Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 3/15 kur. 21-24
  • Sisi Hatustaafu!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sisi Hatustaafu!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Kinachowafanya Wafurahi
  • Utayari wa Kujirekebisha
  • Kustahimili Chini ya Matatizo ya Afya
  • Hangaiko Linaloendelea
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 3/15 kur. 21-24

Sisi Hatustaafu!

“SISI HATUSTAAFU” ndiyo taarifa unayopata unapotembelea makao fulani yasiyo ya kawaida katika Tokyo, Japani. Familia moja ya wanaume na wanawake 22, wenye umri wa wastani wa miaka 70, waishi huko. Wameunganishwa si kwa uhusiano wa kifamilia bali na upendezi wa aina moja—utumishi wa mishonari. Wamevumilia katika kazi ya kuhubiri wakati wote kwa jumla ya miaka 1,026! Washiriki watatu walio na umri mkubwa zaidi walizaliwa katika 1910. Saba kati yao walianza utumishi wao wa wakati wote wakiwa matineja. Tisa kati yao wameona ukuzi wa kazi ya kuhubiri Ufalme katika Japani tangu mwanzo wayo baada ya Vita ya Ulimwengu 2.—Isaya 60:22.

Hata hivyo, hili jengo la orofa sita lililokuwa zamani tawi la Watch Tower ni mahali pa kitia moyo, hasa kwa sababu ya roho, ule mwelekeo unaoenea, wa wamishonari wanaoishi hapo. Ingawa wengi wao hawajiwezi kikamili kwa sababu ya umri na afya mbaya, hakuna yeyote wa mashujaa hawa wa kiroho aliye tayari kuacha. Mashahidi Wajapani wamewajengea upya kabisa jengo hili, wakiwaandalia Jumba la Ufalme katika orofa ya chini na lifti.

Kinachowafanya Wafurahi

Baada ya kuwa katika mgawo wao kwa miaka mingi, hawa wamishonari wanahisi kwamba hapa ndipo nyumbani kwao. “Niliporudi Australia kwa ajili ya mkusanyiko wa wilaya wakati wa kiangazi kilichopita,” akasema mmoja wa washiriki wa familia hiyo aliye mzee-mzee kuliko wote, “baada ya majuma mawili nilikuwa tayari kurudi nyumbani!” Wanawapenda watu wanaotumikia na wamesitawisha shauku yenye kina sana kwao. Wamishonari wote hufurahia barua na simu zinazowakumbusha matendo ya siku zilizopita.

Hilo ndilo tokeo la huduma yenye juhudi. Wakisukumwa na upendo kwa Yehova, wamishonari hao wamehubiri Neno la Mungu kwa uharaka chini ya hali tofauti-tofauti. (Linganisha 2 Timotheo 4:2.) “Tulijizoeza kuwa wenye shangwe kwa sababu tu tunamtumikia Yehova,” asema Vera MacKay, aliyetumika katika Japani kwa miaka 37. “Hata ikiwa hakuna anayekuja mlangoni, tupo hapo kutoa ushahidi kuhusu Yehova.”

Kumi na wawili wa wamishonari hawa hawajawahi kuolewa, lakini wanafurahi kuweza kumtumikia Bwana bila kukengeushwa fikira. (1 Wakorintho 7:35) Gladys Gregory, aliyetumika akiwa mishonari kwa miaka 43, ni mmoja wao. Yeye asema hivi: “Ili niwe na uhuru mwingi kwa ajili ya utumishi wa Yehova, niliingia katika kazi ya upainia, baadaye nikaenda Gileadi [Watchtower Bible School of Gilead], kisha kwenye kazi ya mishonari. Bila kuwa nimeweka nadhiri yoyote ya kukaa mseja, nimedumisha useja, na kama ilivyo kwa marafiki kadhaa, sijajutia jambo hilo.”

Utayari wa Kujirekebisha

Ingawa watu fulani huwa wenye kusumbua wanapozeeka, wamishonari wamekuwa tayari kujirekebisha. Lois Dyer, Molly Heron, na Lena na Margrit Winteler walikuwa katika kao dogo la mishonari katika makazi ya Tokyo. Waliishi huko kwa zaidi ya miaka 20 nao wakawapenda watu wa mahali hapo. Katika maeneo yao, akina Winteler, waliokuwa dada za kimwili, walikuwa na watu 40 wa kuwapelekea magazeti kwa ukawaida, na Molly na Lois walikuwa na 74 wa kuwapelekea magazeti. Halafu, Sosaiti ikawauliza wahamie kwenye makao hayo ya mishonari ya orofa sita kitovuni mwa Tokyo. “Nilihuzunika na kukosa furaha mwanzoni,” akubali Lena. Hata hivyo, kama ilivyokuwa wakati wote, walijirekebisha kwenye mgawo wao mpya. Wanahisije sasa? “Wenye shangwe sana,” ajibu Lena. “Sasa ndugu wawili wa Betheli wako hapa kutupikia na kutusafishia nyumba. Tunatunzwa vizuri.” Wote wanakubaliana na Lois, anayesema: “Ule utunzi wenye upendo tunaopewa na tengenezo la Yehova hutusaidia kuvumilia.”

Norrine Thompson pia alijirekebisha kwenye hali mpya. “Kwa miaka 15,” yeye asema, “nilikuwa na pendeleo la kuandamana na mume wangu [kutoka New Zealand] katika kazi ya wilaya wakati Japani yote ilikuwa wilaya moja tu.” Hata hivyo, afya ya mume wake ikaharibika, ikambidi ashinde jaribu kubwa zaidi kuliko yote katika maisha yake—kifo cha mumeye miaka 18 iliyopita. “Wakati huo,” yeye asema, “kilichonisaidia kuendelea katika kazi ya mishonari ulikuwa upendo nilioonyeshwa na ndugu kotekote Japani, kutia na sala na kuwa na shughuli nyingi katika utumishi.”

Kustahimili Chini ya Matatizo ya Afya

“Wengi wao wana aina fulani ya tatizo la afya, lakini ni wachangamfu, na tamaa yao ya kutumika ni sifa yenye kutokeza,” asema Albert Pastor, mwangalizi wa makao ya mishonari. Ili kutunza wamishonari, daktari mmoja na mkeye, aliye muuguzi, wamepewa mgawo katika makao hayo.

Siku moja miaka mitatu iliyopita, Elsie Tanigawa, mhitimu wa darasa la 11 la Shule ya Gileadi, kwa ghafula alipofuka jicho lake la kushoto. Miezi minne baadaye, jicho lake la kuume pia liliathiriwa. “Nyakati nyingine mimi hushuka moyo kwa kiasi fulani kwa sababu siwezi kutumika kama nilivyofanya wakati mmoja. Lakini nikiwa na maandalizi yote yenye fadhili ya Sosaiti na msaada wenye upendo wa mwenzi wangu na wengineo, naendelea kupata shangwe katika utumishi wa Yehova,” asema Elsie.

Shinichi Tohara na mkeye Masako, waliokuwa wanadarasa wenzi wa Gileadi wa Elsie, wamekabili majaribu mengi kuhusu afya yao kwa muda wa miaka michache iliyopita. Kwa Shinichi, msemaji mwenye uwezo, ni jambo gumu sana kutoweza kuona maandishi yake kwa sababu ya kupungukiwa uwezo wa kuona. Ingawa amefanyiwa upasuaji mkubwa na mdogo katika miaka ya karibuni, macho yake hung’aa anapozungumza kuhusu mwanafunzi wa Biblia mwenye umri wa miaka 90 anayemsaidia sasa.

Wajapokuwa na “mwiba katika mwili,” wamishonari hawa huona udhaifu wao kama mtume Paulo alivyoona, na kusema: “Niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu.” (2 Wakorintho 12:7-10) Na nguvu nyingi wanazo kwelikweli! Wanakuwa wameamka saa moja kila siku kwa ajili ya ibada ya asubuhi. Baada ya kiamsha kinywa, wale wanaoweza huenda katika huduma ya shambani ya asubuhi mapema.

Richard na Myrtle Shiroma ni miongoni mwa wale waendao katika huduma kwa kawaida. Myrtle amepatwapatwa na ugonjwa wa ghafula wa moyo unaosababishwa na kufinyaa kwa mishipa ya ubongo katika 1978, lakini aliandamana na mumeye katika kazi ya mzunguko hadi Novemba 1987. Sasa Richard, aliye na umri wa miaka 70, humsaidia Myrtle kufanya kila kitu. Yeye huamka saa 11:00 asubuhi, anamwondoa kitandani, anamwosha, anamvisha nguo, anamtia virembeshi kwenye uso wake, na kumlisha kwa kijiko. Kisha anamtoa nje katika kiti chake cha magurudumu kwa ajili ya utumishi wa shambani kila asubuhi, wakienda nyumba kwa nyumba kwa muda wa kama saa moja na baadaye kutolea watu ushahidi katika vituo vya basi. Myrtle hawezi kuzungumza, lakini maneno ya mwisho aliyosema yalikuwa Dendo, dendo, maneno ya Kijapani yanayomaanisha “Kuhubiri, kuhubiri.”

Binti yao, Sandra Sumida, amehamia katika makao ya mishonari kuwasaidia. Mume wa Sandra alikufa hivi karibuni kutokana na ugonjwa wa moyo. Anathamini mpango wenye fadhili wa Watch Tower Society kwa kumpa mgawo wa kurudi Japani kutoka Guam, ambako ametumika akiwa mishonari pamoja na mumeye. “Sikuzote nilihisi sikushiriki vya kutosha katika kusaidia wazazi wangu kwa sababu nilikuwa Guam,” yeye asema. “Dada yangu, Joanne, aliwatunza katika makao haya. Hivyo fursa ilipotokea, nilihisi vyema. Kuhisi nahitajiwa hapa kumekuwa dawa kwangu tangu kifo cha ghafula cha mume wangu.”

