Je, Unajifunza Kutokana na Mfunzi Wetu Mtukufu?
“NILIJIFUNZA sheria kwa miaka mitano katika mojapo vyuo vikuu vilivyo bora zaidi katika Hispania,” akaeleza Julio. “Lakini mambo niliyojifunza nilipoanza kujifunza Biblia yalikuwa bora zaidi. Chuo kikuu kilinifundisha jinsi ya kusoma; lakini Biblia ilinifundisha jinsi ya kuishi.”
Kupitia Biblia tunaweza kufikia mawazo ya Mungu, kanuni zake, na maagizo yake. Maandiko yamfafanua Yehova kuwa “Mfunzi Mtukufu” kwa sababu yeye ndiye mwalimu bora zaidi katika ulimwengu wote mzima. (Isaya 30:20, NW) Kihalisi, andiko la Kiebrania lamwita Yeye “wafunzi”—neno la wingi lionyeshalo ubora. Hilo lapasa kutukumbusha kwamba kufundishwa na Yehova ni bora sana kuliko kufundishwa na mwalimu mwingine yeyote.
Hekima Yenye Kutumika Kutoka kwa Yehova
Ni kwa nini mafundisho ya kimungu yananufaisha? Kwanza, kwa sababu ya mambo yaliyo nayo yenye thamani sana. Mafundisho ya Yehova hutupa “hekima kamili [“yenye kutumika,” NW].” Isitoshe, hekima ipewayo na Mungu ‘huwahifadhi’ waitumiao.—Mithali 3:21, 22; Mhubiri 7:12.
Mtungaji wa Zaburi 119 aling’amua kwamba hekima ya Yehova ilikuwa imemhifadhi katika maisha yake yote. Kwa kielelezo, yeye aliimba: “Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu, kuliko maelfu ya dhahabu na fedha. Kama sheria yako isingalikuwa furaha yangu, hapo ningalipotea katika taabu zangu. Maagizo yako hunitia hekima kuliko adui zangu, kwa maana ninayo sikuzote. Ninazo akili kuliko wakufunzi wangu wote, Maana shuhuda zako ndizo nizifikirizo.”—Zaburi 119:72, 92, 98, 99.
Si mtunga-zaburi pekee ambaye ‘angalipotea katika taabu zake,’ kama isingalikuwa sheria ya Yehova. Rosa, mwanamke mchanga kutoka Hispania, anasadiki kwamba maisha yake yaliokolewa kwa sababu alizitumia kanuni za kimungu. “Kufikia umri wa miaka 26, tayari nilikuwa nimejaribu kujiua mara mbili,” yeye akumbuka.
Rosa alikuwa amejihusisha na umalaya, pamoja na kileo na dawa za kulevya. “Siku moja, nilipokuwa nimetamauka sana,” yeye asema, “wenzi fulani wa ndoa walio Mashahidi walinizungumzia kuhusu jinsi Biblia iwezavyo kutusaidia kutatua matatizo yetu. Nilianza kujifunza Neno la Mungu, nalo lilinistaajabisha sana. Kwa muda wa mwezi mmoja nilipata nguvu ya kuanza upya maisha safi yaliyo mapya kabisa. Sasa kwa vile nilikuwa na kusudi maishani, sikuhitaji tena kutegemea kileo au dawa za kulevya. Na kwa kuwa nilitaka sana kuwa rafiki wa Yehova, niliazimia kuishi kwa viwango vyake. Kama isingalikuwa hekima yenye kutumika ya Neno la Mungu, nina hakika kwamba kufikia sasa ningekuwa nimejiua.”
Kwelikweli, hekima kutoka kwa Yehova ni yenye kuokoa uhai. Kwa hiyo, twaweza kunufaika, si tu kwa mambo yaliyomo katika ufundishaji wa kimungu wenye thamani sana bali pia kwa njia ambazo Yehova anatumia kufunza watumishi wake. Kwa kuwa Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alituamuru tuwe walimu na wafanya-wanafunzi, twataka kujifunza njia zenye matokeo zaidi ya kufunza.—Mathayo 28:19, 20.
Matumizi ya Yehova ya Vielezi
Gospeli ya Marko yasema kwamba “bila kielezi [Yesu] hakuwa akisema nao.” (Marko 4:34, NW) Haishangazi kwamba Yesu alikuwa na sifa hii katika mafundisho yake. Yeye aliiga mojapo njia ambazo jumbe za kiunabii za Yehova zilivyowasilishwa kwa taifa la Israeli. Hizo zina vielezi kadhaa vyenye kueleweka wazi.—Isaya 5:1-7; Yeremia 18:1-11; Ezekieli 15:2-7; Hosea 11:1-4.
Kwa kielelezo, ona jinsi Yehova atumiavyo kielezi chenye nguvu kutufundisha kwamba sanamu ni bure. Isaya 44:14-17 yasema: “Yeye hujikatia mierezi. . ., hujichagulia mti mmoja katika miti ya msituni; hupanda mvinje . . . Kisha utamfaa mwanadamu kwa kuni; hutwaa kipande, akaota moto; naam, huuwasha moto, akaoka mkate; naam, huufanya mungu, akauabudu; huifanya sanamu ya kuchonga, akaisujudia. Sehemu moja huiteketeza; kwa sehemu nyingine hula nyama; huoka chakula kiokwacho, akashiba. . . . na kwa sehemu iliyobakia hufanya mungu, yaani, sanamu yake ya kuchonga; husujudu mbele yake akaiabudu, akaiomba, akasema, Uniokoe; maana wewe u mungu wangu.” Vielezi kama hivyo ni vifaa vyenye nguvu sana tuwezavyo kutumia katika kusaidia watu wenye mioyo minyoofu kukataa mafundisho bandia.
Maswali ya Kupekua Moyo
Biblia vilevile ina vielelezo vya jinsi Yehova alivyorekebisha kufikiri kwa baadhi ya watumishi wake kwa kuwauliza maswali yachocheayo kufikiri. Mzee wa ukoo Ayubu alikuwa mmoja wa hawa. Yehova alimsaidia kwa saburi achanganue udogo wake kwa kujilinganisha na Mungu. Mungu alifanya hivyo kupitia mfululizo wa maswali, ambayo Ayubu hakustahili hata kidogo kuyajibu.
“Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya nchi?” Yehova alimwuliza Ayubu. “Ni nani aliyeifunga bahari kwa milango? . . . Je! waweza kuufunga mnyororo wa Kilimia, au kuvilegeza vifungo vya Orioni? . . . Je, wewe una mkono kama Mungu?” Mahoji haya ya kunyenyekeza yalitia ndani swali la maana sana: “Utanitia mimi [Yehova] hatiani, upate kuhesabiwa haki?”—Ayubu 38:4, 8, 31; 40:8, 9.
Maswali hayo yenye kupekua sana yalimfanya Ayubu ang’amue kwamba alikuwa amesema bila kuelewa mambo. Kwa hiyo aliyageuza maneno ya kwanza na kutubu. (Ayubu 42:6) Kama ilivyo katika hali hiyo, maswali yaliyoteuliwa vizuri yaweza kusaidia kurekebisha kufikiri kusikofaa kwa upande wa watoto au wanafunzi wetu wa Biblia.
Kujenga Uhakika
Namna gani kama tunahitaji kusaidia mtu anayejihisi hafai au hawezi kutimiza jambo fulani? Yenye msaada katika hali hiyo ni mazungumzo kati ya Yehova na nabii wake Musa. Mungu alipompa Musa mgawo wa kuwa msemaji wake mbele ya Farao na Waisraeli, nabii huyo alihisi hawezi kufanya kazi hiyo. “Mimi si mwepesi wa kusema,” yeye akasema. Lakini, Mungu akajibu: “Ni nani aliyekifanya kinywa cha mwanadamu? . . . si mimi, BWANA? Basi sasa, enenda, nami nitakuwa pamoja na kinywa chako, na kukufundisha utakalolinena.”—Kutoka 4:10-12.
Yehova alimpa ndugu ya Musa Haruni mgawo wa kuwa msemaji wake, nao wakakamilisha kazi yao katika Misri. (Kutoka 4:14-16) Mashahidi wa Yehova wengi wamekuwa na hisia kama za Musa za kujihisi kutostahili wanaposhiriki kwa mara ya kwanza katika huduma ya nyumba kwa nyumba au katika ushahidi wa barabarani. Kama ilivyo na hali ya Musa, kujua kwetu kwamba Yehova anatuunga mkono na kwamba tutaandamana na mhudumu mwenye ujuzi kwaweza kutusaidia kushinda hali yetu ya kusitasita. Jinsi tu Musa alivyoweza kusitawisha uhakika kufikia hatua ya kutoa hotuba zenye nguvu zipatikanazo kotekote katika kitabu cha Biblia cha Kumbukumbu la Torati, kwa msaada wa Yehova sisi pia twaweza kusitawisha uwezo wa kusema.
Somo la Kuonekana Wazi
Tamaa ya moyoni ya kuwasaidia wengine pia ni muhimu sana. Hiyo ni sifa ambayo nabii Yona hakuwa nayo. Yehova alimpa Yona mgawo wa kuonya watu wa Ninawi juu ya uharibifu uliokaribia wa jiji hilo. Kwa kushangaza, Waninawi walitubu. (Yona 3:5) Matokeo yakawa kwamba Yehova aliahirisha msiba huo. Lakini, badala ya kufurahia mafanikio ya kazi yake ya kuhubiri, Yona alihisi kwamba utabiri wake haungetimizwa. Yehova alimsaidiaje kuwa na maoni mazuri?
Yehova alitumia mtango kumfundisha Yona umuhimu wa kujali wengine. Mtango huo ulikua kimwujiza kwa usiku mmoja tu na kuandaa kivuli chenye kuburudisha kwa Yona, ambaye alikuwa ametengeneza vyungani vya Ninawi. Yona akaanza ‘kufurahi sana’ kwa sababu ya mtango huo mdogo. Lakini Yehova akasababisha buu fulani liharibu ule mtango hivi kwamba ukakauka. Akihatarishwa na jua na upepo wenye joto jingi, Yona alikasirika na kusema: “Ni afadhali nife mimi kuliko kuishi.” (Yona 4:5-8) Somo lilikuwa nini kati ya mambo haya yote?
Yehova alisema na Yona akamwambia hivi: “Wewe umeuhurumia mtango, ambao hukuufanyia kazi, wala kuuotesha; uliomea katika usiku mmoja, na kuangamia katika usiku mmoja; na mimi, je! haikunipasa kuuhurumia Ninawi, mji ule mkubwa; ambamo ndani yake wamo watu zaidi ya mia na ishirini elfu, wasioweza kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto; tena wamo wanyama wa kufugwa wengi sana?”—Yona 4:9-11.
Ni somo lenye kuonekana wazi lenye nguvu kama nini! Yona alipendezwa zaidi na mtango kuliko maelfu ya watu. Ingawa ni sawa kuhangaikia sehemu yoyote ya uumbaji wa Mungu, kusaidia kuokoa maisha ya watu ni kazi yetu iliyo muhimu zaidi.
Kufundisha kwa Saburi
Kama Yona alivyogundua, si rahisi nyakati zote kutimiza huduma yetu. (2 Timotheo 4:5) Lakini, mtazamo wa saburi kuelekea wengine utasaidia.
Unaitikiaje wakati mmojapo wanafunzi wako wa Biblia hashiki mambo kwa haraka au kwa njia fulani haelewi vizuri? Mfunzi Mtukufu wetu hutufundisha jinsi ya kushughulika na tatizo kama hilo. Yeye alionyesha saburi isiyo ya kawaida wakati Abrahamu alipokuwa akimwuliza-uliza maswali kuhusu uharibifu uliokuwa ukikaribia wa Sodoma na Gomora. “Je! utaharibu mwenye haki pamoja na mwovu?” Abrahamu akauliza. “Huenda wakawapo wenye haki hamsini katika mji,” Abrahamu akasihi. “Utauharibu wala hutauacha mji kwa ajili ya hao hamsini wenye haki waliomo?” Jibu la Yehova lilimchochea Abrahamu aendelee kumsihi mpaka idadi ilipopunguzwa hadi kumi. Yehova alijua kwamba ni familia ya Loti pekee iliyostahili kuhifadhiwa, na maandalizi yalikuwa yamefanywa kwa kusudi hilo. Lakini kwa saburi Mungu alimruhusu Abrahamu aendelee kumwuliza maswali mpaka alipofahamu ukuu wa rehema ya Yehova.—Mwanzo 18:20-32.
Yehova alifahamu udogo wa uelewevu wa Abrahamu na hisia zake zenye hangaiko. Sisi pia tukifahamu mapungukio ya mwanafuzi wetu, hayo yatatusaidia kuonyesha saburi huku akijitahidi kuelewa fundisho fulani au kushinda zoea lililomshika sana.
Endelea Kujifunza Kutoka kwa Yehova
Bila shaka Yehova Mungu ni Mfunzi Mtukufu. Kupitia njia kama vielezi, maswali, na masomo ya vitu vionekanavyo, yeye hutupa uelewevu kwa saburi. Kwa kadiri ambayo twaiga njia zake za kufundisha, sisi wenyewe tutakuwa walimu bora zaidi.
Kwa kuwa wale wafundishao wengine hawapaswi kupuuza kujifunza wenyewe, ni lazima tuendelee ‘kufundishwa na Yehova.’ (Isaya 54:13) Isaya aliandika hivi: “Macho yako yatawaona waalimu wako [“Mfunzi Mtukufu,” NW]; na masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii, ifuateni mgeukapo kwenda mkono wa kulia, na mgeukapo kwenda mkono wa kushoto.” (Isaya 30:20, 21) Kwa kuendelea kutembea katika njia ya Yehova na kuwasaidia wengine kufanya hivyo, twaweza kuwa na pendeleo la pekee la kujifunza kutokana na Mfunzi Mtukufu wetu kwa milele.
[Picha katika ukurasa wa 28]
Yehova alimwuliza Ayubu: “Je! tai hupaa juu kwa amri yako, na kufanya kioto chake mahali pa juu?”
[Picha katika ukurasa wa 28]
Kwa kupitia mtango, Yehova alimfundisha Yona kuhangaikia watu zaidi