Familia Zenye Uaminifu Zaharakisha Ukuzi Katika Sri Lanka
ILIYOITWA Ceylon hadi 1972, Sri Lanka ni kisiwa chenye kupendeza chenye bichi zilizozingirwa na aina ya minazi, mfululizo wa milima, na majangwa madogo-madogo. Kwenye sehemu zilizoinuka, Adams Peak, chenye kimo cha meta 2243, ni mahali patakatifu kwa dini nne kubwa.a Karibu na hapo pana Mwisho wa Ulimwengu, ambao ni mharara ambapo genge la mawe hushuka kwa kina kirefu sana zaidi ya meta 1500. Mahali hapo ni mojapo sehemu zenye kupendeza sana za Sri Lanka.
Wakaaji milioni 18 wa Sri Lanka wana asili yenye kupendeza. Tangu karne ya tano K.W.K., watu wa asili ya Kihindi na Kizungu kutoka kaskazini mwa India wameishi katika kisiwa hicho. Wao ni Wasinhala, ambao sasa ni robo tatu ya wakaaji wa huko. Halafu, kufikia mwisho wa karne ya 12, kulikuwa kumekuja kikundi kikubwa cha Watamil kutoka kusini mwa India; hawa sasa wanaishi hasa upande wa kaskazini na mashariki mwa kisiwa hicho. Wareno, Waholanzi, na Waingereza pia waliacha uvutano wenye kudumu tangu siku za ukoloni. Kuongezea hayo, mabaharia kutoka Uarabuni na peninsula za Maleya wanakaa miongoni mwa wenyeji wa huko. Pia kuna vikundi vya Wazungu, Waparsi, Wachina, na wengineo.
Zaidi ya mchangamano wa jamii, lugha na dini katika Sri Lanka kuna asili mbalimbali za watu. Lugha kubwa katika kisiwa hicho ni Kisinhala, Kitamil, na Kiingereza. Wasri Lanka walio wengi huzungumza angaa mbili za lugha hizo tatu. Asili za kikabila pia zina fungu kubwa katika dini za watu hao. Wasinhala wengi ni wa dini ya Buddha, huku wengi wa Watamil ni Wahindu. Kwa kawaida wale wenye asili ya Waarabu au ya Maleya hufuata Uislamu, na wale wa asili ya Kizungu kwa ujumla ni washiriki wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, Ukatoliki na Uprotestanti.
Kuikabili Kazi Yenye Kusisimua
Hali hizo zote hutokeza mwito mkubwa kwa Mashahidi wa Yehova katika Sri Lanka. Wao hufanya kazi kwa bidii ili watimize amri hii ya Yesu: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Wajapokabili lugha hizo mbalimbali, wahubiri wa habari njema huenda wakazungumza na Wabuddha, Wahindu, washiriki wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, na vilevile wakanao kuwapo kwa Mungu—hayo yote kwa muda wa saa chache za kuhubiri.
Ili wapate matokeo katika huduma yao, wahubiri hao lazima wabebe magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na fasihi nyinginezo za Biblia katika Kitamil, Kisinhala, na Kiingereza. Wale wawezao kubeba mzigo mzito hubeba hata Biblia katika lugha hizo. Wahubiri hao majuzi walipata shangwe nyingi sana wakati broshua Je! Kweli Mungu Anatujali? na Our Problems—Who Will Help Us Solve Them? na ile trakti Je! Ulimwengu Huu Utaokoka? zilipotangazwa katika lugha hizo tatu wakati huohuo. Hilo liliwapa vifaa vingi vya kazi.
Mashahidi wamefanya kazi kwa bidii tangu 1912, wakati Charles Taze Russell, aliyekuwa msimamizi wa International Bible Students Association wakati huo, alipotembelea Ceylon kwa muda mfupi. Hata hivyo, ukuzi wenye kutokeza haukuonekana hadi wahitimu wa Watchtower Bible School of Gilead walipofika huko katika 1947. Tangu hapo, wahubiri katika Sri Lanka wamefurahia matokeo mazuri kutokana na kazi yao ya kuhubiri. Katika 1994 wahubiri wa Ufalme 1,866 waliongoza, kwa wastani, mafunzo ya Biblia nyumbani 2,551 kila mwezi. Na hudhurio la Ukumbusho la 6,930 lilikuwa karibu mara nne ya idadi ya wahubiri katika makutaniko yote. Ni baraka ya ajabu jinsi gani!
Ikilinganishwa na nchi nyinginezo, maendeleo katika Sri Lanka huenda yakaonekana kuwa ya chini. Kisababishi kimoja chaelekea kuwa ushikamano wenye nguvu wa kifamilia. Hata hivyo, ushikamano wa kifamilia waweza kuwa wenye manufaa pia. Afisa wa jeshi la Kiroma Kornelio alipochukua msimamo wake kuelekea kweli, familia yake ilimuunga mkono. (Matendo 10:1, 2, 24, 44) Kitabu cha Matendo pia hutaja familia nyingine za Kikristo zenye nguvu, kutia ndani ile ya Lidia, Krispo, na yule mlinzi wa gereza la Paulo na Sila.—Matendo 16:14, 15, 32-34; 18:8.
Kwa kweli, ushikamano wenye nguvu wa kifamilia huenda ukawa na faida palipo na utaratibu mzuri na udumifu mwaminifu. Akifikiria na maneno ya Isaya 60:22, (NW) mishonari wa muda mrefu Ray Matthews aonelea hivi: “Inaonekana kwamba sasa Yehova anaharakisha mambo kwa wakati unaofaa, si kwa watu mmoja-mmoja tu bali pia kwa familia nzima-nzima.”
Familia Zenye Utaratibu Zaleta Sifa
Bila shaka kuna familia kama hizo zenye uaminifu katika Sri Lanka leo. Kwa kielelezo, kuna familia ya Sinnappa yenye utaratibu mzuri iishiyo katika Kotahena, eneo la Colombo, jiji kuu la Sri Lanka. Ingawa kichwa cha familia hiyo, Marian, alikufa hivi karibuni, mkeye, Annamma, na watoto wao 12 kati ya wale 15, wenye umri kuanzia miaka 13 hadi 33, wanaendelea kutumikia Yehova wakiwa familia nzima. Wakati huu, watoto wanane wamebatizwa, na watatu ni watumishi wa wakati wote, wakitumika wakiwa mapainia wa kawaida. Wengine watatu huchukua utumishi wa painia-msaidizi mara kwa mara. Miongoni mwa wachanga wa familia hiyo mna wahubiri wanne wasiobatizwa. Kuongezea hayo, wajukuu wanne, ingawa bado ni wachanga sana, wanajifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo katika Kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Colombo North.
Annamma alisikia habari njema za Ufalme kwa mara ya kwanza katika 1978 alipokubali nakala ya Mnara wa Mlinzi. Funzo la Biblia lilianzishwa, na baada ya kumaliza fasihi ya Biblia Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, Annamma aliweka maisha yake wakfu kwa Yehova Mungu na kubatizwa, hivyo akiweka kielelezo cha kwanza kwa wengi wa familia yake.
Kama yule mwanajeshi Kornelio, Annamma ana utaratibu mzuri katika nyumba yake. “Ilitubidi kupanga kwa ajili ya mikutano ya Kikristo na makusanyiko—bila kutaja shule,” Annamma akumbuka. “Ilikuwa shida kupata nguo, lakini kwa baraka ya Yehova tuliweza kushona nguo mpya wakati wa kila kusanyiko. Familia nzima ilifika ikiwa imevalia na kulishwa vizuri—na tabasamu kubwa pia.”
Watoto hao hukumbuka kwa furaha utaratibu wa familia yao. Ili kusaidia familia nzima ihudhurie mikutano ya Kikristo, kwa ujumla wale wakubwa walipewa madaraka ya pekee. Kwa kielelezo, Mangala alifua nguo, na Winnifreda alizipiga pasi. Winnifreda, aliyesaidia pia wale wachanga kuvaa, asema: “Kila mmoja alionekana amevalia vizuri sana walipokuwa wakiondoka nyumbani.”
Maandalizi ya kiroho vilevile yalikuwa na utaratibu mzuri vivyo hivyo. Binti Pushpam, ambaye ni painia wa kawaida sasa, akumbuka hivi: “Kila siku, familia yetu ilifurahia kusoma Biblia na kusoma andiko la Biblia la kila siku pamoja.” Annamma aongeza hivi: “Kila mtoto ana nakala yake mwenyewe ya Biblia, Mnara wa Mlinzi, na vichapo vinginevyo. Mimi husikiliza kwa makini maelezo yao yote kwenye mikutano. Ikifaa, mimi hurudia habari hiyo nyumbani nikitia moyo na kurekebisha. Usiku sisi hukutana kumaliza siku kwa sala ya familia yetu.”
Wale watoto wakubwa ni wenye msaada katika kusaidia Annamma kuandaa elimu nzuri ya Kikristo kwa wote katika familia. Hata hivyo, ratiba hiyo yenye mambo mengi, haizuii tamaa yao ya kushiriki habari njema huko nje. Kwa ujumla, washiriki kadhaa wa familia hiyo huongoza mafunzo 57 ya Biblia nyumbani na watu katika ujirani. Ndugu-mkwe Rajan atoa maelezo haya: “Familia hii huongoza mafunzo ya Biblia yenye maendeleo. Mke wangu, Pushpam, tayari amekuwa na pendeleo la kuona mmoja wa wanafunzi wake akiweka maisha yake wakfu kwa Yehova.”
Lilikuwa jambo lenye kutazamisha sana katika Kotahena wakati familia kubwa kama hiyo iliacha Kanisa Katoliki ya Kiroma. Ingawa kasisi mwenyewe hakutembelea familia hiyo ajue sababu, aliwaambia watu wa kawaida wa kanisa wapeleleze. Mazungumzo kadhaa yalitokea, mengi yakihusu fundisho la Utatu. Sikuzote Annamma alimtegemea Yehova na Biblia kutetea imani yake. Andiko alilopenda sana katika mazungumzo hayo lilikuwa Yohana 17:3.
Familia ya Sinnappa yaonyesha wazi kwamba utaratibu mzuri na bidii-nyendelevu yaweza kuleta matokeo yenye kuridhisha. Kwa jitihada zao zenye bidii, kizazi kipya cha wahubiri wa Ufalme kinakua, hayo yote yakimletea Yehova sifa.
Upinzani Huunganisha Familia Katika Ibada ya Kweli
Familia ya Ratnam inaishi kilometa chache kutoka kwa familia ya akina Sinnappa, katika Narhenpitya, eneo jingine la Colombo. Wao pia mbeleni walikuwa wa Katoliki ya Kiroma. Katika 1982, Mashahidi waliokuwa kwenye huduma ya nyumba kwa nyumba walimkuta Balendran, mume wa binti wa kwanza, Fatima. Funzo la Biblia lilianzishwa pamoja na familia nzima. Baada ya muda mfupi watoto wao watatu walikuwa wakimuuliza nyanya yao Ignasiamal kuhusu jina la Mungu. Watoto hao walipompa jibu kuwa ni “Yehova,” waliamsha kupendezwa kwa nyanya, na funzo la Biblia lilianzishwa pamoja naye. Baadaye, binti zake wawili, Jeevakala na Stella, walijiunga na funzo hilo, na kufikia 1988 wote watatu walibatizwa.
Wakati uleule, Balendran na Fatima walishiriki kweli na dada mwingine wa Fatima, Mallika, na mumeye, Yoganathan. Kufikia 1987 mume na mke huyo walibatizwa, nao wametia ndani ya watoto wao wawili upendo unaoendelea kukua kwa Yehova. Pushpa, dada mwingine wa Fatima, akafuata. Alijiweka wakfu na kubatizwa katika 1990. Alipokuwa Tokyo, mumeye Eka, alitumikia katika kutaniko la Kiingereza, naye Pushpa akamsaidia mwana wao mchanga, Alfred, kukua katika njia ya Yehova.
Kufikia sasa, watoto wanne kati ya kumi wa familia ya Ratnam wamechukua msimamo wao kwa ajili ya ibada ya kweli. Kwa furaha, wengine watatu wanafanya maendeleo mazuri katika mafunzo yao ya Biblia ya kibinafsi. Miongoni mwa wajukuu 11, msichana mmoja, Pradeepa, tayari amebatizwa. Wachanga wengine saba wanapewa maagizo kwa ukawaida kupitia mafunzo ya Biblia ya familia yao. Kwa kuongezea, jumla ya mafunzo 24 ya Biblia nyumbani yanaongozwa pamoja na watu wenye kupendezwa katika ujirani.
Yote hayo hayakutokea kwa urahisi. Mwanzoni, kulikuwa na upinzani wa familia. Baba yao, Muthupillai, na ndugu zao wakubwa walikuwa wakipinga sana yeyote wa familia yao asihudhurie mikutano kwenye Jumba la Ufalme au kushiriki katika kazi ya kuhubiri hadharani. Ingawa upinzani mwingine ulikuwa wa kujali usalama wao binafsi, Muthupillai aongeza hivi: “Nilikuwa nimejitoa kabisa kwa ‘watakatifu’ nami sikukubali familia yangu iache Kanisa Katoliki.” Hata hivyo, sasa anaamini kwamba wanaabudu Mungu wa kweli kwa sababu anaweza kuona faida ambazo imani yao imewaletea.
Kwa kielelezo, wakati mmoja mwenye nyumba walimoishi aliyekuwa wa dini ya Buddha alitisha kuwaondoa kutoka kwa nyumba yake kwa kutumia uchawi. Akaja usiku mmoja na kuweka matunda ya ndimu yenye “uchawi” kuzunguka nyumba hiyo. Hofu ikawashika majirani wenye ushirikina, ambao wote walikuwa wakitarajia tukio baya kupata familia ya Ratnam. Hata hivyo, Ignasiamal alipogundua jambo hilo, yeye na watoto waliyaondoa matunda hayo bila hofu—hakuna tukio baya lililowapata. Tendo lao la ujasiri likawa ushahidi katika eneo hilo, likiwafanya watu wawastahi sana. Stella akaweza kuanzisha mafunzo mawili ya Biblia kwenye ujirani. Kwa kutiwa moyo na jambo hilo, mke wa mwanaye aitwaye Nazeera pia akakubali funzo la Biblia.
Akikumbuka baraka nyingi ambazo familia yake imepata, Ignasiamal aonelea hivi: “Nafurahi sana kuona ukuzi wa kiroho katika familia. Tumebarikiwa na Yehova kwa sababu upinzani umepungua, na umoja wa familia yetu umeongezeka.”
Familia hizi kubwa zimekuwa baraka kama nini. Zimeungana na familia zilizo ndogo, familia zenye mzazi mmoja, na Wakristo waseja wanaojitahidi kwa bidii kuharakisha utangazaji wa habari njema za Ufalme katika “nchi ing’aayo,” kama jina Sri Lanka linavyomaanisha. Pamoja na Wakristo wenzao ulimwenguni pote, Mashahidi Wasri Lanka wanatazamia kurudishwa kwa Paradiso, ambayo hata sasa huenda tukakumbuka tuonapo bichi na milima yenye kupendeza ya Sri Lanka.
[Maelezo ya Chini]
a Bonde kubwa humo lafikiriwa kuwa uwayo wa Adamu, Buddha, Siva, na “Mtakatifu” Thomas, katika hekaya za Kiislamu, Kibuddha, Kihindu, na za kanisa.
[Picha katika ukurasa w24, 25]
Wengi katika Sri Lanka wanaitikia kuhubiri na kufundisha kwa Wakristo