“Je, Naota Ndoto?”
Ripoti ifuatayo yatoka Malawi kuhusu mmojawapo “Wasifaji Wenye Shangwe” Mikusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova yenye kutokeza iliyofanywa huko katika kiangazi cha 1995.
“ISHARA imewekwa kwa mara ya kwanza katika miaka 29, kando ya barabara kuu, iliyo karibu nusu ya njia kuelekea ukingo wa Ziwa Malawi. Hiyo ishara inasema hivi, ‘Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova.’
“Lori kubwa limeegeshwa kando ya ishara hiyo, na wajumbe zaidi ya 200 kutoka mji wa Mzuzu wanatoka ndani yalo. Wameleta mafurushi ya nguo, blanketi, sufuria, ndoo, chakula, kuni, na Biblia ili kujiunga na ndugu na dada zao wapatao 3,000 kutoka sehemu nyinginezo.
“Huku tukiendelea kuwasalimu ndugu wanaotoka katika hilo lori, George Chikako, mwenye miaka 63, awasili, akisukuma baiskeli yake katika mchanga, akiwa ameiendesha muda wa siku mbili kutoka Nkhotakota. Katika miaka mingi, Ndugu Chikako alitumikia vifungo vinne vya gereza kwa sababu ya kukataa kwake kuacha kanuni za Biblia. Binamu yake alikufa kutokana na mapigo aliyopokea alipokuwa amefungwa gerezani. ‘Je, naota ndoto?’ Ndugu Chikako auliza. ‘Mkusanyiko huu unafanywa waziwazi mchana, na watu hawa wanaimba nyimbo za Ufalme kwa sauti kubwa! Kwa miaka mingi sana, tumelazimika kukutana katika giza la usiku, kuimba nyimbo za Ufalme kwa sauti ya chini, na kuisugua mikono yetu pamoja badala ya kupiga makofi. Sasa tunakutana hadharani, na watu wanashangaa kuona kwamba sisi ni wengi sana huku walipofikiri sisi ni wachache tu!’
“Mahali pa mkusanyiko pana ua wa nyasi na pameezekwa kwa matete machache ili kuandaa kivuli. Vibanda vidogo vya nyasi na vyumba vya kulala visivyo na dari vilijengwa ili kuwapa wajumbe makao. Hewa ya usiku imejaa sauti tamu zenye kupendeza zisizozuiwa tena kwa sababu ya kuhofu mnyanyaso.
“Yafaa kama nini kwamba kichwa cha mkusanyiko ni ‘Wasifaji Wenye Shangwe’!”
[Hisani]
Mountain High Maps® Copyright © 1995 Digital Wisdom, Inc.