchi hizo mbili za Ujerumani kuwa kitu kimoja kijamii, kisiasa, na kiuchumi inathibitika kuwa kubwa.

Kulingana na ile ripoti ya pekee “162 Tage Deutsche Geschichte” (Siku 162 za Historia ya Ujerumani) katika gazeti Der Spiegel, baada ya kule kuunganishwa upya hofu ilienea juu ya ukosefu wa kazi za kuajiriwa, infleshoni, na kuongezeka kwa kodi. “Je! nitapata malipo ya kutosha ya uzeeni?” wengi waliuliza katika ile iliyokuwa Ujerumani Mashariki. Namna gani makao? “Kotekote katika Ujerumani Mashariki, majengo ya zamani yanaharibika, majengo ya barabara nzima hayakaliki.” Uchafuzi ulifikia viwango vyenye kutia hofu.

Wakikabili mchafuko huo wa kijamii na wa kiuchumi, Mashahidi wa Yehova katika ile iliyokuwa Ujerumani Mashariki wamekabilianaje na hali?

Kuweka Jicho Likiwa Limekazwa Ifaavyo

Mashahidi wa Yehova hawana mipaka ya kiitikadi. Imani yao yenye msingi wa Biblia ni ileile, iwe ni Mashariki au Magharibi. Mazingira yao ya kijamii yakiwa katika hali ya kubadilika, Mashahidi walio wengi hudumisha usawaziko wa kiroho kwa kuweka macho yao yakiwa yamekaziwa ule mradi mkuu wa kumtumikia Yehova. Kwa nini hilo ni jambo la lazima?

Kwa sababu “mandhari ya ulimwengu huu yanabadilika.” (1 Wakorintho 7:31, NW) Mzee mmoja Mkristo asema kwamba kuhubiri chini ya marufuku kabla ya Wende kulitaka moyo mkuu; kuliwafundisha Mashahidi wamtegemee Yehova na kuliwazoeza katika kuitumia Biblia. Lakini sasa, “tunapaswa kuwa waangalifu zaidi tusije tukakengeushwa na upendo wa vitu vya kimwili na mahangaiko ya maisha.”

Mara nyingi uhuru na maendeleo hukadiriwa kulingana na vitu vya kimwili. Watu wengi katika mkoa huu huhisi uhitaji wa kulipia wakati au anasa walizokosa. Hilo ni wazi zaidi wakati mtu aendeshapo gari kupitia zile barabara za mawemawe katika miji na vijiji vya Thuringia na Saksoni kule kusini. Huenda barabara zikahitaji kutengenezwa, huenda nyumba zikawa za kiasi, lakini kuna vyombo vingi kama nini vya kunasia programu za televisheni kutoka kwenye satelaiti! Ni rahisi kwa mtu kudanganywa aamini kwamba usalama na furaha hutokana na kuwa na kila kitu kionwacho na macho. Huo ni mtego hatari kama nini!

Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alisema juu ya hatari ya kutoa uangalifu usiofaa kwa vitu vya kimwili na mahangaiko ya maisha. “Msijiwekee hazina duniani,” yeye akaonya. Aliongeza hivi: “Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi [sahili, NW] mwili wako wote utakuwa na nuru.” (Mathayo 6:19, 22) Yeye alimaanisha nini? Jicho sahili ni lile ambalo limekaziwa kitu fulani na ambalo huipitishia akili taswira zilizo wazi. Jicho la kiroho lililo sahili huweka taswira ya Ufalme wa Mungu ikiwa wazi. Kwa hiyo azimio la Mkristo la kuweka jicho lake likiwa sahili, likiwa limekaziwa Ufalme wa Mungu, na kusukuma mahangaiko yawe nyuma humsaidia aendelee kuwa na usawaziko wa kiroho.

Hilo laweza kutolewa kielezi na ono la mume na mke fulani kutoka Zwickau, Saksoni, walioonyesha kupendezwa na Biblia wakati wa Wende. Biashara yao ilikuwa yenye kutumia wakati mwingi sana, lakini walitanguliza faida za kiroho, wakihudhuria mikutano yote ya Kikristo. “Kulingana na biashara yetu, sisi hatuna wakati wa kutosha,” wao wakakiri, “lakini kiroho twahitaji wakati huo.” Ni uamuzi wenye hekima kama nini!

Fikiria pia, familia moja katika Plauen, katika Saksoni pia. Mume alikuwa fundi wa saa, fundi stadi mwenye biashara yake mwenyewe. Baada ya Wende, kodi ya mahali alipotumia ilipanda sana. Afanye nini? “Ingegharimu fedha nyingi, na nilijifunza kuifanya kweli iwe jambo la maana zaidi maishani mwangu.” Kwa hiyo alihamia mahali pasipofaa sana lakini palipokuwa na kodi ya chini zaidi. Ndiyo, fundi huyo wa saa alijifunza upesi sana juu ya kuweka jicho lake likiwa sahili.

Lakini, wachache walijifunza hivyo kwa kuchelewa mno. Mzee mmoja Mkristo alianza biashara akisababu kwamba ule uchumi wa soko-huru uliokuwa umeanzishwa karibuni ungekuwa na matokeo mazuri. Mwangalizi mmoja asafiriye alimhimiza kwa fadhili asiruhusu shughuli za kibiashara zikandamize hali ya kiroho. Lakini, kwa kusikitisha, hilo ndilo lililotukia. Miezi kadhaa baadaye ndugu huyu alijiuzulu asiwe mzee. Baadaye aliandika hivi: “Kwa msingi wa ono langu mwenyewe, ningeshauri ndugu yeyote anayejitahidi kufikia mapendeleo ya utumishi asianzishe biashara yake mwenyewe.” Hilo halimaanishi kwamba kuwa na biashara yako mwenyewe ni jambo baya kwa Mkristo. Lakini iwe tuna biashara yetu wenyewe au la, kukazia fikira nyingi mno mahangaiko ya kiuchumi kwaweza kutufanya tuwe watumwa wa utajiri bila kujua. Yesu alionyesha matokeo ya hilo: “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu.” (Mathayo 6:24) Yule mtunga-shairi Mjerumani Goethe alisema hivi: “Hakuna walio utumwani zaidi kuliko wale waaminio kimakosa kwamba wako huru.”

Tukiwa katika dhoruba halisi huenda tukahitaji kukengeza au kukinga macho kwa mikono ili kukazia macho yetu mradi wetu. Tuzungukwapo na msukosuko wa kisiasa, kiuchumi au kijamii, ni lazima tukaze fikira zetu ili kuendelea kuutazama mradi wetu wa kiroho. Baadhi ya Wakristo wanafanya nini ili kuweka jicho lao likiwa sahili katika kazi ya Ufalme?

Utendaji wa Ufalme Ulioongezeka

Kotekote katika ile iliyokuwa Ujerumani Mashariki, Mashahidi wanatumia wakati mwingi zaidi kuhubiri kuliko wakati mwingine wowote. Katika miaka miwili iliyopita, wakati wa wastani uliotumiwa katika utumishi wa shambani uliongezeka kwa asilimia 21. Tokeo ni ongezeko lenye kutokeza la asilimia 34 katika mafunzo ya Biblia nyumbani. Zaidi ya hayo, idadi ya mapainia wa kawaida kwa wakati huu imeongezeka mara nne zaidi ya vile ilivyokuwa miaka miwili tu iliyopita! Wengine wanapokuwa na wasiwasi na kulalamika, Wakristo zaidi ya 23,000 katika ile iliyokuwa Ujerumani Mashariki mpaka sasa wanakabiliana na hali hiyo kwa kuweka jicho lao likiwa sahili. Hilo limechangia lile ongezeko lenye kustaajabisha katika utendaji wa Ufalme.—Linganisha Yoshua 6:15.

