“Kuliko Mji wa Nguvu”
“KWA viwango vya sasa, karibu asilimia 40 ya watoto wa U.S. watashuhudia mvunjiko wa ndoa za wazazi wao kabla ya wao kufikia [miaka] 18.” (Science, Juni 7, 1991) Hiyo ni takwimu yenye kuogopesha kama nini! Kwa nini hilo hutukia?
Hakimu wa mahakama ya familia na ya kushughulikia wasia Edward M. Ginsburg, alitoa maoni yake alipohojiwa na The Boston Globe. Alisema hivi: “Sisi ni jamii yenye ubinafsi. Twataka [mambo] kwa ajili ‘yangu.’ Twauliza, ‘Mimi nitafaidikaje sasa?’ Twataka kuridhishwa mara iyo hiyo.”
Ubinafsi huo ambao si wenye ukomavu huongoza kwenye uchungu na ugomvi katika ndoa. Hakimu Ginsburg asema kwamba wenzi wa ndoa wafikiapo mahakama ya talaka mwishowe, mume na mke wataka kutetewa. Wao wataka mtu fulani awaambie kwamba wao ndio wanasema kweli na kwamba mwenzi wao ndiye amekosea. Wao wataka mtu fulani aseme: “Umeshinda pigano.”
Maneno yake yatukumbusha mithali moja iliyopuliziwa: “Ndugu aliyechukizwa ni mgumu kuliko mji wa nguvu; na mashindano ni kama mapingo ya ngome.” (Mithali 18:19) Ndiyo, ugomvi ufyatukapo katika ndoa, wale wanaopigana waweza kukosa kuwa wenye kusababu ifaavyo na kuwa wagumu. Mara nyingi, wao hukataa katakata kuafikiana, kama vile “mji wa nguvu” uliozingiwa.
Je! hali yapaswa iwe hivyo? La, kuna njia tofauti. Ndoa ni zenye nguvu na zenye kudumu wakati wote wawili wanapoyatii tangu mwanzo, maneno haya ya mtume Paulo: “Iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.” (Waefeso 4:32) Je! ni rahisi kukuza sifa hizo? Sivyo sikuzote. Lakini talaka ni rahisi kadiri gani? Mizigo ya kihisiamoyo na ya kifedha iletwayo na ndoa iliyovunjika huumiza kadiri gani? Na namna gani watoto, ambao mara nyingi huendelea kuathiriwa vibaya na talaka ya wazazi wao kufikia maisha yao ya utu mzima?
Ni bora zaidi kwa wenzi wote wawili kujitahidi kuhifadhi ndoa na wasikatae kuafikiana, kama vile “mji wa nguvu.” Shauri hili la Paulo kwa Wakristo latumika hasa kwa waume na wake waliooana: “Jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.”—Wakolosai 3:14.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]
The Complete Encyclopedia of Illustration/J. G. Heck