Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Kuwafikia Watu wa Namna Zote na Kweli
MTUME Paulo alikuwa mpiga-mbiu mwenye bidii wa Ufalme wa Mungu. Hakuruhusu upinzani uzuie utume wake wa kuihubiri “habari njema.” (1 Wakorintho 9:16; Matendo 13:50-52) Paulo aliwasihi wengine wafuate kielelezo chake.—1 Wakorintho 11:1.
Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa jitihada zao za kuhubiri kwa kuazimia. Kwa kweli, wao husema na wengine katika “majira yenye kufaa” na katika “majira yenye taabu” ili watimize kazi yao walioagizwa na Mungu ya ‘kufanya wanafunzi.’ (2 Timotheo 4:2; Mathayo 28:19, 20) Hata katika nchi ambako wao hupatwa na upinzani, watu wenye moyo wa haki wanafikiwa na ule ujumbe ulio wa maana sana juu ya Ufalme wa Mungu, kama yaonyeshavyo mambo yaliyoonwa yafuatayo.
◻ Katika kisiwa kimoja magharibi mwa Pasifiki ambako kazi ya Mashahidi wa Yehova iko chini ya marufuku, mvulana mwenye umri wa miaka 12 alijikuta amezungukwa na mashirika mabaya shuleni. Wengi wa wanadarasa wake walivuta sigareti, walisoma fasihi za kiponografia, waliwasumbua walimu, na kushiriki katika mapigano kwa ukawaida. Hali ilipata kuwa mbaya sana hivi kwamba huyo mvulana alimwomba babake kama angeweza kuhamia shule nyingine. Lakini baba alisababu pamoja na mwanaye dhidi ya wazo hilo, kwa kuwa alihisi kwamba mwenendo wa wanafunzi katika shule nyingine za karibu haungekuwa tofauti. Hata hivyo, angemsaidiaje mtoto wake?
Huyo baba alikumbuka akiwa na kitabu cha vijana nyumbani. Kilikuwa zawadi kutoka kwa mtu wa ukoo aliyekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo alikitafuta hicho kitabu, na alipokiona, alimpatia mwanaye. Kichwa chacho kilikuwa Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi.a Huyo mvulana aliipata sura “Naweza Kukabilianaje na Msongo wa Marika?” kuwa yenye kusaidia hasa. Haikumfunza umuhimu wa kudumisha hali ya kujistahi tu bali ilimfunza pia jinsi ya kusema la kwa busara wakati wengine walipojaribu kumsonga afuate mwendo usio wa hekima. Kwa kutumia kanuni za Kimaandiko zipatikanazo ndani ya hicho kitabu, huyo mwanamume kijana alijifunza jinsi ya kukabiliana kwa mafanikio na msongo wa marika.
Kwa kuona mabadiliko hayo chanya na mengine katika mwanaye, baba aliamua kukisoma hicho kitabu. Akipendezwa na mashauri yenye kutumika yapatikanayo ndani ya hicho kitabu, baba aliomba Mashahidi wa Yehova funzo la Biblia nyumbani. Baadaye washiriki wengine wa familia yake walijiunga naye katika hilo funzo. Tokeo likawa nini? Huyo mvulana, ndugu yake mchanga, babake, na babu na nyanya yake sasa ni Mashahidi wa Yehova.
◻ Katika nchi hiyohiyo, Mashahidi wa Yehova wawili walifungwa gerezani kwa sababu ya utii wao kamili wa kanuni za Biblia. Hata hivyo, hawakuruhusu hali yao iwazuie kusema kwa ushujaa juu ya Ufalme wa Mungu. Walimfikia ofisa wa gereza, wakapata ruhusa ya kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana humo. Walifurahi jinsi gani wakati wafungwa 14 walipoonyesha kupendezwa na Biblia, wakajiunga na hao Mashahidi kwa tukio hilo muhimu! Baada ya kuachiliwa kwao, baadhi yao waliendelea kujifunza Biblia na kushirikiana na Mashahidi wa Yehova.
Katika nchi zaidi ya 25, Mashahidi wa Yehova huteseka kama tokeo la marufuku au aina mbalimbali za upinzani au mnyanyaso. Hata hivyo, kama mitume, wanaendelea “bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.”—Matendo 5:42.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.