Mkusanyiko wa Ethiopia “Ufundishajiwa Kimungu”—Wakati wa Shangwe ya Pekee
HUO haukuwa mkusanyiko wa wilaya wa kwanza wa Ethiopia baada ya wao kupata uhuru, lakini kwa hakika ulikuwa wa pekee. Tangu kupata utambuzi wa kisheria mnamo Novemba 11, 1991, Mashahidi wa Yehova walikutana kwa mara ya tatu katika stediamu iliyo kubwa zaidi nchini humo, Stediamu ya Jiji, katika kitovu chenyewe cha Addis Ababa. Kwa kuwa mwanzoni uwanja huu haukuweza kupatikana Jumapili na majengo mengine makubwa vya kutosha hayakuweza kupatikana, programu ilijazanishwa ndani ya siku tatu, kutoka Alhamisi hadi Jumamosi, Januari 13-15, 1994.
Siku hizi tatu hazikuwa tu na halihewa nzuri yenye kiasi chini ya anga buluu bali pia zilikuwa na mnurisho wa kiroho kukiwa na uvutano kamili wa “Ufundishaji wa Kimungu.” Kichwa hicho cha mkusanyiko kilitokeza waziwazi kwa herufi za Kiamhari, kikiwa katika mazingira yenye kuvutia ya mpango wa maua ulioizunguka jukwaa.
Lakini ni nini kilichofanya mkusanyiko huo uwe wa pekee? Pamoja na programu yenye habari nyingi, fikira na hisia za kila mtu zilikaziwa udugu wetu wa kimataifa wenye upendo na yale madhihirisho ya wazi ya baraka ya Mungu juu ya watu wake kwa namna ya ukuzi wa Ufalme. Kulikuwa na wajumbe wageni wapatao 270 kutoka mabara 16, kutia na hata Jibuti na Yemeni. Zaidi ya nusu walitoka katika halihewa yenye baridi kali ya Ulaya na Amerika Kaskazini. Wageni walitia ndani washiriki wawili wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, Lloyd Barry na Daniel Sydlik.
Ukaribishaji-wageni wa kidesturi wa Kiethiopia pamoja na upendo wa kuhisiwa moyoni kuelekea ndugu zao waliokuwa wamezuru ulitokeza shangwe nyingi mno ulioshinda vizuizi vya lugha. Hawakusalimiana kwa mkono tu bali kwa kukumbatiana na kubusiana, hadi mara sita! Wageni wengi walikuwa wamesoma juu ya kazi ya Ufalme katika Ethiopia nao walijua kwamba ndugu zao Waethiopia walikuwa washikaji wa uaminifu-maadili waliotahiniwa na waliokuwa wamedumu kupitia vifungo vya gerezani na namna nyinginezo za mnyanyaso.a Lakini wajumbe waliokuwa wakizuru walishangaa kuona vijana wengi sana wakionyesha nyuso zenye furaha na adabu inayopungua katika mabara mengi leo. Dada wengi Waethiopia walivaa marinda yao meupe ya kitamaduni yaliyotarizwa kwa ustadi, jambo lililoongezea kwelikweli ile roho ya sherehe.
Ubatizo mnamo Ijumaa ulithibitika kuwa wenye kusisimua. Mstari mrefu wa watu 530 waliojiweka wakfu karibuni, kutoka umri wa miaka 10 hadi 80, ulinyooka kufikia nusu ya ule uwanja wa michezo katika stediamu. Hiyo ilikuwa idadi kubwa zaidi ya vile yeyote alikuwa ametazamia—zaidi ya 1 kwa kila Mashahidi 7 nchini. Ulikuwa uthibitisho ulioje wa baraka ya Yehova juu ya watu wake hapa! Kulikuwa na machozi mengi ya shangwe watu walipoona hilo, jambo lililoongezewa uzuri na kule kuimba kuzuri kwa wale wajumbe Waitalia zaidi ya 40. Wengi walifikiria yale maneno ya kiunabii ya Isaya 60:5: “Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, na moyo wako utatetemeka na kukunjuka; kwa kuwa wingi wa bahari utageuzwa kukujia, utajiri wa mataifa utakuwasilia.”
Sababu za Pekee za Shangwe
Baraka ya Yehova ilikaziwa zaidi mnamo Ijumaa, wakati ile mianzo midogo ya kazi ya Ufalme katika Ethiopia ilipopitiwa katika mahojiano. Haya yaliongozwa pamoja na kikundi cha wamishonari wa mapema waliokuwa wametumikia hapo katika miaka ya 1950 na 1970. Watu zaidi ya 8,000 waliwasikia Ray Casson, John Kamphuis, na Haywood Ward wakisimulia kazi yao ya elimu ya Biblia, kuanzia mnamo Septemba 14, 1950, walipowasili Addis Ababa. Serikali ya ubeberu ya siku hizo ilitaka kwamba wawe wenye bidii katika elimu kwa ujumla. Kwa hiyo walianzisha shule kwa ajili ya elimu ya watu wazima katika kitovu cha mji, wakitoa masomo mbalimbali. Lakini walipokuwa hawafundishi, wamishonari hawa walijitahidi kuendeleza elimu iliyokazia ufundishaji wa kimungu. Walilazimika kung’ang’ana kujifunza Kiamhari, lugha iliyo gumu kuelewa ikiwa na herufi za alfabeti 250. Karibu nusu ya mwaka ilipita kabla ya wao kufanikiwa katika kuongoza funzo lao la Biblia nyumbani la kwanza. Karibu miaka 43 baadaye, walikutana na watu barabarani waliokumbuka hawa waliokuwa walimu wa shule hapo awali. Lakini kwenye mkusanyiko, walishangilia kuungana pamoja tena na wale waliokuwa wanafunzi wao wa Biblia hapo awali waliokuja kuwa watu imara katika imani, na waliowajulisha kwa watoto na wajukuu wao wenyewe wa kiroho.—1 Wathesalonike 2:19, 20.
Wale wasikilizaji wenye shangwe na wenye usikivu sana walipiga makofi kwa muda mrefu si kwa sababu tu ya yale mahojiano pamoja na wale waliokuwa wamishonari bali pia kwa sababu ya zile ripoti na salamu zilizotoka Israeli, Italia, Kanada, Kenya, Marekani, Uholanzi, Uingereza, na Ujerumani—zilizoletwa na wawakilishi wageni. Hilo lilikazia tena ule udugu wa ulimwenguni pote wenye upendo wa watu wa Mungu. Hotuba kuu zilizotolewa na ndugu watiwa-mafuta kutoka kwa Baraza Linaloongoza, pamoja na sala zao zenye kuhisiwa moyoni, ziligusa sana mioyo ya wasikilizaji pia. Vijana katika stediamu hiyo waliweza kujishirikisha na waigizaji katika ile drama juu ya vijana wanaomkumbuka Muumba wao, drama hiyo ikiwa imetolewa kwa njia ya asili sana na yenye uchangamfu. Kwa kuongezea vitolewaji vipya katika Kiingereza, vitolewaji vipya vitatu vya Kiamhari vilisababisha idili nyingi.b
Katika vipindi vya pumziko na nyakati nyinginezo, kulikuwa na fursa nzuri za kufahamiana na watu wengi mmoja-mmoja wenye thamani kubwa. Mathalani, hapohapo kwenye mstari wa kwanza, akiwa na bakora iliyofanyizwa kwa mikono, paliketi mhubiri mkongwe zaidi katika Ethiopia, Tulu Mekuria. Mwaka uliopita, akiwa na umri wa ukongwe sana wa 113, yeye alibatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwenye mkusanyiko huu alikuwa na shangwe ya kumwona mke wake mwenye umri wa miaka 80 akifuata kielelezo chake, akiwa dada yake wa kiroho pia. Kuwapo kwake muda wa programu yote ulikuwa kichocheo kizuri kwa wale wenye umri mdogo zaidi. Mmoja wao alikuwa Yohanes Gorems, ambaye akiwa na umri wa 16 na akiwa bado ni mwanafunzi wa shule ametumikia kwa miaka minne tayari akiwa mhubiri aliye painia wa kawaida. Yeye na mapainia wengine wenye umri wa kwenda shuleni ambao hata ni wenye umri mdogo zaidi wamejifunza kununua wakati ufaao, kama vile kwa kutoa ushahidi mapema asubuhi wakiwa njiani kwenda shuleni au kwa kutumia vipindi mbalimbali vya pumziko na baada ya saa za shule.
Ni Vielelezo Vilivyoje vya Uaminifu-Maadili!
Mamia ya wasikilizaji walikuwa wamejionea vifungo vya gerezani na mateso wakiwa chini ya serikali zilizopita. Mandefro Yifru akumbuka miaka mitano ya jinsi hiyo akiwa gerezani, lakini sasa yeye hufurahia kutumikia katika Addis Ababa katika ile ofisi iliyoanzishwa hivi karibuni, itunzayo utafsiri, uchapishaji, na usafirishaji. Kijana mwingine anayetumikia pamoja naye, Zecarias Eshetu, hakuachilia uaminifu-maadili wake miaka minane iliyopita wakati baba yake alipouawa kimakusudi kwa ajili ya kudumisha kutokuwamo kwa Kikristo muda wa miaka mitatu akiwa gerezani. Zecarias, aliye mmoja kati ya watoto watano, alikuwa na umri wa miaka kumi wakati baba yake alipoenda gerezani. Meswat Girma na dada yake, Yoalan, wakiwa sasa katika miaka yao ya mwisho-mwisho ya utineja na wakiwa shuleni bado, humkumbuka baba yao kutokana na picha pekee, kwani walikuwa wadogo sana alipouawa kwa ghafula kwa ajili ya kutokuwamo kwake. Uaminifu-mshikamanifu wake uliwachochea, na wote wawili wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida, kama vile baba yao alivyokuwa akifanya wakati wa kifo chake.
Mshikaji wa uaminifu-maadili mwingine alikuwa Tamirat Yadette, anayetumikia akiwa painia wa pekee katika mkao wenye kupendeza wa Bonde la Ufa. Kwa sababu ya kutokuwamo kwake kwa Kikristo, yeye alitumia miaka mitatu akiwa katika magereza saba tofauti-tofauti, nyakati nyingine akiwa amefungwa minyororo na kupigwa vikali sana. Hata hivyo, akiwa gerezani yeye alisaidia watu zaidi ya 12 wachukue msimamo wao kwa ajili ya Ufalme wa Mungu.
Tesfu Temelso, anayetumikia sasa akiwa mwangalizi wa mzunguko, alifungwa gerezani mara 17 muda wa miaka yake akiwa painia wa pekee. Yeye ana makovu kutokana na mapigo, lakini anasisimuka kuona makutaniko katika migawo yake ya awali. Ndugu na dada wengi kutoka Kutaniko la Akaki walipatwa na vifungo vya gerezani na ukatili, hata hivyo kutaniko hilo limeongezeka kufikia wahubiri zaidi ya mia moja. Wamejenga Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwanza katika Ethiopia. Kutoka Dese, mji ulio katika mazingira bora sana karibu kilometa 300 kaskazini mwa jiji kuu, kulikuja kikundi cha watu watano waliokabili kifo na kumwona ndugu wa mahali hapo akifa kutokana na mateso aliyotendwa. Mzee mmoja miongoni mwao, Maseresha Kasa, alieleza kwamba alidumu muda wa kifungo cha gerezani cha miaka sita, lakini si kwa sababu alikuwa wa kipekee kwa njia yoyote ile, bali kwa sababu tu alijifunza kumtegemea Yehova.—Warumi 8:35-39; linganisha Matendo 8:1.
Hata hivi karibuni, wengine wameonyesha uaminifu wao wakiwa chini ya mtihani. Kikundi kikubwa kilikuja mkusanyikoni kutoka katika nchi ya karibu ambako, kwa sababu ya kutokuwamo kwao, Mashahidi walikuwa wamenyimwa ulinzi wa polisi, hati za kusafiri, hati za ndoa, utibabu wa hospitali, na kazi. Vita ilipokuwa ikipiganwa karibu na Mesewa, iliyo bandari ya Eritrea kwenye Bahari Nyekundu, kutaniko zima, lenye jumla ya watu 39, kutia na watoto, waliishi kwa karibu miezi minne chini ya daraja lenye kimo cha chini jangwani ili kuponyoka lile mimino la makombora juu ya nyumba zao lililosababishwa na serikali ya awali. Katika mazingira haya ya jangwani yenye joto na unyimivu, mazungumzo yao juu ya andiko la siku na mikutano mingine iliwapa nguvu nyingi na ushikamano wa karibu na Yehova na pia kati ya mmoja na mwenzake. Dada mapainia wa pekee wawili waliokuwa wakitumikia karibu na chanzo cha Blue Nile walivumilia matisho kutoka kwa ghasia ya watu na usumbufu uliochochewa na Kanisa Orthodoksi, lakini hao wawili walidumu wakawaona wanafunzi wa Biblia kadhaa wakifananisha wakfu wao kwa ubatizo kwenye mkusanyiko huu.
Ndugu mmoja alisimulia jaribu lake la kutengwa mbali na wengine akiwa kazini katika ule mkoa mkavu wa Ogaden ulio barani sana, si mbali na Somalia. Aliendelea kuwa hai kiroho kwa kuhubiri kisha kufanya mikutano pamoja na wale wenye kupendezwa, kutia na madaktari wa kitiba, walionufaika kutokana na ufundishaji wa kimungu na ambao sasa huwafundisha wengine. Kielelezo kingine chema cha ushikaji wa uaminifu-maadili kilikuwa cha painia wa kawaida katika Addis Ababa ambaye, katika 1992, alipigwa kikatili akaachwa kuwa amekufa na ghasia ya watu waliochochewa na mapadri wa dini ya Orthodoksi. Kwa furaha, alipata nafuu naye huendelea akitumikia katika eneo lilo hilo. Ile tabasamu nyangavu usoni pake haifunui uchungu wowote. Kwake yeye, kama ilivyo na wale wengine wote waliotahiniwa na wale walio wapya zaidi, Mkusanyiko huu “Ufundishaji wa Kimungu” ulikuwa sikukuu yenye shangwe.
Mkusanyiko uliongozwa kwa utaratibu, ukifanya wageni wafikirie kwamba wajitoleaji waliohusika walikuwa wamekuwa na miaka mingi ya uzoefu. Kwa kweli, wao wamefanya maendeleo ya haraka katika miaka hii miwili ambayo imepita. Mkusanyiko huo wa siku tatu ulikwisha upesi mno. Hudhurio-kilele mnamo Jumamosi lilikuwa 9,556. Televisheni ya kitaifa, redio, na magazeti ya habari yaliandaa habari yenye upendelevu. Wote waliweza kuona kwamba Yehova alikuwa akiwafanya watu wake watajirike kiroho. Wasikilizaji walitia ndani maelfu ya wenye kupendezwa ambao wameanza kunufaika kutokana na “Ufundishaji wa Kimungu.” Shamba lililo pana limefunguliwa wazi kwa Mashahidi wa Yehova katika nchi hii yenye karibu watu milioni 50, na mkusanyiko uliwaimarisha wote katika azimio lao la kutumia wakati unaobaki katika mfumo huu wa mambo kusaidia wale wenye mioyo myeupe wanufaike pia kutokana na ufundishaji wa kimungu.
[Maelezo ya Chini]
a Ona 1992 Yearbook of Jehovah’s Witnesses, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Kupata Faida Zote za Ujana Wako, Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha, na Mashahidi wa Yehova—Wanafanya Mapenzi ya Mungu kwa Umoja Ulimwenguni Pote.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Addis Ababa, Januari 13-15, 1994
[Picha katika ukurasa wa 24]
Kikundi cha mapainia katika Addis Ababa (kulia); washikaji wa uaminifu-maadili ambao wote walikuwa wamefungwa gerezani (chini); Shahidi mwenye umri wa miaka 113 pamoja na mke wake