Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 4/15 kur. 8-10
  • Kampeni ya Kutoa Ushahidi Yenye Mafanikio Katika Ugiriki

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kampeni ya Kutoa Ushahidi Yenye Mafanikio Katika Ugiriki
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Maofisa wa Serikali Waitikia
  • Viongozi wa Mashtaka Waitikia
  • Watunza-Maktaba Waitikia
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 4/15 kur. 8-10

Kampeni ya Kutoa Ushahidi Yenye Mafanikio Katika Ugiriki

MASHAHIDI WA YEHOVA wamekabili kwa muda mrefu upinzani katika Ugiriki. Polisi, mahakama, na maofisa wa serikali wamewanyanyasa Mashahidi, mara nyingi kwa sababu ya mkazo kutoka kwa makasisi wa dini ya Othodoksi ya Ugiriki. Nyakati fulani kisababu kimekuwa ile sheria ya Ugiriki inayokataza kugeuza imani, nyakati nyingine ni kukataa kwa Mashahidi kwenda vitani au kukataa kutiwa damu mishipani kwenye kutegemea Biblia.—Isaya 2:2-5; Matendo 15:28, 29.

Wakijaribu kuendeleza uelewevu mzuri kati ya wenye mamlaka wenye moyo wa haki katika Ugiriki, Mashahidi wapatao 200 ambao serikali ya Ugiriki huwatambua kuwa wahudumu wa kidini, pamoja na wengine walio wafanyakazi wa sheria, hivi majuzi walihusika katika kampeni ya nchi nzima. Walitoa broshua iliyotengenezwa kipekee, yenye kichwa Jehovah’s Witnesses in Greece, pamoja na kile kitabu Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom. Pia walitoa hati kadhaa ambazo huonyesha kwamba hakuna sababu halali ya kuwanyanyasa Mashahidi wa Yehova. Hao Mashahidi waliwatembelea wakuu wa polisi, meya mbalimbali wa miji, viongozi wa mashtaka, na maofisa wengineo.

Itikio lilikuwa nini? Mamia ya mambo mazuri yaliyoonwa. Fikiria vielelezo kadhaa.

Kamanda wa kituo cha polisi katika Makedonia Magharibi aliwakaribisha akina ndugu na kusema: “Nimewajua ninyi watu kwa muda mrefu, . . . nami nimevutiwa na utaratibu wenu. . . . Mimi sikubaliani na ile sheria inayopinga kugeuza imani, na ikiwa ningekuwa na uwezo, ningeifutilia mbali.”

Makamanda wa vituo mbalimbali vya polisi katika miji mingi walisema mambo kama haya: “Nawapongeza kwa ajili ya utumishi wa kijamii mnaotoa.” “[Ninyi Mashahidi wa Yehova] hamna matatizo na polisi; mnatimiza kazi yenu kwa jamii.” “Sisi hatuna matatizo yoyote nanyi. Twawaheshimu na kuwathamini.”

Katika Piraeus ofisa wa juu katika polisi wa usalama aliwaambia akina ndugu, akitokwa na machozi, kwamba anajua kusali kwa Yehova Mungu kwa kutumia jina lake kupitia Yesu Kristo. Yeye aliwashangaza hao Mashahidi hata zaidi alipowaambia kwamba alijua kwamba walikuwa wakitarajia mnyanyaso kwa kiasi fulani kabla ya Har–Magedoni, na alitumaini kwamba Mungu atamtumia kuwasaidia wakati huo! Alikubali mwaliko wa hao ndugu ili awe na mazungumzo zaidi.

Maofisa wa Serikali Waitikia

Meya mmoja katika Thessaly alisema hivi juu ya kitabu Proclaimers: “Chastahili kuwekwa katika maktaba ya manispaa—mahali kiwezapo kuonekana kwa urahisi!” Wakati huohuo akaondoa vitabu kutoka kwa rafu na kukiweka kitabu Proclaimers hapo ili jalada lake lionekane.

Katika kaskazini mwa Ugiriki, meya fulani alikaribisha ziara ya akina ndugu kwa uchangamfu na kusema: “Ninyi ndio watu wazuri zaidi ambao ningependa kuwa nao katika manispaa yangu.” Meya mwenye fadhili katika kaskazini mwa Euboea aliwaambia akina ndugu: “Mimi nilikuwa ofisa wa kijeshi. Lakini ninyi—nawathamini sana.” Yeye alikubali hoja zilizotolewa na wale Mashahidi kwa furaha. Walipoonyesha baadhi ya vitabu vilivyotangazwa na Watch Tower Society, alisema: “Nikiahidi kuvisoma vyote, je, mtanipa?” Wakajibu: “Bila shaka—ni vyako!” Alipendezwa sana hata hakutaka kuwaruhusu akina ndugu waondoke.

Kwenye kiunga kimoja katika Attica, meya fulani alikubali kwa furaha fasihi waliyotoa akina ndugu akawaomba waendelee kumletea vichapo vya Sosaiti. Walipokuwa wakiondoka, aliwaambia: “Watu wamevunjwa moyo sana na wanasiasa nao watafuta kweli halisi kwingineko. Mimi nina hakika kwamba kuanzia sasa mtakuwa na kazi nyingi kwa kuwa mna hiyo kweli.”

Viongozi wa Mashtaka Waitikia

Ndugu waliomtembelea naibu wa kiongozi wa mashtaka katika kaskazini mwa Ugiriki wakumbuka: “Yeye alipendezwa na vichapo vyetu na utoaji wetu, na vilevile juhudi zetu za kuhakikisha kwamba watu wetu hawabaki bila usaidizi wowote wakabilipo suala lenye uzito la kutiwa damu mishipani. Hatimaye akatushukuru na kutupongeza kwa uchangamfu kwa sababu ya kuchukua hatua ya kwanza kumtembelea na kumpa habari. Baadaye, tukagundua kuwa miaka minne mapema alikuwa amewaita polisi na kuamrisha kushikwa kwa ndugu wawili waliokuwa katika huduma ya shambani.”

Mawakili wawili Mashahidi waliotembelea afisi za viongozi wa mashtaka katika Athens walishangaa kumwona kiongozi wa mashtaka wa zamani ajulikanaye na kuheshimiwa sana akiwaendea. Aliwapeleka kando na kuwaambia kwamba ile sheria inayopinga kugeuza imani haina msingi wowote nayo husababisha vurugu katika mfumo wa mahakama katika Ugiriki. Aliwashukuru kwa kuwasalimu kwa mkono kwa njia ya uchangamfu.

Kaskazini mwa Ugiriki, kiongozi wa mashtaka alikuwa mwenye urafiki sana naye alikubali fasihi. Alipokuwa akifungua kurasa za kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, alishangazwa sana kuona sura tofauti-tofauti katika yaliyomo. Yeye alisema hivi: “Mambo ambayo kitabu hiki kinashughulikia, sijapata kamwe kuyaona katika kanisa la Othodoksi.”

Kiongozi wa mashtaka katika Boeotia alikubali kwamba yeye, wakati uliopita, alikuwa ametoa amri za kutia damu Mashahidi fulani dhidi ya mapenzi yao. Lakini baada ya ndugu kusababu naye juu ya hilo jambo, yeye alitangaza hivi: “Sitaamurisha hivyo tena kamwe wakati ujao!” Alifikia mkataa wa kwamba Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali ya Mashahidi wa Yehova ya huko ionwe ili vibadala vyote vya damu vitumiwe. Kwa furaha alikubali kitabu Vijana Huuliza.

Watunza-Maktaba Waitikia

Hizo habari zilitolewa pia kwa watunza-maktaba wengi. Kwenye maktaba moja katika Athens, mtunza-maktaba mmoja mpole alikubali fasihi na kusema: “Ni vema sana kwamba mlituletea vitabu vyenu kwa sababu vingi vya vitabu tulivyo navyo kwenye maktaba yetu vyawapinga. . . . Kasisi mmoja alikasirishwa sana kuona vitabu vyenu katika maktaba. . . . Si kitu. Maoni yote lazima yasikiwe.”

Ofisa katika maktaba ya manispaa katika Krete, ambaye alikuja kuwajua Mashahidi wa Yehova katika kambi ya kijeshi, aliwaambia ndugu kwamba alikuwa amevutiwa sana na kukataa kwa Mashahidi kushiriki katika vita. Alijiuliza tena na tena, ‘Kwa nini watu hawa wateseke?’ Alikubali fasihi kutoka kwa akina ndugu na kusema haya juu ya kampeni yao ya wakati huo: “Mmefanya kazi nzuri sana nanyi mlipaswa kufanya hili miaka mingi iliyopita. . . . Katika Ugiriki kuna upendeleo mwingi.” Aliwaomba ndugu kumtembelea tena karibuni.

Wakati wa kampeni hii ya pekee, ndugu waliangusha vitabu Proclaimers zaidi ya 1,000, broshua Jehovah’s Witnesses in Greece 1,600, pamoja na mamia ya vitabu na magazeti. Lililo zuri hata zaidi ni kwamba waliongea uso kwa uso na mamia ya maofisa wa Ugiriki. Sasa ni tumaini la watumishi waaminifu wa Yehova katika Ugiriki na ulimwenguni pote kwamba wenye mamlaka wenye moyo wa haki wa Ugiriki hawatawabagua Mashahidi wa Yehova.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki