Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Mungu alimwonya Kaini kwamba ‘dhambi ilikuwa ikimwotea mlangoni, nayo ilimtamani yeye,’ ambalo laonekana kurejezea hayawani-mwitu na windo lake. (Mwanzo 4:7) Kwa nini hiyo lugha itumiwe ikiwa kabla ya Furiko, wanyama walikula mimea pekee?
Katika vitabu vilivyoandikwa na Musa, twapata mistari kadhaa inayoonyesha mambo ya hakika au matukio ya kihistoria ambayo huenda yakaonekana hayafai katika kikao chayo cha kihistoria.
Kwa kielelezo, masimulizi kwenye Mwanzo 2:10-14 yatoa mambo madogo-madogo ya kijiografia juu ya bustani la Edeni. Musa aliandika kwamba mto mmoja ulikuwa “ndio unaopita mbele ya Ashuru.” Lakini bara la Ashuru lilipata jina lalo kutoka kwa Ashuru, mwana wa Shemu aliyezaliwa baada ya Furiko. (Mwanzo 10:8-11, 22; Ezekieli 27:23; Mika 5:6) Yaonekana, katika masimulizi yake sahihi yaliyopuliziwa, Musa alitumia tu neno “Ashuru” kurejezea mkoa uliofahamiwa na wasomaji wake.
Fikiria kielelezo kingine kutoka kwa sura za mapema za Mwanzo. Baada ya Adamu na Hawa kutenda dhambi na kuondoshwa kwenye bustani, Yehova aliwazuia wasirudi. Jinsi gani? Mwanzo 3:24 lasema hivi: “Akamfukuza huyo mtu, akaweka Makerubi, upande wa mashariki wa bustani ya Edeni, na upanga wa moto uliogeuka huko na huko, kuilinda njia ya mti wa uzima.” Angalia, “upanga wa moto.” Je! Mungu ndiye alibuni panga?
Hatuhitaji kukata maneno kwamba Muumba wetu mwenye upendo ndiye alikuwa wa kwanza kubuni panga jinsi tunavyozijua. Adamu na Hawa waliona kitu chenye moto kikizunguka mbele ya malaika. Hilo lilikuwa nini hasa? Kufikia wakati Musa alipoandika kitabu cha Mwanzo, panga zilijulikana sana na zilitumiwa katika vita. (Mwanzo 31:26; 34:26; 48:22; Kutoka 5:21; 17:13) Kwa hiyo maneno ya Musa “upanga wa moto” yaliwezesha wasomaji wake kwa kadiri fulani waone akilini kile kilichokuwako kwenye mwingilio wa Edeni. Habari iliyojulikana katika siku ya Musa ilichangia uelewevu wa mambo hayo. Na ni lazima lugha ambayo Musa alitumia ilikuwa sahihi, kwani Yehova aliitia ndani ya Biblia.—2 Timotheo 3:16.
Namna gani Mwanzo 4:7? Hapo Mungu alimwonya Kaini hivi: “Ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde.” Kama ilivyoonyeshwa, lugha yaonekana ikifanya wonyesho wa taswira ya hayawani-mwitu mwenye njaa akinyemelea ili kumrukia na kumla windo lake.
Hata hivyo, ithibati katika Biblia huonyesha kwamba Adamu na Hawa walikuwa na amani pamoja na wanyama wote. Huenda ikawa baadhi ya wanyama walihisi starehe sana wakiwa karibu na wanadamu, hata wakinufaika na kuishi karibu nao. Wengine walikuwa hayawani-mwitu, wanyama waliotafuta kwa asili makazi yaliyo mbali na wanadamu. (Mwanzo 1:25, 30; 2:19) Lakini, Biblia haidokezi kwamba wanyama wowote waliwinda wanyama wengine au wanadamu. Mwanzoni, Mungu alipanga chakula cha wanyama na watu pia kiwe mimea hasa. (Mwanzo 1:29, 30; 7:14-16) Hilo halikubadilika mpaka baada ya Furiko, kama vile Mwanzo 9:2-5 lionyeshavyo.
Namna gani basi, onyo la Mungu kwa Kaini, jinsi tusomavyo kwenye Mwanzo 4:7? Kwa hakika taswira ya hayawani mkali ambaye amenyemelea akiwa tayari kumrukia windo ingalikuwa rahisi kueleweka katika siku za Musa, nasi pia twaielewa. Kwa hiyo, mara nyingine tena, huenda ikawa Musa alikuwa akitumia lugha ambayo ingewafaa wasomaji waliofahamu ulimwengu wa baada ya Furiko. Na hata ikiwa Kaini hakuwa ameona kamwe kiumbe cha jinsi hiyo, yeye angaliweza kuelewa onyo lililofananisha ile tamaa yenye dhambi aliyokuwa nayo, na hayawani mwenye njaa, atafutaye chakula.
Sehemu za msingi zipaswazo kutuathiri zaidi ni hizi: Fadhili isiyostahiliwa ya Mungu katika kumwonya Kaini, thamani ya kukubali shauri kwa unyenyekevu, jinsi wivu uwezavyo kumfisidi mtu kwa urahisi, na jinsi tupaswavyo kuchukua kwa uzito maonyo mengine ya kimungu ambayo Mungu alituwekea katika Maandiko.—Kutoka 18:20; Mhubiri 12:12; Ezekieli 3:17-21; 1 Wakorintho 10:11; Waebrania 12:11; Yakobo 1:14, 15; Yuda 7, 11.