Je, Ni Desturi ya Ibada Isiyo na Maana?
SAKRAMENTI ya ungamo imefanywa na Wakatoliki kwa karne nyingi. Hata hivyo, kwa walio wengi hiyo ni kawaida ya ibada isiyo na maana. Akitafakari ujana wake, mkuu mmoja wa shule ya sekondari aitwaye Bob asema hivi: “Nilikuwa tineja, na hata wakati huo sikulichukua ungamo kwa uzito.” Kwa nini? Kwake, ungamo lilikuwa limekuwa desturi ya ibada isiyo na maana. Yeye aeleza hivi: “Ungamo lilikuwa ni kama kubeba mzigo wako wote uliojaa dhambi hadi kwa mtoza-ushuru katika uwanja wa ndege. Yeye akuuliza maswali kuhusu dhambi zako kisha akuacha upite baada ya kulipa kodi ya vitu ulivyonunua ng’ambo.”
Vivyo hivyo, Frank Wessling, akiandika katika U.S. Catholic, aeleza zoea la ungamo kuwa “mwongozo wa hatua kwa hatua uliorahisishwa kabisa, kuanzia ondoleo la dhambi za kawaida kupitia sala za toba zilizokaririwa hadi tendo la desturi ya ibada la utubio.” Wessling amaliziaje? “Mimi nasadiki kwamba Ungamo linafaidi mtu,” yeye asema. “Lakini njia ambayo Wakatoliki hulifanya haifai.”
Biblia hueleza ungamo kwa njia tofauti kabisa. La maana zaidi ni ungamo kwa Mungu. (Zaburi 32:1-5) Na mwanafunzi Mkristo Yakobo aliandika hivi: “Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana. Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa.”—Yakobo 5:14, 16.
Mkristo aliyelemewa na dhambi aweza kuita waangalizi wa kutaniko, wawezao kutoa shauri la kibinafsi na lenye kutumika kutoka katika Biblia ili kumsaidia mtenda-dhambi aache mwendo wake wa dhambi. Waangalizi hao wanaweza kutoa kitia-moyo kifaacho waonapo maendeleo ya yule anayeugua kiroho. Ni tofauti iliyoje na desturi ya ibada ya ungamo iliyo ya kawaida tu inayozoewa na makanisa leo! Watiwapo nguvu na msaada wa kibinafsi wa wazee wa kutaniko, watenda-dhambi wenye kutubu wanaweza kupata pumziko alilohisi Daudi, kama alivyosema katika zaburi: “Nalikujulisha dhambi yangu, wala sikuuacha upotovu wangu. Nalisema, nitayakiri [“nitaungama,” NW] maasi yangu kwa BWANA, nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu.”—Zaburi 32:5.