Mungu Anataka Tufanye Nini?
“Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.”—1 YOHANA 5:3.
1, 2. Kwa nini haishangazi kwamba Mungu ana matakwa kwa wale watakao kumwabudu kwa njia ya kukubalika?
“DINI yangu yanipendeza!” Je, sivyo wasemavyo watu mara nyingi? Lakini, kwa kweli, swali lapaswa liwe, “Je, dini yangu inampendeza Mungu?” Ndiyo, Mungu ana matakwa kwa wale wanaotaka kumwabudu kwa kukubalika. Je, hilo litushangaze? Sivyo hasa. Tuseme ungekuwa na nyumba yenye kupendeza, ambayo ulirekebisha upya hivi majuzi kwa gharama kubwa. Je, ungemruhusu mtu yeyote yule aishi huko? Bila shaka la! Yeyote yule ambaye angekuwa mpangaji angelazimika kutimiza matakwa yako.
2 Vivyo hivyo, Yehova ameandalia familia ya kibinadamu makao haya ya kidunia. Chini ya utawala wa Ufalme wake, karibuni dunia ‘itarekebishwa upya’—itageuzwa kuwa paradiso yenye kupendeza. Yehova atatimiza hili. Kwa gharama kubwa kwake mwenyewe, alimtoa Mwanaye mzaliwa-pekee ili kuwezesha hilo. Kwa hakika, ni lazima Mungu awe ana matakwa kwa wale watakaoishi huko!—Zaburi 115:16; Mathayo 6:9, 10; Yohana 3:16.
3. Solomoni alitoaje muhtasari wa yale ambayo Mungu atazamia tufanye?
3 Twaweza kupataje kujua matakwa ya Mungu? Yehova alimpulizia Mfalme Solomoni mwenye hekima atoe muhtasari wa yale ambayo Yeye atazamia tufanye. Baada ya kutafakari juu ya mambo yote aliyokuwa amefuatia—kutia na utajiri, miradi ya ujenzi, upendezi wa muziki mbalimbali, na upendo wa kimahaba—Solomoni alifikia utambuzi huu: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Mhubiri 12:13, italiki ni zetu.
“Amri Zake Si Zenye Kulemea”
4-6. (a) Ni nini maana halisi ya neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘-enye kulemea’? (b) Kwa nini twaweza kusema kwamba amri za Mungu si zenye kulemea?
4 “Uzishike amri zake.” Kwa msingi, hilo ndilo Mungu atazamia tufanye. Je, anaomba mengi mno? La hasha. Mtume Yohana atuambia jambo fulani lenye kutia moyo sana juu ya amri, au matakwa, ya Mungu. Aliandika hivi: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.”—1 Yohana 5:3.
5 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘-enye kulemea’ lamaanisha kihalisi “-zito.” Laweza kurejezea jambo lililo gumu kuishi kulingana nalo au lililo gumu kufuata. Kwenye Mathayo 23:4, neno lilo hilo linatumiwa kufafanua ile “mizigo mizito,” yaani amri na mapokeo ya kufanywa na wanadamu, ambayo waandishi na Mafarisayo waliwekea watu. Je, unapata maana ya mkataa unaofikiwa na mtume Yohana mwenye umri mkubwa? Amri za Mungu si mzigo mzito wenye kulemea, wala si ngumu sana tusiweze kuzitimiza. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 30:11.) Kinyume cha hilo, tunapompenda Mungu, kutimiza matakwa yake hutufurahisha. Hutupa sisi fursa yenye thamani ya kuonyesha kumpenda kwetu Yehova.
6 Ili kuonyesha kumpenda kwetu Mungu, twahitaji kujua kimahususi yale ambayo yeye atazamia tufanye. Acheni sasa tuchunguze matano kati ya matakwa ya Mungu. Tufanyapo hivyo, kumbuka yale aliyoandika Yohana: ‘Amri za Mungu si zenye kulemea.’
Kuendelea Kutwaa Ujuzi juu ya Mungu
7. Wokovu wetu wategemea nini?
7 Takwa la kwanza ni kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu. Fikiria maneno ya Yesu yaliyorekodiwa katika Yohana sura ya 17. Kikao kilikuwa usiku wa mwisho wa uhai wa Yesu akiwa binadamu. Yesu alikuwa ametumia sehemu kubwa ya jioni hiyo akiwatayarisha mitume wake kwa ajili ya kuondoka kwake. Yesu alihangaikia wakati ujao wao, wakati ujao wao udumuo milele. Akiinua macho yake mbinguni, yeye alisali kwa ajili yao. Katika mstari wa 3, twasoma hivi: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ Ndiyo, wokovu wao ulitegemea ‘kuendelea kwao kutwaa ujuzi’ juu ya Mungu na pia Kristo. Hilo latuhusu sisi pia. Ili tupate wokovu, ni lazima tuendelee kutwaa ujuzi huo.
8. ‘Kuendelea kutwaa ujuzi’ juu ya Mungu kwamaanisha nini?
8 “Kuendelea kutwaa ujuzi” juu ya Mungu kwamaanisha nini? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa “kuendelea kutwaa ujuzi” lamaanisha “kupata kujua, kufahamu,” au “kuelewa kikamili.” Ona pia, kwamba ufasiri “kuendelea kutwaa ujuzi” wadokeza kwamba hiyo ni hatua yenye kuendelea. Hivyo, kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu kwamaanisha kupata kumjua si kijuujuu bali kindani, kusitawisha urafiki wenye uelewevu pamoja naye. Uhusiano wenye kuendelea pamoja na Mungu huleta ujuzi wenye kuongezeka daima juu yake. Hatua hiyo yaweza kuendelea milele, kwani hatutajifunza kamwe mambo yote juu ya Yehova.—Waroma 11:33.
9. Twaweza kujifunza nini juu ya Yehova kutoka kitabu cha uumbaji?
9 Twaendeleaje kutwaa ujuzi juu ya Mungu? Kuna vitabu viwili viwezavyo kutusaidia. Kimoja ni kitabu cha uumbaji. Vitu ambavyo Yehova ameumba—vyenye uhai na pia visivyo na uhai—hutupa sisi ufahamu fulani wenye kina juu ya aina ya mtu alivyo. (Waroma 1:20) Fikiria vielelezo fulani. Kunguruma kwa poromoko la maji lenye fahari, kuponda-ponda kwa mawimbi wakati wa dhoruba, mwono wa mbingu zenye nyota katika usiku usio na mawingu—je, mambo kama hayo hayatufundishi kwamba Yehova ni Mungu aliye “hodari kwa nguvu”? (Isaya 40:26) Mtoto achekaye aonapo kitoto cha mbwa kikifuata-fuata mkia wacho au kitoto cha paka kikicheza na tufe la uzi wa sufu—je, hilo halidokezi kwamba Yehova, “Mungu mwenye furaha,” ana ucheshi? (1 Timotheo 1:11) Ladha ya mlo mtamu, harufu yenye kupendeza ya maua shambani, rangi nyangavu za kipepeo mwororo, sauti za ndege wakiimba wakati wa masika, kumbatio changamfu la mpendwa—je, hatutambui kutokana na mambo haya kwamba Muumba wetu ni Mungu mwenye upendo, anayetaka tufurahie uhai?—1 Yohana 4:8.
10, 11. (a) Ni mambo gani juu ya Yehova ambayo hatuwezi kujifunza kutoka kitabu cha uumbaji? (b) Ni majibu ya maswali yapi yanayopatikana katika Biblia tu?
10 Hata hivyo, kuna mpaka kwa yale tuwezayo kujifunza juu ya Yehova kutokana na kitabu cha uumbaji. Kwa kielelezo: Jina la Mungu ni nani? Kwa nini aliumba dunia akawaweka wanadamu juu yayo? Kwa nini Mungu anaruhusu uovu? Wakati ujao una nini kwa ajili yetu? Ili kupata majibu kwa maswali hayo, ni lazima tuendee kile kitabu kingine kinachotoa ujuzi juu ya Mungu—Biblia. Katika kurasa zacho, Yehova hufunua mambo juu yake mwenyewe, kutia na jina lake, utu wake, na makusudi yake—habari ambayo hatuwezi kupata kutoka chanzo kingine chochote.—Kutoka 34:6, 7; Zaburi 83:18; Amosi 3:7.
11 Katika Maandiko, Yehova hutoa pia ujuzi muhimu juu ya watu wengine ambao twahitaji kujua juu yao. Kwa kielelezo, Yesu Kristo ni nani, naye ana sehemu gani katika kutimizwa kwa makusudi ya Yehova? (Matendo 4:12) Shetani Ibilisi ni nani? Yeye huwaongoza watu vibaya katika njia zipi? Twaweza kuepukaje kuongozwa vibaya naye? (1 Petro 5:8) Majibu yenye kuokoa uhai ya maswali haya yanapatikana katika Biblia tu.
12. Ungeelezaje ni kwa nini kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu na makusudi yake si mzigo wenye kulemea?
12 Je, kuendelea kutwaa ujuzi huo juu ya Mungu na makusudi yake ni mzigo wenye kulemea? La hasha! Je, waweza kukumbuka jinsi ulivyohisi ulipojifunza kwa mara ya kwanza kwamba jina la Mungu ni Yehova, kwamba Ufalme wake utarudisha Paradiso kwenye dunia hii, kwamba alimtoa Mwana wake mpendwa awe fidia kwa ajili ya dhambi zetu, pamoja na kweli nyinginezo zenye thamani? Je, hilo halikuwa kama kuondoa shela ya ukosefu wa ujuzi na kuona mambo kwa wazi kwa mara ya kwanza? Kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu si mzigo wenye kulemea. Ni jambo lenye kupendeza!—Zaburi 1:1-3; 119:97.
Kufikia Viwango vya Mungu
13, 14. (a) Tuendeleapo kutwaa ujuzi juu ya Mungu, ni mabadiliko gani tunayohitaji kufanya maishani mwetu? (b) Mungu anataka kwamba tuepuke mazoea gani yasiyo safi?
13 Tuendeleapo kutwaa ujuzi juu ya Mungu, twapata kung’amua kwamba twahitaji kufanya mabadiliko katika maisha zetu. Hilo latuleta kwenye takwa la pili. Ni lazima tufikie viwango vya Mungu vya mwenendo sawa na kukubali kweli yake. Kweli ni nini? Je, kwa kweli Mungu hujali kile tunachoamini na kile tunachofanya? Ni wazi kwamba watu wengi leo hawaoni kwamba anajali. Ripoti iliyochapishwa na Kanisa la Uingereza katika 1995 ilidokeza kwamba kuishi pamoja bila kufunga ndoa hakupasi kuonwa kuwa dhambi. “Maneno ‘kuishi katika dhambi’ yaaibisha na si yenye kusaidia,” akasema askofu mmoja wa kanisa.
14 Kwa hiyo basi, je, “kuishi katika dhambi” si dhambi tena? Yehova hutuambia kwa udhahiri kabisa jinsi ahisivyo juu ya mwenendo wa aina hiyo. Neno lake, Biblia, hutaarifu hivi: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila kutiwa unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Kufanya ngono kabla ya ndoa huenda kusiwe dhambi kwa maoni ya makasisi na waenda-kanisani wasio na uzuizi kiadili, lakini ni dhambi nzito machoni pa Mungu! Ndivyo na uzinzi, ngono ya maharimu (watu wa ukoo), na ugoni-jinsia-moja. (Mambo ya Walawi 18:6; 1 Wakorintho 6:9, 10) Mungu ataka kwamba tuepuke mazoea ya aina hiyo, anayoona kuwa yasiyo safi.
15. Matakwa ya Mungu huhusishaje njia tunayowatendea wengine na pia kile tunachoamini?
15 Hata hivyo, haitoshi kuepuka tu mazoea ambayo Mungu huona kuwa yenye dhambi. Matakwa ya Mungu hutia ndani pia njia tunayotendea wengine. Katika familia, yeye atazamia mume na mke wapendane na kustahiana. Mungu anataka wazazi watunze mahitaji ya watoto wao ya kimwili, ya kiroho, na ya kihisia-moyo. Anawaambia watoto wawe watiifu kwa wazazi wao. (Mithali 22:6; Wakolosai 3:18-21) Na namna gani itikadi zetu? Yehova Mungu anataka tuepuke itikadi na desturi zinazotokana na ibada isiyo ya kweli au ambazo hupinga ile kweli safi inayofundishwa katika Biblia.—Kumbukumbu la Torati 18:9-13; 2 Wakorintho 6:14-17.
16. Eleza ni kwa nini kufikia viwango vya Mungu vya mwenendo sawa na kukubali kweli yake si mzigo wenye kulemea.
16 Je, kufikia kwetu viwango vya Mungu vya mwenendo sawa na kukubali kweli yake ni mzigo wenye kulemea? Sivyo tunapofikiria manufaa—ndoa ambazo katika hizo mume na mke wanapendana na wana itibari katika mmoja na mwenzake badala ya ndoa ambazo zimevunjika kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu; makao ambako watoto huhisi wanapendwa na wanatakwa na wazazi wao badala ya familia ambazo katika hizo watoto wanahisi hawapendwi, wanapuuzwa, na hawatakwi; dhamiri safi na afya njema badala ya hisia za kuwa na hatia na mwili uliokumbwa na UKIMWI au maradhi mengine ya kupitishwa kingono. Kwa hakika, matakwa ya Yehova hayatunyimi chochote kile tunachohitaji ili kufurahia uhai!—Kumbukumbu la Torati 10:12, 13.
Stahi Uhai na Damu
17. Yehova huonaje uhai na damu?
17 Upatanishapo maisha yako na viwango vya Mungu, unapata kuthamini jinsi uhai ulivyo wenye thamani kikweli. Acheni sasa tuzungumzie takwa la tatu la Mungu. Ni lazima tustahi uhai na damu. Uhai ni mtakatifu kwa Yehova. Wapaswa uwe hivyo, kwa maana yeye ndiye Chanzo cha uhai. (Zaburi 36:9) Kwani, hata uhai wa mtoto asiyezaliwa bado aliye ndani ya mama yake ni wenye thamani kwa Yehova! (Kutoka 21:22, 23) Damu huwakilisha uhai. Kwa hiyo, damu ni takatifu pia machoni pa Mungu. (Mambo ya Walawi 17:14) Basi, si ajabu kwamba Mungu atazamia tuone uhai na damu jinsi anavyoviona.
18. Maoni ya Yehova juu ya uhai na damu yataka tufanye nini?
18 Kustahi uhai na damu kwataka tufanye nini? Tukiwa Wakristo, sisi hatuhatarishi uhai wetu bure ili kupata msisimko tu. Sisi ni wenye kujali usalama, kwa hiyo tunahakikisha kwamba magari yetu na nyumba zetu ni salama. (Kumbukumbu la Torati 22:8) Hatutumii tumbaku, hatutafuni miraa, au kutumia dawa zisababishazo uraibu au za kulevya ili kuona raha. (2 Wakorintho 7:1) Kwa sababu twamsikiliza Mungu asemapo ‘jiepusheni na damu,’ haturuhusu damu itiwe miilini mwetu. (Matendo 15:28, 29) Ingawa twapenda uhai, hatutajaribu kuokoa uhai wetu wa sasa kwa kuvunja sheria ya Mungu na hivyo kuhatarisha taraja letu la uhai udumuo milele!—Mathayo 16:25.
19. Eleza jinsi tunavyonufaika kutokana na kustahi uhai na damu.
19 Je, kuona kwetu uhai na damu kuwa takatifu ni mzigo wenye kulemea? La, hasha! Ebu fikiria. Je, uhuru pasipo kansa ya mapafu inayosababishwa na kuvuta tumbaku ni mzigo wenye kulemea? Je, kuponyoka uraibu wa kiakili na wa kimwili wa madawa yenye kudhuru ni mzigo wenye kulemea? Je, kuepuka kupatwa na UKIMWI, mchochota wa ini, au maradhi mengine yanayotokana na utiaji-damu mishipani ni mzigo wenye kulemea? Kwa wazi, kujiepusha kwetu na tabia na mazoea yenye kudhuru ni kwa faida yetu.—Isaya 48:17.
20. Familia moja ilinufaikaje kutokana na kuwa na maoni ya Mungu juu ya uhai?
20 Fikiria ono hili. Miaka kadhaa iliyopita, mwanamke Shahidi aliyekuwa na mimba ya karibu miezi mitatu na nusu alianza kutokwa na damu jioni moja naye akapelekwa hospitali mbio. Baada ya daktari kumchunguza, mwanamke huyo alimsikia akimwambia mmoja wa wauguzi kwamba wangelazimika kuikomesha mimba hiyo. Akijua maoni ya Yehova juu ya uhai wa watoto wasiozaliwa bado, yeye alikataa katakata utoaji-mimba akimwambia daktari hivi: “Ikiwa yu hai, mwache humo!” Aliendelea kutokwa na damu mara kwa mara, lakini miezi kadhaa baadaye alizaa kabla ya wakati wake, kitoto kivulana chenye afya, ambaye sasa ni mwenye umri wa miaka 17. Alieleza hivi: “Mwana wetu aliambiwa haya yote, naye alisema anaterema kwamba hakutupwa. Ajua kwamba sababu tu ya yeye hata kuwa hai ni kumtumikia kwetu Yehova.” Kwa hakika, kuwa na maoni ya Mungu juu ya uhai hakukuwa mzigo wenye kulemea kwa familia hii!
Kutumikia Pamoja na Watu wa Yehova Waliofanywa Kuwa Tengenezo
21, 22. (a) Yehova atazamia tumtumikie pamoja na nani? (b) Watu wa Mungu waliofanywa kuwa tengenezo wanaweza kutambuliwaje?
21 Sisi hatuko peke yetu katika kufanya mabadiliko yanayohitajiwa ili kuzipatanisha maisha zetu na viwango vya Mungu. Yehova ana watu kwenye dunia hii, naye atazamia tumtumikie pamoja nao. Hilo latuleta kwenye takwa la nne. Ni lazima tumtumikie Yehova pamoja na tengenezo lake lenye kuelekezwa kwa roho.
22 Lakini, watu wa Mungu waliofanywa kuwa tengenezo wanaweza kutambuliwaje? Kulingana na viwango vilivyomo katika Maandiko, wao wana upendo halisi miongoni mwao wenyewe, wana staha yenye kina kuelekea Biblia, wanaheshimu jina la Mungu, wanahubiri juu ya Ufalme wake, nao si sehemu ya ulimwengu huu mwovu. (Mathayo 6:9; 24:14; Yohana 13:34, 35; 17:16, 17) Kuna tengenezo moja tu la kidini kwenye dunia hii lililo na alama hizi zote za Ukristo wa kweli—Mashahidi wa Yehova!
23, 24. Twaweza kuonyesha kwa kielezi gani kwamba kumtumikia Yehova pamoja na watu wake waliofanywa kuwa tengenezo si mzigo wenye kulemea?
23 Je, kumtumikia Yehova pamoja na watu wake waliofanywa kuwa tengenezo ni mzigo wenye kulemea? La hasha! Kinyume cha hilo, ni pendeleo lenye thamani kuwa na upendo na utegemezo wa familia ya ulimwenguni pote ya ndugu na dada Wakristo! (1 Petro 2:17) Ebu wazia umeokoka mvunjiko wa meli na wajipata majini, uking’ang’ana kuelea. Unapohisi kwamba huwezi kuvumilia zaidi, mkono wakufikilia kutoka katika mashua ya kuokolea uhai. Ndiyo, kuna waokokaji wengine! Katika mashua hiyo ya kuokolea uhai, wewe na wengine mnapiga makasia kwa zamu hadi pwani mkiwachukua waokokaji wengine njiani.
24 Je, sisi hatumo katika hali iyo hiyo? Tumevutwa kutoka katika “maji” yenye hatari ya ulimwengu huu mwovu kuingia katika “mashua ya kuokolea uhai” ya tengenezo la kidunia la Yehova. Humo, twatumikia sambamba tuelekeapo “pwani” ya ulimwengu mpya wenye uadilifu. Misongo ya maisha haya ikitufanya tuchoke njiani, twashukuru kama nini kwa msaada na faraja ya waandamani Wakristo wa kweli!—Mithali 17:17.
25. (a) Tuna wajibu gani kuelekea wale ambao wangali katika “maji” ya ulimwengu huu mwovu? (b) Ni takwa gani la Mungu litakalozungumziwa katika makala inayofuata?
25 Namna gani wengine—watu wenye mioyo ya haki ambao wangali katika “maji”? Tuna wajibu wa kuwasaidia waingie katika tengenezo la Yehova, sivyo? (1 Timotheo 2:3, 4) Wanahitaji msaada ili wajifunze yale ambayo Mungu anataka. Hilo latuleta kwenye takwa la Mungu la tano. Ni lazima tuwe wapiga-mbiu waaminifu-washikamanifu wa Ufalme wa Mungu. Yanayohusishwa katika hilo yatazungumziwa katika makala ifuatayo.
Je, Wakumbuka?
◻ Kwa nini amri za Mungu si zenye kulemea?
◻ Tunaendeleaje kutwaa ujuzi juu ya Mungu?
◻ Kwa nini kufikia viwango vya Mungu vya mwenendo sawa na kukubali kweli yake si mzigo wenye kulemea?
◻ Maoni ya Mungu juu ya uhai na damu yataka tufanye nini?
◻ Mungu atazamia tumtumikie pamoja na nani, nao waweza kutambuliwaje?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Twajifunza juu ya Yehova kutoka kitabu cha uumbaji na kutoka Biblia
[Hisani]
Mamba: Kwa hisani ya Australian International Public Relations; dubu: Safari-Zoo of Ramat-Gan, Tel Aviv