Hali Ifaayo Ukuzi Katika Guinea ya Ikweta
UKUZI mkubwa ndilo wazo la kwanza apatalo msafiri ndege yake ituapo katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Guinea ya Ikweta. Barabara ya ndege inazungukwa na miti mikubwa ambayo hufanya majengo ya uwanja wa ndege yaonekane mafupi. Mimea mizuri husitawi kutoka ufukoni hadi vilele vya milima, huku ikichochewa na mvua nyingi na hali joto ya kufaa ya mwaka mzima katikati ya miaka ya 1980.
Aina nyingine ya ukuzi mkubwa unaendelea pia katika Guinea ya Ikweta, “ukuzi ambao Mungu hutoa.” (Wakolosai 2:19, NW) Kama ofisa wa Ethiopia ambaye alitafuta msaada kutoka kwa Filipo, wengi hapa wana hamu ya kuelewa Maandiko. (Matendo 8:26-39) Si jambo la ajabu kwa mtu kumfikia mmoja wa Mashahidi wa Yehova mtaani na kumwomba funzo la Biblia. Wale Mashahidi 325 hivi wa Guinea ya Ikweta wanaongoza zaidi ya mafunzo ya Biblia elfu moja.
Kupanda Mbegu Katika Siku za Mapema
Guinea ya Ikweta, nchi ndogo kuliko zote za Afrika ipo kusini ya Nigeria na Kamerun. (Ona ramani.) Habari njema zililetwa hapa kwanza na Mashahidi wa Nigeria ambao walikuja kutafuta kazi katika mashamba ya kakao. Ingawa makutaniko kadhaa ya Kiingereza yalianzishwa, baadaye yalivunjwa ndugu hao walipolazimika kurudi Nigeria. Hata hivyo, mara baada ya uhuru kutolewa kwa Guinea ya Ikweta katika 1968, wenzi wa ndoa watatu wamishonari wa Watchtower walipewa mgawo hapa. Hawakuweza kukaa muda mrefu kwa sababu ya magumu ya kisiasa lakini ushahidi wao ulitokeza matokeo mazuri.
Santiago, mmoja wa hao wamishonari alikutana na Buenaventura, mtu mrefu, mwenye nguvu ajulikanaye na wenyeji kuwa mtu mwenye uwezo usio wa kawaida. Alikuwa mtu wa kidini ambaye aliheshimu Biblia, lakini alikuwa mwenye hasira sana. Tukano dogo sana lilitosha kumfanya ampige mtu. Alipokasirika akiwa katika baa, watu wote waliopo walitawanyika, hata wakitokea madirishani ili kuepuka mapigo yake. Kwa kweli, alipokuwa anamsikiliza Santiago, alidhamiria kumpiga ikiwa angeshindwa kutokeza ithibati ya Kimaandiko kusadikisha yale aliyosema. ‘Hakuna mtu awezaye kumdanganya mtu mwenye uwezo usio wa kawaida,’ akajiambia mwenyewe. Alivutwa na yale aliyoyasikia hasa kuhusu tumaini la uhai udumuo milele katika paradiso duniani, hivyo akakubali funzo la Biblia.
Kadiri funzo lilivyoendelea, tamaa ya Buenaventura ya kuishi milele katika Paradiso ikawa yenye nguvu, na alijifunza kwamba alipaswa kupatanisha maisha yake na viwango vya Mungu ili kupata zawadi hiyo. Akitambua kwamba Wakristo wa kweli hawapaswi ‘kulipa ovu kwa ovu,’ alianza kufanya jitihada za moyo mnyoofu kudhibiti hasira yake.—Warumi 12:17.
Jaribu halisi lilikuja siku moja ambapo bila ya kukusudia aligonga bilauri ya mteja fulani katika baa. Mtu huyo alikasirika na kumpiga. Mara moja, wengine katika baa walitawanyika, wakitarajia ugomvi utokee. Lakini kwa unyenyekevu Buenaventura alilipia bilauri iliyovunjika, alimnunulia mtu huyo kinywaji kingine na aliomba radhi kwa sababu ya ujinga wake. Majirani walipoona kwamba funzo la Biblia lilikuwa limembadili hivyo, watu kadhaa walitaka kujifunza naye. Buenaventura alipobatizwa, alikuwa tayari anaongoza mafunzo matano ya Biblia. Ametumikia akiwa mzee kwa miaka mitano iliyopita, na ingawa bado watu humwita mtu mwenye uwezo usio wa kawaida, wao humwita hivyo kiutani.
“Wenye Kuona Uhitaji Wao wa Kiroho”
Wakati wa miaka ya 1970 Mashahidi wenyeji wachache waliendelea kuhubiri na kukutana pamoja kwa kadiri walivyoweza. Baadaye, wenzi wa ndoa kadhaa wamishonari Wahispania walikuja kusaidia. Andrés Botella ambaye ametumikia Guinea ya Ikweta kwa miaka 12, akumbuka kwamba mara baada ya kuwasili, alivutiwa na jinsi watu walivyokuwa “wenye kuona uhitaji wao wa kiroho” kwelikweli. (Mathayo 5:3, NW) “Imekuwa furaha ya kweli kujifunza Biblia pamoja na watu wenye uthamini hivyo,” yeye asema.
Mary, dada Mhispania, alikuwa akijifunza Biblia na mwanamke mchanga aitwaye María ambaye alitaja kwamba wazazi wake, Francisco na Fausta, walikuwa wanapendezwa pia kujifunza. Kwa vile Mary alikuwa akiongoza mafunzo 15 na wazazi wa María walikuwa wakiishi mbali, majuma kadhaa yalipita kabla hajaweza kuwatembelea.
Hatimaye, Mary na mume wake Serafín, walikutana na hao wazazi, wakati huo tayari walikuwa na kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniania na Biblia, na walikuwa na hamu ya kuanza kujifunza. Kwa hiyo walianza mara moja. Serafín aligundua kwamba wazazi wa María walifahamu sana yale waliyokuwa wanajifunza. Jambo lilo hilo lilitokea tena wakati wa ziara ya pili ambapo walimaliza sura ya pili. “Ilikuwa karibu sawa na kujifunza na Mashahidi wawili waliobatizwa,” akumbuka Serafín. Katika ziara ya tatu, kwa kuwa ilionekana walijua mambo waliyokuwa wanajifunza vizuri sana, Serafín alipendekeza wawe na kipindi cha maswali-na-majibu ili kupima kiasi ambacho hasa walielewa. Aligundua kwamba Francisco na Fausta walikuwa wamejifunza kitabu chote wenyewe!
Ujuzi wao mpya ulikuwa umewaathirije? Kwa kupatana na yale ambayo walikuwa wamejifunza, tayari walikuwa wameacha kuhudhuria mikutano ya uasiliani-roho na walivunja uhusiano na Kanisa Katoliki. Zaidi ya hayo, Francisco aliacha kuvuta tumbaku, na waliacha kula nyama ambayo haikuondolewa damu sawasawa. Kwa vile kwa wazi walifanya yote waliyokuwa wamejifunza, walitiwa moyo kuanza kushiriki ujuzi wao pamoja na wengine. Mara moja walianza kuhubiria jirani zao. Katika miezi mitatu tu, walistahili ubatizo. Francisco sasa ni mtumishi wa huduma, na kwa sababu ya kielelezo chao kizuri na bidii katika kuhubiri, watatu kati ya binti zao sasa ni Mashahidi, wana wawili huhudhuria mikutano, na watu wengine sita wa ukoo wanajifunza.
Si muda mrefu baada ya kubatizwa, Francisco alikutana na Pablo, Mkatoliki mwenye bidii ambaye alitumikia akiwa mtunza vifaa vitakatifu wa kanisa lake. Pablo alihubiri wakati wowote kasisi alipokosekana. Ikiwa mshiriki wa kanisa alikuwa mgonjwa, alimtembelea; ikiwa mtu fulani hakuonekana kanisani, Pablo alimtembelea ili kumpa kitia-moyo; na ikiwa mtu fulani alikufa, alifanya yote aliyoweza ili kuiliwaza familia. Kwa kueleweka, Pablo alipendwa sana na washiriki wote wa kanisa la eneo lake.
Kwa vile Pablo alikuwa na staha ya kina kuelekea Biblia, mara moja alikubali toleo la Francisco la kujifunza pamoja naye. Kwa haraka Pablo aliona jinsi ujumbe wa Biblia ulivyokuwa wenye maana, na baada ya mafunzo marefu aliamua kutumia baadhi ya maandiko aliyokuwa amejifunza katika moja ya “ziara za uchungaji” zake kwa mshiriki wa kanisa aliyekuwa mgonjwa. Muda mfupi baadaye, katika moja ya mahubiri yake ya Jumapili, Pablo alieleza umuhimu wa kutumia jina la Mungu, Yehova, na kwa nini hatupaswi kutumia mifano.
Kwa kuwa aliukubali ukweli kwa haraka, alitazamia kwamba washiriki wengine wa kanisa lake wangeitikia vivyo hivyo. Lakini baada ya kuhubiri mara tatu au nne kwa kutegemea Biblia, Pablo aligundua kwamba watu hawakufurahia habari aliyokuwa anaitoa. Hivyo aliamua kuachana na kanisa na kushirikiana kwa ukawaida na Mashahidi wa Yehova. Katika miezi michache alistahili ubatizo na sasa ni mhubiri mwenye bidii wa habari njema. Ingawa hawezi kuhubiri wakati wote, kwa sasa anaongoza mafunzo ya Biblia kumi.
Kuendeleza Ukuzi kwa Kukusanyika Pamoja
Mashahidi katika Guinea ya Ikweta huchukua kwa uzito amri ya Biblia ya kutoacha kukusanyika pamoja. (Waebrania 10:25) Tangu 1994 kazi ilipotambuliwa rasmi na serikali, ndugu wamekuwa na hamu ya kupata Majumba ya Ufalme yafaayo. Kwa kweli mengi ya makutaniko yamejenga majumba yayo yenyewe au yanaendelea kufanya hivyo.
Katika Mongomo, ambako hudhurio katika mikutano ya Jumapili kwa kawaida hufikia mara mbili na nusu ya idadi ya watangazaji wa Ufalme, kutaniko limekuwa likijitahidi kujenga mahali pakubwa pa kukutania. Kwa kawaida dini nyingine katika Mongomo huajiri wafanyakazi ili kujenga makanisa yao, hivyo kazi ya Mashahidi wa mahali hapo haikukosa kuonekana. Siku moja pasta wa Iglesia Nueva Apostólica (Kanisa Jipya la Kimitume) alifika katika eneo la ujenzi kumuuliza mmoja wa wazee ni kiasi gani amekuwa akiwalipa wafanyakazi hao wenye juhudi. Pasta alisema kwamba ingawa aliwaajiri waashi wa kanisa lake mwenyewe, kazi ilikuwa ikiiendelea polepole sana. Alijiuliza ikiwa angeweza kuajiri wafanyakazi waliokuwa wanajenga Jumba la Ufalme. Alipoambiwa kwamba Mashahidi wote walikuwa wakifanya kazi bila malipo, aliondoka akiwa ameduwaa.
Kwa wale wanaoishi mbali na Jumba la Ufalme, kuhudhuria mikutano kwaweza kuhitaji dhabihu ya kiasi fulani. Juan, kijana mwanamume aliyebatizwa 1994 alikabili hali hii. Alisikia kuhusu ukweli akiwa Gabon, ambako alijifunza nusu ya kwanza ya kitabu Kuishi Milele. Kisha alirudi Guinea ya Ikweta, katika kijiji cha nyumbani kwake kiasi cha kilometa 100 kutoka Mongomo. Hili lilimtokezea ugumu katika kuendelea na funzo lake. Lakini hakuzuiwa. Kila mwezi, alifunga safari ya muda wa saa nane kwa baiskeli hadi Mongomo, ambako Santiago, mmoja wa wazee wenyeji, aliongoza funzo pamoja naye. Alikaa Mongomo kwa siku chache na alijifunza mara tatu au nne katika muda huo aliokaa huko. Kwa njia hii aliweza kumaliza funzo lake na kustahili ubatizo.
Juan aendeleaje kuwa mwenye nguvu kiroho akiwa na ushirika mdogo sana na Wakristo wengine? Zaidi ya yote ni kwa kuwa mhubiri wa habari njema mwenye bidii. Aliwahubiria watu wote katika kijiji chake, na alipobatizwa alikuwa anaongoza mafunzo ya Biblia 13. Sita kati ya wanafunzi wake waliambatana naye kwenda kwenye kusanyiko la siku ya pekee katika Mongomo ili kushuhudia ubatizo wake. Sasa huongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi kwa ukawaida na watu wanaopendezwa katika eneo lake, na kwa kawaida karibu watu 20 huhudhuria.
Kumwagilia Mbegu Maji kwa Subira
Ukuzi mwingine wa kiroho huchukua muda. Mara nyingine subira kubwa inahitajika ili kuona mbegu ikitokeza tunda hatimaye. Hili lilikuwa kweli kuhusu Paca, ambaye alisikia habari njema mara ya kwanza katika 1984 wakati Edita, dada painia, alipomhubiri sokoni. Edita alipomtembelea Paca nyumbani kwake juma lililofuata Paca alikubali funzo la Biblia. Ingawa hakuwa anafanya maendeleo ya haraka, Edita aliendelea kwa sababu aliona sifa nzuri katika Paca. “Alionekana kuwa mtu wa mfano wa kondoo,” aeleza Edita, “nikasali kwa Yehova ili afungue moyo wake.”
Paca aliendelea na funzo lake kwa kukatiza-katiza kwa miaka minne na nusu lakini alifanya maendeleo madogo sana. Kwa hiyo, walipomaliza kitabu Kuishi Milele, Edita alifanya mazungumzo ya wazi pamoja na Paca kuhusu umuhimu wa kuchukua kweli kwa uzito. Katika jitihada yake ya kufikia moyo wa Paca, Edita hata alitokwa na machozi.
“Shauri lile la kutoka moyoni lilinigusa kweli kweli,” akumbuka Paca. “Kuanzia wakati huo na kuendelea nilianza kufanya mabadiliko maishani mwangu. Nilijiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na mwaka uo huo nikawa mtangazaji asiyebatizwa. Siku niliyobatizwa hatimaye ilikuwa siku ya furaha kupita zote maishani mwangu!” Shauku ya Paca ya sasa yatofautiana na ubaridi wake wa kwanza. Sasa anaongoza mafunzo ya Biblia 13, na bila shaka yeye ni mwenye subira kwa wale wasiofanya maendeleo ya haraka.
Kusaidia Watu Waboreshe Maisha Yao
Kwa kuishi kulingana na viwango vya Biblia, Mashahidi wa Yehova katika Guinea ya Ikweta wamejipatia sifa ya ufuatiaji wa haki na adabu. Mtu mmoja ambaye bila shaka alivutiwa na mwenendo wao, alimfikia mzee wa Kutaniko la Bata na kumuuliza: “Je, una kitabu Kutoa Sababu?b Nimechoshwa kabisa na kuwa mlimwengu. Ningependa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova!”
Antonio, mtumishi wa huduma katika Kutaniko la Malabo, ni kielelezo halisi cha mlimwengu ambaye alikuja kuwa Shahidi. Kabla hajajifunza Biblia, aliishi maisha ya ufisadi. Alitumia nyingi za fedha alizopata akiwa fundi wa saa katika kunywa pombe na pia aliishi maisha yasiyo na adili. Ni nini kilichomsaidia kubadili mtindo-maisha wake? Alivutwa sana na kile kinachotaarifiwa kwa dhati katika 1 Wakorintho 6:9, 10: “Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, . . . wala walevi.” Alitambua kwamba ili kuwa na upendeleo wa Mungu, anapaswa kubadili njia yake ya maisha. Kwa sababu hiyo alianza kuchunguza mashirika yake. (Mithali 13:20) Marafiki wa zamani walipomtembelea kumwalika kwenda kunywa, alikataa mwaliko wao na badala ya kwenda nao akawatolea ushahidi. Baada ya muda mfupi waliacha kumsumbua.
Je, ilistahili jitihada zote hizo? “Nina furaha sana kwamba nimebadili njia yangu ya maisha,” aeleza Antonio. “Afya yangu ni bora zaidi ingawa nimo katika miaka yangu ya 60, ilhali marafiki wangu wa zamani ama wamekufa ama wana afya mbaya. Sasa nina marafiki wa kweli badala ya wale ambao hutaka tu mwandamani ambaye yuko tayari kuwalipia kinywaji kingine. Zaidi ya yote, nina uhusiano mzuri na Mungu. Sasa ninatumikia nikiwa painia wa kawaida, na nina funzo la Biblia na mtu ambaye ana tatizo la kunywa, hivyo naweza kutumia yaliyonipata kumsaidia.”
Kuwa Watumwa wa Mungu
Karibu miaka 200 iliyopita, watu kando-kando ya pwani ya Guinea ya Ikweta walikusanywa na kusafirishwa kwenda Amerika wakiwa watumwa. Leo, wengi wanajitolea kuwa watumwa—watumwa wa Mungu. Aina hii ya utumwa umewaletea uhuru wa kweli, ukiwaweka huru na mafundisho ya Kibabiloni na mazoea ya uasiliani-roho. Pia umewafunza kuishi maisha yenye kuridhisha na yenye matokeo. Wamepata kujionea kile alichoahidi Yesu: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”—Yohana 8:32.
Watu 1,937 walihudhuria sherehe ya Ukumbusho katika 1995—karibu mara sita ya idadi ya watangazaji katika nchi hiyo—kuna matumaini makubwa ya ukuzi wa kiroho. Kadiri Mashahidi katika Guinea ya Ikweta waendeleapo kwa bidii kupanda na kumwagilia maji mbegu ya ukweli, wana hakika kwamba ‘Mungu ataendelea kuikuza.’ (1 Wakorintho 3:6) Bila shaka yoyote, kuna hali nzuri ifaayo ukuzi wa kiroho katika Guinea ya Ikweta!
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.