Waweza Kuwa na “Moyo wa Simba”
NYAKATI nyingine Biblia hutumia simba akiwa ufananisho wa moyo mkuu na ujasiri. Wanaume mashujaa na wenye moyo mkuu wanafafanuliwa kuwa na “moyo wa simba,” nao waadilifu wanasemwa kuwa “wajasiri kama simba.” (2 Samweli 17:10; Mithali 28:1) Hasa achokozwapo simba huonyesha kwamba anastahili sifa yake ya kuwa “hodari kupita wanyama wote.”—Mithali 30:30.
Yehova Mungu hulinganisha azimio lake la kuwalinda watu wake na kule kutokuwa na woga kwa simba. Isaya 31:4, 5 hutaarifu hivi: “Kama vile ilivyo simba angurumapo na mwana-simba juu ya mawindo yake, wachungaji wengi wakiitwa ili kumpiga, lakini hatiwi hofu na sauti zao, wala kufanya woga kwa sababu ya mshindo wao; ndivyo BWANA wa majeshi atakavyoshuka ili kufanya vita juu ya mlima Sayuni . . . Ataulinda na kuuokoa, atapita juu yake na kuuhifadhi.” Kwa njia hiyo Yehova huwahakikishia watumishi wake utunzaji wake wenye utendaji, hasa wakabilipo taabu.
Biblia humlinganisha mpinzani wa wanadamu aliye mkubwa zaidi ya wote, Shetani Ibilisi, na simba angurumaye, mwenye njaa kali. Ili kuepuka kuwa windo lake, twaambiwa hivi katika Maandiko: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda.” (1 Petro 5:8, NW) Njia moja ya kufanya hivyo ni kuepuka usingizi wa kiroho ulio hatari. Kuhusiana na hilo Yesu alisema hivi: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya.” (Luka 21:34-36) Ndiyo, kuwa macho kiroho katika “siku [hizi] za mwisho” kwaweza kutupa sisi “moyo wa simba,” ulio ‘imara, umtumainio BWANA.’—2 Timotheo 3:1; Zaburi 112:7, 8.