Hangaiko Linaloendelea

Ingawa wamishonari wanahisi matokeo ya hali ya umri wa uzee, wanakataa kuacha roho yao ya mishonari. (Zaburi 90:10; Warumi 5:12) Jerry na Yoshi Toma, waliokuwa wa kwanza miongoni mwa wahitimu wa Gileadi kuja Japani, bado huenda katika eneo la biashara mjini Shibuya. “Tulipokuja kwenye jengo la orofa mbili lililokuwa hapa katika 1949, tulienda pango kwa pango. Sasa Tokyo imebadilika kuwa jiji kuu. Tumezeeka na hatuwezi kufanya mengi kama tulivyofanya zamani. Lakini tunaporudi kutoka kuhubiri, huwa tumeburudika sana,” asema Yoshi.

Lillian Samson amekuwa mishonari katika Japani kwa miaka 40 naye huonea shangwe sana huduma yake. “Sasa ninamsaidia mwanamke wa umri wa miaka 80 aliyejifunza na mwenzi wangu, Adeline Nako, aliyerudi Hawaii kumtunza mama yake aliye mgonjwa. Mwanamke huyu amekuwa mhubiri wa Ufalme karibuni baada ya kushinda tatizo la kuabudu mababu waliokufa. Yeye alienda hekaluni na kumwambia mke wa kuhani, ‘Mimi nimekuwa Mkristo!’” Akiwa na shangwe kama hizo maishani mwake, Lillian hajapata kamwe kughairi siku ile alipoacha kazi ya kimwili akiwa na umri wa miaka 19, na kuanza kupainia.

Ruth Ulrich na Martha Hess, wenzi wamishonari kwa zaidi ya miaka 45, wametumika kutoka makao haya ya mishonari kwa miaka 35. Wao wamejisitawisha vizuri katika eneo hilo. Siku moja mwangalizi wa mzunguko alimwambia Martha hivi: “Naweza kuomba uso wako niende nao mlango kwa mlango?” Watu waliujua uso wa Martha nao walikuja kwake kuchukua magazeti, huku ikiwa vigumu kwa mwangalizi wa mzunguko kuanzisha mazungumzo.

Ruth ana mwanamke mmoja anayempelekea magazeti kwa ukawaida na ambaye hawezi kusoma kwa sababu ya matatizo yake ya afya. Bado mwanamke huyo anaendelea kupokea magazeti na hata alikubali kitabu chenye jalada gumu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu. Ruth alishindwa kujua ikiwa alipaswa kuendelea kupeleka magazeti kwa sababu hakuna aliyeonekana akisoma fasihi. Halafu siku moja mume wa mwanamke huyu akamwendea Ruth akiwa na kitabu Kutafuta, akasema: “Hiki ni kitabu cha ajabu! Nimekisoma chote mara mbili.” Ruth alianzisha funzo la Biblia pamoja naye na mkeye.

Makao haya ya mishonari yenyewe huvutia watu wenye kupendezwa. Jioni moja, kijana mmoja alikuja kwenye makao hayo na kusema: “Nimeambiwa kwamba nikija hapa, naweza kupata msaada wa kujifunza Biblia.” Alianza kufundishwa Biblia. Akiwa mpishi katika mkahawa wa Kichina, yeye alifanya kazi na mwanamke mmoja aliyekuwa ametengwa na ushirika kwa muda wa miaka mingi. Magazeti yaliyoangushwa wakati mhubiri alipoenda kwenye mkahawa huo yalifika jikoni. Mpishi huyo kijana akayapenda naye akaanza kumuuliza maswali yule aliyekuwa Shahidi zamani. Akiwa hawezi kuyajibu, akamwambia atembelee makao ya mishonari. Sasa kijana huyo anatumika akiwa mtumishi wa huduma na painia. Muda si muda, mwanamke huyo aliyetengwa na ushirika alirudishwa katika tengenezo, na mwishowe akawa painia wa kawaida.

Wamishonari wote katika makao hayo wanathamini yale Yehova amewafanyia. Walitoka Australia, Kanada, Hawaii, Uswisi, na Marekani, na 11 walitoka katika darasa la 11 au madarasa ya mapema zaidi ya shule ya mishonari ya Gileadi. Wao wameona kuendelea kwa kazi ya Ufalme katika Japani nao wanashiriki maneno ya Mfalme Daudi, aliyesema: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.” (Zaburi 37:25) Kwa uthamini wa utunzi wa Mungu wenye upendo, wamishonari hawa wameazimia kutostaafu bali kuendelea mbele kumtumikia Yehova.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki