Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 4/15 uku. 29
  • “Kuuza Chumvi” Katika Msumbiji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kuuza Chumvi” Katika Msumbiji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 4/15 uku. 29

“Kuuza Chumvi” Katika Msumbiji

FRANCISCO COANA, mshiriki wa halmashauri ya nchi ya Msumbiji, alikuwa katika “kambi za kuelimishwa upya” kwa miaka kumi. Aeleza ono lake: “Nilijua tungekaa hapa kwa muda mrefu, kwa hiyo nilimwuliza mwangalizi wa mzunguko ikiwa ningeweza kuendelea na upainia wa kawaida. Lakini ningeweza kuwekaje wakati wa kutosha katika huduma ya peupe, kwa kuwa karibu kila mtu katika kambi alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova? Nilisema kwamba ningeenda Milange, mji ulio umbali wa kilometa 47, kutafuta watu wa kuwahubiri.

“Ingawa hatukuruhusiwa kisheria kuondoka kambini peke yetu, sheria hiyo haikufuatwa kimakini. Naweza kukumbuka nikienda kichakani, nikipiga magoti, na kusali ili nipate njia ya kuhubiria wenyeji. Upesi Yehova akajibu.

“Nilikutana na mtu aliyekuwa na baiskeli nami nikafanya mapatano naye. Alikubali kwamba kama ningelima shamba lake la robo-tatu ya hektari kabla ya msimu wa mvua, angelipa kwa kunipa baiskeli yake. Kwa hiyo kila asubuhi nililima mashamba yake. Yehova alibariki mpango huo, kwa kuwa hatimaye nilipata baiskeli yangu.

“Matokeo yalikuwa kwamba niliweza kufikia mji mkubwa wa Milange na kuendelea na upainia wangu kwa matokeo katika shamba hili lenye mazao. Kwa kuwa kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku, ilikuwa lazima nitafute mbinu ya kueleza watu kweli. Huku vitabu na magazeti yakiwa yamefungwa ndani ya shati langu, niliweka chumvi katika mfuko na kuanza kuuza chumvi. Badala ya kuiuza kwa meticais 5, nilitoza meticais 15. (Kama ingekuwa bei rahisi mno, watu wangeinunua yote, na ningekosa chumvi ya kutumia katika kuhubiri!) Mazungumzo yangu yalikuwa namna hii:

“‘Habari! Nauza chumvi leo.’

“‘Bei gani?’

“‘Meticais 15.’

“‘Hapana. Hiyo ni ghali sana!’

“‘Ndiyo, nakubali ni ghali. Lakini ukifikiri ni ghali sasa, ngoja kwa muda fulani kwa sababu itakuwa ghali zaidi katika wakati ujao. Je, ulijua jambo hili lilitabiriwa katika Biblia?’

“‘Sijapata kusoma hiyo katika Biblia yangu.’

“‘Ndiyo, imo. Kalete Biblia yako, nikuonyeshe.’

“Kwa hayo mazungumzo yangeanza tukitumia Biblia yake, ili yangu ibaki ndani ya shati langu. Ningerejezea Ufunuo sura ya 6, kuhusu hali za hatari na ukosefu wa chakula. Nikitambua itikio zuri, ningetoa Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele au Good News to Make You Happy na kuanzisha funzo la Biblia kamili.

“Matokeo yakawa kwamba niliweza kuanzisha kikundi cha watu 15 wenye kupendezwa katika Milange. Lakini haikuchukua muda mrefu kabla wenye mamlaka kutambua utendaji wetu. Siku moja nilipokuwa nikiongoza funzo la Biblia, polisi waliingia ghafula na kutushika. Sisi sote, kutia na watoto wadogo wa familia hiyo, tulipelekwa katika jela ya mahali hapo. Baada ya kukaa huko kwa mwezi mmoja, sisi sote tulirudishwa kambini tena.”

Maono hayo hayakupunguza bidii ya ndugu zetu. Badala ya hivyo, Francisco na familia yake, pamoja na maelfu ya ndugu zao waliokuwa katika kambi, sasa wanaabudu na kuhubiri kwa uhuru katika Msumbiji.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki