Je! Waweza Kuonyesha Saburi?
YEHOVA alimwambia Abramu: “Toka wewe katika nchi yako . . . uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako.” (Mwanzo 12:1, 2) Abramu alikuwa mwenye miaka 75 wakati huo. Yeye alitii na kwa hekima akaonyesha saburi maisha yake yote, akimngojea Yehova.
Hatimaye, Mungu alitoa ahadi hii kwa Abrahamu (Abramu) mwenye saburi: “Hakika yangu kubariki nitakubariki, na kuongeza nitakuongeza.” Na mtume Paulo aliongeza hivi: “Na hivyo kwa kuvumilia [kuonyesha saburi, Abrahamu, NW] akaipata ile ahadi.”—Waebrania 6:13-15.
Saburi ni nini? Kamusi huifasili kuwa uwezo “wa kungojea kitu kwa utulivu” au wa kudhihirisha “uvumilivu baada ya uchokozi au mkazo.” Kwa hiyo saburi yako hutahiniwa inapobidi umngoje mtu fulani au kitu fulani, au unapochokozwa au unapokuwa chini ya mkazo. Katika hali hizo mtu mwenye saburi huendelea kuwa mtulivu; yule asiye na saburi huwa mwenye haraka-haraka na mwenye kukasirika haraka.
Ulimwengu Wetu wa Kisasa Usio na Saburi
Hasa katika maeneo mengi ya jijini, mkazo huwekwa juu ya mwendo wa kasi, si saburi. Kwa mamilioni ya watu wanaoishi katika majiji yaliyosongamana watu, kila siku huanza wakati kengele ya saa inapogonga asubuhi. Hiyo huanzisha mwendo wa mbio-mbio—kwenda mahali fulani, kuona mtu fulani, kutimiza jambo fulani. Je! ni ajabu kwamba wengi wanahangaika na hawana saburi?
Je! wewe hukasirika wengine wanapokukosea? “Mimi sipendi mtu akichelewa,” asema Albert. Wengi wangekubali kwamba kumngojea mtu fulani ambaye amechelewa huleta mkazo, hasa ikiwa kuna jambo la kutimizwa kabla ya wakati fulani. Kuhusu Mtawala wa Newcastle, aliyekuwa mwanasiasa Mwingereza wa karne ya 18, ilisemwa hivi: ‘Yeye hupoteza nusu saa kila asubuhi, naye hujaribu kuikomboa mchana kutwa lakini hafanikiwi.’ Kama ungelazimika kumtegemea mtu kama huyo siku kwa siku, je, ungeendelea kuwa mwenye saburi?
Unapoendesha gari, je, wewe hukasirishwa upesi, husita kungoja, au unashawishwa kusafiri kwa mwendo wa kasi mno? Katika hali hizo, mara nyingi kukosa saburi huleta msiba. Wakati wa 1989, katika ile iliyokuwa wakati huo Ujerumani Magharibi, aksidenti zaidi ya 400,000 za barabara kuu zilitokeza majeraha au kifo. Kati yazo, 1 katika 3 zilisababishwa na kuendesha ama kwa kasi mno ama karibu mno na gari lililokuwa mbele. Kwa hiyo, angalau kwa kadiri fulani kukosa saburi kulisababisha majeraha au vifo vya watu zaidi ya 137,000. Hasara kubwa kama nini kwa sababu ya kukosa saburi!
“Mimi huona vigumu kuendelea kuwa mwenye saburi mtu anaponikatiza wakati wote,” alalamika Ann, “au mtu fulani anapojisifu sana.” Karl-Hermann akiri kwamba saburi yake hutahiniwa na “vijana wasio na heshima kwa wazee-wazee.”
Hali hizo na nyinginezo zaweza kukufanya ukose saburi. Basi, wewe waweza kusitawishaje saburi zaidi?
Yehova Aweza Kuimarisha Saburi Yako
Watu wengi hufikiri kwamba saburi huonyesha kutoweza kufanya uamuzi au kuwa dhaifu. Hata hivyo, kwa Yehova, hiyo huonyesha nguvu. Yeye mwenyewe “huvumilia [ni mwenye saburi, NW] . . . maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.” (2 Petro 3:9) Kwa hiyo, ili kuimarisha uvumilivu wako mwenyewe, kaa karibu na Yehova na umtegemee kwa moyo wako wote. Kuimarisha uhusiano wako na Mungu ni hatua moja iliyo ya maana zaidi ili kusitawisha mwelekeo wenye saburi.
Isitoshe, ni jambo la maana kujua makusudi ya Yehova kwa ajili ya dunia na wanadamu. Abrahamu “alikuwa akiutazamia mji wenye misingi [Ufalme wa Mungu], ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu.” (Waebrania 11:10) Vivyo hivyo, itanufaisha kuona waziwazi ahadi za kimungu na kuridhika kumngojea Yehova. Ndipo utang’amua kwamba badala ya kuonyesha hali ya kusita-sita, saburi hasa huwaelekeza watu kwenye ibada ya kweli. Kwa hiyo, “uhesabuni uvumilivu wa [saburi ya, NW] Bwana wetu kuwa ni wokovu.”—2 Petro 3:15.
Vipi ikiwa hali zako za kibinafsi zatahini saburi yako karibu kufikia upeo? Je! wasioamini hukuletea mkazo wenye kutaabisha? Je! umekuwa na ugonjwa wa muda mrefu unaoonekana kama hauishi? Katika hali kama hiyo, zingatia moyoni yale ambayo mwanafunzi Yakobo aliandika. Baada ya kurejezea kigezo ambacho manabii walitoa katika kuonyesha saburi, yeye alifunua siri ya kubaki mtulivu chini ya mkazo mkubwa. Yakobo alisema hivi “Mtu wa kwenu amepatikana na mabaya? na aombe.”—Yakobo 5:10, 13.
Mwombe Mungu kwa bidii aimarishe saburi yako na akusaidie udhibiti hali yako ya moyo ukiwa jaribuni. Mgeukie Yehova mara kwa mara, naye atakusaidia utambue hali au tabia za wengine zinazotisha hasa utulivu wako. Kusali kabla ya kukabili hali zinazoelekea kuwa zenye kujaribu kwaweza kukusaidia ubaki mtulivu.
Maoni Yafaayo Juu Yako na Wengine
Ili kudumisha mtazamo wenye utulivu, ni lazima ujione wewe na wengine katika njia inayofaa. Hiyo yawezekana kupitia funzo la Biblia, kwani hiyo huonyesha kwamba kila mtu amerithi kutokamilika na hivyo ana udhaifu mbalimbali. Zaidi ya hiyo, ujuzi wa Biblia utakusaidia ukue katika upendo. Sifa hiyo ni ya maana ili kuwaonyesha wengine saburi.—Yohana 13:34, 35; Warumi 5:12; Wafilipi 1:9.
Upendo na hamu ya kusamehe yaweza kukutuliza unapokasirika. Ikiwa mtu fulani ana tabia zinazokuudhi, upendo utakukumbusha kwamba ni tabia hizo usizopenda, wala si mtu mwenyewe. Fikiria ni mara ngapi udhaifu wako mwenyewe unavyojaribu saburi ya Mungu na kuwaghadhabisha wengine.
Pia maoni yaliyo sahihi juu yako mwenyewe yatakusaidia kungoja kwa saburi. Mathalani, je, umekuwa ukifikilia mapendeleo katika utumishi wa Yehova, na hufanikiwi? Je! unaona saburi yako ikifikia mwisho? Ikiwa ndivyo, basi kumbuka kwamba shina la kukosa sana saburi ni kiburi. Sulemani alisema hivi: “Ni afadhali mtu mwenye saburi kuliko yule mwenye roho ya kiburi.” (Mhubiri 7:8, NW) Naam, kiburi ni kizuizi kikubwa cha kusitawisha saburi. Je! si kweli kwamba ni rahisi zaidi kwa mtu mnyenyekevu kungoja kwa utulivu? Kwa hiyo, sitawisha unyenyekevu, na utaweza kukubali vema zaidi kukawizwa ukiwa na amani ya akili.—Mithali 15:33.
Saburi Huleta Thawabu Nyingi
Abrahamu ajulikana hasa kwa sababu ya imani yake. (Warumi 4:11) Lakini saburi ilifanya imani yake idumu. Thawabu yake ilikuwa nini kwa sababu ya kumngojea Yehova?
Yehova alizidi kumtumaini Abrahamu. Hivyo jina la Abrahamu likawa kuu na wazao wao wakawa taifa kubwa. Mataifa yote ya dunia yaweza kujibarikia kupitia mbegu yake. Abrahamu alitumikia akiwa msemaji wa Mungu na hata akiwa kifani cha Muumba. Je! kungaliweza kuwa na thawabu nyingine kubwa zaidi kwa ajili ya imani na saburi ya Abrahamu?
“Bwana ni mwingi wa rehema” kuelekea Wakristo wanaovumilia majaribu kwa saburi. (Yakobo 5:10, 11) Watu kama hao huwa na dhamiri safi kwa sababu ya kufanya mapenzi yake. Kwa hiyo katika hali yako, ukimngojea Yehova na kuvumilia majaribu kwa saburi, uvumilivu wako utatokeza kibali na baraka za Yehova.
Saburi hutumikia watu wa Mungu vizuri katika kila upande wa maisha. Watumishi wawili wa Yehova, waitwao Christian na Agnes, waligundua hilo walipoamua kuchumbiana. Walikawiza uchumba wao kwa sababu ya staha yao kwa wazazi wa Christian waliohitaji wakati wa kupata kumjua Agnes. Tendo hilo lilikuwa na tokeo gani?
“Ni baadaye tu ndipo tulipong’amua jinsi saburi yetu ilivyokuwa ya maana kwa wazazi wetu,” aeleza Christian. “Kungoja kwetu kwa saburi hakukuharibu uhusiano kati ya mke wangu nami. Bali kulikuwa jiwe la kwanza la ujenzi katika uhusiano wetu na wazazi wangu.” Naam, saburi huleta thawabu nyingi.
Saburi pia huendeleza amani. Familia na marafiki watafurahi kwamba hauzushi ugomvi juu ya kila udhaifu wao. Utulivu na uelewevu wako, wakati wengine wanapofanya makosa utazuia hali zenye kuaibisha. Mithali moja ya China husema: “Kuonyesha saburi kunapokuwa hasira kutakuepusha siku mia moja za masikitiko.”
Saburi huboresha utu wako, na hukusaidia udumishe sifa zako nyinginezo zikiwa katika hali nzuri. Hiyo hufanya imani yako idumu, amani yako iendelee daima, na upendo wako uwe usiotikisika. Kuonyesha saburi kutakusaidia kuwa mwenye furaha unapoonyesha fadhili, wema, na upole. Kuonyesha saburi huongeza nguvu inayohitajiwa ili kusitawisha ustahimilivu na kujidhibiti.
Basi ngojea kwa saburi utimizo wa ahadi za Yehova, nawe kwa hakika utakuwa na wakati ujao mzuri ajabu. Kama Abrahamu, ‘kupitia imani na saburi, na uzirithi ahadi.’—Waebrania 6:12.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Uhusiano wa karibu pamoja na Yehova utakusaidia kuonyesha saburi, kama vile Abrahamu alivyoonyesha