Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 10/15 kur. 14-17
  • Kufikia Watu wa Aina Zote Katika Athens la Kisasa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kufikia Watu wa Aina Zote Katika Athens la Kisasa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Eneo Lenye Namna-Namna
  • Vitu Vinavyotamanika vya Mataifa Vinaingia
  • Wabarikiwa kwa Matokeo Mazuri
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 10/15 kur. 14-17

Kufikia Watu wa Aina Zote Katika Athens la Kisasa

MTUME Paulo alipotembelea Athens karibu 50 W.K., jiji hilo bado lilikuwa kituo kikubwa cha biashara, ingawaje halikuwa na utukufu walo wa kale. Kitabu fulani cha kihistoria chasema: “[Athens] liliendelea kuwa jiji kuu la Ugiriki lenye mambo ya kiroho, usanii, na vilevile kuwa mahali pazuri pa kutembelewa na watu waliokuwa na elimu na wakuu wa enzi hiyo.”

Alipokuwa huko, huenda Paulo alipata fursa ya kuhubiria Wayahudi, Waathens wapagani, na watu kutoka sehemu nyingi tofauti. Akiwa mwalimu aliye macho na mwenye ufundi, alisema katika hotuba moja kwamba Mungu aliwapa “watu wote uhai na pumzi,” kwamba “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu,” na kwamba “wapaswa wote kila mahali kutubu” kwa sababu Yeye ataihukumu “dunia inayokaliwa.”—Matendo 17:25-31, NW.

Eneo Lenye Namna-Namna

Katika miongo ya karibuni Athens limekuwa tena jiji lenye kuvutia watu kutoka sehemu zote. Wajumbe na wafanyakazi wa kijeshi wameenda huko wakiwa wafanyakazi wa kigeni. Vijana kutoka Afrika na Mashariki ya Kati wanaishi huko wakiwa wanafunzi wa chuo kikuu. Wafanyakazi kutoka nchi za Afrika, Asia, na Ulaya Mashariki wamemiminika huko. Kuna Wafilipino wengi na wengine kutoka Kusini-Mashariki mwa Asia, walioenda kutafuta kazi za nyumbani. Na kuna wakimbizi wengi wanaomiminika daima kutoka nchi za ujirani na sehemu zenye misukosuko duniani pote.

Hali hiyo hutokeza ugumu kwa wahubiri wa habari njema ya Ufalme wa huko. Wengi wa wakaaji wa muda hujua Kiingereza, lakini wengine hujua lugha za kwao pekee. Watu hawa hutoka kwa tamaduni na dini nyingi tofauti-tofauti. Miongoni mwa wageni, unaweza kupata watu wanaodai kuwa Wakristo, Waislamu, Wahindu, Wabuddha, wanimisti, wagnosti, na watheisti. Mashahidi wa Yehova ni lazima wajifunze kubadilisha utoaji wao ili ufae hali tofauti-tofauti za watu hawa.

Kwa kuwa wengi wa wageni hawa wamepatwa na hali ngumu, mara nyingi wana maswali juu ya maana ya uhai na mataraja ya wakati ujao. Wengine wao wanaiheshimu sana Biblia nao hawaoni ugumu wa kukubali isemayo. Wengi katika eneo hilo lenye namna mbalimbali za watu ni wanyenyekevu, wapole, na wenye njaa ya kweli. Wao huhisi uhuru zaidi wa kuitafuta kweli kwa sababu wako mbali na familia zao na mazingira ya kwao.

Kutaniko la kwanza la Kiingereza lilianzishwa katika Athens katika 1986 ili lihubiri eneo hilo. Ukuzi umekuwa wa ajabu. Muda wa miaka mitano iliyopita, karibu wapya 80 wamebatizwa. Tokeo ni kwamba kutaniko la Kiarabu, kutaniko la Wapoland, na kwa kipindi fulani, kikundi cha Kifaransa vimeanzishwa katika Athens. Wengine kutoka kutaniko la Kiingereza wamehama Athens ili kusaidia makutaniko mengine kama hayo na vikundi kama hivyo katika Thesalonike upande wa kaskazini, katika Heraklion, Krete, na Piraeus, bandari la Athens. Je, ungependa kukutana na wageni fulani waliojifunzia kweli Athens?

Vitu Vinavyotamanika vya Mataifa Vinaingia

Thomas alizaliwa Asmara, Eritrea, akalelewa akiwa Mkatoliki mwenye kujitoa sana. Akiwa na umri wa miaka 15, aliingia katika makao ya watawa. Akamuuliza hivi mmoja wa wakuu wa makao ya watawa: “Inawezekanaje kwamba Mungu mmoja awe Miungu watatu?” Mkuu huyo akajibu: “Kwa sababu sisi hukubali yale papa husema kuhusu mambo ya kiroho. Zaidi ya yote, jambo hilo ni fumbo, nawe ni mchanga sana usiweze kulifahamu.” Baada ya kukaa miaka mitano katika makao ya watawa, Thomas akaondoka, akiwa amevunjika moyo na kuvurugwa na mwenendo na mafundisho ya kanisa. Hata hivyo, hakuwa ameacha utafutaji wake wa Mungu wa kweli.

Siku moja muda mfupi baada ya kuhamia Athens, alipata nakala ya Mnara wa Mlinzi mlangoni pake, ambayo ilikuwa na jalada lenye kichwa “Unaweza Kupata Afya Bora na Furaha.” Aliisoma mara kadhaa. Ndani ya gazeti hilohilo, alisoma kwamba tunapaswa kutafuta kwanza Ufalme wa Mungu na uadilifu wake. (Mathayo 6:33) Thomas alipiga magoti na kumwomba Mungu amwonyeshe jinsi ya kufanya hivyo, akiahidi: “Ukinionyesha jinsi ya kutafuta Ufalme wako, nitatoa miezi sita ya maisha yangu kujifunza jinsi ya kukutumikia.” Baada ya hapo, katika juma la nne, Mashahidi wawili wakabisha mlango wake. Thomas akakubali funzo la Biblia mara moja, na miezi kumi baadaye akabatizwa. Yeye asema: “Kwa kweli Yehova alijibu sala yangu, naye alinipa fursa ya kuwa mmoja wa Mashahidi wake. Sasa upendo wake hunisukuma kutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wake katika maisha yangu.”

Walipokuwa wakihubiri mlango kwa mlango, Mashahidi wengine wawili walikuta jina la kigeni kando ya kengele ya mlangoni.

“Mnataka nini?” sauti ya mwanamke ikasikika kwenye chombo cha kuwasiliana.

Mmoja wa Mashahidi hao akasema kwamba walikuwa wakijaribu kutafuta watu wanaojua Kiingereza ambao wanapendezwa na Biblia.

“Ninyi ni wa dini gani?” mwanamke huyo akauliza.

“Sisi ni Mashahidi wa Yehova.”

“Aha, vizuri! Njooni hadi orofa ya juu kabisa.”

Walifanya hivyo, na mlango wa lifti ulipofunguka, mtu mkubwa sana mwenye mwelekeo hasi akasimama hapo. Lakini mwanamke yule akapaaza sauti kutoka ndani.

“Waruhusu waingie. Nataka kuzungumza nao.”

Ikawa kwamba mwanamke huyo alikuwa akisafiri ulimwenguni pamoja na timu ya michezo ya mume wake, na siku iliyotangulia tu, alikuwa amesali apate Mashahidi wa Yehova. Hivyo funzo la Biblia likaanzishwa mara moja. Kwa kuwa wakati wao wa kukaa Ugiriki ulikuwa mfupi, walipanga kujifunza mara tatu kwa juma, kitabu Kuishi Milele kikamalizwa kwa majuma kumi tu.

Musimu wa michezo uliofuata uliwarudisha Ugiriki. Mke huyo akarudia funzo lake na kufanya maendeleo mazuri sana. Baada ya miezi kadhaa, alijiunga na Mashahidi katika kazi ya kuhubiri akiwa mhubiri asiyebatizwa na haraka akaanzisha funzo lake la kwanza la Biblia. Pamoja na nani? Mumeye, aliyevutiwa sana na Mashahidi na mabadiliko ya mkeye.

Allan, mwana wa pasta Mprotestanti, alilelewa Afrika Kusini. Tangu umri wa mapema sana, alikuwa amesadiki kwamba Biblia ni ufunuo uliopuliziwa kutoka kwa Mungu. Akiwa hajaridhika na dini yake, aligeukia falsafa na siasa, lakini hayo yalimwacha akihisi utupu kuliko wakati mwingine wowote. Baada ya kuhamia Ugiriki, hisia yake ya utupu ikazidi. Alihisi kwamba maisha yake hayakuwa na kusudi, kwamba alikuwa katika barabara isiyoongoza popote.

Usiku mmoja jambo fulani likatendeka. “Nilipiga magoti na kumwambia Mungu jinsi nilivyokuwa nikihisi ndani,” Allan aeleza. “Kwa machozi ya huzuni kwa ajili ya mwendo wangu wa maisha, nilimwomba Mungu aniongoze kwa wafuasi wake wa kweli. Niliahidi kwamba ningetembea katika nuru ya uongozi wake.” Katika juma hilo, alikuwa dukani akaanza kuzungumza na mwanamke mmoja, mwenye duka hilo, aliyekuwa Shahidi. Mazungumzo hayo yakaleta badiliko kwelikweli kwa maisha ya Allan. “Siku zilizofuata, zikabomoka zile itikadi nilizopenda kama vile: Utatu, moto wa mateso, kutokufa kwa nafsi—zote kwa wazi zikiwa si mafundisho ya Biblia.” Kwenye Jumba la Ufalme, mume na mke Mashahidi wakajitoa kujifunza Biblia pamoja naye. Alikubali na kufanya maendeleo haraka. “Kweli ilinifanya nilie kwa furaha,” Allan akumbuka, “nayo iliniweka huru.” Mwaka mmoja baadaye akabatizwa. Leo anafurahi kutumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kutaniko la kwao.

Elizabeth ametoka Nigeria, ambako alikuwa amemtafuta Mungu katika dini mbalimbali lakini akabaki bila uradhi. Lililomwogopesha zaidi lilikuwa fundisho la kuteswa milele katika moto wa helo. Alipohamia Athens pamoja na familia yake, Mashahidi wawili wakaja mlangoni pake, na funzo la Biblia likaanzishwa. Elizabeth alisisimuka kujifunza kwamba Mungu hatesi watu, bali ameandaa tumaini la uhai udumuo milele katika dunia iliyo paradiso. Alikuwa na mimba ya mtoto wake wa nne, ambayo alitaka kutoa. Akajifunza katika Biblia maoni ya Yehova juu ya utakatifu wa uhai. Sasa ana binti mrembo. Elizabeth alifanya maendeleo haraka sana na mara akabatizwa. Ingawa ana watoto wanne na kazi ya kuajiriwa ya wakati wote, anaweza kufanya upainia msaidizi karibu kila mwezi. Amebarikiwa kuona mumeye akianza kujifunza Biblia. Yeye asema: “Mwishowe nilimpata Mungu wa kweli na ibada ya kweli, hayo yote kwa ajili ya Yehova na tengenezo lake lenye upendo.”

Wengi wa watu katika eneo hilo lenye namna nyingi za watu wanapatikana katika kazi ya barabarani, lakini inahitaji udumifu ili wasitawishe kupendezwa. Ndivyo ilivyokuwa na mwanamke mmoja mchanga aitwaye Sallay, kutoka Sierra Leone. Shahidi mmoja alimpa trakti, akachukua anwani yake, na kufanya mpango ili arudiwe. Sallay alipendezwa na kukubali funzo la Biblia, lakini kwa sababu ya mikazo kutoka kazini na magumu mengine, funzo hilo halikuongozwa kwa ukawaida. Kisha akahama kwa ghafula bila kutaja makao yake mapya. Shahidi yule akazidi kwenda makao yale ya zamani, na mwishowe Sallay akapeleka ujumbe kwa Shahidi huyo aje kwenye makao yake mapya.

Sasa funzo likawa la kawaida zaidi kidogo ingawa Sallay alikuwa katika miezi yake ya mwisho ya ujauzito. Baada ya mtoto kuzaliwa, Sallay akawa mhubiri asiyebatizwa. Yote hayo huenda yakaonekana kuwa rahisi kwake kutimiza, lakini kwa kweli haikuwa hivyo. Saa 12:30 asubuhi, ni lazima awe tayari kusafiri kwa muda wa nusu saa kwa basi kupeleka mtoto wake shule ya nasari, ikifuatwa na safari nyingine ya muda wa saa moja kwa basi kuelekea kazini. Baada ya kufanya kazi yake ya kusafisha, yeye husafiri kurudi nyumbani. Ujapokuwa upinzani kutoka kwa mumeye, jioni za mikutano, au aendapo katika utumishi wa shambani, yeye husafiri kwa muda wa saa nzima kwa basi kwenda na saa nyingine kurudi. Huku akimwonyesha mumeye upendo na saburi, alifanya maendeleo hadi hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Vipi mumeye? Alihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo na kukubali funzo la Biblia.

Wabarikiwa kwa Matokeo Mazuri

Kwa wengi wa watu hawa, kukaa kwao Athens ni kwa muda tu. Wengi hurudi katika nchi zao walikotoka ili kushiriki habari njema na watu wa ukoo na marafiki. Wengine huhamia nchi tofauti za Magharibi na kuendelea kumtumikia Yehova. Wale wakaao Ugiriki hufurahia matokeo mazuri wakiwatolea ushahidi watu wa nchi yao waliohamia huko pia. Katika visa vingine mbegu za ukweli zilipata matokeo baada tu ya wageni hao kuhamia nchi nyingine na kutembelewa na Mashahidi.

Yote hayo yathibitisha kwamba Yehova hana upendeleo. Yeye hukubali watu kutoka kila taifa wamhofuo na kupenda uadilifu. (Matendo 10:34, 35) Kwa watu kama hao wenye mfano wa kondoo, kuhamia kwao nchi nyingine kutafuta vitu vya kimwili kulitokeza baraka nyingi sana kuliko walivyokuwa wametazamia—ujuzi wa Mungu wa kweli, Yehova, na ahadi yake ya uhai udumuo milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. Ndiyo, Yehova amebariki kwelikweli jitihada za kufikia watu wenye kuzungumza lugha za kigeni katika Athens la kisasa!

[Picha katika ukurasa w16]

Watu kutoka nchi nyingi wanasikia habari njema katika Athens

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki