Somo Kutokana na Ndege na Maua
NI KITU gani mara nyingi huhangaisha watu leo zaidi ya mengineyo yote? Kwa walio wengi, ni kuwa na pesa za kutosha kuandalia familia zao au kuweza kuboresha hali yao ya maisha.
Kupata pesa za kutosha kujiandalia na kuandalia familia kulikuwa tatizo kubwa pia Yesu Kristo alipokuwa duniani. Lakini yeye alionya kwamba hangaiko hili linalostahili laweza kuwa sumbuko sana likimaliza mambo ya kiroho. Ili kutoa kielezi cha maana ya hilo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake watazame sana ndege na maua.
Ndege huhitaji kula kila siku—ikilinganishwa wanahitaji zaidi ya chakula tunachohitaji kwa sababu ya uwezo wao wa kuyeyusha chakula haraka mwilini. Zaidi ya hayo, hawawezi kupanda mbegu, hawawezi kuvuna, wala kuweka akiba ya chakula cha wakati ujao. Hata hivyo, kama vile Yesu alivyoona, ‘Baba yetu wa mbinguni huwalisha.’ (Mathayo 6:26) Vilevile, Mungu huyavisha kwa mapambo mazuri zaidi “maua ya mashamba” yaliyo maridadi.—Mathayo 6:28-30.
Yesu atuhakikishia kwamba tukiweka mahitaji ya kimwili mahali pafaapo na kutanguliza mambo ya kiroho, Mungu atahakikisha kwamba sisi pia tuna chakula na nguo tunazohitaji. Ikiwa Yehova Mungu hutunza ndege na maua, kwa kweli atatunza wale wampendao na ‘watafutao kwanza ufalme wake, na haki yake.’ (Mathayo 6:33) Je, unatanguliza masilahi ya Ufalme wa Mungu maishani mwako?