Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Je, Yesu sasa aijua tarehe ya Har–Magedoni?
Yaonekana kuwa jambo linalofaa sana kuamini kwamba aijua tarehe.
Huenda watu fulani wakajiuliza ni kwa nini swali hilo hata latokea. Yaelekea ni kwa sababu ya maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Mathayo 24:36: “Habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake.” Angalia kwa uangalifu maneno “wala Mwana.”
Mstari huu ni sehemu ya jibu la Yesu kwa swali hili la mitume: “Mambo haya yatatukia lini? Ni ishara gani itakayoonyesha kuja kwako na mwisho wa dunia?” (Mathayo 24:3, HNWW) Katika unabii wake ulio mashuhuri sasa kuhusu uthibitisho mbalimbali unaofanyiza “ishara,” yeye alitabiri vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya dunia, mnyanyaso wa Wakristo wa kweli, na mambo mengine duniani ambayo yangeonyesha kuwapo kwake. Kwa ishara hiyo wafuasi wake wangeweza kufahamu kwamba mwisho ulikuwa karibu. Alionyesha ukaribu huo kwa kutoa kielezi cha mtini uanzapo kutoa majani, ikionyesha kwamba kiangazi kilikuwa karibu. Aliongeza hivi: “Hali kadhalika, nanyi, mtakapoona mambo haya yote yakitendeka, jueni kwamba Mwana wa Mtu yuko karibu.”—Mathayo 24:33, HNWW.
Lakini Yesu hakusema ni lini hasa mwisho ungekuja. Badala ya hivyo, alitaarifu yale tusomayo kwenye Mathayo 24:36. Hivyo ndivyo Biblia Union Version ya Kiswahili husema, na Biblia nyingi za kisasa husomwa vivyo hivyo. Hata hivyo, tafsiri nyingine za zamani hazina maneno “wala Mwana.”
Kwa kielelezo, tafsiri ya Douay Version ya Katoliki husomwa hivi: “Lakini kuhusu siku na saa hiyo hakuna ajuaye, si malaika wa mbinguni, ila Baba peke yake.” Tafsiri ya King James Version husomwa vivyo hivyo. Kwa nini maneno “wala [au, ama] Mwana” hayakutiwa ndani, ingawa yanapatikana kwenye Marko 13:32? Kwa sababu huko nyuma mwanzoni mwa karne ya 17 wakati tafsiri hizo mbili zilipotayarishwa, hati zilizotumiwa na watafsiri hazikuwa na maneno hayo. Lakini, tangu wakati huo, hati nyingi za Kigiriki za zamani zaidi zimevumbuliwa. Hati hizo, ambazo zakaribia zaidi wakati wa maandishi ya awali ya Mathayo, zina maneno “wala Mwana” kwenye Mathayo 24:36.
Kwa kupendeza, tafsiri ya Jerusalem Bible ya Katoliki inatia ndani hayo maneno, pamoja na kielezi-chini kinachosema kwamba tafsiri ya Vulgate ya Kilatini haikutia ndani maneno hayo “labda kwa sababu za kitheolojia.” Bila shaka! Watafsiri au wanakili walioamini Utatu huenda wakashawishwa kutotia ndani maneno yaliyoonyesha kwamba Yesu hakuwa na ujuzi ambao Baba yake alikuwa nao. Yesu angeweza kukosaje kujua jambo fulani la hakika ikiwa yeye na Baba yake walikuwa sehemu ya Mungu wa utatu?
Vivyo hivyo, A Textual Commentary on the Greek New Testament, ya B. M. Metzger, yasema hivi: “Maneno ‘wala Mwana’ hayamo katika nyingi za [hati] zenye ushahidi wa Mathayo, kutia na maandishi ya Byzantium ya baadaye. Kwa upande mwingine, mifano bora zaidi ya aina za maandishi za Kialeksandria, Kimagharibi, Kikaisaria ina hayo maneno. Yawezekana zaidi kwamba maneno hayo hayakutiwa ndani kwa sababu ya ugumu wa mafundisho ambao yanatokeza kuliko kwamba maneno hayo yaliongezwa kwenye” Marko 13:32.—Italiki ni zetu.
“Mifano [hiyo] bora” ya hati za mapema huunga mkono usomaji unaotokeza mfululizo unaofaa kuhusiana na ujuzi. Malaika hawakujua saa ya mwisho; wala Mwana hakujua; ila Baba peke yake. Na hilo lapatana na maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Mathayo 20:23, ambapo alikiri kwamba hakuwa na mamlaka ya kutoa mahali mashuhuri katika Ufalme, lakini Baba alikuwa nayo.
Kwa hiyo, maneno ya Yesu mwenyewe huonyesha kwamba alipokuwa duniani yeye hakujua tarehe ya ‘mwisho wa ulimwengu.’ Je, amepata kuijua tangu wakati huo?
Ufunuo 6:2 lamfafanua Yesu akiwa ameketi juu ya farasi mweupe na kwenda “akishinda tena apate kushinda.” Kisha wafuata wapanda-farasi wanaowakilisha, vita, njaa kuu, na tauni, sawa na vile tumeona tangu Vita ya Ulimwengu 1 ilipoanza 1914. Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba katika 1914, Yesu alitawazwa awe Mfalme wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu, yule atakayeongoza katika pigano linalokuja dhidi ya uovu duniani. (Ufunuo 6:3-8; 19:11-16) Sasa kwa kuwa Yesu amepewa nguvu kuwa yule atakayeshinda katika jina la Mungu, yaonekana kuwa jambo linalofaa kwamba Baba yake amemwambia wakati mwisho utakapokuja, atakapopata “kushinda.”
Sisi tulio duniani hatujaambiwa tarehe hiyo, kwa hiyo maneno ya Yesu yangali yanatuhusu sisi: “Angalieni, kesheni, [ombeni], kwa kuwa hamjui wakati ule utakapokuwapo. . . . Hilo niwaambialo ninyi, nawaambia wote, Kesheni.”—Marko 13:33-37.