Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 4/15 kur. 7-9
  • Shangwe Akibani kwa Wale Waipatao Ile Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Shangwe Akibani kwa Wale Waipatao Ile Kweli
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mafundisho ya Kweli ya Biblia Huleta Shangwe
  • Kanuni za Kweli za Biblia Huleta Shangwe
  • Shangwe Lazima Isitawishwe
  • Kushughulika na Hali Mwenzi wa Ndoa Anapokusaliti
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • ‘Endelea Kutembea Katika Kweli’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Shiriki Shangwe ya Kutoa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Shangwe​—Sifa Inayotoka kwa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 4/15 kur. 7-9

Shangwe Akibani kwa Wale Waipatao Ile Kweli

KATIKA chumba chake cha juu, Mfinland mmoja alipata kitabu The Divine Plan of the Ages. Alianza kukisoma papo hapo, na baada ya muda mfupi alijiambia, ‘Hii ni kweli; hii ni kweli.’ Aliposhuka kutoka chumba cha juu, alimwambia mkeye, “Nimeipata dini ya kweli.”

Njia ambayo mtu huyu aliipata kweli ni ono lisilo la kawaida, lakini Mashahidi wa Yehova walio wengi wangeweza kusimulia mwitikio kama huo. Wote wanaweza kukuambia juu ya shangwe ipatikanayo kwa kuipata kweli. Maono yafuatayo yanaonyesha jambo hilo.

Mafundisho ya Kweli ya Biblia Huleta Shangwe

Margarita Königer alilelewa Munich, Ujerumani, wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Kupigwa bomu na uchomaji wa nyumba yalikuwa mambo ya kawaida. Ndugu yake alikufa vitani. Alipokuwa akihudhuria ibada za kanisa za Katoliki, alisikia sala zikisemwa kwa niaba ya wanajeshi Wajerumani na kwa kiongozi, Hitler. Baada ya vita, alipata udhamini wa kuhudhuria chuo kimoja katika Marekani ikiwa sehemu ya programu ya kubadilishana wanafunzi. Aligundua kwamba watu walikuwa wenye urafiki kwake, hivyo alishangaa ni kitu gani kilichochochea watu, ambao tamaa yao ya asili ni kuishi kwa amani, kutoaminiana na kuchukiana wakati wa kipindi cha vita. Aliporudi Munich, alikutana na Mashahidi wa Yehova, na kupitia funzo la Biblia pamoja nao, alipata majibu kwa maswali yake. Yeye asema: “Nilionyeshwa katika Biblia kwamba nguvu za roho waovu zinahusika . . . Biblia huwaita ‘wakuu wa ulimwengu’ na, kwa kweli, husema kwamba Shetani ‘anaudanganya ulimwengu wote.’ . . . Nikiona matendo ya mataifa na ya watu yasiyo ya kimungu, ya kishetani, jibu hilo ni lenye kufikiri kuzuri na la kuridhisha kama nini!”—Waefeso 6:12; Ufunuo 12:9.

Margarita aendelea kusema: “Nilipata shangwe kubwa kujifunza juu ya uandalizi wa Mungu wa kutatua matatizo ya dunia. La, haitakuwa kupitia kwa akili na usimamizi wa kibinadamu, kama vile ionyeshwavyo na waelimishaji wa kilimwengu. Badala ya hivyo, Biblia huonyesha kwamba serikali mpya ya kimbingu itasimamia mambo ya dunia. . . . Yesu Kristo aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi: ‘Ufalme wako uje.’ . . . Nikaanza kuona kwamba ufalme huu ni serikali halisi na kwamba ni kupitia huo tu ndiyo amani ya kweli ya ulimwenguni pote itapatikana.” Kwa kipindi cha karibu miaka 30, Margarita ametumika akiwa mishonari katika nchi tano za Afrika—akitumia miaka 19 ya mwisho kuitangaza kweli kwa watu wanyenyekevu wa Ouagadougou, Burkina Faso.

Ono la Margarita si la kipekee. Wengi wameitikia kwa uchanya vivyo hivyo walipogundua kwamba makasisi wa Jumuiya ya Wakristo katika sehemu zote mbili za vita huomba Mungu wapate ushindi. Wenye mioyo minyoofu huona sababu nzuri ya maelezo ya Biblia kwamba Mungu hahusiki katika vita vya wanadamu bali kwamba hivi hutokea kwa sababu “dunia yote hukaa katika yule mwovu” kuwa yenye kusababu kuzuri. Hawa wenye kuitafuta kweli hujifunza kwamba Wakristo wa kweli hawapaswi kuwa “wa ulimwengu” bali kudumisha kutokuwamo katika mambo yayo. Wakitambua kwamba Mashahidi wa Yehova wamechukua msimamo huo, hawa wapya wenye kupendezwa husadiki kwamba wameipata kweli. Hawa hukua katika tumaini na shangwe wanapopata ujuzi ulioongezeka kuhusu sababu ya Mungu kuruhusu uovu na jinsi hivi karibuni atakavyoleta hali za amani na uadilifu duniani kupitia Ufalme wake.—1 Yohana 5:19; Yohana 17:16; Mathayo 6:9, 10.