Utendaji uliopanuka wamaanisha kwamba eneo linatunzwa vema katika sehemu ya kusini, ambako Mashahidi wengi huishi. Majina mengi ya mahali hapo ni ya maana na yanafahamiwa katika historia. Ikiwa unapenda sana vyombo vya kauri, utautambua mji wa Meissen, karibu na Dresden, kuwa chanzo cha baadhi ya kauri za ulimwengu zilizo nyepesi zaidi. Sasa Meissen ni makao ya wahubiri 130 hivi wa Ufalme. Au fikiria Weimar, “jiji kuu la kale la Ujerumani.” Ukumbusho wa Goethe-Schiller ulio katika kitovu cha mji huo hushuhudia uhusiano wenye heshima kati ya Weimar na waandikaji hao wawili nao ni chanzo cha fahari kwa wengi huko. Leo Weimar waweza kuonea fahari wahubiri wao zaidi ya 150 wa habari njema.

Hata hivyo, mambo ni tofauti sana kaskazini, kukiwa na wahubiri wachache zaidi na mwendo mrefu zaidi kati ya makutaniko. Kazi ni haba hasa. Wengi walio na kazi wana msongo wa kufanya kazi ya ziada ili waweze kudumisha kazi yao. Ndugu mmoja anayetumikia akiwa mhubiri wa wakati wote huko kaskazini aeleza hivi: “Chini ya marufuku kila ndugu alihitaji ulinzi wa Yehova katika utumishi wa shambani, lakini kupata kazi hakukuwa jambo gumu. Sasa hali imegeuka. Tuna uhuru wa kuhubiri, lakini tunahitaji mwongozo wake kwa habari ya kazi ya kuajiriwa. Badiliko hilo si rahisi sana kuzoea.”

Je! wahubiri hufurahia kuweza kuhubiri mara nyingi zaidi? Maoni ya Wolfgang ni haya: “Ni bora zaidi kwa mhubiri yuleyule kufanya eneo lilelile mara kwa mara. Watu huzidi kumtumaini na ni wenye kuwasiliana zaidi.” Kwa kuongezea hilo, wenye nyumba “hawaoni aibu tena kuongea juu ya dini mlangoni, hata wakati ambapo wapita-njia wako karibu vya kutosha kuweza kusikia yale yasemwayo. Dini si mwiko tena.” Ralf na Martina wakubali. “Twaonea shangwe kufanyia kazi eneo letu mara nyingi zaidi. Twaweza kupata kuwajua watu binafsi na twasisimuka pia juu ya ule unamna-namna mwingi wa fasihi unaopatikana.”

Uthamini kwa Ajili ya Fasihi Yetu

Ralf na Martina huthamini hasa kile kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? Kwa wengi waliokubali kutokuwako kwa Mungu katika ile iliyokuwa Ujerumani Mashariki, kitabu hiki kinathibitika kuwa msaada wa ajabu wa kujifunza Biblia. Walitamani pia kichapo kidogo zaidi chenye habari iyo hiyo. “Tulisisimuka kama nini broshua Je! Kweli Mungu Anatujali? ilipotolewa kwenye ‘Wachukuaji Nuru’ Mkusanyiko wa Wilaya wa 1992 katika Dresden. Lilikuwa jibu kwa sala zetu.”

Wengi wasio Mashahidi wamekuja kupendezwa na vichapo vya Watch Tower. Katika Julai 1992 mhadhiri mmoja wa elimu ya kijamii aliandika kuonyesha “staha [yake] nyingi sana na shukrani changamfu zaidi” kwa ajili ya vichapo, atumiavyo kutayarisha mihadhara. Katika Januari 1992 mwanamke mmoja katika Rostock alikubali nakala moja ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kutoka kwa Mashahidi wawili waliokuja mlangoni pake. Aliandikia ofisi ya tawi ya Ujerumani hivi: “Mimi ni wa Kanisa la Kilutheri. Ninastahi sana utendaji wa tengenezo la Mashahidi wa Yehova. Wao husema kwa kuazimia kwamba mwanadamu hawezi kuwako tena bila mwongozo wa Mungu.”

Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamewatolea washiriki wayo kiasi gani cha mwongozo wa kiroho? Lile gazeti mashuhuri la habari Die Zeit lilieleza katika Desemba 1991 kwamba ilihali Kanisa la Kilutheri lilikuwa “limejinyoosha katika utukufu kwa muda mfupi likiwa mama ya mapinduzi yenye amani, yaonekana umashuhuri walo unazidi kufifia.” Kwa kweli, mwakilishi mmoja wa Kanisa la Kilutheri aliomboleza hivi: “Watu waliona kimakosa maisha katika mfumo wa soko-huru kuwa paradiso.” Mshiriki mmoja wa kanisa katika Magdeburg aliandikia ofisi ya tawi katika Ujerumani akiomba habari. Kwa nini? “Baada ya miaka kadhaa ya kutabasamu katika hali ya kutoamini,” akaandika muungwana huyo, “sasa nimesadiki kabisa kwamba ulimwengu huu umo katika siku zao za mwisho na kwamba tutakabili matatizo makubwa hivi karibuni.”—2 Timotheo 3:1-5.

Kujenga kwa Ajili ya Upanuzi

Kabla ya Wende, Majumba ya Ufalme hayakuruhusiwa katika Ujerumani Mashariki. Sasa yanahitajiwa kwa haraka; kuyajenga kunatangulizwa. Hiyo ni sehemu nyingine ya ibada ya kweli ambayo imepatwa na mabadiliko yenye kutokeza. Ono la ndugu mmoja laonyesha jinsi ambavyo badiliko hilo limetukia kasi.

Katika Machi 1990, muda wa saa kadhaa tu baada ya Mashahidi wa Yehova kupokea utambuzi wa kisheria katika Ujerumani Mashariki, ndugu mmoja alialikwa kuhutubia kikundi cha Mashahidi, akitumia maikrofoni kwa mara ya kwanza maishani mwake. Miaka miwili na nusu baadaye, kutaniko ambalo ashirikiana nalo liliweka wakfu Jumba la Ufalme jipya kabisa. Kufikia mwisho wa 1992, Majumba ya Ufalme saba yalikuwa yamejengwa kwa ajili ya makutaniko 16. Mengine zaidi ya 30, pamoja na Jumba la Kusanyiko lenye kuvutia, yanapangwa kujengwa.

Jicho Likiwa Limekaziwa Ufalme wa Mungu

“Muda mfupi baada ya Wende,” asema Mzee mmoja Mkristo, “watu wengi waliikataa Biblia. Waliweka tumaini lao katika serikali mpya, iliyoahidi hali bora zaidi hatimaye.” Je! tumaini lao lilitimizwa? “Katika muda wa miaka miwili walibadili maoni yao. Sasa watu hukubaliana nasi kwamba serikali za kibinadamu haziwezi kamwe kuleta amani na uadilifu.”

Watu wengi mno walishangilia wakati ujamaa mgumu katika Ujerumani Mashariki uliposhindwa, wakikaribisha kile walichoona kuwa kipindi chenye mafanikio cha itikadi ya Magharibi. Lakini walikata tamaa. Haidhuru ni serikali gani inayotawala, Mashahidi wa Yehova huweka jicho lao likiwa sahili na kukaziwa kikiki Ufalme wa Mungu, ung’aao kama nyota mbinguni. Tumaini hilo halitakatisha tamaa kamwe.—Warumi 5:5.

[Maelezo ya Chini]

a Ona “Yehova Alitutunza Chini ya Marufuku,” Sehemu 1-3, katika Mnara wa Mlinzi matoleo ya Aprili 15, Mei 1, na Mei 15, 1992.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mashahidi katika Ujerumani wanatumia uhuru wao ili kuhusika zaidi na zaidi katika utendaji wa Ufalme

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki