Je, Wakumbuka?
Je, umethamini kusoma matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Basi, ona ikiwa waweza kujibu maswali yafuatayo:
◻ Je, maneno ya Yesu, “Mkisamehe dhambi za watu wowote, zadumu wakiwa wamesamehewa hizo,” yamaanisha kwamba Wakristo waweza kusamehe dhambi? (Yohana 20:23,NW)
Hakuna msingi wa Kimaandiko wa kukata kauli kwamba Wakristo kwa ujumla, au hata wazee waliowekwa rasmi katika makutaniko, wana mamlaka ya kimungu ya kusamehe dhambi. Muktadha wa maneno ya Yesu waonekana kuonyesha kwamba kupitia utendaji-kazi wa roho, mitume walikuwa wameandaliwa mamlaka ya pekee ya kusamehe au kutosamehe dhambi. (Ona Matendo 5:1-11; 2 Wakorintho 12:12.)—4/15, ukurasa 28.
◻ Ni nini chenye kutokeza kuhusu tafsiri ya J. J. Stewart Perowne ya kitabu cha Zaburi, iliyotangazwa kwa mara ya kwanza katika 1864?
Katika tafsiri yake Perowne alijaribu kushikamana “kwa ukaribu na namna ya lugha ya Kiebrania, katika msemo na katika muundo wa kisarufi wa maneno.” Kwa kufanya hivyo alipendelea kurudishwa kwa lile jina la kimungu katika ile namna “Yehova.”—4/15, ukurasa 31.
◻ Yesu aliwapa wafuasi wake mwongozo gani kwa habari ya shughuli zao pamoja na serikali za ulimwengu?
Yesu alisema: “Mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu.” (Mathayo 22:21) Pia alisema: ‘Mtu akikulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili.’ (Mathayo 5:41) Hapa Yesu alikuwa akitolea kielezi kanuni ya kuwa tayari kunyenyekea matakwa halali, iwe ni katika mahusiano ya kibinadamu au katika matakwa ya kiserikali yanayopatana na sheria ya Mungu.—(Luka 6:27-31; Yohana 17:14, 15.)—5/1, ukurasa 12.
◻ Yamaanisha nini ‘kuenenda katika kweli’? (Zaburi 86:11)
Hili latia ndani kufuata matakwa ya Mungu na kumtumikia kwa uaminifu na unyoofu. (Zaburi 25:4, 5; Yohana 4:23, 24)—5/15, ukurasa 18.
◻ Ni nini kilichotimizwa na Yehova kumtuma Yona Ninawi?
Jinsi mambo yalivyotokea, utendaji wa kuhubiri wa Yona ulionyesha tofauti kati ya Waninawi wenye kutubu na Waisraeli wenye shingo ngumu, ambao hawakuwa na imani na unyenyekevu. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 9:6, 13; Yona 3:4-10.)—5/15, ukurasa 28.
◻ Ni nani Nyoka na ni nani “mwanamke” wanaorejezewa kwenye Mwanzo 3:15?
Nyoka si yule nyoka halisi bali yule aliyemtumia nyoka huyo, Shetani Ibilisi. (Ufunuo 12:9) “Mwanamke” si Hawa bali ni tengenezo la kimbingu la Yehova, mama ya watumishi wake watiwa-mafuta kwa roho walio duniani. (Wagalatia 4:26)—6/1, ukurasa 9.
◻ Mtu aweza kutokaje katika Babiloni Mkubwa na kupata usalama? (Ufunuo 18:4)
Ni lazima ajitenge kabisa na matengenezo bandia ya kidini na pia na desturi zayo na roho yanayositawisha kisha apaswa kukimbilia usalama katika tengenezo la kitheokrasi la Yehova. (Waefeso 5:7-11)—6/1, ukurasa 18.
◻ Kwa nini tai anatajwa mara nyingi katika Maandiko?
Waandikaji wa Biblia walirejezea kwa njia isiyo ya moja kwa moja sifa za tai ili kutolea kielezi mambo kama hekima, ulinzi wa kimungu na wepesi.—6/15, ukurasa 8.
◻ Je, watumishi wa Mungu leo walio na tumaini la kidunia wana kiasi kilekile cha roho ya Mungu kama walicho nacho Wakristo watiwa-mafuta kwa roho?
Kimsingi, jibu ni, ndiyo. Roho ya Mungu hupatikana kwa kiasi kilekile kwa jamii zote mbili, na kiasi kilekile cha ujuzi na uelewevu hupatikana kwa jamii zote mbili.—6/15, ukurasa 31.
◻ Kwa nini inatunufaisha leo kuchunguza utumishi mtakatifu uliofanywa na makuhani Waisraeli kwenye hekalu Yerusalemu?
Kwa kufanya hivyo twaweza kuthamini kikamili zaidi ule mpango wenye rehema ambao kwa huo wanadamu wenye dhambi leo wapatanishwa pamoja na Mungu. (Waebrania 10:1-7)—7/1, ukurasa 8.
◻ Hekalu la pili lililojengwa Yerusalemu lilifikiaje utukufu mkubwa zaidi kuliko lile lililojengwa na Sulemani?
Hekalu la pili lilidumu miaka 164 zaidi ya lile la Sulemani. Waabudu wengi zaidi kutoka mabara mengi zaidi walimiminika kwenye nyua zalo. La maana zaidi, hekalu hilo la pili liliheshimiwa kuwa na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, akifundisha katika nyua zalo.—7/1, kurasa 12, 13.
◻ Mungu alitokeza hekalu lake la kiroho lini?
Hilo lilikuwa katika mwaka wa 29 W.K. Mungu alipoonyesha kukubali kwake sala ya Yesu ya ubatizo. (Mathayo 3:16, 17) Kukubali kwa Mungu kule kutolewa kwa mwili wa Yesu kulimaanisha kwamba, katika maana ya kiroho, madhabahu iliyo kubwa zaidi kuliko ile katika hekalu la Yerusalemu ilikuwa imeanza kutenda kazi.—7/1, kurasa 14, 15.
◻ Kwa nini tuwe wenye kusamehe?
Kumsamehe mtu aliyefanya jambo la kuudhi ambaye ameomba msamaha ni jambo la maana ikiwa tutadumisha muungano wa Kikristo. Uhasama na kufungia moyoni kinyongo kutatunyang’anya amani ya akili. Ikiwa sisi ni watu wasiosamehe, kuna hatari kwamba siku fulani Yehova hatatusamehe dhambi zetu tena. (Mathayo 6:14, 15)—7/15, ukurasa 19.
◻ Waisraeli wangewezaje kuwa watakatifu?
Utakatifu ungewezekana tu kwa kuwa kwao na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, yule Mungu mtakatifu, na kwa ibada yao safi kwake. Walihitaji ujuzi sahihi wa “Aliye Mtakatifu Zaidi Sana” ili wapate kumwabudu katika utakatifu, katika usafi wa kimwili na kiroho. (Mithali 2:1-6; 9:10, linganisha NW.)—8/1, ukurasa 11.