Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Mwanafunzi Yakobo alimaanisha nini aliposema: “Ndugu zangu, msiwe waalimu wengi, mkijua ya kuwa tutapata hukumu kubwa zaidi”?—Yakobo 3:1.
Kwa hakika Yakobo hakuwa akiwavunja moyo Wakristo wasiwafundishe wengine kweli. Kwenye Mathayo 28:19, 20, Yesu aliwaamuru wanafunzi wake ‘wakafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, na kuwafundisha kuyashika yote aliyowaamuru.’ Hivyo, Wakristo wote wapaswa kuwa walimu. Mtume Paulo aliwashauri Wakristo Waebrania kwa sababu bado hawakuwa walimu. Yeye aliandika hivi: “Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu.”—Waebrania 5:12.
Basi, Yakobo alikuwa akizungumza juu ya nini? Alikuwa akirejezea wale walio na mapendeleo ya kipekee ya kufundisha kutanikoni. Kwenye Waefeso 4:11, twasoma hivi: “Naye [Yesu Kristo, aliye Kichwa cha kutaniko] alitoa wengine kuwa mitume; na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti; na wengine kuwa wachungaji na waalimu.” Kulikuwa na mapendeleo ya pekee ya kufundisha miongoni mwa makutaniko ya karne ya kwanza kama yalivyo leo. Kwa kielelezo, Baraza Linaloongoza linawakilisha “mtumwa mwaminifu mwenye akili” nalo lina daraka la pekee la kuangalia ufundishaji wa makutaniko ya ulimwenguni pote. (Mathayo 24:45) Waangalizi wasafirio na wazee wa makutaniko pia wana madaraka ya kipekee ya kufundisha.
Je, Yakobo alikuwa akiambia wanaume Wakristo waliostahili kwamba hawapaswi kukubali fungu la kuwa mwalimu kwa ajili ya hofu ya hukumu nzito zaidi ya Mungu? La hasha. Cheo cha mzee ni pendeleo kubwa, kama ionyeshwavyo na 1 Timotheo 3:1, lisemalo: “Mtu akitaka kazi ya askofu [“mwangalizi”, NW], atamani kazi njema.” Moja la matakwa ya kuwekwa rasmi kuwa mzee wa kutaniko ni ‘kujua kufundisha.’ (1 Timotheo 3:2) Yakobo hakupinga maneno ya Paulo yaliyopuliziwa.
Hata hivyo, inaonekana kwamba katika karne ya kwanza W.K., wengine walikuwa wakijipa cheo cha kuwa walimu, ingawa hawakustahili na hawakuwekwa rasmi. Inawezekana, walihisi kwamba kulikuwa na umashuhuri fulani katika fungu hilo, nao walitamani utukufu wa kibinafsi. (Linganisha Marko 12:38-40; 1 Timotheo 5:17.) Mtume Yohana alimtaja Diotrefe, ‘aliyependa kuwa wa kwanza, lakini hakumkubali Yohana.’ (3 Yohana 9) Timotheo wa kwanza 1:7 husema juu ya watu fulani ‘waliopenda kuwa waalimu wa sheria, ingawa hawakuyafahamu waliyosema wala mambo yale waliyoyanena kwa uthabiti.’ Maneno ya Yakobo 3:1 yafaa hasa kwa wanaume watamanio kuwa walimu lakini walio na nia mbaya. Watu kama hao wanaweza kudhuru sana kondoo na hivyo wangepokea hukumu nzito zaidi.—Warumi 2:17-21; 14:12.
Yakobo 3:1 ni kikumbusho kizuri pia kwa wale ambao wamestahili na kutumikia wakiwa walimu. Kwa kuwa wamekabidhiwa mengi, mengi yatatakwa kutoka kwao. (Luka 12:48) Yesu alisema hivi: “Kila neno lisilo maana, watakalolinena wanadamu, watatoa hesabu ya neno hilo siku ya hukumu.” (Mathayo 12:36) Hilo ni kweli hasa kwa wale ambao maneno yao yana uvutano mwingi, wazee waliowekwa rasmi.
Wazee watatoa hesabu ya njia ambayo wanawatendea kondoo wa Yehova. (Waebrania 13:17) Wayasemayo huathiri maisha ya watu. Hivyo, mzee ni lazima awe mwangalifu asipendekeze maoni yake mwenyewe au kutendea vibaya kondoo kama Mafarisayo walivyofanya. Ni lazima ajitahidi kuonyesha upendo wenye kina kama ule Yesu alionyesha. Katika hali yoyote ya kufundisha, na hasa anapohusika katika mambo ya kihalmashauri, ni lazima mzee afikirie maneno yake kwa uangalifu, asitumie maneno ambayo hajayafikiria vizuri au kueleza maoni yake mwenyewe. Kwa kumtegemea Yehova kabisa-kabisa, Neno lake, na miongozo yake kupitia tengenezo lake, mchungaji atapokea baraka nyingi za Mungu, wala si “hukumu kubwa zaidi.”