Kanuni za Kweli za Biblia Huleta Shangwe

Daniel Rosero wa Ekuado alihisi kwamba maisha hayakuwa na maana, hivyo alianza kunywa kupindukia. Kanisa alilokuwa akihudhuria lilimfundisha kwamba jambo moja tu alilokuwa akitazamia lilikuwa kifo na moto wa helo. Yeye aliitikia, “Nitachomeka, hivyo acha ninywe!” Yeye alikuwa na familia ya watu wanane ambayo hakuwa akiitunza, naye sikuzote alikuwa akipigana na mkeye, Delia. Badiliko lilitokea Jumapili moja asubuhi walipotembelewa na Mashahidi wa Yehova na kuanza kujifunza Biblia. Mara ya kwanza Daniel alipohudhuria kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova, alitambua kwamba alikuwa ameipata kweli. Yeye asema: “Tengenezo hilo lilinishangaza. Watu walipatana, wengi, pamoja. Ungeweza kuhisi upendo katika umati huo. Hakuna aliyevuta sigareti. Hakuna lugha chafu. . . . Nakumbuka nikiwazia, ‘Hii ndiyo kweli!’ Si woga wa kifo au wa mwisho wa ulimwengu ulionisukuma. Ilikuwa ni usafi wa tengenezo hilo.”

Familia yote ya Rosero ikawa Mashahidi wa Yehova. Maisha yao ya familia na hali yao ya kiuchumi ikaboreka walipotumia kanuni za Biblia. Delia Rosero asema: “Unajua kuboreka kote kwa maisha yangu ni kwa sababu ya kweli ya Biblia. Nani ajuaye watoto wangu wangekuwa wapi bila Neno la Mungu? Wote saba wamebatizwa na ni wenye usawaziko. Kweli imeniletea maisha mapya na furaha mpya kabisa.”

Ono hilo la familia ya Rosero si la kipekee. Wengi katika siku yetu wanatatizwa na matatizo. Sababu moja ni kwamba viwango vya maadili vinavyotolewa na Biblia haviheshimiwi tena, kama vilivyoheshimiwa na vizazi vya mapema. Dini nyingi zimefuata mwelekeo huu, ama kwa kuachilia mambo ama kwa sababu wanahisi kwamba kwa sababu za hali kubadilika maadili ya kale hayatumiki. Kwa hiyo, kama vile wengineo, familia ya Rosero waliachwa wapapase-papase bila mwongozo wa Biblia. Hata hivyo, watu wanyenyekevu kama hao wanapokuja kufahamu maoni ya Mungu juu ya maadili na maisha ya familia, bila kukawia wanatumia yale wanayojifunza. Kutokana na masimulizi hayo twaweza kuona matokeo mazuri ya kufanya hivyo.

Shangwe Lazima Isitawishwe

Hata hivyo, hii haimaanishi kwamba Mkristo huhisi shangwe daima. Bila shaka, matatizo ambayo watu kwa jumla hukabili, kama vile ukosefu wa kazi, ugonjwa, na kifo, huathiri Wakristo vilevile. Wakristo pia lazima waingie katika pigano la kuendelea dhidi ya hali za kutokamilika na udhaifu wao. Simulizi la Biblia lasema kwamba Loti ‘alihuzunishwa sana na mwenendo wa ufisadi wa hao wahalifu’ katika jiji la Sodoma. Wakristo waaminifu hawawezi kuzuia hisia kama hizo waonapo hali mbovu zikienea.—2 Petro 2:7, 8.

Hata hivyo, waliopata kweli wana faida. Kwa kielelezo, mwamini anayeombolezea mtu fulani aliyekufa hahitaji ‘kuhuzunika kama wengine wasio na matumaini.’ Huzuni yake haitakuwa bila mipaka. Ndivyo ilivyo kuhusu matatizo mengine pia. Mtu aliyeipata kweli anajua kwamba magumu ya sasa ni ya muda tu. Tumaini hufanya iwe rahisi kuvumilia chini ya matatizo. Mtindo-maisha uliosawazika pia husaidia.—1 Wathesalonike 4:13.

Paulo aliwapa Wakristo himizo hili: “Furahini katika Bwana sikuzote; tena nasema, Furahini.” (Wafilipi 4:4) Hili laonyesha kwamba ingawa sisi sote twaweza kupata shangwe, inawezekana pia tuikose. Masumbufu ya mfumo huu wa mambo yaweza kuwa kikwazo. Kwa kuongezea, Biblia hutuambia kwamba twahitaji kusitawisha shangwe, mojapo ya matunda ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Ukiendelea kutwaa ujuzi wa ile kweli na kujikumbusha juu ya utajiri wa kiroho iliyokuletea na inaendelea kukuletea, shangwe yako haitapungua. Itaongezeka zaidi tukaribiapo wakati ambapo Mungu “atafuta kila chozi” katika macho ya watu na wakati “maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Wengi huvutiwa na shangwe na mpango mzuri katika makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki